-
RohoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Ni jambo linalofaa kuangaliwa kwamba wakati Elisabeti alipopokea roho takatifu kisha “akapaaza sauti kubwa,” yeye hakuwa katika mkutano wa ibada bali alikuwa akimsalimu mtu wa ukoo aliyemtembelea. (Luka 1:41, 42) Kama ilivyoandikwa katika Matendo 4:31, wakati roho takatifu iliposhuka juu ya kusanyiko la wanafunzi, mahali hapo palitikiswa, lakini matokeo ya roho hiyo juu ya wanafunzi hao hayakuwa kutetemeka au kujiviringisha, bali ‘walisema neno la Mungu kwa ujasiri.’ Vivyo hivyo leo, ujasiri wa kusema neno la Mungu, kuhubiri kwa bidii—hayo ndiyo mambo yanayoonyesha kwamba mtu ana roho takatifu.
Gal. 5:22, 23: “Matunda ya roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Mtu anapowatafuta watu ambao kweli wana roho ya Mungu, anapaswa kuangalia matunda hayo wala si kupaaza sauti na kuruka-ruka.)
Je, uwezo wa kusema kwa msisimko mkubwa katika lugha ambayo mtu hajajifunza kamwe unathibitisha kwamba yeye ana roho ya Mungu?
Ona kichwa “Kusema kwa Lugha.”
Je, maponyo ya kimuujiza yanayofanywa leo hutokana na roho ya Mungu?
Ona kichwa “Uponyaji.”
Ni nani anayebatizwa kwa roho takatifu?
Ona ukurasa wa 309, chini ya kichwa “Ubatizo,” pia kichwa “Kuzaliwa Mara ya Pili.”
Je, mwanadamu ana sehemu ya roho ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa?
Eze. 18:4: “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (ZSB hutafsiri neno la Kiebrania neʹphesh katika mstari huu kuwa “nafsi,” kwa hiyo inasema kwamba ni nafsi inayokufa. Tafsiri fulani zinazotafsiri neno neʹphesh kuwa “nafsi” katika maandiko mengine hutumia neno “yule” au “yeyote” katika mstari huu. Kwa hiyo, neʹphesh, nafsi, ndiyo mtu, si sehemu yake isiyo na mwili inayoendelea kuishi mwili wake unapokufa.) (Ili kupata habari zaidi, ona kichwa “Nafsi.”)
Zab. 146:4: “Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Neno la Kiebrania lililotafsiriwa hapa “roho” linatokana na neno ruʹach. Watafsiri fulani hulitafsiri kuwa “pumzi.” Wakati hiyo ruʹach, au nguvu za utendaji, inapouacha mwili, mawazo ya mtu hupotea: hayaendelei kuishi katika makao mengine.)
Mhu. 3:19-21: “Kuna mwisho ambao huwafikia wana wa binadamu na mwisho ambao huwafikia wanyama, nao hufikiwa na mwisho uleule. Anavyokufa mmoja, ndivyo anavyokufa yule mwingine; nao wote wana roho moja, hivi kwamba mwanadamu si bora kuliko mnyama, kwa kuwa yote ni ubatili. Wote wanaenda mahali pamoja. Wote wametoka katika mavumbi, nao wote wanarudi mavumbini. Ni nani anayejua roho ya wana wa binadamu, ikiwa inapanda juu; na roho ya mnyama, ikiwa inashuka chini duniani?” (Kwa sababu wanadamu wamerithi dhambi na kifo kutoka kwa Adamu, wote hufa na kurudi mavumbini, kama vile wanyama. Lakini je, kila mwanadamu ana roho inayoendelea kuishi ikiwa kama mtu mwenye akili baada ya kuacha kutenda kazi mwilini? Hapana; mstari wa 19 unajibu kwamba wanadamu na wanyama “wote wana roho moja.” Kwa kutegemea tu uchunguzi wa wanadamu, hakuna anayeweza kujibu kwa mamlaka swali lililo katika mstari wa 21 kuhusu roho. Lakini Neno la Mungu linajibu kwamba wanadamu hawana kitu chochote kutokana na kuzaliwa ambacho huwafanya wawe bora kuliko wanyama wakati wanapokufa. Hata hivyo, kwa sababu ya mpango wenye rehema wa Mungu kupitia Kristo, wanadamu walio na imani wamepewa tazamio la kuishi milele. Wanyama hawajapewa tazamio hilo. Kwa wanadamu wengi, hilo litafanywa kupitia ufufuo, wakati nguvu za utendaji kutoka kwa Mungu zitakapowapa tena uhai.)
Luka 23:46: “Yesu akaita kwa sauti kubwa na kusema: ‘Baba, ninaikabidhi roho [Kigiriki, pneuʹmaʹ] yangu mikononi mwako.’ Alipokuwa amesema jambo hilo, akakata pumzi.” (Ona kwamba Yesu alikata pumzi. Wakati roho yake ilipotoka, hakushika njia kwenda zake mbinguni. Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu siku ya tatu. Kisha, kama andiko la Matendo 1:3, 9 linavyoonyesha, alimaliza siku 40 zaidi ndipo akapanda mbinguni. Kwa hiyo, maneno ambayo Yesu alisema wakati wa kufa kwake yalimaanisha nini? Alikuwa akisema alijua kwamba, alipokufa, matazamio yake ya uzima wa wakati ujao yalikuwa kabisa mkononi mwa Mungu. Ili kupata maelezo zaidi kuhusu ‘roho ambayo humrudia Mungu,’ ona ukurasa wa 224, 225, chini ya kichwa “Nafsi.”)
Mtu Akisema—
‘Je, una roho takatifu?’
Unaweza kujibu hivi: ‘Ndiyo, na ndiyo sababu nimekuja kukutembelea leo. (Mdo. 2:17, 18)’
Au unaweza kusema: ‘Hiyo ndiyo inayoniwezesha kushiriki huduma ya Kikristo. Lakini nimeona kwamba watu wana maoni yanayotofautiana kuhusu kile kinachoonyesha kwamba mtu kweli ana roho ya Mungu. Wewe unaangalia mambo gani?’ Kisha unaweza kuongezea: (Zungumzia baadhi ya habari zilizo katika ukurasa wa 243, 244.)
-
-
Roho ya UlimwenguKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Roho ya Ulimwengu
Maana: Nguvu zinazowachochea wanadamu ambao si watumishi wa Yehova Mungu, zikiwafanya watu hao waseme na kutenda mambo kulingana na tabia fulani ya kawaida. Ijapokuwa watu hutenda kulingana na mapendezi yao binafsi, wale walio na roho ya ulimwengu wana maelekeo fulani ya msingi, njia za kutenda mambo, na miradi maishani ambayo ni kawaida ya mfumo wa mambo uliopo ambao mungu na mtawala wake ni Shetani.
Kwa nini mtu anapaswa kuhangaikia kwa uzito asitiwe uchafu na roho ya ulimwengu?
1 Yoh. 5:19: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Shetani amesitawisha roho inayotawala fikira na shughuli za wanadamu ambao si watumishi waliokubaliwa wa Yehova. Ni roho ya ubinafsi na kiburi ambayo imeenea sana hivi kwamba ni kama hewa ambayo wanadamu wanapumua. Tunahitaji kuwa waangalifu sana ili tusijiweke chini ya mamlaka ya Shetani kwa kuruhusu roho hiyo iongoze maisha yetu.)
Ufu. 12:9: “Yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.” (Tangu jambo hilo litukie, baada ya kuzaliwa kwa Ufalme mwaka wa 1914, uvutano wa Shetani na roho wake waovu umeongezeka sana kati ya wanadamu. Roho yake imewachochea watu wawe na ubinafsi na jeuri zaidi. Hasa wale wanaojaribu kumtumikia Yehova husongwa sana ili wawe sehemu ya ulimwengu, watende kama wengine wanavyotenda, na kuacha ibada ya kweli.)
-