Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Serikali
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Serikali ya Mungu ndiyo suluhisho pekee la kweli kwa matatizo ya wanadamu

      Matatizo yanayohitaji kusuluhishwa yanataka nguvu, uwezo, na sifa ambazo wanadamu hawana. Mungu anaweza kuwaweka huru wanadamu kutoka katika uvutano wa Ibilisi na roho wake waovu, na Mungu ameahidi kufanya hivyo, lakini hakuna mwanadamu anayeweza kufanya hivyo. Mungu amefanya uandalizi wa kufanya yale ambayo sayansi ya tiba haiwezi kamwe kutimiza—kuondoa dhambi, hivyo kukomesha magonjwa na kifo na kufanya iwezekane watu wawe jinsi wanavyotaka kuwa kikweli. Muumba ana ujuzi unaohitajiwa (kuhusu dunia na taratibu zote za uhai) ili kusuluhisha matatizo ya uzalishaji wa chakula na kuzuia uchafuzi hatari, lakini mara nyingi jitihada za wanadamu huleta matatizo zaidi. Neno la Mungu tayari linageuza maisha ya watu hivi kwamba wale wanaoitikia uongozi wake wanakuwa wenye fadhili, watu wenye upendo na maadili bora, jamii ya watu wanaokataa kutumia silaha dhidi ya wanadamu wenzao na wanaoishi kwa amani na undugu wa kweli ijapokuwa wanatoka katika mataifa, rangi, na makabila yote.

      Ufalme wa Mungu utaondoa wakati gani mfumo wa ulimwengu uliopo sasa? Ona vichwa “Vipindi vya Wakati” na “Siku za Mwisho.”

  • Shetani Ibilisi
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Shetani Ibilisi

      Maana: Kiumbe wa roho ambaye ni mpinzani mkuu wa Yehova Mungu na wa wote wanaomwabudu Mungu wa kweli. Alipewa jina Shetani kwa sababu alianza kumpinga Yehova. Shetani pia anaitwa Ibilisi, kwa sababu yeye ndiye mchongezi mkuu wa Mungu. Shetani anaitwa nyoka wa zamani, labda kwa sababu alimtumia nyoka katika Edeni kumdanganya Hawa, na kwa sababu hiyo jina “nyoka” likaja kumaanisha “mdanganyifu.” Katika kitabu cha Ufunuo, mfano wa joka mkubwa anayenyafua unatumiwa kumhusu Shetani.

      Tunaweza kujuaje kama kweli kuna mtu huyo wa roho?

      Biblia ndiyo chanzo kikuu cha uthibitisho. Humo anaitwa kwa jina mara nyingi (Shetani mara 52, Ibilisi mara 33). Pia ushahidi wa kuwako kwa Shetani unaotoka kwa mtu aliyejionea kwa macho umeandikwa humo. Shahidi huyo aliyemwona kwa macho ni nani? Yesu Kristo, aliyeishi mbinguni kabla ya kuja duniani, mara nyingi alisema kumhusu mwovu huyo kwa kumtaja jina.—Luka 22:31; 10:18; Mt. 25:41.

      Yale ambayo Biblia inasema kumhusu Shetani Ibilisi yanapatana na akili. Uovu ambao wanadamu kwa ujumla wanapata haulingani na nia mbovu ya wale wanaousababisha. Maelezo ya Biblia kuhusu mwanzo wa Shetani na matendo yake yanaonyesha wazi kwa nini, ijapokuwa wengi wanatamani kuishi kwa amani, wanadamu wamesumbuliwa na chuki, jeuri, na vita kwa maelfu ya miaka na kwa nini hayo yamefikia kiwango kinachotisha kuwaangamiza wanadamu wote.

      Ikiwa kweli hakuna Ibilisi, kukubali mambo ambayo Biblia inasema kumhusu hakungemletea mtu faida inayodumu. Hata hivyo, mara nyingi watu ambao zamani walishiriki katika mambo ya uchawi au walioshiriki katika vikundi vya kuwasiliana na pepo wanasema kwamba wakati huo walitaabishwa sana kwa sababu ya kusikia “sauti” kutoka kwa vitu visivyoonekana, “walipagawa” na watu wenye kupita uwezo wa wanadamu, n.k. Walipata kitulizo cha kweli wakati walipojifunza yale ambayo Biblia inasema kuhusu Shetani na roho wake waovu, wakatumia shauri la Biblia linalowaagiza watu waache mazoea ya kuwasiliana na pepo, nao wakatafuta msaada wa Yehova kupitia sala.—Ona ukurasa wa 140-145, chini ya kichwa “Kuwasiliana na Pepo.”

      Kuamini kwamba Shetani yuko hakumaanishi kukubali wazo la kwamba yeye ana pembe, mkia uliochongoka, na uma mkubwa na kwamba anawachoma watu motoni. Biblia haisemi kwamba Shetani yuko hivyo. Hiyo ni kazi ya wachoraji wa zamani waliofuata mifano ya Pan, ambaye ni mungu katika hekaya za Wagiriki, na maandishi yanayoitwa Inferno yaliyoandikwa na mshairi Mwitaliano, Dante Alighieri. Badala ya kufundisha kwamba watu wanachomwa motoni, Biblia inasema waziwazi kwamba “wafu, hawajui lolote kamwe.”—Mhu. 9:5.

      Je, Shetani ni uovu tu ulio ndani ya watu?

      Andiko la Ayubu 1:6-12 na 2:1-7 husema kuhusu mazungumzo kati ya Yehova Mungu na Shetani. Ikiwa Shetani angekuwa uovu ulio ndani ya mtu, basi katika kisa hiki ingemaanisha uovu huo umo ndani ya Yehova. Lakini hayo hayapatani hata kidogo na yale ambayo Biblia inatuambia kumhusu Yehova, kwamba “ndani yake hamna ukosefu wowote wa uadilifu.” (Zab. 92:15; Ufu. 4:8) Inastahili kuangaliwa kwamba maandishi ya Kiebrania yanatumia neno has·Sa·tanʹ (yule Shetani) katika masimulizi yaliyo katika Ayubu, kuonyesha kwamba anayezungumziwa ni yule mpinzani mkuu wa Mungu.—Ona pia Zekaria 3:1, 2, kielezi-chini katika chapa ya Marejeo ya NW.

      Andiko la Luka 4:1-13 husema kwamba Ibilisi alijaribu kumshawishi Yesu atende aliyotaka. Masimulizi hayo yanaeleza maneno ambayo Ibilisi alisema na majibu ambayo Yesu alitoa. Je, Yesu alikuwa akishawishiwa na uovu uliokuwa ndani yake mwenyewe? Maoni hayo hayapatani na jinsi Biblia inavyosema kwamba Yesu hakuwa na dhambi. (Ebr. 7:26; 1 Pet. 2:22) Ijapokuwa katika Yohana 6:70 neno la Kigiriki di·aʹbo·losʹ linatumiwa kueleza sifa mbaya ambayo ilikuwa imesitawi katika Yuda Iskariote, katika Luka 4:3 jina hili ho di·aʹbo·losʹ (yule Ibilisi) limetumiwa, nalo linamaanisha mtu halisi.

      Je, kumlaumu Ibilisi ni njia tu inayotumiwa kujaribu kuepuka daraka kwa ajili ya hali mbaya?

      Watu fulani humlaumu Ibilisi kwa yale ambayo wao wenyewe wanafanya. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba mara nyingi wanadamu wanachukua sehemu kubwa ya lawama kwa ubaya wanaopata, iwe ni mikononi mwa wanadamu wengine au kutokana na mwenendo wao wenyewe. (Mhu. 8:9; Gal. 6:7) Ingawa hivyo, Biblia inatujulisha kuhusu hila na kuwako kwa adui huyo anayepita uwezo wa mwanadamu ambaye amewaletea wanadamu huzuni nyingi sana. Inaonyesha jinsi tunavyoweza kutoka chini ya uongozi wake.

      Shetani alitoka wapi?

      Kazi zote za Yehova ni kamilifu; yeye siye mwanzilishi wa ukosefu wa uadilifu; kwa hiyo hakumuumba yeyote akiwa mwovu. (Kum. 32:4; Zab. 5:4) Yule aliyekuja kuwa Shetani hapo mwanzoni alikuwa mwana mkamilifu wa kiroho wa Mungu. Aliposema kwamba Ibilisi “hakusimama imara katika kweli,” Yesu alionyesha kwamba wakati mmoja huyo alikuwa “katika kweli.” (Yoh. 8:44) Lakini, kama walivyo viumbe wote wa Mungu wenye akili, mwana huyo wa kiroho alipewa uhuru wa kuchagua. Alitumia vibaya uhuru wake wa kuchagua, akaruhusu maoni ya kujitafutia umashuhuri yasitawi moyoni mwake, akaanza kutamani ibada iliyokuwa ya Mungu peke yake, na kwa hiyo akamshawishi Adamu na Hawa wamsikilize yeye kuliko kumtii Mungu. Basi kupitia matendo yake, yeye mwenyewe akajifanya Shetani, jina linalomaanisha “mpinzani.”—Yak. 1:14, 15; ona pia ukurasa wa 55, chini ya kichwa “Dhambi.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki