-
Sikukuu ya KuzaliwaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
“Wagiriki waliamini kwamba kila mtu alikuwa na roho au daemon mwenye kumlinda aliyekuwapo wakati wa kuzaliwa kwake na kumlinda maishani. Roho huyo alikuwa na uhusiano wa kifumbo pamoja na mungu ambaye mtu huyo alizaliwa katika sikukuu yake ya kuzaliwa. Waroma pia waliunga mkono wazo hilo. . . . Wazo hilo liliendelezwa katika imani ya binadamu na linaonekana katika malaika mlinzi, mama wa ubatizo na mtakatifu mlezi. . . . Desturi ya kuwasha mishumaa juu ya keki ilianzishwa na Wagiriki. . . . Keki za asali za mviringo kama mwezi na zenye kuwashwa kwa mishumaa midogo ziliwekwa juu ya madhabahu za hekalu la [Artemi]. . . . Mishumaa ya sikukuu za kuzaliwa, katika hekaya za watu, ina uwezo wa pekee wa kuwapa watu yale wanayotamani. . . . Mishumaa midogo iliyowashwa na mioto ya dhabihu imekuwa na maana ya pekee ya kifumbo tangu mwanadamu alipoisimamishia miungu yake madhabahu mara ya kwanza. Kwa hiyo mishumaa ya sikukuu ya kuzaliwa ni heshima na sifa kwa mtoto wa sikukuu hiyo ya kuzaliwa na huleta bahati njema. . . . Salamu za sikukuu ya kuzaliwa na heri njema ni sehemu muhimu ya sikukuu hiyo. . . . Mwanzoni wazo hilo lilianzia katika uchawi. . . . Salamu za sikukuu ya kuzaliwa zinaweza kuleta mema au mabaya kwa sababu mtu huwa karibu zaidi na ulimwengu wa roho katika siku hiyo.”—The Lore of Birthdays (New York, 1952), Ralph na Adelin Linton, uku. 8, 18-20.
Si vibaya familia na marafiki kukusanyika ili kula, kunywa, na kufurahi
Mhu. 3:12, 13: “Hakuna jambo lingine bora kwao kuliko mtu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.”
Ona pia 1 Wakorintho 10:31.
-
-
Siku za MwishoKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Siku za Mwisho
Maana: Biblia hutumia maneno haya “siku za mwisho” kurejezea kipindi cha kumalizia kinachoelekeza kwenye kutekelezwa kwa hukumu iliyowekwa na Mungu. Huo ndio utakaokuwa mwisho wa mfumo wa mambo. Siku za mwisho za mfumo wa Kiyahudi pamoja na ibada yake iliyotegemea hekalu la Yerusalemu zilifika kati ya mwaka wa 33 mpaka 70 W.K. Mambo yaliyotukia wakati huo yanafanana na mambo ambayo yangetimia kwa kiwango kikubwa zaidi ulimwenguni pote wakati ambapo mataifa yote yatakabili kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu. Siku za mwisho za mfumo mbovu wa mambo uliopo, wa ulimwenguni pote, zilianza mwaka wa 1914.
Ni nini kinachoonyesha kwamba leo tunaishi katika “siku za mwisho”?
Biblia inasimulia matukio na hali zinazotofautisha kipindi hiki muhimu. Ile “ishara” ina sehemu nyingi; kwa hiyo lazima utimizo wa sehemu zote za ishara hiyo uonwe waziwazi katika kipindi kimoja. Sehemu mbalimbali za ile ishara zimeandikwa katika Mathayo sura za 24, 25, Marko 13, na Luka 21; kuna maelezo zaidi katika 2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4, na Ufunuo 6:1-8. Tutachunguza sehemu chache zenye kutokeza za ishara hiyo.
“Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme” (Mt. 24:7)
Vita vimeharibu maisha duniani kwa maelfu ya miaka. Kumekuwako na vita kati ya mataifa na ndani ya mataifa. Lakini kuanzia mwaka wa 1914 vita vya kwanza vya ulimwengu vilipiganwa. Hayo hayakuwa mapambano tu kati ya majeshi mawili. Kwa mara ya kwanza, mataifa yote makubwa yalikuwa vitani. Mataifa mazima mazima—kutia ndani raia—yalitayarishwa ili kuunga mkono vita. Imekadiriwa kwamba kufikia mwisho wa vita hivyo asilimia 93 ya idadi ya watu ulimwenguni ilihusika. (Kuhusu umuhimu wa mwaka wa 1914 katika historia, ona ukurasa wa 289, 290.)
Kama ilivyotabiriwa katika Ufunuo 6:4, ‘amani iliondolewa duniani.’ Kwa hiyo, kumeendelea kuwa na misukosuko ulimwenguni tangu mwaka wa 1914. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipiganwa kutoka mwaka wa 1939 hadi 1945. Kulingana na Admeri mstaafu, Gene La Rocque, kufikia mwaka wa 1982 vita vingine 270 vilikuwa vimepiganwa tangu mwaka wa 1945. Watu zaidi ya milioni 100 wameuawa vitani katika karne ya 20. Pia, kulingana na chapa ya 1982 ya World Military and Social Expenditures, mwaka huo watu milioni 100 walishiriki katika mambo ya kijeshi moja kwa moja au kwa njia nyingine.
Je, kuna mambo zaidi yanayohitajiwa ili kutimiza sehemu hii ya unabii? Kuna makumi ya maelfu ya silaha za nyukilia zilizo tayari kutumiwa. Wanasayansi mashuhuri wamesema kwamba ikiwa mataifa yangetumia hata kisehemu kidogo cha zana zao za nyukilia, ustaarabu na hata jamii nzima za wanadamu zingeharibiwa. Lakini unabii wa Biblia hausemi kwamba mambo yatakuwa hivyo.
“Kutakuwa na upungufu wa chakula . . . mahali pamoja baada ya pengine” (Mt. 24:7)
Kumekuwa na visa vingi vya njaa katika historia ya mwanadamu. Karne ya 20 imekumbwa na njaa kadiri gani? Vita vya ulimwengu vilisababisha njaa kila mahali barani Ulaya na Asia. Afrika imekumbwa na ukame, ambao umetokeza upungufu mkubwa wa chakula. Mwishoni mwa mwaka wa 1980, Shirika la Chakula na Kilimo lilikadiria kwamba watu milioni 450 walikuwa na njaa kiasi cha kufa, na watu wapatao bilioni moja hawakuwa na chakula cha kutosha. Kati ya hao, watu wapatao milioni 40 kwa kweli wanakufa kila mwaka—miaka fulani hesabu hiyo hufikia milioni 50—kwa sababu ya upungufu wa chakula.
Je, upungufu huu wa chakula ni wa pekee? Andiko la Ufunuo 6:6 lilionyesha kwamba kiasi kidogo cha vyakula vya msingi kama vile ngano au shayiri kingekuwa kikiuzwa kwa mshahara wa siku moja (dinari; ona Mathayo 20:2) lakini akiba za bidhaa kama vile mafuta ya mizeituni na divai zinazotumiwa na watu walio matajiri hazingeharibiwa. Kwa hiyo, inaonekana kwamba watu wengi wangepungukiwa huku wengine wakipata wanachotaka. Hali hiyo haipatikani sehemu moja tu, bali ndivyo ilivyo duniani pote. Mwaka wa 1981 gazeti The New York Times lilisema hivi: “Maendeleo katika viwango vya maisha na mahitaji yanayoongezeka ya chakula katika sehemu zote za ulimwengu yamefanya bei za chakula ziongezeke, na kufanya iwe vigumu zaidi kwa nchi maskini zaidi kuagiza chakula wanachohitaji kutoka katika nchi nyingine.” Katika nchi nyingi chakula kinachokuzwa, hata kwa msaada wa sayansi ya kisasa, hakiwezi kulingana na ongezeko la watu. Wataalamu wa kisasa wa chakula hawaoni utatuzi halisi wa tatizo hilo.
“Kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi” (Luka 21:11)
Ni kweli kwamba kulikuwako matetemeko makubwa katika karne zilizopita; zaidi ya hayo, wanasayansi sasa wanagundua matetemeko zaidi ya milioni moja kwa mwaka kwa kutumia vifaa vyao ambavyo vinapima kwa wepesi. Lakini watu hawahitaji vyombo vya pekee ili kujua kwamba kuna tetemeko kubwa la nchi.
Je, kweli kumekuwapo na matetemeko mengi makubwa ya nchi tangu mwaka wa 1914? Kwa kutumia habari zilizopatikana kutoka National Geophysical Data Center huko Boulder, Colorado, pamoja na vitabu kadhaa vya marejeo, hesabu ilifanywa mwaka wa 1984 iliyotia ndani matetemeko ya nchi yaliyokuwa na vipimo vya angalau 7.5 au zaidi katika kipimo cha Richter, au yaliyosababisha uharibifu wa dola milioni tano (za Marekani) au zaidi katika mali, au ambapo watu 100 au zaidi walikufa. Ilikadiriwa kwamba kwa muda wa miaka 2000 kabla ya mwaka wa 1914 matetemeko 856 ya nchi kama hayo yalikuwa yametokea. Kadirio hilohilo lilionyesha kwamba katika miaka 69 tu baada ya 1914 kulikuwako matetemeko 605 kama hayo. Hilo lamaanisha kwamba, kwa kulinganishwa na miaka 2,000 iliyotangulia, wastani wa kila mwaka umekuwa mara 20 zaidi tangu mwaka wa 1914.
“Katika mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni” (Luka 21:11)
Mwishoni mwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu homa ya Kihispania ilienea duniani pote, na kuua zaidi ya watu milioni 20 na kwa kiwango kisicho na kifani katika historia ya magonjwa. Ijapokuwa kumekuwa na maendeleo katika sayansi ya tiba, kila mwaka vifo vingi husababishwa na kansa, ugonjwa wa moyo, magonjwa mengi ya zinaa, UKIMWI, mkacho, malaria, upofu unaosababishwa na usubi, na ugonjwa wa Chagas.
‘Kuongezeka kwa uasi-sheria pamoja na upendo wa walio wengi zaidi kupoa’ (Mt. 24:11, 12)
Mtaalamu wa elimu ya jinai asema hivi: “Jambo la ajabu kuhusu uhalifu ulimwenguni ni kwamba unaenea na kuongezeka kila mahali. Ni sehemu chache sana zisizo na uhalifu, na huenda hivi karibuni zikakumbwa na wimbi la uhalifu.” (The Growth of Crime, New York, 1977, Sir Leon Radzinowicz na Joan King, uku. 4, 5) Ongezeko hilo ni halisi; si kwamba tu habari zinaripotiwa vizuri zaidi. Ni kweli kwamba vizazi vilivyopita vilikuwa na wahalifu pia, lakini uhalifu wa leo hauna kifani. Watu wenye umri mkubwa wamejionea wenyewe jambo hilo.
Uasi-sheria unaotajwa katika unabii huo unatia ndani kupuuza sheria za Mungu, kujitanguliza maishani badala ya kumtanguliza Mungu. Kwa sababu ya mtazamo huo, talaka zinaongezeka, ngono nje ya ndoa na ngono kati ya watu wa jinsia moja zinakubaliwa, na makumi ya mamilioni ya mimba zinatolewa kila mwaka. Uasi-sheria (katika Mathayo 24:11, 12) unahusianishwa na uvutano wa manabii wa uwongo, wale wanaopuuza Neno la Mungu na kufuata mafundisho yao wenyewe. Kufuata falsafa zao badala ya kushikamana na Biblia huchangia ukosefu wa upendo ulimwenguni. (1 Yoh. 4:8) Soma maelezo hayo katika 2 Timotheo 3:1-5.
“Kutakuwa na mambo yenye kuogopesha” (Luka 21:11)
“Leo maisha yetu yanatawaliwa na woga,” likasema jarida U.S. News & World Report. (Oktoba 11, 1965, uku. 144) “Wanadamu hawajawahi kuwa waoga kama walivyo leo,” likasema gazeti la Kijerumani Hörzu.—Na. 25, Juni 20, 1980, uku. 22.
Woga huo husababishwa na mambo mengi: uhalifu wa kijeuri, ukosefu wa kazi ya kuajiriwa, kuyumba-yumba kwa uchumi kwa sababu mataifa mengi yana madeni makubwa, kuchafuliwa kwa mazingira ulimwenguni pote, ukosefu wa upendo katika familia, na kuhisi kwamba wanadamu wamo katika hatari ya kuangamizwa na nyukilia.
‘Wafuasi wa kweli wa Kristo watachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina lake’ (Mt. 24:9)
Hawateswi kwa sababu ya kujiingiza katika siasa bali ‘kwa sababu ya jina la Yesu Kristo,’ kwa sababu wafuasi wake hushikamana naye akiwa Masihi Mfalme wa Yehova, kwa sababu wanamtii Kristo badala ya kumtii mtawala yeyote duniani, kwa sababu wanashikamana kwa uaminifu na Ufalme wake nao hawajiingizi katika mambo ya serikali za wanadamu. Kama historia inavyoonyesha leo, hayo ndiyo mambo ambayo yamewapata Mashahidi wa Yehova duniani pote.
‘Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi’ (Mt. 24:14)
Ujumbe ambao ungehubiriwa ni kwamba Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo umeanza kutawala mbinguni, kwamba hivi karibuni utakomesha mfumo wote mbovu wa mambo, kwamba chini ya utawala wake wanadamu watafanywa kuwa wakamilifu na dunia itakuwa paradiso. Habari njema hizo zinahubiriwa leo katika nchi na visiwa zaidi ya 200, mpaka sehemu za mbali zaidi za dunia. Mashahidi wa Yehova hutumia mamia ya mamilioni ya saa katika utendaji huo kila mwaka, wakihubiri nyumba kwa nyumba ili watu wengi iwezekanavyo wapate nafasi ya kusikia.
Matukio yote hayo ya “siku za mwisho” yanaelekeza wapi?
Luka 21:31, 32: “Mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu [yaani, wakati ambapo ufalme huo utaharibu ulimwengu mbovu na kuanza kuongoza mambo ya dunia]. Kwa kweli nawaambia ninyi, Kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo yote yatukie.” (Ishara hiyo imekuwa ikitimia tangu mwaka wa 1914. Kwa hiyo, wakati unaobaki ni lazima uwe mfupi sana. Hali za ulimwengu zinaonyesha waziwazi kwamba hivyo ndivyo ilivyo.)
Kwa nini Mashahidi wa Yehova husema kwamba “siku za mwisho” zilianza mwaka wa 1914?
Mwaka wa 1914 umetiwa alama na unabii wa Biblia. Kuhusu orodha ya matukio, ona ukurasa wa 397-399, chini ya kichwa “Vipindi vya Wakati.” Usahihi wa tarehe hiyo umethibitika kwa kuwa hali za ulimwengu zilizotabiriwa zingetokea wakati huo zimetimia tangu mwaka wa 1914 kama ilivyotabiriwa. Mambo yaliyotajwa juu yanaonyesha hivyo.
Wanahistoria wanauonaje mwaka wa 1914?
“Tukitazama jinsi mambo yalivyokuwa, tunaona waziwazi leo kwamba kutokea kwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kuliingiza karne ya 20 katika wakati ambao mwanahistoria Mwingereza, Arnold Toynbee, aliuita ‘Wakati wa Taabu Nyingi.’ Tangu hapo ustaarabu wetu haujarudia tena hali nzuri. Misukosuko yote ya nusu karne kufikia sasa ilianzia mwaka wa 1914 moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja.”—The Fall of the Dynasties: The Collapse of the Old Order (New York, 1963), Edmond Taylor, uku. 16.
-