-
DhambiKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Mwa. 1:27: “Mungu akamuumba mtu [Adamu] kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba.” (Kwa hiyo, jambo ambalo ni sawa kwa Adamu lilikuwa kuonyesha sifa takatifu za Mungu, kukubali na kuthamini mwelekezo wa Mungu. Kukosa kufanya hivyo kulikuwa ni kukosa kuifikia alama, kufanya dhambi. Ona Waroma 3:23, pia 1 Petro 1:14-16.)
Efe. 2:1-3: “Ninyi [Wakristo] ndio ambao Mungu alifanya kuwa hai ingawa mlikuwa wafu katika makosa na dhambi zenu, ambazo wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii. Ndiyo, wakati fulani sisi sote tulijiendesha katikati yao kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanayopendwa na mwili na fikira, nasi kiasili tulikuwa watoto wa ghadhabu sawa na wale wengine.” (Tukiwa wazao wa Adamu mtenda-dhambi, sisi tulizaliwa katika dhambi. Tangu kuzaliwa, moyo wetu una mwelekeo wa kutenda mabaya. Tusipozuia maelekeo hayo mabaya, huenda mwishowe tukaizoea njia hiyo ya maisha. Huenda hata ikaonekana kuwa “jambo la kawaida” kwa sababu wengine walio karibu nasi wanafanya mambo hayo. Lakini Biblia inatambulisha yaliyo mema na yaliyo mabaya kwa maoni ya Mungu, kwa sababu ya jinsi alivyomfanya mwanadamu na kusudi lake kwa wanadamu. Tukimsikiliza Muumba wetu na kumtii kwa upendo, maisha yatakuwa yenye maana sana kwa kadiri tusivyopata kujua, nasi tutakuwa na wakati ujao wa milele. Muumba wetu anatukaribisha kwa uchangamfu tuonje ili tuone jinsi maisha hayo yalivyo mazuri.—Zab. 34:8.)
Dhambi ina matokeo gani juu ya uhusiano wa mtu na Mungu?
1 Yoh. 3:4, 8: “Kila mtu aliye na mazoea ya kufanya dhambi anazoea pia kufanya uasi-sheria, na kwa hiyo dhambi ni uasi-sheria. Yeye ambaye huendelea kufanya dhambi hutokana na Ibilisi.” (Jambo hilo ni zito kama nini! Wale wanaochagua kimakusudi maisha ya dhambi, wakizoea kuitenda, Mungu anawaona kuwa wahalifu. Njia ambayo wamechagua ndiyo ile ambayo Shetani mwenyewe alichagua pale mwanzoni.)
Rom. 5:8, 10: “Tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu. . . . Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake.” (Ona kwamba watenda-dhambi wanaitwa adui za Mungu. Basi, ni jambo la hekima kama nini kujifaidi wenyewe na uandalizi ambao Mungu amefanya ili tupatanishwe naye!)
1 Tim. 1:13: “Nilionyeshwa rehema [asema mtume Paulo], kwa sababu nilikosa ujuzi nami nilitenda kwa ukosefu wa imani.” (Lakini Bwana alipomwonyesha njia iliyo sawa, hakukataa kuifuata.)
2 Kor. 6:1, 2: “Tukifanya kazi pamoja naye, tunawasihi ninyi pia msipokee fadhili zisizostahiliwa za Mungu kisha mkose kusudi lake. Kwa maana anasema: ‘Katika wakati unaokubalika nilikusikia, na katika siku ya wokovu nilikusaidia.’ Tazama! Sasa ndio wakati unaokubalika hasa. Tazama! Sasa ndiyo siku ya wokovu.” (Sasa ndio wakati ambapo nafasi ya wokovu inapatikana. Mungu hatawaonyesha milele wanadamu wenye dhambi fadhili hizo zisizostahiliwa. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusikose kusudi la fadhili hizo.)
Dhambi inaweza kuondolewaje?
Ona kichwa, “Fidia.”
-
-
DiniKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Dini
Maana: Namna ya ibada. Inatia ndani maoni ya kidini, imani, na mazoea; hayo huenda yakawa ya kibinafsi, au yakaungwa mkono na tengenezo fulani. Kwa kawaida dini inatia ndani imani katika Mungu au katika miungu kadhaa; au huona wanadamu, vitu, tamaa, au nguvu fulani kuwa vitu vya kuabudiwa. Dini nyingi zinategemea uchunguzi wa wanadamu juu ya mambo ya asili; pia kuna dini iliyofunuliwa. Kuna dini ya kweli na ya uwongo.
Kwa nini kuna dini nyingi sana?
Kadirio lililofanywa karibuni lilionyesha kwamba kuna dini kubwa 10 na madhehebu 10,000. Kati ya hizo, 6,000 ziko Afrika, 1,200 ziko Marekani, na mamia katika nchi nyingine.
Mambo mengi yamesababisha kuongezeka kwa vikundi vipya vya kidini. Wengine wamesema kwamba dini hizo zote ni njia mbalimbali za kutoa kweli ya kidini. Lakini unapolinganisha mafundisho na mazoea yake pamoja na Biblia utaona kwamba kuna dini nyingi kwa sababu watu wanawafuata wanadamu badala ya kumsikiliza Mungu. Inafaa kuangaliwa kwamba, kwa kadiri kubwa, mafundisho ambayo wote wanashikilia, lakini yanayotofautiana na Biblia, yalianzia Babiloni la kale. (Ona ukurasa wa 28-30, chini ya kichwa “Babiloni Mkubwa.”)
-