Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uhai
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Je, kuna uhai katika sayari nyingine?

      Gazeti The New York Times linasema hivi: “Kutafutwa kwa viumbe vyenye akili kwingineko ulimwenguni . . . kulianza miaka 25 iliyopita . . . Kazi hiyo kubwa mno inayohusisha kuchunguza mamia ya mabilioni ya nyota, kufikia sasa haijatoa uthibitisho ulio wazi kwamba kuna uhai nje ya Dunia.”—Julai 2, 1984, uku. A1.

      The Encyclopedia Americana yasema: “Hakuna sayari nyingine [nje ya mfumo wetu wa jua] ambazo zimeonekana waziwazi. Lakini kwa kila sayari ambayo huenda iko nje ya mfumo wa jua, kuna uwezekano wa kwamba uhai ulianza, kisha ukageuka na kuingia katika ustaarabu ulioendelea.” (1977, Buku la 22, uku. 176) (Tangu wakati huo, sayari nyingi zimegunduliwa nje ya mfumo wetu wa jua, lakini hakuna uthibitisho wowote wa kwamba kuna uhai katika yoyote ya sayari hizo. Hata hivyo, kama maneno hayo yanavyoonyesha, je, inawezekana kwamba sababu kubwa ya kazi hiyo yenye gharama kubwa sana ya kutafuta viumbe vingine katika anga la juu ni ile tamaa ya kupata uthibitisho wa nadharia ya mageuzi, uthibitisho fulani wa kwamba mwanadamu hakuumbwa na Mungu na kwa hiyo hawezi kutozwa hesabu na Yeye?)

      Biblia inafunua kwamba uhai hauko katika dunia hii peke yake. Kuna watu wa roho—Mungu na malaika—ambao akili na uwezo wao unapita wa mwanadamu kwa mbali sana. Tayari wamewasiliana na wanadamu, wakieleza asili ya uhai na utatuzi wa matatizo mazito yanayoukabili ulimwengu. (Ona vichwa “Biblia” na “Mungu.”)

  • Uhuru
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Uhuru

      Maana: Hali ya kutowategemea wengine, kutotii mwelekezo wao au uvutano wao. Kwa kuwa wana uhuru wa kuchagua, kiasili wanadamu hutamani kuwa na kadiri fulani ya uhuru. Hata hivyo, inapopita kiasi, tamaa hiyo inaweza kutokeza kutotii, au hata uasi.

      Watu wanapopuuza viwango vya Biblia, je, kwa kweli wanapata uhuru?

      Rom. 6:16, 23: “Je, hamjui kwamba ikiwa mnaendelea kujitoa wenyewe kwa yeyote kuwa watumwa ili kumtii yeye, ninyi ni watumwa wake kwa sababu mnamtii yeye, ama watumwa wa dhambi kwa kutazamia kifo ama wa utii kwa kutazamia uadilifu? . . . Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”

      Gal. 6:7-9: “Msipotoshwe: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia; kwa sababu yeye anayepanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake, lakini yeye anayepanda kwa roho atavuna uzima wa milele kutokana na roho. Kwa hiyo na tusife moyo katika kufanya yaliyo mema.”

      Maadili kuhusu ngono: “Yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Kor. 6:18) “Yeyote anayefanya uzinzi na mwanamke . . . anaiangamiza nafsi yake mwenyewe.” (Met. 6:32) (Kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja, ona Waroma 1:24-27.) (Huenda ngono haramu, zikaonekana kuwa zenye kufurahisha kwa wakati huo. Lakini hutokeza magonjwa mabaya, mimba isiyotakiwa, utoaji-mimba, wivu, dhamiri mbaya, maumivu ya moyoni, na bila shaka kukosa kibali cha Mungu, ambaye anatupa tumaini la kuishi wakati ujao.)

      Kutafuta mali: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu. Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:9, 10) “Nitaiambia nafsi yangu: ‘Nafsi yangu, una vitu vyema vingi vilivyokusanywa kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na kujifurahisha.’ Lakini Mungu akamwambia, ‘Wewe usiye na akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Basi, vitu ulivyoviweka akiba vitakuwa vya nani?’ Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.” (Luka 12:19-21) (Mali za kimwili hazileti furaha ya kudumu. Jitihada za kutafuta mali mara nyingi hutokeza familia zisizo na furaha, afya mbaya, hali mbaya ya kiroho.)

      Kunywa pombe kupita kiasi: “Ni nani aliye na ole? Ni nani aliye na wasiwasi? Ni nani aliye na ugomvi? Ni nani aliye na mahangaiko? Ni nani aliye na majeraha yasiyo na sababu? Ni nani aliye na macho mazito? Ni wale wanaokaa muda mrefu kwenye divai, wale wanaoenda kutafuta divai iliyochanganyika. Mwisho wake inauma kama nyoka, nayo hutoa sumu kama nyoka.” (Met. 23:29, 30, 32) (Mwanzoni, huenda ikaonekana kwamba kunywa pombe kunamsaidia mtu asahau matatizo yake, lakini hakuyatatui. Mtu anapotokwa na ulevi, bado matatizo yanamngojea, mara nyingi mengine huwa yameongezeka. Mtu anapokunywa kupita kiasi, pombe humfanya akose kujiheshimu, inaharibu afya yake, maisha yake ya familia, uhusiano wake pamoja na Mungu.)

      Dawa za Kulevya: Ona ukurasa wa 48-54, chini ya kichwa “Dawa za Kulevya.”

      Mashirika mabaya: Ikiwa watu fulani wangekuambia kwamba wanajua jinsi ya kupata pesa nyingi bila kufanya kazi nyingi, je, ungeenda pamoja nao? “Usiende njiani pamoja nao. Zuia mguu wako usiende katika barabara yao. Maana miguu yao hukimbilia ubaya mtupu, nao huharakisha kwenda kumwaga damu.” (Met. 1:10-19) Ikiwa mtu si mwabudu wa Yehova, lakini anaonekana kuwa mzuri kweli kweli, je, ungemwona kuwa rafiki anayefaa? Shekemu alikuwa mwana wa mkuu wa nchi ya Kanaani, na Biblia husema kwamba alikuwa “mwenye kuheshimika zaidi katika nyumba nzima ya baba yake,” lakini “akamchukua [Dina], akalala naye, akamnajisi.” (Mwa. 34:1, 2, 19) Kwa kuwa huenda watu wengine wasiamini kweli ambazo umejifunza kutoka katika Neno la Mungu, unapaswa kuwa na maoni gani kuwaelekea? “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Kor. 15:33) Yehova angeonaje ikiwa ungewachagua watu wasiompenda wawe rafiki zako? Msemaji wa Yehova alimwambia hivi mfalme wa Yuda aliyefanya hivyo: “Kwa sababu hiyo kuna ghadhabu juu yako inayotoka mbele za uso wa Yehova.”—2 Nya. 19:1, 2.

      Ni nani aliyewachochea wanadamu watumie uhuru wao kujiamulia wenyewe bila kujali amri za Mungu?

      Mwa. 3:1-5: “Basi nyoka [akitumiwa kuwa msemaji wa Shetani; Ona Ufunuo 12:9] . . . akaanza kumwambia mwanamke: ‘Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?’ Mwanamke akamjibu na kumwambia nyoka: ‘Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani. Lakini kuhusu kula matunda ya mti ulio katikati ya bustani, Mungu amesema, “Msiyale, wala msiyaguse ili msife.”’ Ndipo nyoka akamwambia mwanamke: ‘Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.’”

      Ni roho gani inayomchochea mtu anapopuuza mapenzi ya Mungu ili atosheleze tamaa zake binafsi?

      Efe. 2:1-3: “Ninyi ndio ambao Mungu alifanya kuwa hai ingawa mlikuwa wafu katika makosa na dhambi zenu, ambazo wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu [ambao Shetani ndiye mtawala wake], kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii. Ndiyo, wakati fulani sisi sote tulijiendesha katikati yao kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanayopendwa na mwili na fikira, nasi kiasili tulikuwa watoto wa ghadhabu sawa na wale wengine.”

      Ni mitazamo gani ya kutaka kuwa huru ambayo wale wanaodai kwamba wanamtumikia Mungu ni lazima waepuke?

      Met. 16:18: “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.”

      Met. 5:12: “Nawe utalazimika kusema: ‘Nimechukia nidhamu kama nini nao moyo wangu umedharau karipio kama nini!’” (Mtazamo huo unaweza kumwongoza mtu katika matatizo mazito, kama muktadha unavyoonyesha.)

      Hes. 16:3: “Basi wakakutana dhidi ya Musa na Haruni [ambao Yehova alikuwa akiwatumia wakiwa waangalizi kati ya watu wake] na kuwaambia: ‘Imetosha, kwa sababu kusanyiko lote, wote hao ni watakatifu na Yehova yuko katikati yao. Kwa nini, basi, mjiinue wenyewe juu ya kutaniko la Yehova?’”

      Yuda 16: “Watu hawa ni wanung’unikaji, walalamikaji juu ya fungu lao maishani, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe, na vinywa vyao husema mambo ya kujigamba, huku wakisifu kwa kustaajabia watu mashuhuri kwa ajili ya faida yao wenyewe.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki