-
UhuruKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
3 Yoh. 9: “Diotrefe, anayependa kuwa na mahali pa kwanza katikati yao, hapokei kwa heshima jambo lolote kutoka kwetu.”
Met. 18:1: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.”
Yak. 4:13-15: “Haya, basi, ninyi ambao husema: ‘Leo au kesho tutasafiri kwenda jiji fulani nasi tutakaa mwaka mmoja huko, tutafanya biashara na kupata faida,’ ingawa hamjui uzima wenu utakuwa namna gani kesho. Kwa maana ninyi ni ukungu unaotokea kwa muda kidogo na kisha kutoweka. Badala yake, mnapaswa kusema: ‘Yehova akipenda, tutaishi na pia kufanya hili au lile.’”
Mtu huongozwa na nani wakati tamaa yake ya kuwa na uhuru inapomfanya aige mambo ya ulimwengu nje ya kutaniko la Kikristo? Na Mungu anaonaje jambo hilo?
1 Yoh. 2:15; 5:19: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake.” “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”
Yak. 4:4: “Yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.”
-
-
Ukumbusho (Mlo wa Jioni wa Bwana)Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Ukumbusho (Mlo wa Jioni wa Bwana)
Maana: Mlo wa kukumbuka kifo cha Yesu Kristo; kwa hiyo, huo ni ukumbusho wa kifo chake, kifo ambacho kimekuwa na matokeo makubwa kuliko kile cha mtu mwingine yeyote. Hili ndilo tukio pekee ambalo Bwana Yesu Kristo aliwaamuru wanafunzi wake walifanyie ukumbusho. Pia unaitwa Mlo wa Jioni wa Bwana.—1 Kor. 11:20.
Ukumbusho una umuhimu gani?
Yesu aliwaambia hivi mitume wake waaminifu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Alipokuwa akiwaandikia washiriki wa kutaniko la Kikristo lililozaliwa kwa roho, mtume Paulo aliongeza hivi: “Kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapofika.” (1 Wakorintho 11:26) Kwa hiyo, Ukumbusho unakazia kwa njia ya pekee umuhimu wa kifo cha Yesu Kristo katika kutimiza kusudi la Yehova. Unakazia maana ya kifo cha kidhabihu cha Yesu hasa kuhusiana na agano jipya na matokeo ya kifo chake kwa wale watakaokuwa warithi pamoja naye wa Ufalme wa mbinguni.—Yoh. 14:2, 3; Ebr. 9:15.
Ukumbusho pia unatukumbusha kwamba kifo cha Yesu na jinsi kilivyotimizwa, kupatana na kusudi la Mungu kama lilivyoandikwa katika Mwanzo 3:15 na baadaye katika maandiko mengine, kilitumika kulitetea jina la Yehova. Kwa kudumisha utimilifu kwa Yehova mpaka kifo chake, Yesu alithibitisha kwamba dhambi ya Adamu haikuwa kwa sababu ya kasoro yoyote katika njia ambayo Muumba alimuumba mwanadamu bali kwamba inawezekana kwa mwanadamu kudumisha ujitoaji-kimungu mkamilifu hata akiwa chini ya mkazo mkali. Kwa njia hiyo, Yesu alimtetea Yehova Mungu akiwa Muumba na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu. Zaidi ya hayo, Yehova alikuwa amekusudia kwamba kifo cha Yesu kiandae dhabihu kamilifu ya kibinadamu inayohitajiwa ili kuwafidi watoto wa Adamu, na hivyo kuwawezesha mabilioni ya watu walio na imani waishi milele katika dunia paradiso, na hivyo kutimiza kusudi la kwanza la Yehova na kuonyesha upendo wake mkubwa kwa ajili ya wanadamu.—Yoh. 3:16; Mwa. 1:28.
Yesu alikuwa na mzigo mzito kama nini usiku ule wa mwisho duniani akiwa mwanadamu! Alijua jambo ambalo Baba yake wa mbinguni alikuwa amekusudia kwa ajili yake, lakini alijua pia kwamba alipaswa kujithibitisha kuwa mwaminifu chini ya jaribu. Ikiwa angeshindwa, hiyo ingekuwa shutuma kubwa kwa Baba yake na hasara kwa wanadamu! Kwa sababu ya yote ambayo yangetimizwa kupitia kifo chake, inafaa sana kwamba Yesu aliagiza kikumbukwe.
Mkate na divai vinavyotumiwa kwenye Ukumbusho vinamaanisha nini?
Yesu alisema hivi kuhusu mkate usio na chachu ambao aliwapa mitume wake alipoanzisha Ukumbusho: “Huu unamaanisha mwili wangu.” (Marko 14:22) Mkate huo ulikuwa mfano wa mwili wake mwenyewe wenye nyama usio na dhambi. Huo ungetolewa kwa ajili ya matarajio ya uzima wa wakati ujao wa wanadamu, na katika pindi hii uangalifu wa pekee unaelekezwa kwenye matarajio ya uzima ambao kinafanya yawezekane kwa wale ambao wangechaguliwa kushiriki pamoja na Yesu katika Ufalme wa mbinguni.
Alipokuwa akipitisha divai kwa mitume wake waaminifu, Yesu alisema: “Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi.” (Marko 14:24) Divai hiyo ilikuwa mfano wa damu yake mwenyewe ya uzima. Kupitia damu yake iliyomwagwa, wale wanaoiamini watasamehewa dhambi. Katika pindi hii Yesu alikuwa akikazia kutakaswa dhambi ambako damu hiyo ingefanya kuwezekane kwa ajili ya wale wanaotarajia kuwa warithi pamoja naye. Maneno yake yanaonyesha pia kwamba kupitia damu hiyo lile agano jipya, kati ya Yehova Mungu na kutaniko la Kikristo lililotiwa mafuta kwa roho, lingeanza kutenda kazi.
Ona pia ukurasa wa 205-207, chini ya kichwa “Misa.”
Ni nani wanaopaswa kula mkate na kunywa divai?
Ni nani waliokula wakati Yesu alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana muda mfupi kabla ya kufa? Ni wale wafuasi kumi na mmoja waaminifu ambao Yesu aliwaambia: “Ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:29) Hao wote walikuwa watu waliokuwa wakialikwa washiriki pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni. (Yoh. 14:2, 3) Wote wanaokula mkate na kunywa divai leo wanapaswa pia kuwa watu ambao Kristo anaingiza katika lile ‘agano kwa ajili ya ufalme.’
Ni wangapi wanaokula? Yesu alisema kwamba ni “kundi dogo” tu ndio wangepewa thawabu ya Ufalme wa mbinguni. (Luka 12:32) Hesabu kamili ni 144,000. (Ufunuo 14:1-3) Kikundi hicho kilianza kuchaguliwa mwaka wa 33 W.K. Basi, kupatana na akili, kungekuwa na hesabu ndogo tu ya wenye kula sasa.
Je, andiko la Yohana 6:53, 54 linaonyesha kwamba ni wale tu wanaokula na kunywa ndio watakaopata uzima wa milele?
Yohana 6:53, 54: “Yesu akawaambia: ‘Kwa kweli kabisa ninawaambia, Ninyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu wenyewe. Yule ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele, nami nitamfufua katika siku ya mwisho.’”
-