-
Ukumbusho (Mlo wa Jioni wa Bwana)Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Yohana 6:53, 54: “Yesu akawaambia: ‘Kwa kweli kabisa ninawaambia, Ninyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu wenyewe. Yule ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele, nami nitamfufua katika siku ya mwisho.’”
Kwa wazi basi, tendo hilo la kula na kunywa linapasa kufanywa kwa njia ya mfano; kama sivyo yule anayetenda hivyo atakuwa akiivunja sheria ya Mungu. (Mwa. 9:4; Mdo. 15:28, 29) Hata hivyo, inafaa kukumbuka kwamba maneno ya Yesu katika Yohana 6:53, 54, hayakusemwa kuhusiana na kuanzishwa kwa Mlo wa Jioni wa Bwana. Kati ya wote waliomsikiliza, hakuna aliyekuwa na wazo lolote kuhusu sherehe ya mkate na divai iliyotumiwa kuwakilisha nyama na damu ya Kristo. Mpango huo haukuanzishwa mpaka mwaka mmoja hivi baadaye, na habari za mtume Yohana kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana hazianzi mpaka baada ya zaidi ya sura saba (katika Yohana 14) katika Injili yenye jina lake.
Basi, mtu anawezaje ‘kuula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake’ kwa njia ya mfano ikiwa si kwa kula mkate na kunywa divai kwenye Ukumbusho? Kumbuka Yesu alisema kwamba wale wanaokula na kunywa kwa njia hiyo watakuwa na “uzima wa milele.” Katika mstari wa 40, alipokuwa akieleza jambo ambalo ni lazima watu wafanye ili wapate uzima wa milele, alisema mapenzi ya Baba yake ni nini? Kwamba “kila mtu ambaye humtazama Mwana na kumwamini awe na uzima wa milele.” Kupatana na akili, basi, mtu ‘huula mwili wake na kunywa damu yake’ katika njia ya mfano kwa kuwa na imani katika nguvu zenye kukomboa za mwili na damu ya Yesu vilivyotolewa katika dhabihu. Wote ambao watapata uzima kamili, iwe mbinguni pamoja na Kristo au katika Paradiso duniani, wanahitaji kuwa na imani.
Ukumbusho unapaswa kusherehekewa mara ngapi na wakati gani?
Yesu hakusema waziwazi ulipaswa kusherehekewa mara ngapi. Alisema tu: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Paulo alisema: “Kwa maana kila mara mnapokula mkate huu na kunywa kikombe hiki, mnaendelea kukitangaza kifo cha Bwana, mpaka atakapofika.” (1 Kor. 11:26) Maneno “kila mara” si lazima yamaanishe mara nyingi kwa mwaka; yanaweza kumaanisha kila mwaka kwa kipindi cha miaka mingi. Ukifanya ukumbusho wa tukio fulani, kama vile siku ya arusi, au taifa likifanya ukumbusho wa tukio muhimu katika historia yake, hilo hufanywa mara ngapi? Mara moja kwa mwaka katika tarehe ya ukumbusho wa tukio hilo. Hayo yanapatana pia na uhakika wa kwamba Mlo wa Jioni wa Bwana ulianzishwa katika tarehe ya Pasaka ya Wayahudi, ambayo ilikuwa sherehe ya kila mwaka ambayo haikuwa tena lazima ishikwe na Wayahudi waliokuwa wamekuwa Wakristo.
Mashahidi wa Yehova huadhimisha Ukumbusho baada ya jua kutua katika Nisani 14, kulingana na kalenda ya Kiyahudi iliyotumiwa na wengi katika karne ya kwanza. Siku ya Wayahudi huanza wakati jua linapotua na huendelea mpaka jua linapotua siku inayofuata. Kwa hiyo, Yesu alikufa siku ileile aliyoanzisha Ukumbusho kwenye kalenda ya Kiyahudi. Mwanzo wa mwezi wa Nisani ni wakati wa kutua kwa jua baada ya mwezi mpya karibu na siku-mlingano wakati wa masika, mwezi ulipoonekana katika Yerusalemu. Tarehe ya Ukumbusho ni siku 14 baada ya hapo. (Kwa hiyo, huenda tarehe ya Ukumbusho ikakosa kulingana na ile ya Pasaka inayoshikwa na Wayahudi wa siku hizi. Kwa nini? Mwanzo wa miezi yao ya kalenda umewekwa ulingane na tarehe ya mwezi mpya ulio angani, si kulingana na kuonekana kwa mwezi mpya Yerusalemu, ambao huenda ukaonekana baada ya saa 18 mpaka 30. Pia, Wayahudi wengi leo hushika Pasaka siku ya Nisani 15, wala si siku ya 14 kama alivyofanya Yesu kulingana na yaliyoandikwa katika Sheria ya Musa.)
-
-
UlimwenguKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Ulimwengu
Maana: Neno “ulimwengu” linapotafsiriwa kutoka neno la Kigiriki koʹsmos, linaweza kumaanisha (1) wanadamu kwa ujumla, bila kutia ndani hali yao ya kiadili au mwendo wao wa maisha, (2) mazingira ambamo mtu huzaliwa na kuishi, au (3) wanadamu ambao Mungu hawakubali kuwa watumishi wake. Watafsiri fulani wa Biblia wametoa mawazo yasiyo sahihi kwa kutumia pia neno “ulimwengu” kuwa neno linalolingana na maneno ya Kigiriki yanayomaanisha “dunia,” “dunia inayokaliwa,” na “mfumo wa mambo.” Mazungumzo yafuatayo yanakazia fikira maana ya tatu kati ya zile maana za “ulimwengu” zilizotangulia kuonyeshwa.
-