-
Shetani IbilisiKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Watu fulani hurejezea andiko la Ufunuo 20:3 (lililonukuliwa hapo juu) ili kuunga mkono wazo hilo. Wao husema kwamba “abiso,” au “shimo pasipo mwisho” (ZSB), huwakilisha dunia ikiwa katika hali ya ukiwa. Je, hiyo ni kweli? Andiko la Ufunuo 12:7-9, 12, (ZSB) huonyesha kwamba wakati fulani kabla ya kutupwa kwake katika abiso, Shetani ‘anatupwa’ kutoka mbinguni kuja duniani, ambako anawaletea wanadamu ole nyingi. Kwa hiyo, wakati andiko la Ufunuo 20:3 (ZSB) linaposema kwamba Shetani ‘anatupwa katika shimo pasipo mwisho,’ hakika haachwi tu mahali alipo tayari—akiwa bila kuonekana lakini akiwa amefungiwa katika ujirani wa dunia. Yeye anaondolewa na kupelekwa mbali kutoka hapo, ili “asipate kudanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie.” Ona kwamba andiko la Ufunuo 20:3 linasema kwamba, mwishoni mwa ile miaka elfu, si mataifa yanayofunguliwa kutoka katika abiso, bali ni Shetani. Shetani atakapofunguliwa, watu ambao hapo zamani walifanyiza mataifa hayo watakuwa tayari wapo.
Nyakati nyingine, andiko la Isaya 24:1-6 na Yeremia 4:23-29 (UV) hutumiwa kuunga mkono imani hiyo. Maandiko hayo yanasema hivi: “Tazama, BWANA ameifanya dunia kuwa tupu, aifanya ukiwa . . . dunia hii itafanywa tupu kabisa, na kuharibiwa kabisa; maana BWANA amenena neno hilo.” “Naliiangalia nchi, na tazama, ilikuwa ukiwa . . . Nikaangalia, na tazama, hapakuwa na mtu hata mmoja . . . Maana BWANA asema hivi, Nchi yote itakuwa ukiwa . . . Kila mji umeachwa, hapana hata mtu mmoja akaaye ndani yake.” Unabii huo unamaanisha nini? Ulitimizwa mara ya kwanza juu ya Yerusalemu na nchi ya Yuda. Katika kutekeleza hukumu yake, Yehova aliwaruhusu Wababiloni waishambulie nchi hiyo. Mwishowe yote iliachwa ukiwa, bila kitu. (Ona Yeremia 36:29.) Lakini Mungu wakati huo hakuwaondoa watu katika dunia yote, wala hatafanya hivyo sasa. (Ona ukurasa wa 69-72, chini ya kichwa “Dunia,” pia kichwa “Mbingu.”) Hata hivyo, ataifanya ukiwa kabisa sehemu ya kisasa inayofananishwa na Yerusalemu lisilo na uaminifu, yaani, Jumuiya ya Wakristo, ambayo kwa mwenendo wake usio mtakatifu inalishutumu jina la Mungu, na sehemu nyingine zote za tengenezo la Shetani linaloonekana.
Badala ya kuwa ukiwa kabisa, wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, na wakati Shetani atakapokuwa katika abiso, dunia yote itakuwa paradiso. (Ona “Paradiso.”)
-
-
SikukuuKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Sikukuu
Maana: Siku ambazo watu hawaendi kazini na shuleni ili kuadhimisha tukio fulani. Huenda siku hizo pia zikawa vipindi vya sherehe za familia au za jamii. Huenda washiriki wakaziona kuwa ni sikukuu za kidini au za kijamii au kilimwengu.
Je, mwadhimisho wa Krismasi unapatana na Biblia?
Tarehe ya mwadhimisho
Cyclopædia ya M’Clintock na Strong inasema: “Mungu hakuagiza Krismasi iadhimishwe, wala mwadhimisho huo hautokani na A[gano] J[ipya]. A[gano] J[ipya] wala chanzo kingine chochote, hakitaji siku ya kuzaliwa kwa Kristo.”—(New York, 1871) Buku la 2, uku. 276.
Luka 2:8-11 huonyesha kwamba wakati wa kuzaliwa kwa Yesu, wachungaji walikuwa nje usiku. Kitabu Daily Life in the Time of Jesus chaeleza: ‘Wakati wa baridi kali, makundi ya wanyama hayakutoka nje; na hilo pekee linaweza kuthibitisha kwamba tarehe ya Krismasi, ya wakati wa baridi kali, haiwezi kuwa sahihi, kwa kuwa Injili husema kwamba wachungaji walikuwa nje.’—(New York, 1962), Henri Daniel-Rops, uku. 228.
The Encyclopedia Americana husema hivi: “Sababu ya kuchagua Desemba 25 kuwa siku ya Krismasi haieleweki waziwazi, lakini inaaminiwa kwamba siku hiyo ilichaguliwa ili ilingane na sherehe za kipagani zilizotukia karibu na wakati ambapo jua huwa mbali zaidi na ikweta, wakati wa baridi kali, siku zinapoanza kurefuka, ili kusherehekea ‘kuzaliwa upya kwa jua.’ . . . Satanalia ya Kiroma (sikukuu ya zohali, mungu wa kilimo, na ya nguvu mpya za jua), pia iliadhimishwa wakati huo, na inaonekana kwamba desturi fulani za Krismasi zilianzia katika mwadhimisho huo wa kale wa kipagani.”—(1977), Buku la 6, uku. 666.
New Catholic Encyclopedia inakubali hivi: “Tarehe ya kuzaliwa kwa Kristo haijulikani. Injili hazitaji siku wala mwezi . . . Kulingana na nadharia iliyotolewa na H. Usener . . . na inayokubaliwa na wasomi wengi leo, kuzaliwa kwa Kristo kulipewa tarehe ambayo jua linakuwa mbali zaidi na ikweta, wakati wa baridi kali, (Desemba 25 katika kalenda ya Julias, Januari 6 katika kalenda ya Misri), kwa sababu siku hiyo, jua lilipoanza kurudi kwenye anga za kaskazini, waabudu wa kipagani wa Mithra walisherehekea dies natalis Solis Invicti (kuzaliwa kwa jua lisiloshindika). Katika Desemba 25, 274, Aurelian alikuwa amemtangaza mungu-jua kuwa mdhamini mkuu wa milki na kumjengea hekalu katika Uwanja wa Martius. Krismasi ilianza wakati madhehebu ya jua yalipositawi nchini Roma.”—(1967), Buku la 3, uku. 656.
Watu wenye hekima, au Mamajusi, walioongozwa na nyota
Mamajusi hao walikuwa wanajimu kutoka mashariki. (Mt. 2:1, 2) Ijapokuwa unajimu unapendwa na watu wengi leo, Biblia inapinga kabisa zoea hilo. (Ona ukurasa wa 175, 176 chini ya kichwa “Majaliwa.”) Je, Mungu angewaelekeza kwa Yesu aliyezaliwa karibuni watu wenye mazoea ambayo Yeye mwenyewe anayashutumu?
-