-
Urithi wa UpapaKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Mt. 26:52, UV: “Ndipo Yesu akamwambia, Rudisha upanga wako mahali pake, maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.”
1 Yoh. 3:10-12, BHN: “Asiyempenda ndugu yake, huyo si mtoto wa Mungu. Hiyo ndiyo tofauti iliyoko kati ya watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi. . . . Tunapaswa kupendana! Tusiwe kama Kaini ambaye, kwa kuongozwa na yule Mwovu, alimwua ndugu yake.”
Kutokana na yaliyotangulia, je, kwa kweli wale wanaodai kuwa warithi wa mitume wamefundisha na kutenda yale ambayo Kristo na mitume wake walitenda?
-
-
UtatuKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Utatu
Maana: Fundisho kuu la dini za Jumuiya ya Wakristo. Kulingana na Imani ya Athanasia, kuna Watu watatu wa kimungu (Baba, Mwana, Roho Mtakatifu), inasemekana kwamba kila mmoja ni wa milele, kila mmoja ni mweza-yote, hakuna aliye mkubwa au mdogo kuliko mwingine, kila mmoja ni Mungu, na hata hivyo wote pamoja ni Mungu mmoja tu. Maelezo mengine kuhusu fundisho hilo hukazia kwamba hao “Watu” watatu si watu mbalimbali bali ni maumbo matatu ambayo Mungu hukaa ndani yake. Kwa hiyo Wana-Utatu fulani hukazia imani yao kwamba Yesu Kristo ni Mungu, au kwamba Yesu na Roho Mtakatifu ni Yehova. Hilo si fundisho la Biblia.
Fundisho la Utatu lilitoka wapi?
The New Encyclopædia Britannica husema: “Neno Utatu, wala fundisho la wazi kama hilo, halipatikani katika Agano Jipya, wala Yesu na wafuasi wake hawakukusudia kupinga ile Shema katika Agano la Kale: ‘Sikiliza, Ee Israeli; BWANA, Mungu wetu, BWANA, ndiye mmoja’ (Kum. 6:4). . . . Fundisho hilo lilisitawi hatua kwa hatua kwa muda wa karne kadhaa na kupitia mabishano mengi. . . . Kufikia mwisho wa karne ya 4 . . . fundisho la Utatu likawa jinsi lilivyo leo hii.”—(1976), Micropædia, Buku la 10, uku. 126.
New Catholic Encyclopedia hueleza hivi: “Maneno ‘Mungu mmoja katika Watu watatu’ hayakuthibitishwa imara, nayo hayakuwa sehemu kamili ya maisha ya Wakristo na imani yao, kabla ya mwisho wa karne ya 4. Lakini ni maneno hayo hasa ambayo yalianza kuitwa kwanza fundisho la Utatu. Kati ya Mababa wa Kimitume, hakukuwa na jambo lolote linalokaribia hata kidogo mawazo au maoni hayo.”—(1967), Buku la 14, uku. 299.
Katika The Encyclopedia Americana tunasoma hivi: “Ukristo ulitokana na dini ya Kiyahudi na dini ya Kiyahudi iliamini kabisa Umoja [waliamini kwamba Mungu ni mtu mmoja tu]. Imani ya Utatu ya karne ya nne haikuonyesha kwa usahihi fundisho la kwanza la Kikristo kuhusu umbo la Mungu; badala ya hivyo, ilikuwa imepotoka kutoka katika fundisho hili.”—(1956), Buku la 27, uku. 294L.
Kulingana na kichapo Nouveau Dictionnaire Universel, “Utatu wa Plato, ambao wenyewe ulikuwa ni kupangwa upya tu kwa miungu mitatu-mitatu ya watu wa zamani, unaonekana kuwa ndio utatu unaopatana na akili ya kifalsafa ya sifa zilizotokeza yale maumbo matatu au watu wa kimungu ambao makanisa ya Kikristo hufundisha. . . . Wazo hili la mwanafalsafa Mgiriki [Plato, karne ya nne K.W.K.] la utatu wa kimungu . . . linapatikana katika dini zote za kale [za kipagani].”—(Paris, 1865-1870), kilichohaririwa na M. Lachâtre, Buku la 2, uku. 1467.
John L. McKenzie, S.J., katika kitabu chake Dictionary of the Bible, anasema: “Utatu wa watu katika umoja wa asili hufafanuliwa katika maneno ya ‘mtu’ na ‘asili’ ambayo ni maneno ya kifalsafa ya Kigiriki; kwa hakika maneno hayo hayapatikani katika Biblia. Mafafanuzi ya utatu yalitokana na mabishano ya muda mrefu ambapo maneno hayo na mengine kama vile ‘asili iliyoko ya vitu vyote’ na ‘asili kuu,’ yalitumiwa kimakosa na wanatheolojia fulani kumhusu Mungu.”—(New York, 1965), uku. 899.
Hata ingawa, kama vile Wana-Utatu wanavyokubali, neno “Utatu” wala fundisho la Utatu halipatikani katika Biblia, je, mawazo yanayotiwa katika fundisho hilo yanapatikana humo?
Je, Biblia hufundisha kwamba “Roho Mtakatifu” ni mtu?
Maandiko fulani yanayotaja roho takatifu (“Roho Mtakatifu,” UV) huenda yakaonekana kumaanisha mtu. Kwa mfano, roho takatifu huitwa msaidizi (Kigiriki, pa·raʹkle·tos; “Mtulizaji,” VB) ambaye ‘hufundisha,’ ‘hutoa ushahidi,’ ‘husema’ na ‘husikia.’ (Yoh. 14:16, 17, 26; 15:26; 16:13) Lakini maandiko mengine husema kwamba watu ‘walijazwa’ roho takatifu, kwamba wengine ‘walibatizwa’ nayo au ‘walipakwa mafuta’ nayo. (Luka 1:41; Mt. 3:11; Mdo. 10:38) Bila shaka maandiko hayo ya mwisho yanayoitaja roho hayawezi kurejelea mtu. Ili kuelewa yale ambayo Biblia hufundisha kwa ujumla, ni lazima maandiko hayo yote yafikiriwe. Ni jambo gani linalopatana na akili? Kwamba maandiko ya kwanza yaliyotajwa hapa yanatumia maneno ya mfano, yanayoifanya roho takatifu ya Mungu au nguvu zake za utendaji, zionekane kuwa kama mtu. Biblia hufanya vivyo hivyo kuhusu maneno kama vile hekima, dhambi, kifo, maji, na damu. (Ona pia ukurasa wa 242, 243, chini ya kichwa “Roho.”)
-