Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Watakatifu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Mtu Akisema—

      ‘Je, unaamini watakatifu?’

      Unaweza kujibu hivi: ‘Unamaanisha watakatifu gani?’ Mtu huyo akimtaja Maria na/au mitume, labda unaweza kuongeza hivi: (1) ‘Ndiyo, wanatajwa katika Maandiko Matakatifu, nami naamini yaliyoandikwa humo. Lakini hasa napendezwa na yale wanayofanya leo na jinsi yanavyotuhusu sisi, na je, wewe? . . . Nimeona jambo fulani lenye kupendeza sana juu yao humu katika Maandiko Matakatifu, nami ningependa nilisome pamoja na wewe. (Ufu. 5:9, 10)’ [Angalia, kwa ajili ya matumizi ikiwa swali linatokezwa kuhusu maneno yanayotumiwa katika andiko hilo: UV husema “wanamiliki juu ya nchi.” ZSB husema “wanatawala juu ya dunia.” VB husema “wataitawala dunia.” Lakini BHN husema “watatawala duniani.” NAJ husema “watatawala ulimwenguni.”] (2) ‘Uzima chini ya serikali hiyo utakuwaje? (Ufu. 21:2-4)’

      Au unaweza kusema (ikiwa wakati fulani wewe ulikuwa Mkatoliki): ‘Kwa miaka mingi nilishiriki katika sikukuu za watakatifu nami nilisali kwao kwa ukawaida. Kisha nikasoma jambo fulani katika Maandiko Matakatifu lililonifanya kufikiria yale niliyokuwa nikifanya. Tafadhali, acha nikuonyeshe jambo hilo. (Ona ukurasa wa 406.)’

  • Wayahudi
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
    • Wayahudi

      Maana: Kama linavyotumiwa na watu wengi leo, neno hili linarejezea watu wenye asili ya Kiebrania na wengine ambao wamegeuzwa imani na kuwa wafuasi wa dini ya Kiyahudi. Pia Biblia inataja kwamba kuna Wakristo walio Wayahudi kiroho ambao wanafanyiza “Israeli wa Mungu.”

      Je, Wayahudi wa asili leo ni watu wa Mungu waliochaguliwa?

      Wayahudi wengi huamini hivyo. Encyclopaedia Judaica (Jerusalem, 1971, Buku la 5, safu ya 498) inasema hivi: “WATU WALIOCHAGULIWA, ni jina la kawaida la watu wa Israeli, linaloonyesha kwamba watu wa Israeli wana uhusiano wa pekee na usio na kifani pamoja na Mungu wa ulimwengu wote. Hilo ni wazo kuu katika historia ya Wayahudi.”—Ona Kumbukumbu la Torati 7:6-8; Kutoka 19:5.

      Watu wengi katika Jumuiya ya Wakristo huamini vivyo hivyo. Sehemu ya jarida Journal and Constitution la Atlanta (Januari 22, 1983, uku. 5-B) yenye kichwa “Dini” ilisema hivi: “Tofauti na mafundisho ya karne nyingi ya kanisa kwamba Mungu alikuwa ‘amewatupilia mbali watu wake Israeli’ na badala yao akaweka ‘Israeli mpya,’ yeye [Paul M. Van Buren, mwanatheolojia kwenye Chuo Kikuu cha Temple huko Philadelphia] anasema sasa makanisa yanathibitisha kwamba ‘lile agano kati ya Mungu na Wayahudi ni la milele. Badiliko hilo la ajabu limefanywa na Waprotestanti na Wakatoliki, pande zote mbili za Atlantiki.’” The New York Times (Februari 6, 1983, uku. 42) liliongeza hivi: “‘Wainjilisti wa mrengo wa kulia wanavutiwa sana na Waisraeli, nao huamini kwamba kila jambo ambalo Waisraeli hufanya lazima liungwe mkono, kwa sababu Mungu yuko upande wa Israeli,’ akasema Timothy Smith, profesa wa theolojia kwenye Chuo Kikuu cha Johns Hopkins ambaye pia ni mwinjilisti wa Wesley.” Baadhi ya watu katika Jumuiya ya Wakristo wanatarajia kwamba mwishoni, Waisraeli wote watageuzwa imani na kuokolewa. Wengine hufikiri kwamba sikuzote kumekuwa na uhusiano wa kudumu kati ya Mungu na Israeli, kwa hiyo wao hudai kwamba watu wa Mataifa tu ndio wanaopaswa kupatanishwa kupitia Kristo.

      Hebu fikiria: Baada ya uhamisho wa Babiloni, Waisraeli waliporudishwa kwenye nchi yao, watu hao walipaswa kurudisha ibada ya kweli katika nchi yao waliyopewa na Mungu. Mmoja wa miradi ya kwanza ilikuwa ni kujengwa upya kwa hekalu la Yehova huko Yerusalemu. Hata hivyo, tangu Waroma walipoharibu Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., hekalu hilo halijapata kujengwa upya kamwe. Badala yake, msikiti wa Kiislamu umejengwa mahali palipokuwa hekalu hilo. Ikiwa leo, Wayahudi wanaodai kuwa chini ya Sheria ya Musa, wangekuwa Yerusalemu wakiwa watu wa Mungu waliochaguliwa, je, hekalu lililotengwa kwa ajili ya ibada yake halingekuwa limejengwa upya?

      Mt. 21:42, 43: “Yesu akawaambia [wakuu wa makuhani na wanaume wazee kati ya Wayahudi wa Yerusalemu]: ‘Je, hamkusoma kamwe katika Maandiko, “Jiwe ambalo wajenzi walilikataa ndilo limekuwa jiwe kuu la pembeni. Limetokana na Yehova, nalo ni la kustaajabisha machoni petu”? Ndiyo sababu ninawaambia ninyi, Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.’”

      Mt. 23:37, 38: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na ambaye huwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara ngapi nilitaka kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka. Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”

      Je, agano la Mungu pamoja na Abrahamu linatoa uhakikisho kwamba bado Wayahudi ni watu wa Mungu waliochaguliwa?

      Gal. 3:27-29: “Ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hakuna Myahudi wala Mgiriki, hakuna mtumwa wala mtu huru, hakuna mwanamume wala mwanamke; kwa maana ninyi nyote ni mtu mmoja katika muungano na Kristo Yesu. Zaidi ya hayo, ikiwa ninyi ni wa Kristo, ninyi kwa kweli ni uzao wa Abrahamu, warithi kuhusiana na ahadi.” (Kwa hiyo, kwa maoni ya Mungu, kuwa uzao wa Abrahamu hakutegemei kuzaliwa kutokana na ukoo wa Abrahamu.)

      Je, Wayahudi wote watageuzwa wamwamini Kristo na kupata wokovu wa milele?

      Rom. 11:25, 26: “Sitaki ninyi, akina ndugu, mkose kuijua siri hii takatifu, kusudi msiwe wenye busara machoni penu wenyewe: kwamba, kwa sehemu, kumekuwa na kutiwa uzito kwa hisi za Israeli mpaka hesabu kamili ya watu wa mataifa iwe imeingia, na kwa namna hii [Kigiriki, houʹtos] Israeli wote wataokolewa.” (Ona kwamba kuokolewa kwa “Israeli wote” kunatimizwa, si kwa Wayahudi wote kugeuzwa imani, bali kwa ‘kuingia’ kwa watu kutoka mataifa mengine. Watafsiri fulani hutafsiri mstari wa 26 hivi: “Ndipo Israeli wote wataokoka.” Lakini A Manual Greek Lexicon of the New Testament [Edinburgh, 1937, G. Abbott-Smith, uku. 329] hufafanua maana ya houʹtos kuwa “kwa namna hii, basi, hivyo.”)

      Ili kuelewa kwa usahihi andiko la Waroma 11:25, 26, tunapaswa pia kukumbuka maneno haya yanayotangulia katika Waroma: “Yeye si Myahudi aliye hivyo kwa nje, wala kutahiriwa si kule ambako ni kwa nje juu ya mwili. Bali yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani, na kutahiriwa kwake ni kule kwa moyo kupitia roho, wala si kupitia sheria zilizoandikwa.” (2:28, 29) “Si wote wanaotokana na Israeli ni ‘Israeli’ kikweli.”—9:6.

      Je, Wayahudi wanapaswa kumwamini Yesu Kristo ndipo waokolewe?

      Andiko la Isaya 53:1-12 lilitabiri kifo cha Masihi ili ‘achukue dhambi ya watu wengi na kuingilia kati kwa ajili ya wakosaji.’ Andiko la Danieli 9:24-27 lilihusianisha kuja kwa Masihi na kifo chake pamoja na ‘kukomeshwa kwa makosa, na kumalizwa kabisa kwa dhambi.’ Maandiko hayo mawili yanaonyesha kwamba Wayahudi walihitaji kutetewa na kusamehewa dhambi. Je, wangeweza kumkataa Masihi kisha wawe na kibali cha Yule aliyemtuma?

      Mdo. 4:11, 12, NW: “[Kuhusu Yesu Kristo, mtume Petro aliongozwa na roho takatifu kuwaambia watawala Wayahudi na wanaume wazee katika Yerusalemu hivi:] Hilo ndilo ‘jiwe ambalo ninyi wajenzi mlilitendea kana kwamba si la maana ambalo limekuwa jiwe kuu la pembeni.’ Zaidi ya hayo, hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo lazima sisi tupate kuokolewa.” (Ijapokuwa taifa la Israeli la asili halina kibali cha pekee cha Mungu, Wayahudi mmoja-mmoja, kama watu wengine wa mataifa yote, wanaweza kupata wokovu kupitia Yesu yule Masihi.)

      Je, mambo yanayotendeka katika Israeli leo ni utimizo wa unabii wa Biblia?

      Eze. 37:21, 22: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amesema hivi: ‘Tazama, ninawachukua wana wa Israeli kutoka katikati ya mataifa ambako wameenda, nami nitawakusanya kutoka pande zote na kuwaleta katika nchi yao. Nami kwa kweli nitawafanya kuwa taifa moja katika nchi hiyo, kwenye milima ya Israeli, na mfalme mmoja atakuwa mfalme wao wote.’” (Leo, Waisraeli hawatawaliwi na mfalme wa ukoo wa Daudi. Taifa lao ni jamhuri.)

      Isa. 2:2-4: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote yatamiminika huko. Na vikundi vingi vya watu hakika vitaenda na kusema: ‘Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova, kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.’ . . . Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.” (Leo, huko Yerusalemu, ambako zamani hekalu lilikuwako hakuna “nyumba ya Mungu wa Yakobo,” lakini, badala yake, kuna msikiti wa Kiislamu. Nao Waisraeli wala jirani zao hawana mpango wowote wa ‘kufua panga zao ziwe majembe.’ Wanajilinda kwa kuwa tayari kivita.)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki