-
Ninaweza Kupata Uhuru Zaidi Jinsi Gani?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
SURA YA 3
Ninaweza Kupata Uhuru Zaidi Jinsi Gani?
“Laiti wazazi wangu wangeniruhusu niende matembezi nikiwa peke yangu wakati mwingine.”—Sarah, mwenye umri wa miaka 18.
“Kila mara mimi huwauliza wazazi wangu kwa nini hawaniamini na kunipa ruhusa ninapotaka kwenda matembezi na rafiki zangu. Mara nyingi wao hunijibu: ‘Tunakuamini. Lakini hatuwaamini rafiki zako.’”—Christine, mwenye umri wa miaka 18.
KAMA Sarah na Christine, je, wewe hutamani kuwa na uhuru zaidi? Ili kuupata, lazima kwanza wazazi wako wakuamini. Hata hivyo, sifa ya kuaminika ni kama pesa. Kuzipata ni vigumu, kuzipoteza ni rahisi, na hata ukipewa kiasi gani, hazitoshi kamwe. “Kila mara ninapotaka kwenda matembezi, wazazi wangu huniuliza maswali yasiyo na mwisho, ‘Unaenda wapi? Utakuwa na nani? Unaenda kufanya nini? Utarudi saa ngapi?’,” asema Iliana mwenye umri wa miaka 16. “Ninajua ni wazazi wangu, lakini maswali yao yanaudhi!”
Unaweza kufanya nini ili wazazi wako wakuamini zaidi na kukupa uhuru zaidi? Kabla ya kujibu swali hilo, acha tuone ni kwa nini kutumainiana ni jambo gumu kati ya wazazi na vijana wengi.
Matatizo Unapokua
Biblia inasema kwamba “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ndivyo pia na mwanamke. Iwe wewe ni mvulana au msichana, kubalehe kunakutayarisha kwa ajili ya maisha ya utu uzima—wakati ambapo utakuwa tayari kuondoka nyumbani na labda kuwa na familia yako mwenyewe.a
Hata hivyo, kuwa mtu mzima si kama mlango ambao unaingia tu unapofikia umri fulani. Badala yake ni kama ngazi unazopanda hatua kwa hatua wakati wa kipindi chote cha kubalehe. Ni kweli kwamba huenda wewe na wazazi wako mkawa na maoni tofauti kuhusu hatua ambazo umepiga. “Nina umri wa miaka 20 na bado naulizwa maswali,” asema Maria anayeona kwamba wazazi wake hawaamini kwamba anaweza kuchagua marafiki wazuri. “Wazazi wangu wanafikiri kwamba sina ujasiri wa kutosha kuondoka hali mbaya inapotokea. Nimejaribu kuwaambia kwamba tayari nimejiondoa katika hali nyingi mbaya, lakini wapi!”
Kama maneno ya Maria yanavyoonyesha, kutoaminiwa kunaweza kutokeza matatizo makubwa kati ya vijana na wazazi wao. Je, hivyo ndivyo familia yenu ilivyo? Ikiwa ndivyo, unaweza kufanya nini ili wazazi wako wakuamini zaidi? Na ikiwa wameacha kukuamini kwa sababu ya jambo fulani lisilo la hekima ulilofanya, unaweza kufanya nini ili kurudisha imani waliyokuwa nayo?
Onyesha Kwamba Unaweza Kuaminika
Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza: “Endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5) Ni kweli kwamba hakuwa akizungumza hasa na vijana. Lakini kanuni hiyo inaweza kutumika. Mara nyingi uhuru unaopata hulingana na kadiri unavyoaminika. Haimaanishi kwamba unahitaji kuwa mkamilifu. Kila mtu hukosea. (Mhubiri 7:20) Hata hivyo, kwa ujumla, inawezekana kwamba mwenendo wako unawafanya wazazi wako wasikuamini?
Kwa mfano, mtume Paulo aliandika: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Jiulize, ‘Ninawaambia wazazi wangu kweli nyakati zote kuhusu ninakoenda na mambo ninayofanya?’ Fikiria maelezo ya vijana fulani ambao wamejichunguza kwa uangalifu na kuona kwamba wanahitaji kufanya marekebisho. Baada ya kusoma maelezo yao, jibu maswali yanayofuata.
Lori: “Nilikuwa nikimtumia barua-pepe kisiri mvulana fulani niliyempenda. Wazazi wangu waligundua na kuniambia niache. Nikawaambia nitaacha, lakini sikuacha. Niliendelea kwa mwaka mzima. Nilikuwa nikimtumia mvulana huyo barua-pepe, wazazi wangu wanagundua, ninaomba msamaha na kuahidi kwamba nitaacha, lakini ninaendelea. Ilifikia hatua ambapo wazazi wangu hawakuniamini kamwe kuhusu lolote!”
Unafikiri ni kwa nini wazazi wa Lori waliacha kumwamini? ․․․․․
Kama wewe ungekuwa ndiye mzazi wa Lori, ungefanya nini, na kwa nini? ․․․․․
Lori alipaswa kufanya nini baada ya wazazi wake kuzungumza naye kuhusu tatizo lake? ․․․․․
Beverly: “Wazazi wangu hawakuniamini inapohusu wavulana, lakini sasa ninaelewa ni kwa nini. Nilikuwa nikiwachezea kimapenzi wavulana mawili walionizidi umri kwa miaka miwili. Nilikuwa nikizungumza nao kwa muda mrefu kwenye simu, na katika vikusanyiko mbalimbali ningezungumza nao peke yao. Wazazi wangu walininyang’anya simu kwa mwezi mmoja, na hawakuniruhusu niende popote pamoja na wavulana hao.”
Kama wewe ungekuwa mzazi wa Beverly, ungefanya nini, na kwa nini? ․․․․․
Unafikiri vizuizi ambavyo wazazi wa Beverly walimwekea havikustahili? Ikiwa havikustahili, ni kwa nini? ․․․․․
Beverly angeweza kufanya nini ili wazazi wake waanze kumwamini tena? ․․․․․
Kuaminiwa Tena
Namna gani ikiwa, kama vijana waliotajwa hapo juu, mwenendo wako umewafanya wazazi wako wasikuamini? Hata ikiwa hivyo ndivyo ilivyo, uwe na hakika kwamba unaweza kubadili hali. Jinsi gani?
Haikosi wazazi wako watakuamini zaidi na kukupa uhuru zaidi ukiendelea kujiendesha kwa njia inayofaa. Msichana anayeitwa Annette, alijionea hilo mwishowe. Anasema: “Unapokuwa na umri mdogo, huelewi kabisa kwa nini ni jambo la maana kuwa mwenye kuaminika. Sasa najiona kuwa mwenye kuwajibika zaidi na kwamba ninahitaji kujiendesha kwa njia itakayowafanya wazazi wangu waendelee kuniamini.” Siri ni nini? Badala ya kulalamika kwamba wazazi wako hawakuamini, jitahidi sikuzote kujiendesha kwa njia inayofaa. Huenda utapata uhuru zaidi.
Kwa mfano, je, unategemeka katika mambo yaliyoorodheshwa hapa chini? Tia alama ya ✔ katika kisanduku kilicho kando ya mambo unayohitaji kufanyia kazi.
□ Kurudi nyumbani wakati niliowekewa na wazazi
□ Kutimiza ahadi zangu
□ Kutunza wakati
□ Kutumia pesa kwa hekima
□ Kumaliza kazi za nyumbani
□ Kutoka kitandani bila kuambiwa-ambiwa
□ Kudumisha chumba changu kikiwa safi
□ Kusema kweli
□ Kuwa na usawaziko kuhusu matumizi ya simu au kompyuta
□ Kukubali makosa na kuomba msamaha
□ Jambo lingine ․․․․․
Kwa nini usiazimie kuthibitika kuwa mwaminifu katika mambo uliyotia alama? Fuata himizo hili la Biblia: ‘Ondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wako wa kwanza.’ (Waefeso 4:22) ‘Acha Ndiyo yako imaanishe Ndiyo.’ (Yakobo 5:12) “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.” (Waefeso 4:25) “Watiini wazazi wenu katika kila jambo.” (Wakolosai 3:20) Baada ya muda, maendeleo yako yatakuwa wazi kwa watu wengine, kutia ndani wazazi wako.—1 Timotheo 4:15.
Lakini namna gani ukihisi kwamba hata baada ya kufanya yote uwezayo, bado wazazi wako hawakupi uhuru unaostahili? Unaweza kuzungumza nao kuhusu jambo hilo. Badala ya kulalamika kwamba wao wanahitaji kukuamini zaidi, waulize kwa heshima wanataka wewe ufanye nini ili wakuamini. Waeleze waziwazi unachokusudia kufanya ili wakuamini zaidi.
Usitazamie wazazi wako wakubaliane nawe mara moja. Bila shaka, wangependa kuhakikisha kwamba utatimiza ahadi zako. Tumia kipindi hicho kujithibitisha kuwa unaaminika. Baada ya muda, wazazi wako watakuamini zaidi na kukupa uhuru zaidi. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa kwa Beverly aliyetajwa mapema. “Si rahisi kuaminiwa lakini ni rahisi sana kuacha kuaminiwa,” anasema huku akiongezea, “nimeanza kuaminiwa sasa, na ninahisi vizuri!”
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 22
Je, wazazi wako wametalikiana? Unaweza kuwa na usawaziko jinsi gani wakati ambapo kila kitu kinaonekana kwenda kombo maishani mwako?
[Maelezo ya Chini]
ANDIKO MUHIMU
“Msitumie uhuru wenu kama kisingizio cha kutenda uovu.” —1 Petro 2:16, Neno—Biblia Takatifu.
PENDEKEZO
Badala ya kulinganisha vizuizi ulivyo navyo sasa na uhuru ambao ndugu au dada yako mkubwa anao, linganisha vizuizi ulivyokuwa ukiwekewa ulipokuwa na umri mdogo zaidi na uhuru ulio nao sasa.
JE, WAJUA . . . ?
Kupewa uhuru usio na mipaka si ishara ya kupendwa na wazazi bali ni ishara ya kupuuzwa na wazazi.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Nitakuwa mwenye kutegemeka zaidi katika mambo yafuatayo: ․․․․․
Wazazi wangu wakiacha kunitumaini, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini huenda wazazi wako wakasita kukupa uhuru zaidi hata unapojitahidi sana kuwa mtu mwenye kutegemeka?
● Kwa nini wakati mwingine kupata uhuru zaidi kunategemea jinsi unavyopashana habari na wazazi wako?
[Blabu katika ukurasa wa 24]
“Ninapozungumza na wazazi wangu, ninawaambia waziwazi matatizo yangu na mambo yanayonihangaisha. Nafikiri hilo linafanya iwe rahisi kwao kuniamini.”—Dianna
[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 23]
Kufikia kuwa mtu mzima anayeaminiwa ni kama kupanda ngazi hatua kwa hatua katika kipindi chote cha kubalehe
[Mchoro]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
UTU UZIMA
KUBALEHE
UTOTO
-
-
Kuna Ubaya wa Kutaka Faragha?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
-
-
SURA YA 15
Kuna Ubaya wa Kutaka Faragha?
Tia alama ya ✔ kando ya jibu ambalo huenda ukachagua katika kila moja ya hali zifuatazo:
1. Uko katika chumba chako cha kulala kisha ndugu au dada yako anaingia bila kubisha.
□ ‘Ni sawa tu. Mimi pia hufanya hivyo nyakati nyingine.’
□ ‘Huo ni utovu wa adabu! Namna gani ikiwa ninavaa?’
2. Umerudi tu nyumbani na wazazi wako wanaanza kukurushia maswali. “Ulikuwa wapi? Ulikuwa ukifanya nini? Ulikuwa na nani?”
□ ‘Ni sawa tu. Mimi huwaambia kila kitu.’
□ ‘Inaudhi sana! Wazazi wangu hawaniamini!’
HUENDA ulipokuwa na umri mdogo, suala la faragha halikuwa jambo kubwa sana. Ndugu na dada zako wadogo walipoingia chumbani mwako ghafla, uliwakaribisha bila kulalamika. Wazazi wako walipokuuliza swali lolote, uliwajibu bila kusitasita. Wakati huo, hukuwa na siri zozote. Sasa unatamani kuwa na faragha. “Mimi hufurahi kufanya mambo fulani kivyangu,” asema Corey mwenye umri wa miaka 14. Acha tuone maeneo mawili ambayo unapojaribu kupata faragha huenda ukakumbana na ugumu.
Unapojaribu Kuwa Peke Yako
Kuna sababu kadhaa halali zinazoweza kukufanya utake kuwa peke yako. Huenda unataka tu ‘kupumzika kidogo.’ (Marko 6:31) Au unapotaka kusali, unaweza kufanya kama Yesu alivyowashauri wanafunzi wake, ‘kuingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, usali kwa Baba yako.’ (Mathayo 6:6; Marko 1:35) Tatizo ni kwamba, unapofunga mlango wa chumba chako cha faragha (ikiwa unacho), huenda wazazi wako wasifikiri kwamba unasali! Na huenda ndugu na dada zako wasielewe wakati unapotaka kuwa peke yako.
Unachoweza kufanya. Badala ya kugombana na wengine kwa sababu ya kutaka faragha, fanya mambo yafuatayo:
● Jaribu kuwawekea ndugu na dada zako sheria fulani zinazoweza kufuatwa ili uwe na wakati wa kuwa peke yako. Ikihitajika, waombe wazazi wako wakusaidie katika jambo hilo.a
● Jaribu kuelewa maoni ya wazazi wako. “Wakati mwingine wazazi wangu hutaka kujua ninafanya nini,” asema Rebekah mwenye umri wa miaka 16. “Lakini kusema kweli ikiwa ningekuwa mzazi, hata mimi ningetaka kujua kijana wangu anafanya nini hasa kwa kuwa vijana wanakabili majaribu ya kila aina!” Kama Rebekah, je, unaweza kuelewa hangaiko la wazazi wako?—Methali 19:11.
● Jiulize hivi kwa unyoofu: ‘Kupitia mwenendo wangu, nimewapa wazazi wangu sababu ya kunishuku hivi kwamba ninapofunga mlango wa chumba changu wanafikiri ninafanya jambo lisilofaa? Nimekuwa nikificha mambo mengi kuhusu maisha yangu mpaka wanahisi kuwa wanahitaji kuwa kama polisi ili wanifahamu?’ Ikiwa sivyo na bado wazazi wako hawakuamini, basi waeleze kwa upole na heshima jinsi unavyohisi. Sikiliza kwa makini mahangaiko yao, na uhakikishe kwamba hufanyi jambo lolote linalochangia tatizo hilo.—Yakobo 1:19.
Unapotafuta Marafiki
Unapobalehe, ni jambo la kawaida kutafuta marafiki nje ya familia yenu. Pia, ni kawaida kwa wazazi wako kutaka kujua rafiki zako ni nani na kile mnachofanya mnapokuwa pamoja. Hata hivyo, wakati mwingine huenda ukahisi kwamba wazazi wako wana wasiwasi usio na msingi. “Kile ninachotaka ni kutumia simu yangu na kutuma barua pepe bila wazazi wangu kunichunguza-chunguza kila baada ya dakika kumi na kuniuliza ninazungumza na nani,” asema Amy, mwenye umri wa miaka 16.
Unachoweza kufanya. Badala ya marafiki wako kuharibu uhusiano wako na wazazi wako, jaribu kufanya mambo yafuatayo.
● Watambulishe marafiki wako kwa wazazi wako. Bila shaka, hungependa wazazi wako wawe kama polisi, lakini ikiwa hutaki wawajue rafiki zako, huenda wakalazimika kufanya hivyo. Kumbuka kuwa wazazi wako wanavyozidi kuwajua watu unaoshirikiana nao ndivyo watakavyozidi kukuruhusu ujichagulie rafiki zako.
● Jichunguze kwa unyoofu: Je, jambo ambalo hasa unatafuta ni kupata faragha au kuficha mambo? Brittany, mwenye umri wa miaka 22, asema hivi: “Ikiwa unaishi nyumbani na wazazi wako wanataka kujua unachofanya, fikira zako zinapaswa kuwa, ‘Kile ninachofanya si kosa, kwa hiyo mbona nijifiche?’ Kwa upande mwingine, ikiwa unahitaji kuficha unachofanya, basi kuna tatizo.”
Jinsi ya Kupata Faragha
Sasa una nafasi ya kuchemsha bongo na utatuzi wa mambo fulani yanayokuhangaisha kuhusu faragha. Kwenye nafasi iliyo hapa chini andika majibu yako kwa maswali yanayoambatana na hatua zifuatazo:
Hatua ya 1: Tambua tatizo. Ni kuhusu mambo gani unahisi ungependa kuwa na faragha?
․․․․․
Hatua ya 2: Fikiria maoni ya wazazi wako. Unafikiri ni nini hasa kinachowahangaisha?
․․․․․
Hatua ya 3: Tafuta suluhisho. Ni katika njia gani huenda unachangia tatizo hilo bila kukusudia? Ni marekebisho gani unayoweza kufanya kupatana na jibu lako hapo juu? Ungependa wazazi wako washughulikie matatizo yako jinsi gani?
․․․․․
Hatua ya 4: Zungumzeni. Eleza jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu faragha.
․․․․․
Je, mmoja wa wazazi wako amelala katika kifo? Ikiwa ndivyo, unaweza kupata faraja wapi?
[Maelezo ya Chini]
ANDIKO MUHIMU
“Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu.”—2 Timotheo 2:15.
PENDEKEZO
Unapozungumza na wazazi wako kuhusu faragha, usinung’unike. Waeleze kinachokuhangaisha hasa. Kuna tofauti gani kati ya manung’uniko na mahangaiko? Kunung’unika ni kukazia mambo ambayo unafikiri wazazi wako wanakosea. Kuzungumzia mahangaiko kutawasaidia ninyi nyote mtafute utatuzi.
JE, WAJUA . . . ?
Kadiri unavyozidi kujifunua kwa wazazi wako, ndivyo wanavyozidi kukuamini.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili wazazi wangu waniamini (au waanze kuniamini tena), nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini wazazi wako wana haki ya kutaka kujua mambo yanayoendelea maishani mwako?
● Kujitahidi kusitawisha ustadi wa kupashana habari na wazazi wako kutakusaidia jinsi gani kupashana habari na watu wengine utakapokuwa mtu mzima?
[Blabu katika ukurasa wa 108]
“Wazazi hawataki upatwe na jambo lolote baya, na nyakati nyingine huenda ikaonekana ni kama wanaingilia mambo yako ya kibinafsi. Huenda hilo lisionekane kuwa sawa. Lakini, kusema kweli, kama ningekuwa mzazi, ningefanya vivyo hivyo.”—Alana
[Picha katika ukurasa wa 109]
Sifa ya kuaminika ni kama mshahara, lazima uufanyie kazi ili uupate
-