Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nina Huzuni Nyakati Zote—Nifanye Nini?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
    • SURA YA 13

      Nina Huzuni Nyakati Zote—Nifanye Nini?

      “Rafiki zangu wanapokuwa na shida, mimi huwa tayari kuwasaidia kutatua matatizo na kuwafariji. Hata hivyo, jambo ambalo wengi hawajui ni kwamba, ninaporudi nyumbani, mimi huingia chumbani mwangu na kulia.”—Kellie.

      “Ninapokuwa na huzuni, mimi hujitenga na wengine. Nikialikwa mahali, ninatoa kisababu cha kutoenda. Mara nyingi watu wa familia yetu hawajui kwamba nina huzuni. Wao hufikiri niko sawa.”—Rick.

      UMEWAHI kuwa na maoni kama ya Kellie au Rick? Ikiwa ndiyo, usikate kauli kwamba una kasoro fulani. Ukweli ni kwamba kila mtu huwa na huzuni mara kwa mara. Hata wanaume na wanawake waaminifu katika Biblia walihuzunika nyakati nyingine.—1 Samweli 1:6-8; Zaburi 35:14.

      Katika visa fulani, huenda ukajua ni kwa nini una huzuni, katika visa vingine huenda usijue. “Si lazima uwe katika hali mbaya ili uwe na huzuni.” asema Anna, mwenye umri wa miaka 19. “Huzuni inaweza kutokea wakati wowote, hata wakati ambapo huna matatizo. Ni jambo lisiloeleweka, lakini ndivyo ilivyo!”

      Haidhuru kisababishi ni nini, au hata kama hakuna kisababishi, unaweza kufanya nini unapolemewa na huzuni? Jaribu mambo yafuatayo:

      1. Zungumza. Akiwa amevurugika, Ayubu alisema: “Nitasema kwa uchungu wa nafsi yangu!”—Ayubu 10:1.

      Kellie: “Baada ya kuzungumza na mtu, mimi huwa na utulivu wa ajabu. Ninahisi kwamba angalau kuna mtu anayenielewa. Anaweza kunishushia kamba na kunitoa shimoni—niwe huru hatimaye!”

      Dokezo: Andika hapa chini jina la rafiki unayeweza kuzungumza naye unapolemewa na huzuni.

      ․․․․․

      2. Andika. Huzuni inapotanda kama wingu maishani mwako, huenda ikafaa uandike jinsi unavyohisi. Katika zaburi zake zilizoongozwa na roho, nyakati nyingine Daudi alieleza hisia zake za huzuni. (Zaburi 6:6) Kuandika hisia hizo kunaweza kukusaidia ‘kulinda hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.’—Methali 3:21.

      Heather: “Kuandika hunisaidia kupanga mawazo yangu yaliyovurugika. Unapoandika kuhusu hisia mbalimbali ulizo nazo, huzuni hupungua.”

      Dokezo: Tumia chati kwenye ukurasa wa 93 kupata msaada wa kushinda hali ngumu. Kufanya hivyo kutakusaidia kupunguza huzuni.

      3. Sali. Biblia inasema ukisali kuhusu mahangaiko yako, ‘amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itaulinda moyo wako na nguvu zako za akili.’—Wafilipi 4:6, 7.

      Esther: “Nilikuwa nikijaribu kuelewa ni kwa nini nimeshuka moyo sana, lakini sikuelewa. Nikamwomba Yehova anisaidie niwe na furaha. Nilikuwa nimechoka kuhuzunika bila sababu. Mwishowe nikafaulu. Usipuuze kamwe nguvu ya sala!”

      Dokezo: Unaposali, fuata mfano wa sala iliyo katika Zaburi 139:23, 24. Mmiminie Yehova moyo wako, na umwombe akusaidie kuelewa chanzo cha huzuni yako.

      Pamoja na madokezo yaliyo juu, Neno la Mungu, Biblia, ni msaada mkubwa. Kujaza akili yako mambo yenye kujenga yanayopatikana katika masimulizi ya Biblia kunaweza kufanya uhisi vizuri. (Zaburi 1:1-3) Madokezo ya usomaji wa Biblia wenye kujenga yanaweza kupatikana kwa kuchunguza kurasa zenye kichwa “Mfano wa Kuigwa” katika mabuku ya kitabu hiki. Katika ukurasa wa 227 wa Buku la 2, utaona jinsi mtume Paulo alivyofanikiwa kushughulika na hisia zisizofaa alizokuwa nazo nyakati nyingine kwa sababu ya kutokamilika.

      Huzuni Inapodumu

      “Asubuhi fulani,” asema Ryan, “ningehisi kwamba ni afadhali kukaa kitandani ili kuepuka kukabili siku nyingine isiyo na maana.” Ryan ana ugonjwa wa kushuka moyo sana, na kuna wengi kama yeye. Kulingana na uchunguzi mbalimbali, kijana 1 kati ya 4 huugua aina fulani ya ugonjwa wa kushuka moyo kabla ya kufikia kuwa mtu mzima.

      Unaweza kujua jinsi gani ikiwa unaugua ugonjwa wa kushuka moyo? Dalili fulani zinatia ndani badiliko kubwa la hisia na mwenendo, kujitenga na watu, kutopendezwa na karibu kila kitu, badiliko kubwa katika mazoea ya kula na kulala, na hisia kali za kujidharau au kuhisi hatia isiyo na msingi.

      Ni kweli kwamba mara kwa mara karibu kila mtu huwa na dalili moja au zaidi kati ya hizo. Hata hivyo, dalili hizo zikiendelea kwa zaidi ya majuma kadhaa, zungumza na wazazi wako ili wafanye mpango umwone daktari. Daktari anaweza kujua iwapo huzuni yako inatokana na ugonjwa fulani.a

      Ikiwa una ugonjwa wa kushuka moyo sana, usiaibike. Baada ya kupata matibabu, wengi wanaougua wamepata nafuu—na huenda hata sasa wana furaha kuliko wakati mwingine wowote! Iwe huzuni yako inasababishwa na kushuka moyo au la, kumbuka maneno yenye kufariji ya Zaburi 34:18: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Namna gani ikiwa una huzuni nyingi sana hivi kwamba umekuwa ukifikiria kujiua?

      [Maelezo ya Chini]

      a Huzuni inapoendelea kwa muda mrefu, vijana fulani huanza kufikiria kujiua. Iwapo umekuwa na mawazo ya aina hiyo, zungumza na mtu mzima unayemwamini haraka iwezekanavyo.—Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 14 ya kitabu hiki.

      ANDIKO MUHIMU

      “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.

      PENDEKEZO

      Eleza jinsi unavyohisi unapokuwa na huzuni na kile unachofikiri kinasababisha huzuni hiyo. Baada ya mwezi mmoja, soma ulichoandika. Hisia zako zimebadilika? Ikiwa zimebadilika, andika kilichokusaidia.

      JE, WAJUA . . . ?

      Ni sawa kulia, hata kama wewe ni mvulana. Pindi moja katika maisha yake, Mfalme Daudi alikiri hivi: “Kila usiku . . . nalilowesha godoro langu kwa machozi yangu.”—Zaburi 6:6, Union Version.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Ili nipate faraja, ninaweza kufanya mambo yafuatayo: ․․․․․

      Kushirikiana na marafiki wafuatao kutanisaidia kupunguza huzuni: ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kulia kuna faida yoyote?

      ● Kuwa pamoja na wengine kunaweza kukusaidia jinsi gani kupunguza huzuni?

      [Blabu katika ukurasa wa 96]

      “Ninapokuwa na huzuni, nahitaji kuepuka kujitenga na watu. Ni kweli kwamba huenda nikahitaji kuwa peke yangu ili kutafakari yanayoendelea na hata labda kulia. Lakini baada ya hapo, najua nahitaji kuwa na watu ili kuondoa akilini kinachofanya niwe na huzuni.”—Christine

      [Chati/​Picha katika ukurasa wa 93]

      Ukurasa wa Mazoezi

      Ili Kupunguza Huzuni Yako

      Kamilisha chati

      Tukio

      Mwalimu ananifanya nijidharau

      Njia isiyofaa

      Nitaacha kutia bidii katika masomo

      Njia nzuri zaidi

      Dokezo: Ona Sura ya 20 ya kitabu hiki

      Tukio

      Rafiki yangu ananipuuza

      Njia isiyofaa

      Nitaeneza uvumia usiofaa kumhusu

      Njia nzuri zaidi

      Dokezo: Ona Sura ya 10 ya Buku la 2

      Tukio

      Wazazi wangu wanatalikiana

      Njia isiyofaa

      Nitakuwa na kinyongo kuelekea mzazi mmoja au wote wawili

      Njia nzuri zaidi

      Dokezo: Ona Sura ya 4 ya kitabu hiki

      Tukio

      ․․․․․

      Njia isiyofaa

      ․․․․․

      Njia nzuri zaidi

      ․․․․․

      Tukio

      ․․․․․

      Njia isiyofaa

      ․․․․․

      Njia nzuri zaidi

      ․․․․․

      [Picha katika ukurasa wa 95]

      Ukijitahidi na kutafuta msaada, unaweza kutoka katika lindi la huzuni

  • Afadhali Nijiue?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
    • SURA YA 14

      Afadhali Nijiue?

      “AFADHALI nife kuliko kuwa hai.” Ni nani aliyesema maneno hayo? Mtu ambaye hakumwamini Mungu? Mtu aliyekuwa amemwacha Mungu? Mtu ambaye Mungu alikuwa amemwacha? Hapana. Mwenye kuyasema ni mtu mwenye kumcha Mungu, lakini aliyekuwa amefadhaika, Yona.—Yona 4:3.

      Biblia haisemi Yona alitaka kujiua. Hata hivyo, maneno yake yanaonyesha jambo moja hakika—nyakati fulani hata mtumishi wa Mungu anaweza kulemewa na mawazo yenye kufadhaisha.—Zaburi 34:19.

      Vijana fulani hufadhaika kabisa hivi kwamba hawaoni haja ya kuendelea kuishi. Huenda wakahisi kama Laura, mwenye umri wa miaka 16, anayesema: “Kwa miaka mingi, nimekuwa na mshuko wa moyo. Mara nyingi nimefikiria kujiua.” Ikiwa unamfahamu mtu ambaye amekuwa akisema kwamba anataka kujiua—au ikiwa wewe mwenyewe umefikiria kujiua—unaweza kufanya nini? Hebu tuchunguze ni kwa nini huenda mtu akawa na mawazo kama hayo.

      Kinachomfanya Mtu Akate Tamaa

      Ni nini kinachoweza kumfanya mtu afikirie kujiua? Huenda mambo kadhaa yakahusika. Kwanza, tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” na vijana wengi wanalemewa na maisha hayo hata zaidi. (2 Timotheo 3:1) Pia, kutokamilika kunaweza kufanya watu fulani wahisi vibaya kujihusu na kuhusu ulimwengu unaowazunguka. (Waroma 7:22-24) Nyakati nyingine hisia hizo hutokana na jinsi wanavyotendewa. Au, huenda ugonjwa ukamfanya mtu ahisi hivyo. Makadirio yenye kushangaza katika nchi moja yanaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 90 ya watu waliojiua walikuwa na ugonjwa fulani wa akili.a

      Bila shaka, kila mtu hupatwa na matatizo. Biblia inasema kwamba “uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Vijana pia wanatiwa ndani. Kwa kweli, vijana wanaweza kuathiriwa sana na matukio mabaya, kama yafuatayo:

      ● Kifo cha mtu wa ukoo, au rafiki

      ● Mgogoro katika familia

      ● Kuanguka mtihani

      ● Kuvunjika kwa uhusiano wa kimahaba

      ● Kutendewa vibaya (kutia ndani kimwili au kingono)

      Ni kweli kwamba, mwishowe karibu kila kijana atapatwa na mojawapo ya hali zilizotajwa. Kwa nini vijana fulani hufanikiwa kukabiliana na hali hizo kuliko wengine? Wataalamu wanasema kwamba vijana wanaokata tamaa huhisi hakuna anayeweza kuwasaidia na matatizo yao hayawezi kutatuliwa. Si kwamba wanataka kufa, ni kwamba wanataka kuondolea mbali maumivu waliyo nayo.

      Kuna Tumaini?

      Huenda unamfahamu mtu ambaye anataka kuondolea mbali maumivu aliyo nayo—anatamani sana kufanya hivyo hivi kwamba amesema anataka kujiua. Katika hali kama hiyo, unaweza kufanya nini?

      Ikiwa rafiki yako ametaabika kiasi cha kutaka kujiua, mhimize atafute msaada. Kisha, zungumza na mtu mzima mkomavu, haidhuru maoni ya rafiki yako. Usihofu kwamba urafiki wenu utaharibika. Kufanya hivyo kwaweza kuokoa uhai wa rafiki yako!

      Lakini namna gani ikiwa wewe mwenyewe umekuwa ukifikiria kujiua? Usifiche hisia zako. Zungumza na mtu fulani—mzazi, rafiki, au mtu yeyote anayekujali, atakayekusikiliza, na kuchukulia mambo unayosema kwa uzito. Kwa kuzungumzia matatizo yako waziwazi, hakuna hasara utakayopata, badala yake, utafaidika sana.b

      Bila shaka, matatizo yako hayatatoweka kwa kuwa tu umezungumza na mtu fulani. Hata hivyo, huenda msaada mkubwa unaohitaji ni kuzungumza na mtu unayeweza kumtumaini ili akusaidie kuiona hali yako kwa njia inayofaa. Huenda hata kufanya hivyo kukakusaidia kutafuta njia nzuri ya kutatua hali.

      Mambo Hubadilika

      Unapokabili matatizo, kumbuka: Hata hali ionekane kuwa mbaya kadiri gani, baada ya muda mambo yatabadilika. Pindi moja, mtunga-zaburi Daudi, ambaye alikuwa na matatizo mengi, alimwambia Mungu hivi katika sala: “Umenibadilishia maombolezo yangu yakawa kucheza dansi.”—Zaburi 30:11.

      Bila shaka, Daudi hakutazamia kucheza dansi kudumu milele. Alijua kutokana na mambo aliyojionea maishani kwamba matatizo huja na kwenda. Umetambua ukweli huo kuhusiana na matatizo yako? Huenda matatizo mengine yakaonekana kuwa yenye kulemea—angalau kwa sasa. Lakini uwe na subira. Mara nyingi mambo hubadilika na kuwa mazuri. Katika visa fulani, matatizo yanaweza kupunguzwa katika njia ambayo hungewazia kamwe. Katika visa vingine, unaweza kugundua njia ya kukabiliana na matatizo, njia ambayo hukuwa umeifikiria awali. Jambo kuu ni kwamba matatizo yanayohangaisha hayatadumu milele.—2 Wakorintho 4:17.

      Faida ya Sala

      Njia ya maana zaidi ya kupashana habari ni kusali. Unaweza kusali kama Daudi: “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofadhaisha, na uone kama ndani yangu mna njia yoyote yenye kuumiza, na uniongoze katika njia ya mpaka wakati usio na kipimo.”—Zaburi 139:23, 24.

      Sala si kama gongo tu la kujitegemeza, kama linalotumiwa na walemavu. Ni njia halisi ya kupashana habari na Baba yako wa mbinguni, anayetaka ‘ummiminie moyo wako.’ (Zaburi 62:8) Fikiria kweli za msingi zifuatazo kumhusu Mungu:

      ● Anafahamu hali zinazokutaabisha.—Zaburi 103:14.

      ● Anakujua vema kuliko unavyojijua.—1 Yohana 3:20.

      ● ‘Anakujali wewe.’—1 Petro 5:7.

      ● Katika ulimwengu wake mpya, Mungu “atafuta kila chozi” kutoka katika macho yako.—Ufunuo 21:4.

      Tatizo Linapotokana na Ugonjwa

      Kama ilivyotajwa mapema, mara nyingi hisia za kutaka kujiua zinatokana na ugonjwa fulani. Ikiwa unaugua ugonjwa fulani, usiaibike kutafuta msaada. Yesu alisema kwamba wenye kuugua wanahitaji tabibu. (Mathayo 9:12) Inapendeza kwamba magonjwa mengi yana tiba. Na matibabu yanaweza kukufanya uhisi vema zaidi!c

      Biblia inatoa ahadi yenye kufariji kwelikweli kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Mungu anasema kwamba wakati huo, “mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Kwa sasa, fanya kila uwezalo kukabiliana na matatizo ya maisha, ukiwa na hakika kwamba katika wakati uliowekwa wa Mungu, tatizo la kushuka moyo halitakuwako.—Ufunuo 21:1-4.

      PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 2, SURA YA 9

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Wazazi wako wanataka kujua kila kitu kuhusu maisha yako—hata mambo mengine ambayo hungependa wajue. Unaweza kufanya nini ili wakupe nafasi unayohitaji?

      [Maelezo ya Chini]

      a Hata hivyo, ni muhimu kujua kwamba vijana wengi walio na ugonjwa wa akili hawajiui.

      b Wakristo wanaotaabika wana msaada mwingine—wazee wa kutaniko.—Yakobo 5:14, 15.

      c Unaweza kupata habari zaidi katika Sura ya 13 ya kitabu hiki.

      ANDIKO MUHIMU

      “Maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”—Wafilipi 4:6, 7.

      PENDEKEZO

      Unapohisi umeshuka moyo, fanya mazoezi ya kutembea. Kufanya mazoezi kunaweza kukufanya uhisi umetulia na kuwa na hali njema.

      JE, WAJUA . . . ?

      Katika visa vya kujiua, hasara si kwa wenye kujiua tu, bali pia jamaa na marafiki.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Nikihisi kuwa sifai na hakuna mtu anayenipenda, nitazungumza na (andika jina la mtu utakayezungumza naye) ․․․․․

      Baraka moja katika maisha yangu ambayo ninaweza kukumbuka na kuithamini ni ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Hata matatizo makubwa ni ya muda tu. Kutafakari ukweli huo kunaweza kukusaidia jinsi gani?

      ● Ni kwa njia gani kujiua ni kumtwika mtu mwingine matatizo yako?

      [Blabu katika ukurasa wa 104]

      “Nyakati nyingine, nilishuka moyo sana hivi kwamba nilitaka kufa tu, lakini sasa nimerudia hali yangu ya kawaida kwa sababu ya kudumu katika sala na kupata matibabu.”—Heidi

      [Picha katika ukurasa wa 100]

      Unapohisi Umelemewa

      Mara kwa mara hata baadhi ya wanaume na wanawake waaminifu wa nyakati za Biblia walihisi kulemewa na mahangaiko ya maisha. Fikiria mifano ifuatayo.

      Rebeka: “Ikiwa hivi ndivyo ilivyo, hasa kwa nini niko hai?”—Mwanzo 25:22.

      Musa: “Tafadhali niue kabisa, . . . wala usiache niutazame msiba wangu.”—Hesabu 11:15.

      Eliya: “Ee Yehova, iondoe nafsi yangu, kwa maana mimi si bora kuliko mababu zangu.”—1 Wafalme 19:4.

      Ayubu: “Laiti ungenificha katika Kaburi, . . . kwamba ungeniwekea kikomo cha wakati na kunikumbuka!”​—Ayubu 14:13.

      Katika kila kisa kilicho juu, mwishowe hali zilibadilika na kuwa nzuri, tena kwa njia ambayo mwenye kuhusika hakuwazia kamwe. Uwe na hakika kwamba inaweza kuwa hivyo kwako pia!

      [Picha katika ukurasa wa 102]

      Hisia za kukata tamaa ni kama mawingu ya dhoruba—baada ya muda yatapita

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki