-
Kwa Nini Niishi Kulingana na Viwango vya Biblia?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 34
Kwa Nini Niishi Kulingana na Viwango vya Biblia?
Unakula chakula cha mchana shuleni pamoja na wasichana wawili wakati mvulana aliyehamia shule yenu karibuni anapoingia.
“Wajua nini, Brett anakupenda kwelikweli,” msichana wa kwanza akuambia. “Mimi huona jinsi anavyokutazama. Macho yake hayabanduki!”
“Tena ngoja nikwambie,” msichana wa pili anong’oneza huku akiinama kukuelekea. “Hana rafiki msichana!”
Tayari unajua. Juzi tu, Brett alikuwa amekualika kwao kwa sherehe. Ijapokuwa hukwenda, umekuwa ukiwazia jinsi ambavyo mambo yangekuwa kama ungeenda.
Msichana wa kwanza anakatiza mawazo yako.
“Laiti nisingekuwa na rafiki mvulana,” anasema. “Ningemkubali mara moja.”
Kisha anakutazama kwa mshangao. Unajua tu atakuuliza nini.
“Na wewe, mbona huna rafiki mvulana?” anakuuliza.
Hupendi hata kidogo swali hilo! Ukweli ni kwamba ungependa kuwa na rafiki mvulana. Lakini umeambiwa unapaswa kungoja hadi utakapokuwa tayari kuolewa. Kama si . . .
“Ni dini yenu, sivyo?” yule msichana wa pili anasema.
‘Amejuaje nilichokuwa nikifikiria?’ unawaza moyoni.
“Wewe nawe, ni Biblia, Biblia, Biblia kila siku,” asema kwa dhihaka. “Kwa nini usifurahie maisha kidogo tu wakati mwingine?”
UMEWAHI kudhihakiwa kwa sababu ya kujitahidi kuishi kulingana na viwango vya Biblia? Ikiwa ndivyo, huenda umekuwa ukijiuliza ikiwa kuna kitu fulani unachokosa. Msichana anayeitwa Deborah alihisi hivyo. Anakumbuka, “Niliona viwango vya Biblia vinaninyima mambo mengi. Nilitamani uhuru ambao wanafunzi wenzangu walikuwa nao.”
Ukweli wa Mambo
Si lazima sikuzote upotee njia ndiyo ujue njia. Kujifunza kutokana na makosa ya wengine ni jambo zuri na linapatana na Maandiko. Ndivyo alivyofanya mtunga-zaburi Asafu. Wakati fulani, aliona viwango vya Mungu vinamnyima mambo mengi. Lakini alipochunguza maisha ya wale walioacha njia za Mungu alijionea ukweli wa mambo. Baadaye Asafu alikata kauli kwamba walikuwa “kwenye udongo unaoteleza.”—Zaburi 73:18.
Ukitafakari hayo, fikiria maelezo yanayofuata ya vijana ambao wakati fulani waliacha viwango vya Biblia na kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa.
● Ni mambo gani yaliyochochea fikira na matendo yako?
Deborah: “Nilipokuwa shuleni kila mtu alikuwa na rafiki, nao walionekana kuwa na furaha. Tulipoenda matembezi nao na kuona wakipigana busu na kukumbatiana, niliwaonea wivu na kuhisi upweke. Mara nyingi nilikuwa nikimwazia kwa saa nyingi mvulana fulani niliyempenda. Kufanya hivyo kulizidisha tamaa yangu ya kutaka kuwa naye.”
Mike: “Nilisoma vitabu na kutazama vipindi vilivyohusu ngono. Kuzungumzia ngono pamoja na rafiki zangu kulizidisha tamaa yangu ya kutaka kujaribu. Halafu, nilipokuwa peke yangu na msichana, nilifikiri kwamba ningeweza kumshikashika kimahaba pasipo kufanya ngono naye, na kwamba ningeweza kuacha wakati wowote.”
Andrew: “Nilikuwa na mazoea ya kutazama ponografia (picha za ngono) katika Intaneti. Nilianza kunywa pombe kupita kiasi. Nami nilikwenda katika sherehe pamoja na vijana ambao hawakuheshimu hata kidogo viwango vya Biblia kuhusu maadili.”
Tracy: “Nilijua akilini kwamba ni vibaya kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa, lakini sikuchukia jambo hilo. Sikupanga kuanza kufanya ngono kabla ya ndoa, lakini hisia zangu zilinilemea. Kwa muda fulani, dhamiri yangu haikunisumbua hata kidogo.”
● Je, maisha hayo yalikuletea furaha?
Deborah: “Mwanzoni, nilijiona huru kwelikweli nami nilifurahi kwamba niko sawa na vijana wenzangu. Lakini hisia hizo hazikudumu. Nilianza kujiona mchafu, mwenye hatia, na mtu asiyefaa kitu. Nilijuta sana kwamba nilipoteza ubikira wangu.”
Andrew: “Ilikuwa rahisi zaidi na zaidi kutosheleza tamaa zisizofaa. Lakini wakati huohuo, nililemewa na hisia za hatia na kujichukia.”
Tracy: “Ukosefu wa adili uliniharibia ujana wangu. Nilidhani mimi na mvulana aliyekuwa rafiki yangu tungekuwa na furaha isiyo na kifani. Haikuwa hivyo. Tulisababishiana maumivu, huzuni, na mfadhaiko. Usiku mmoja baada ya mwingine nilikesha kitandani nikilia, na kutamani kwamba laiti ningefuata maagizo ya Yehova.”
Mike: “Nilianza kuhisi kana kwamba nimekufa. Nilijaribu kupuuza matokeo ya matendo yangu kwa wengine, lakini nikashindwa. Niliumia sana kuona kwamba huku nikitafuta kujifurahisha mwenyewe, nilikuwa nikiwaumiza wengine.”
● Ungewapa ushauri gani vijana wanaoona kwamba viwango vya Biblia vinawanyima mambo mengi?
Tracy: “Ishi kulingana na viwango vya Yehova, na ushirikiane na watu wanaofanya vivyo hivyo. Utakuwa na furaha nyingi zaidi ukifanya hivyo.”
Deborah: “Usijifikirie mwenyewe tu, au mambo unayotaka. Matendo yako yatawaathiri wengine. Ukipuuza shauri la Mungu, utajiletea msiba.”
Andrew: “Kwa sababu ya kukosa ukomavu, unafikiri kwamba maisha ya vijana wenzako yanafurahisha. Mitazamo yao inaweza kukuambukiza. Kwa hiyo chagua rafiki zako kwa hekima. Mtegemee Yehova, nawe utajiepusha na majonzi mengi.”
Mike: “Baadhi ya vitu vyenye thamani sana ambavyo Yehova amekupa ni kujiheshimu na dhamiri safi. Kutupa zawadi hizo kwa sababu tu huwezi kujizuia ni kujidharau. Zungumza na wazazi wako na watu wengine wakomavu kuhusu matatizo yako. Ukifanya kosa, usisite kulifunua na kurekebisha hali hiyo. Ukifuata maagizo ya Yehova, utapata amani ya kweli.”
Viwango vya Biblia—Pingu au Mkanda wa Usalama?
Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” na anataka wewe pia uwe na furaha. (1 Timotheo 1:11; Mhubiri 11:9) Viwango vilivyo katika Biblia vinaweza kukunufaisha. Ni kweli kwamba huenda ukaviona kama pingu zinazokunyima uhuru. Lakini kwa kweli, kanuni za maadili zilizo katika Biblia ni kama mkanda wa usalama unaomlinda abiria asipatwe na madhara.
Bila shaka unaweza kuitumaini Biblia. Ukiamua kuishi kulingana na viwango vyake, utamfurahisha Yehova na wakati uleule utajiletea baraka.—Isaya 48:17.
Unaweza kuwa rafiki ya Mungu. Soma uone jinsi hilo linavyowezekana.
MAANDIKO MUHIMU
“Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”—Isaya 48:17.
PENDEKEZO
Fikiria jinsi unavyoweza kumsadikisha mdogo wako aone hekima ya kufuata viwango vya Biblia. Kuzungumza kuhusu imani yako ni njia nzuri sana ya kukusaidia kujenga imani hiyo moyoni mwako.
JE, WAJUA . . .?
Kwa muda mfupi tu unaweza kuharibu uhusiano wako na Yehova, lakini huenda ikakuchukua miaka mingi kuurekebisha.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Kitakachonisaidia kuona faida ya kufuata viwango vya Biblia ni ․․․․․
Nikianza kuwaonea wivu wale wanaoishi kulingana na viwango vya ulimwengu, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kuhusu matokeo mabaya ya kutotii sheria za Mungu, kwa nini si lazima upotee njia ndio ujue njia?
● Umejifunza nini kutokana na maelezo ya Deborah, Mike, Andrew, na Tracy?
● Kwa nini huenda watu fulani wakaona viwango vya Biblia kama pingu zinazowanyima uhuru, lakini kwa nini maoni hayo yana kasoro?
[Blabu katika ukurasa wa 285]
‘‘Huwezi kulinganisha wasiwasi wa kuogopa kuadhibiwa na maumivu yanayotokana na kuficha kosa.’’—Donna
[Picha katika ukurasa wa 288]
Viwango vya Biblia havikunyimi furaha; vinakulinda
-
-
Ninaweza Kuwa Rafiki ya Mungu Jinsi Gani?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 35
Ninaweza Kuwa Rafiki ya Mungu Jinsi Gani?
Baada ya kukumbwa na jambo fulani lenye kuhuzunisha, Jeremy alianza kuona faida ya kuwa na urafiki pamoja na Mungu. Anasema: “Nilipokuwa na umri wa miaka 12, baba yangu alituacha. Usiku mmoja nilikuwa nikisali kitandani, nikimsihi Yehova amfanye baba yangu arudi nyumbani.”
Akiwa katika hali hiyo, Jeremy alianza kusoma Biblia. Aliposoma Zaburi 10:14, aliguswa moyo sana. Mstari huo unasema hivi kumhusu Yehova: “Mtu mwenye taabu, mvulana asiye na baba, anajikabidhi kwako. Wewe mwenyewe umekuwa msaidizi wake.” Jeremy anasema: “Nilihisi kana kwamba Yehova alikuwa akizungumza nami na kunijulisha kwamba yeye ni msaidizi wangu; yeye ni Baba yangu. Singeweza kupata baba bora kuliko yeye!”
IWE uko katika hali kama ya Jeremy au sivyo, Biblia inaonyesha kwamba Yehova anataka uwe rafiki yake. Biblia inasema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Hebu fikiria maneno hayo: Ijapokuwa huwezi kumwona—na kwa kweli yeye si kijana kama wewe—Yehova Mungu anakualika uwe rafiki yake!
Lakini ili uwe rafiki ya Mungu lazima uchukue hatua fulani. Kwa mfano: Ukipanda ua unajua kwamba halitakua lenyewe. Ili likue, lazima ulitilie maji kwa ukawaida na kuliweka katika mazingira yanayofaa ukuzi. Ndivyo pia na urafiki pamoja na Mungu. Unaweza kuukuza urafiki wa aina hiyo jinsi gani?
Faida ya Kujifunza
Marafiki huwasiliana—kila mmoja husikiliza na kuzungumza. Ndivyo pia na urafiki pamoja na Mungu. Tunaposoma na kujifunza Biblia, tunamsikiliza Mungu.—Zaburi 1:2, 3.
Ni kweli kwamba huenda kiasili hupendi kusoma. Vijana wengi hupenda kutazama televisheni, kucheza, au kuwa tu na marafiki. Lakini ikiwa unataka kuwa rafiki ya Mungu, hakuna njia ya mkato. Lazima umsikilize kwa kujifunza Neno lake.
Hata hivyo, usiwe na wasiwasi. Si lazima kujifunza kuwe jambo lenye kuchosha. Unaweza kujifunza kufurahia kufanya hivyo—hata ikiwa kiasili hupendi kusoma. Jambo la kwanza unalohitaji kufanya ni kutenga wakati wa kujifunza Biblia. “Mimi nina ratiba,” anasema msichana mmoja anayeitwa Lais. “Mimi husoma sura moja ya Biblia kila asubuhi ninapoamka.” Maria, mwenye umri wa miaka 15, ana ratiba tofauti. “Mimi husoma sehemu fulani ya Biblia kila siku kabla ya kwenda kulala,” anasema.
Ili kuanza programu yako mwenyewe ya kujifunza, tazama sanduku lililo katika ukurasa wa 292. Kisha, katika nafasi iliyo hapa chini, andika wakati ambapo unaweza kutumia dakika 30 hivi ukijifunza Neno la Mungu.
․․․․․
Kupanga wakati ni hatua ya kwanza tu. Ukishaanza kujifunza, huenda ukaona kwamba nyakati nyingine si rahisi kusoma Biblia. Huenda ukakubaliana na Jezreel, mwenye umri wa miaka 11, aliyesema hivi waziwazi: “Sehemu fulani za Biblia ni ngumu na si zenye kusisimua sana.” Ikiwa unahisi hivyo, usikate tamaa. Sikuzote ona wakati wa kujifunza kuwa wakati wa kumsikiliza Yehova Mungu, rafiki yako. Mwishowe, kujifunza Biblia kutakuwa jambo lenye kusisimua na lenye faida kwako ikitegemea jitihada zako!
Sala Ni Muhimu
Tunaposali, tunazungumza na Mungu. Hebu wazia jinsi sala ilivyo zawadi ya ajabu! Unaweza kuzungumza na Yehova Mungu wakati wowote, iwe ni mchana au usiku. Anapatikana sikuzote. Pia, anataka kukusikiliza. Ndiyo sababu Biblia inakuhimiza: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.”—Wafilipi 4:6.
Kama andiko hilo linavyoonyesha, kuna mambo mengi unayoweza kumwambia Yehova. Mambo hayo yanaweza kutia ndani matatizo na mahangaiko yako. Pia yanaweza kutia ndani mambo unayothamini kutoka kwake. Wewe huwashukuru rafiki zako kwa mambo mazuri wanayokufanyia, sivyo? Basi, unaweza kumshukuru Yehova pia, ambaye amefanya mengi zaidi kuliko rafiki yeyote anavyoweza kukufanyia.—Zaburi 106:1.
Hapa chini, andika mambo unayothamini kutoka kwa Yehova.
․․․․․
Bila shaka, mara kwa mara wewe huwa na wasiwasi na mahangaiko fulani. Zaburi 55:22 inasema: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”
Hapa chini, andika mambo fulani yanayokuhangaisha ambayo ungependa kusali juu yake.
․․․․․
Mambo Ambayo Umejionea Maishani
Kuna jambo lingine kuhusiana na urafiki wako na Mungu ambalo hupaswi kupuuza. Mtunga-zaburi Daudi aliandika: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” (Zaburi 34:8) Daudi alitunga Zaburi ya 34 baada ya kupitia hali yenye kuogopesha. Alikuwa akimkimbia Mfalme Sauli aliyetaka kumwua—masaibu kwelikweli. Kisha akalazimika kutafuta kimbilio kati ya Wafilisti waliokuwa maadui. Uhai wake ulipokuwa hatarini, Daudi alijifanya mwenda-wazimu na kukimbia.—1 Samweli 21:10-15.
Daudi hakuona kwamba alikuwa ameponea chupuchupu kwa sababu ya werevu wake mwenyewe. Badala yake, alisema kwamba wokovu wake ulitokana na Yehova. Mapema katika zaburi iliyotajwa, aliandika: “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha.” (Zaburi 34:4) Mambo aliyojionea mwenyewe yalimchochea Daudi kuwahimiza wengine ‘waonje na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’a
Kuna jambo lolote maishani mwako linaloonyesha kwamba Yehova anakujali? Ikiwa lipo, liandike hapa chini. Dokezo: Si lazima liwe jambo la ajabu sana. Fikiria baraka unazopata kila siku, ambazo huenda hata ni rahisi kuzipuuza.
․․․․․
Huenda wazazi wako walikufundisha Biblia. Ikiwa ndivyo, hiyo ni baraka. Hata hivyo, bado wewe binafsi unahitaji kukuza urafiki pamoja na Mungu. Ikiwa hujafanya hivyo, unaweza kutumia habari iliyo katika sura hii kuanza kufanya hivyo. Yehova atabariki jitihada zako. Biblia inasema: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata.”—Mathayo 7:7.
PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 38 NA 39
Unaona ni vigumu kuzungumza na wengine kumhusu Mungu? Jifunze jinsi unavyoweza kutetea imani yako.
[Maelezo ya Chini]
a Biblia nyingine hutafsiri maneno “onjeni mwone,” kuwa “jigundulie mwenyewe,” “jionee mwenyewe,” na “kupitia mambo utakayojionea utaona kwamba.”—Contemporary English Version, Today’s English Version, na The Bible in Basic English.
MAANDIKO MUHIMU
“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.
PENDEKEZO
Ukisoma kurasa nne tu za Biblia kila siku, utamaliza kuisoma yote kwa muda wa mwaka mmoja hivi.
JE, WAJUA . . .?
Kusoma kwako kitabu hiki na kufuata mashauri yaliyomo yanayotegemea Biblia ni uthibitisho wa kwamba Yehova anapendezwa na wewe binafsi.—Yohana 6:44.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili kufaidika zaidi na funzo la Biblia la kibinafsi, nita ․․․․․
Ili kuwa na mazoea ya kusali, nita ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Unaweza kufanya nini ili funzo la Biblia liwe lenye kupendeza zaidi?
● Kwa nini Yehova anataka kusikiliza sala za wanadamu ambao si wakamilifu?
● Unaweza kufanya nini ili sala zako ziwe na maana zaidi?
[Blabu katika ukurasa wa 291]
‘‘Nilipokuwa mdogo, sala zangu zilikuwa kama wimbo. Sasa mimi hujaribu kusali kuhusu mambo mazuri na mabaya ya kila siku. Kwa kuwa hakuna siku mbili zinazofanana kabisa, hilo hunisaidia kutorudia-rudia mambo yaleyale.’’—Eve
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 292]
Ichanganue Biblia
1. Chagua simulizi fulani katika Biblia ambalo ungependa kusoma. Sali upate hekima ya kuelewa habari hiyo.
2. Soma simulizi hilo kwa uangalifu. Usiwe na haraka. Unaposoma, piga picha akilini. Jiwazie ukiwa katika hali unayosoma: Jaribu kuona kinachoendelea, kusikia sauti mbalimbali, vuta pumzi na kunusa harufu mbalimbali, onja ladha ya chakula, na kadhalika. Fanya simulizi hilo liwe halisi akilini mwako!
3. Fikiria habari ambayo umesoma. Jiulize maswali kama vile:
● Kwa nini Yehova alitia ndani simulizi hilo katika Neno lake?
● Ni nani wanaostahili kuigwa, na ni nani walio vielelezo vya kuonya?
● Ni jambo gani la maana ninaloweza kujifunza kutokana na usomaji huo?
● Simulizi hilo linanifundisha nini kuhusu Yehova na jinsi anavyofanya mambo?
4. Toa sala fupi kwa Yehova. Mwambie mambo ambayo umejifunza kutokana na funzo lako la Biblia na jinsi unavyopanga kutumia habari hiyo maishani mwako. Mshukuru Yehova sikuzote kwa zawadi ambayo amekupa—Neno lake, Biblia Takatifu!
[Picha]
“Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.”—Zaburi 119:105.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 294]
Tanguliza Mambo ya Maana
Huna wakati wa kusali? Huna wakati wa kujifunza Biblia? Mara nyingi inategemea jinsi unavyopanga mambo yako.
Jaribu zoezi hili: Chukua ndoo, na uweke mawe kadhaa makubwa ndani yake. Kisha jaza mchanga hadi pomoni. Ndoo hiyo imejaa mawe na mchanga.
Sasa mwaga chini kila kitu kutoka katika ndoo hiyo, lakini uhifadhi mawe na mchanga huo. Rudia tena zoezi hilo: Sasa jaza mchanga kwanza, kisha ujaribu kuyaweka mawe ndani ya ndoo. Eti hakuna nafasi? Ni kwa sababu umetangulia kuweka mchanga.
Zoezi hilo linakufundisha nini? Biblia inasema: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Ukitanguliza mambo madogo kama vile burudani, hutapata kamwe nafasi ya kutosha kufanya mambo yaliyo makubwa—mambo ya kiroho. Lakini ukifuata shauri la Biblia, utaona kwamba una nafasi ya kutosha kufanya yote mawili, mambo ya Ufalme na burudani kwa kiasi kinachofaa. Siri ni kujua unachopaswa kutanguliza!
[Picha katika ukurasa wa 290]
Kama ua lililopandwa, urafiki pamoja na Mungu unahitaji kutunzwa vizuri ili ukue
-
-
Ninaweza Kuitetea Jinsi Gani Imani Yangu Katika Mungu?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 36
Ninaweza Kuitetea Jinsi Gani Imani Yangu Katika Mungu?
Ni nini ambacho huenda kikakuzuia kuzungumza na wanafunzi wenzako kuhusu imani yako?
□ Kukosa ujuzi wa Biblia
□ Kuogopa kudhihakiwa
□ Kutojua jinsi ya kuanzisha mazungumzo
Ni njia gani unayoona kuwa rahisi zaidi ya kuzungumza kuhusu imani yako?
□ Kuzungumza na mwanafunzi mmoja-mmoja
□ Kuzungumza mbele ya darasa zima
□ Kuandika insha kuhusu imani yangu inayotegemea Biblia
Andika jina la mwanafunzi unayefikiri anaweza kukubali mazungumzo ya Biblia ikiwa tu ungejua jinsi ya kuanzisha mazungumzo hayo. ․․․․․
WANAFUNZI wengi hawapendi kuzungumza mambo ya Mungu. Anza kuzungumzia jambo lingine lolote—michezo, mavazi, watu wa jinsia tofauti—na mazungumzo yatapamba moto. Lakini ukitaja tu Mungu, kimya chenye kishindo kinazuka.
Si kwamba vijana wenzako hawamwamini Mungu; vijana wengi wanamwamini. Lakini vijana fulani huona aibu kuzungumzia habari hiyo. Huenda wakaonelea kwamba ‘haivutii.’
Namna Gani Wewe?
Ikiwa unasita kuongea na wanafunzi wenzako kuhusu Mungu, inaeleweka. Hakuna mtu anayetaka kukataliwa, sembuse kudhihakiwa! Je, hilo linaweza kutokea unapozungumza kuhusu imani yako? Inawezekana. Kwa upande mwingine, huenda vijana wenzako wakakushangaza. Wengi kati yao wanatafuta majibu ya maswali kama vile: Ulimwengu huu unaelekea wapi? na Kwa nini ulimwengu umejaa taabu? Huenda hata vijana wenzako wakapendelea kuzungumzia mambo hayo na kijana mwenzao badala ya kuyazungumzia na mtu mzima.
Ni kweli, kuzungumza na vijana wenzako kuhusu dini kwaweza kuonekana kuwa jambo gumu kwelikweli. Hata hivyo, huhitaji kuwa mbishi wala hupaswi kuogopa kwamba utashindwa kusema jambo hususa linalofaa. Kuzungumzia imani yako kunaweza kulinganishwa na kupiga chombo fulani cha muziki. Huenda ikawa vigumu mwanzoni. Lakini baada ya kufanya mazoezi ya kutosha inakuwa rahisi zaidi na zaidi, nawe utapata matokeo mazuri ya jitihada zako. Hata hivyo, utaanzisha mazungumzo namna gani?
Kwa kawaida, unaweza kuanza na jambo rahisi. Kwa mfano, huenda tukio la karibuni linapozungumziwa shuleni, unaweza kuongezea maoni yako yanayotegemea Biblia. Au unaweza kujaribu kuongea na mwanafunzi mmoja tu. Au hata, unaweza kufanya kama vijana wengine Wakristo wanavyofanya, wanaweka kitabu kinachozungumzia Biblia juu ya dawati lao waone ikiwa yeyote atavutiwa nacho. Mara nyingi, kitabu hicho huvutia mwanafunzi fulani, kisha mazungumzo yanaanza!
Kati ya njia zilizo juu, ni njia gani ambayo wewe unaweza kujaribu? ․․․․․
Kuna njia nyingine unayoweza kutumia kuzungumza na mwanafunzi mwenzako kuhusu imani yako? Ikiwa ipo, iandike hapa chini.
․․․․․
Nyakati nyingine somo fulani linapofundishwa shuleni hutoa nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu imani yako. Kwa mfano, unaweza kufanya nini somo la mageuzi linapozungumziwa? Unaweza kuitetea imani yako jinsi gani?
Kutetea Uumbaji
“Nadharia ya mageuzi ilipoanza kuzungumziwa darasani, ilikuwa kinyume kabisa na kila kitu nilichokuwa nimefundishwa,” anasema kijana anayeitwa Ryan. “Ilifundishwa kana kwamba ni jambo ambalo limehakikishwa, na hilo liliniogopesha.” Msichana anayeitwa Raquel anasema jambo kama hilo. “Niliingiwa na wasiwasi wakati mwalimu wa somo la jamii aliposema kwamba wakati ujao tutazungumzia mageuzi,” anasema. “Nilijua ningelazimika kueleza darasa zima msimamo wangu kuhusu suala hilo lenye kuzua ubishi.”
Wewe huhisije somo la mageuzi linapofundishwa shuleni? Unaamini kwamba Mungu ndiye ‘aliyeumba vitu vyote.’ (Ufunuo 4:11) Unaona kila mahali uthibitisho wa vitu vilivyobuniwa kwa akili nyingi. Hata hivyo, vitabu vya mafunzo vinasema kwamba uhai ulitokana na mageuzi, na ndivyo mwalimu anavyofundisha pia. Wewe ni nani upinge maoni ya “wataalamu”?
Usiwe na shaka. Kuna watu wengine pia ambao hawaungi mkono nadharia ya mageuzi. Ukweli ni kwamba hata wanasayansi fulani hawakubaliani na nadharia hiyo. Pia, walimu na wanafunzi wengi hawaikubali.
Hata hivyo, ili kuitetea imani yako kuhusu uumbaji, unahitaji kujua mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu hilo. Hakuna haja ya kubishania mambo ambayo Biblia haitaji moja kwa moja. Fikiria mifano michache.
Kitabu changu cha sayansi kinasema kwamba dunia na sayari nyingine zimekuwapo kwa mabilioni ya miaka. Biblia inasema kwamba dunia na sehemu nyingine za ulimwengu zilikuwapo kabla ya siku ya kwanza ya uumbaji. Kwa hiyo, inawezekana kwamba dunia na sayari nyingine zimekuwapo kwa mabilioni ya miaka.—Mwanzo 1:1.
Mwalimu wetu anasema kwamba dunia haingeweza kuumbwa kwa siku sita tu. Biblia haisemi kwamba siku hizo sita ni vipindi vya siku halisi zenye urefu wa saa 24.
Darasani tulizungumzia mabadiliko mbalimbali ambayo yametokea kwa wanyama na wanadamu. Biblia inasema kwamba Mungu aliumba kila kiumbe hai “kulingana na aina yake.” (Mwanzo 1:20, 21) Haiungi mkono wazo la kwamba uhai ulitokana na vitu visivyo na uhai au kwamba Mungu aliumba chembe moja kisha chembe hiyo ikaanza kugeuka-geuka. Hata hivyo, kila “aina” inaweza kutokeza unamna-namna. Kwa hiyo, kulingana na Biblia, mabadiliko yanaweza kutokea katika viumbe vya “aina” moja.
Unapofikiria mambo ambayo yamezungumziwa katika sura hii, ungejibu nini mwalimu au mwanafunzi akisema:
“Sayansi imethibitisha kwamba tulitokana na mageuzi.”․․․․․
“Siwezi kuamini kwamba kuna Mungu kwa sababu siwezi kumwona.” ․․․․․
Uwe na Imani Thabiti
Ikiwa wazazi wako ni Wakristo, huenda ukaamini uumbaji kwa sababu tu umefundishwa hivyo. Hata hivyo, kwa kuwa sasa unazidi kukua, unapaswa kumwabudu Mungu kwa ‘nguvu zako za kufikiri,’ ukiwa na msingi thabiti wa imani yako. (Waroma 12:1) Kwa hiyo, jiulize, ‘Ni nini kinachonisadikisha kwamba kuna Muumba?’ Sam, mwenye umri wa miaka 14, husadikishwa na mwili wa mwanadamu. “Una sehemu nyingi zenye ufundi wa ajabu,” anasema, “na sehemu zote hufanya kazi kwa upatano mzuri. Haiwezekani kwamba mwili wa mwanadamu ungetokana na mageuzi!” Holly, mwenye umri wa miaka 16, anakubaliana naye. “Tangu nilipopimwa na kupatikana na ugonjwa wa kisukari,” anasema, “Nimejifunza mengi kuhusu jinsi mwili unavyofanya kazi. Kwa mfano, ni ajabu jinsi kongosho—kiungo kidogo ambacho kipo nyuma ya tumbo—kinavyofanya kazi kubwa ya kusawazisha damu na viungo vingine.”
Hapa chini, andika mambo matatu yanayokusadikisha wewe kwamba kuna Muumba.
1. ․․․․․
2. ․․․․․
3. ․․․․․
Hakuna haja ya kuona haya au kuaibika kwa sababu unaamini Mungu na uumbaji. Unapofikiria uthibitisho uliopo, bila shaka utaona kwamba ni jambo linalopatana na akili kuamini kuwa wanadamu walitokana na ubuni wenye akili nyingi.
Kwa hiyo, kuamini mageuzi kunahitaji imani isiyo ya kawaida—ni kama kuamini miujiza pasipo mfanya-miujiza! Baada ya kufikiria jambo hilo ukitumia nguvu zako za kufikiri, utakuwa na ujasiri zaidi wa kutetea imani yako katika Mungu.
Unaona vijana wa rika lako wakibatizwa. Je, uko tayari kuchukua hatua hiyo?
MAANDIKO MUHIMU
“Siionei aibu habari njema; kwa kweli, hiyo ni nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu aliye na imani.”—Waroma 1:16.
PENDEKEZO
Zingatia tabia yako unapozungumza kuhusu imani yako. Ukionekana kana kwamba unaaibika, utajiletea dhihaka kutoka kwa vijana wenzako. Lakini ukizungumza kwa uhakika—kama vile tu wanafunzi wenzako wanavyozungumzia maoni yao—bila shaka watakuheshimu.
JE, WAJUA . . .?
Nyakati nyingine walimu wanapoombwa wathibitishe nadharia ya mageuzi, wanashindwa kufanya hivyo, nao huona kwamba wanaikubali tu kwa sababu ndivyo walivyofundishwa.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ninaweza kuanzisha mazungumzo ya Biblia pamoja na mwanafunzi mwenzangu kwa ․․․․․
Nikiulizwa kwa nini naamini kwamba kuna Muumba, nitasema ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini ni jambo la maana kuzungumza na wengine kuhusu imani yako?
● Ukiwa shuleni, ni njia gani rahisi ya kuzungumzia imani yako kuhusu uumbaji?
● Unaweza kuonyesha jinsi gani shukrani zako kwa Yule aliyeumba vitu vyote?—Matendo 17:26, 27.
[Blabu katika ukurasa wa 299]
‘‘Shule ni eneo la kuhubiri ambalo sisi tu ndio tunaweza kulihubiri.’’—Iraida
[Picha katika ukurasa wa 298]
Kama vile tu kupiga chombo cha muziki, kuzungumza kuhusu imani yako kunahitaji ustadi—ukijizoeza, utakuwa stadi
[Picha katika ukurasa wa 300, 301]
Unaweza kushinda woga wa kutetea imani yako
-