-
Nibatizwe?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 37
Nibatizwe?
Tia alama taarifa zifuatazo ikiwa ni kweli au si kweli:
Kila Mkristo anapaswa kubatizwa.
□ Kweli
□ Si kweli
Kusudi kuu la kubatizwa ni kukuzuia usitumbukie katika dhambi.
□ Kweli
□ Si kweli
Ubatizo ni hatua inayokuelekeza kwenye wokovu.
□ Kweli
□ Si kweli
Usipobatizwa, Mungu hatakuhukumu kwa matendo yako.
□ Kweli
□ Si kweli
Ikiwa rafiki zako wanabatizwa, basi wewe pia uko tayari kubatizwa.
□ Kweli
□ Si kweli
IKIWA unaishi kupatana na viwango vya Mungu, unakuza urafiki pamoja na Mungu, na kuzungumza na wengine kuhusu imani yako, ni kawaida kuanza kufikiria ubatizo. Lakini utajua jinsi gani kwamba uko tayari kuchukua hatua hiyo? Ili kujibu swali hilo, kwanza tuchunguze taarifa zilizo juu na kuona ikiwa ni kweli au si kweli.
● Kila Mkristo anapaswa kubatizwa.
Kweli. Yesu aliagiza wanafunzi wake wabatizwe. (Mathayo 28:19, 20) Hata Yesu mwenyewe alibatizwa. Ili kuwa mfuasi wa Yesu, unahitaji kubatizwa unapokuwa na umri wa kutosha kufanya uamuzi huo na kuwa na tamaa ya kutoka moyoni ya kufanya hivyo.
● Kusudi kuu la kubatizwa ni kukuzuia usitumbukie katika dhambi.
Si kweli. Ubatizo huonyesha waziwazi kwamba umejiweka wakfu kwa Yehova. Ubatizo wako si mkataba unaokuzuia kufanya mambo ambayo moyoni mwako ungependa kuyafanya. Badala yake, unaweka maisha yako wakfu kwa Yehova kwa sababu unataka kuishi kulingana na viwango vyake.
● Ubatizo ni hatua inayokuelekeza kwenye wokovu.
Kweli. Biblia inasema kwamba ubatizo ni muhimu ili kupata wokovu. (1 Petro 3:21) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba ubatizo ni kama bima unayojikatia ili kujilinda usipatwe na madhara endapo msiba utatokea. Unabatizwa kwa sababu unampenda Yehova na unataka kumtumikia kwa moyo wako wote, milele.—Marko 12:29, 30.
● Usipobatizwa, Mungu hatakuhukumu kwa matendo yako.
Si kweli. Andiko la Yakobo 4:17 linasema hivi: “Ikiwa mtu anajua jinsi ya kufanya yaliyo sawa na bado hayafanyi, hiyo ni dhambi kwake”—iwe amebatizwa au sivyo. Kwa hiyo ikiwa unajua yaliyo sawa nawe una umri wa kutosha kuchunguza maisha yako kwa uzito, huenda huu ndio wakati wa kuzungumza jambo hilo na mzazi wako au Mkristo mwingine mkomavu. Kufanya hivyo kutakusaidia kujua jinsi unavyoweza kufanya maendeleo kufikia ubatizo.
● Ikiwa rafiki zako wanabatizwa, basi wewe pia uko tayari kubatizwa.
Si kweli. Uamuzi wa kubatizwa unapaswa kuwa wa hiari. (Zaburi 110:3) Unapaswa kubatizwa ikiwa tu unajua vizuri maana ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na una hakika kwamba uko tayari kubeba jukumu hilo.—Mhubiri 5:4, 5.
Badiliko Kubwa Maishani
Ubatizo ni badiliko kubwa maishani linaloleta baraka nyingi. Pia, ni jukumu zito—la kuishi kulingana na wakfu wako kwa Yehova.
Je, uko tayari kuchukua hatua hiyo? Ikiwa ndivyo, unapaswa kufurahi. Pendeleo kuu zaidi liko mbele yako—pendeleo la kumtumikia Yehova kwa moyo wote na kuishi maisha yanayoonyesha kwamba kwa kweli umejiweka wakfu kwake.—Mathayo 22:36, 37.
Jifunze kuweka miradi ili utumie maisha yako kwa njia bora zaidi.
MAANDIKO MUHIMU
“Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.”—Waroma 12:1.
PENDEKEZO
Ukitegemea mwelekezo kutoka kwa wazazi wako, tafuta mtu katika kutaniko anayeweza kukusaidia kufanya maendeleo ya kiroho.—Matendo 16:1-3.
JE, WAJUA . . .?
Kubatizwa ni sehemu muhimu ya “alama” inayokutambulisha kwa ajili ya wokovu.—Ezekieli 9:4, 6.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili kufanya maendeleo na kufikia ubatizo, nitajitahidi kuelewa vizuri zaidi mafundisho yafuatayo ya Biblia: ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Kwa nini ubatizo ni hatua nzito?
● Ni nini kinachoweza kumfanya kijana achukue hatua ya kubatizwa mapema sana?
● Ni mambo gani yanayoweza kumfanya kijana asitesite bure kujiweka wakfu na kubatizwa?
[Blabu katika ukurasa wa 306]
‘‘Kujua kwamba nimebatizwa kulinisaidia kufanya maamuzi kwa hekima na kutofanya mambo fulani ambayo yangeweza kuwa na matokeo mabaya.’’—Holly
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 307]
Maswali Ambayo Huulizwa Mara Nyingi Kuhusu Ubatizo
Ubatizo unawakilisha nini? Kuzamishwa na kuinuliwa humaanisha kwamba mtu ameacha maisha ya kufanya mapendezi yake mwenyewe, kana kwamba yule mtu wa zamani amekufa, na kuinuliwa akiwa hai, au mtu mpya ili kufanya mapenzi ya Mungu.
Kuweka maisha yako wakfu kwa Yehova kunamaanisha nini? Inamaanisha kujikana mwenyewe, na kuahidi kwamba utatanguliza mapenzi ya Mungu maishani. (Mathayo 16:24) Mtu anapaswa kujiweka wakfu rasmi kupitia sala kwa Yehova kabla ya kubatizwa.
Unapaswa kufanya nini kabla ya kubatizwa? Unapaswa kuwa ukiishi kulingana na Neno la Mungu na kuzungumza na wengine kuhusu imani yako. Unapaswa kujenga urafiki pamoja na Mungu kupitia sala na kujifunza Neno lake. Unapaswa kumtumikia Yehova kwa sababu wewe mwenyewe umeamua kufanya hivyo—lakini si kwa sababu wengine wanakulazimisha ufanye hivyo.
Mtu anapaswa kuwa na umri gani anapobatizwa? Umri si neno. Hata hivyo, unapaswa kuwa na umri wa kutosha, yaani, unapaswa kuwa na ukomavu wa kutosha kuelewa maana ya kujiweka wakfu.
Namna gani ikiwa unataka kubatizwa na wazazi wako wanasema ungoje? Huenda wangependa ujifunze zaidi kuishi maisha ya Kikristo. Usipuuze shauri lao. Tumia wakati huo kukuza urafiki wako na Yehova.—1 Samweli 2:26.
[Sanduku katika ukurasa wa 308, 309]
Ukurasa wa Mazoezi
Unafikiria Kubatizwa?
Kagua maendeleo yako kwa kufikiria maswali na taarifa zilizo hapa chini. Soma maandiko yaliyotajwa kabla ya kuandika majibu.
Unaonyesha jinsi gani kwamba unamtegemea Yehova?—Zaburi 71:5. ․․․․․
Umeonyesha jinsi gani kwamba nguvu zako za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa?—Waebrania 5:14. ․․․․․
Wewe husali mara ngapi? ․․․․․
Wewe hutaja mambo hususa katika sala zako? Sala zako zinafunua nini kuhusu upendo wako kwa Yehova?—Zaburi 17:6. ․․․․․
Andika hapa chini miradi yoyote ambayo ungependa kujiwekea kuhusu sala. ․․․․․
Wewe hujifunza Biblia kibinafsi mara ngapi?—Yoshua 1:8. ․․․․․
Funzo lako la kibinafsi linatia ndani nini? ․․․․․
Andika hapa chini miradi ambayo ungependa kujiwekea kuhusu funzo la kibinafsi. ․․․․․
Wewe hupata matokeo katika huduma yako? (Kwa mfano, unaweza kuwaeleza wengine mafundisho ya msingi ya Biblia? Wewe huwarudia wanaopendezwa? Unajitahidi kuongoza funzo la Biblia?)
□ Ndiyo □ Hapana
Wewe huenda kuhubiri hata ikiwa wazazi wako hawaendi?—Matendo 5:42.
□ Ndiyo □ Hapana
Andika hapa chini miradi yoyote ungependa kujiwekea kuhusu huduma yako.—2 Timotheo 2:15. ․․․․․
Wewe huhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida au mara mojamoja?—Waebrania 10:25. ․․․․․
Unapokuwa katika mikutano, unashiriki jinsi gani? ․․․․․
Wewe huhudhuria mikutano wakati ambapo wazazi wako hawawezi (ikiwa wanakuruhusu kwenda)?
□ Ndiyo □ Hapana
Unaweza kusema kwamba kwa kweli unapenda kufanya mapenzi ya Mungu?—Zaburi 40:8.
□ Ndiyo □ Hapana
Unaweza kutaja visa hususa ambavyo ulisimama imara na kushinda mkazo kutoka kwa vijana wenzako?—Waroma 12:2. ․․․․․
Unapanga kufanya nini ili upendo wako kwa Yehova usipoe?—Yuda 20, 21. ․․․․․
Utaendelea kumtumikia Yehova hata wazazi na rafiki zako wakiacha kumtumikia?—Mathayo 10:36, 37.
□ Ndiyo □ Hapana
[Picha katika ukurasa wa 310]
Kama ndoa, ubatizo ni badiliko kubwa maishani—si jambo linalopaswa kuchukuliwa vivi hivi
-
-
Nitayatumiaje Maisha Yangu?Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
-
-
SURA YA 38
Nitayatumiaje Maisha Yangu?
“Mwanzoni sikujali kuhusu wakati ujao. Lakini nilipokaribia kumaliza shule, nilitambua kwamba ninaingia katika ulimwengu wenyewe, ulimwengu wa watu wazima.”—Alex.
WAZIA kwamba unapanga kufunga safari ya kwenda mbali kutoka nyumbani. Labda utatazama ramani kwanza na kuona njia bora itakayokufikisha huko. Ndivyo pia na kupanga maisha yako ya usoni. “Kuna mengi unayoweza kufanya,” asema Michael, kijana ambaye sasa anatumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Utaamua namna gani jambo la kufanya? “Kwa kujiwekea miradi,” asema Michael.
Uone mradi kama mahali unapokwenda. Hailekei utafika huko kwa kutangatanga bila kusudi. Ingekuwa afadhali kama ungechukua ramani na kupanga safari yako ya mfano. Ukifanya hivyo, utakuwa ukifuata shauri lililo katika Methali 4:26: “Lainisha mapito ya mguu wako.” Tafsiri ya Biblia Habari Njema inatafsiri hivi mstari huo: “Fikiria njia utakayochukua.”
Miaka ijayo, utafanya maamuzi mengi mazito kuhusu ibada, kazi, ndoa, familia, na mambo mengine muhimu. Itakuwa rahisi zaidi kufanya maamuzi kwa hekima ikiwa unajua unakokwenda. Na unapopanga safari ya maisha yako, kuna jambo moja ambalo kwa kweli hupaswi kupuuza.
“Mkumbuke Muumba Wako”
Ili uwe na furaha ya kweli, lazima uzingatie maneno haya ya Mfalme Sulemani mwenye hekima: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” (Mhubiri 12:1) Yaani, maamuzi unayofanya maishani yanapaswa kuongozwa na tamaa ya kumpendeza Mungu.
Kwa nini ni muhimu kuzingatia hilo? Biblia inasema hivi katika Ufunuo 4:11: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Viumbe vyote, mbinguni na duniani, vina deni la kumrudishia shukrani Muumba. Je, unamshukuru kwa kukupa “uhai na pumzi na vitu vyote”? (Matendo 17:25) Je, huchochewi kumfanyia jambo fulani Yehova Mungu ili kumwonyesha shukrani zako kwa yote ambayo amekufanyia?
Wakimkumbuka Muumba wao, vijana wengi ambao ni Mashahidi wa Yehova wameamua kumtumikia wakati wote. Fikiria utumishi mbalimbali wenye kusisimua unaoweza kufanya.
Upainia. Mapainia wa kawaida hutumia muda mwingi katika huduma. Kupitia mazoezi na uzoefu, wameboresha stadi zao wakiwa walimu wa Biblia.
Kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. Wengine wamehamia sehemu ambazo zina watangazaji wachache wa Ufalme. Wengine hujifunza lugha mpya na kutumikia katika kutaniko la lugha ya kigeni au hata kuhamia nchi ya kigeni.a
Utumishi wa umishonari. Mapainia wanaostahili wenye afya nzuri na nguvu huzoezwa ili wakatumikie katika nchi za kigeni. Wamishonari huishi maisha yenye kusisimua na yenye kusudi.
Utumishi wa Betheli. Washiriki wa familia ya Betheli hutumikia katika ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Katika nchi fulani kazi hiyo hutia ndani kuchapisha na kusafirisha vitabu na magazeti ya Biblia.
Utumishi wa kimataifa. Watumishi wa kimataifa husafiri kwenda nchi nyingine ili kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya ofisi za tawi.
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Wazee na watumishi wa huduma waseja wanaostahili huzoezwa kushughulikia mambo ya tengenezo na kutoa hotuba. Ndugu fulani waliozoezwa hupata mgawo wa kwenda nchi nyingine.
Kupanga Safari Yako
Utumishi wa wakati wote ni mradi mzuri, nao huleta baraka nyingi. Hata hivyo, utahitaji kufikiria na kupanga mapema. Kwa mfano, jiulize, ‘Nina uwezo na stadi gani zitakazoniwezesha kujitegemeza mwenyewe?’
Kelly alitaka sana kuwa painia, kwa hiyo alipanga kazi atakayofanya. “Nilihitaji kuchagua kazi ambayo ingeniruhusu kujitegemeza mwenyewe huku nikiendelea na huduma yangu,” anasema.
Kelly alipata mafunzo kupitia programu ya mafunzo ya kazi hususa alipokuwa katika shule ya sekondari. Hilo lilimwezesha kufikia mradi wake. “Nilitaka kufanya utumishi wa wakati wote,” asema Kelly. “Mambo mengine yote yalikuwa sehemu ya pili.” Kelly anafurahia uamuzi huo. “Naona kwamba nilifanya uamuzi bora zaidi,” anasema.
Omba Maelekezo
Ikiwa unatembea katika eneo geni, haikosi wakati fulani utahitaji kuomba maelekezo. Unaweza kufanya vivyo hivyo unapopanga maisha yako ya wakati ujao. Omba ushauri kutoka kwa wengine. Andiko la Methali 20:18 linasema: “Kwa shauri mipango yenyewe hufanywa imara.”
Wazazi wako wanaweza kukusaidia sana. Unaweza pia kuomba ushauri kutoka kwa Wakristo wakomavu ambao maisha yao yanaonyesha kwamba wamepata hekima inayotoka kwa Mungu. “Tafuta watu wazima walio mifano mizuri katika kutaniko lenu au makutaniko yaliyo karibu,” anapendekeza Roberto, Mwanabetheli aliye na umri wa miaka 20 na kitu.
Zaidi ya wote, Yehova Mungu anataka kukusaidia ufanye maamuzi maishani yatakayokuletea furaha nyingi. Kwa hiyo, mwombe akusaidie ‘uendelee kufahamu yale yaliyo mapenzi yake’ kuhusu wakati wako ujao. (Waefeso 5:17) Katika kila sehemu ya maisha yako, fuata himizo la Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”
Unaweza kupata habari zaidi kwa kutazama DVD yenye kichwa: “Young People Ask—What Will I Do With My Life?” Inapatikana katika lugha zaidi ya 30
[Maelezo ya Chini]
MAANDIKO MUHIMU
“‘Mnijaribu . . . ,’ Yehova wa majeshi amesema, ‘kama sitawafungulia ninyi malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’”—Malaki 3:10.
PENDEKEZO
Zungumza na wale ambao wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa muda mrefu. Waulize ni kwa nini walichagua kufanya hivyo na wamepata baraka gani.
JE, WAJUA . . .?
Umeme unaweza kuendesha chombo. Vivyo hivyo, roho takatifu ya Mungu inaweza kukuchochea kutimiza mengi katika utumishi wake.—Matendo 1:8.
HATUA ZA KUCHUKUA!
Ili niwe na shangwe zaidi katika huduma, nitazungumza na ․․․․․
Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․
UNA MAONI GANI?
● Una vipawa na ujuzi gani?
● Unaweza kutumia vipawa vyako jinsi gani ili kumsifu Yehova?
● Ni utumishi gani wa wakati wote uliotajwa katika makala hii unaokuvutia zaidi?
[Blabu katika ukurasa wa 313]
‘‘Nawaheshimu sana wazazi wangu. Bidii yao katika huduma, jinsi ambavyo wamekabiliana na hali ngumu ya kiuchumi, na jinsi walivyonitia moyo nishiriki katika huduma ya wakati wote, yote hayo yalinichochea sana.’’—Jarrod
[Sanduku katika ukurasa wa 314]
Ukurasa wa Mazoezi
Miradi Yangu
Tia alama miradi ambayo ungependa kujiwekea. Tumia nafasi zilizoandaliwa kuongeza miradi mingine ambayo ungependa kuifikia.
Miradi ya Huduma
□ Kuongeza wakati ninaotumia katika huduma kufikia saa ․․․․․ kila mwezi
□ Kuwaachia watu vitabu, magazeti, na vijitabu ․․․․․ kila mwezi
□ Kutumia Biblia ninapozungumzia imani yangu
□ Kufanya ziara za kurudia ․․․․․ kila mwezi
□ Kuanzisha funzo la Biblia
Miradi mingine: ․․․․․
Miradi ya Kujifunza
□ Kusoma kurasa ․․․․․ za Biblia kila siku
□ Kutayarisha mikutano ya kila juma
□ Kufanya utafiti kuhusu habari zifuatazo za Biblia: ․․․․․
Miradi ya Kutimiza Kutanikoni
□ Kutoa angalau maelezo mara moja katika kila mkutano
□ Kuanzisha mazungumzo pamoja na mtu mwenye umri mkubwa ambaye ningependa kumfahamu vizuri
□ Kumtembelea mshiriki wa kutaniko aliye mzee kwa umri au dhaifu kimwili
Miradi mingine: ․․․․․
Tarehe ya Leo ․․․․․
Baada ya miezi sita, chunguza uone umepiga hatua kiasi gani katika kutimiza miradi yako. Fanya mabadiliko au uongeze miradi mingine kulingana na uhitaji.
[Picha katika ukurasa wa 312]
Kuwa na miradi kutakuzuia usipoteze nguvu zako bure na hivyo kutofika popote
-