Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Somo la 31. Yesu Kristo Mfalme aliye mbinguni akiwa mbele ya utukufu wa Yehova.

      SOMO LA 31

      Ufalme wa Mungu Ni Nini?

      Ufalme wa Mungu ndio ujumbe muhimu zaidi katika Biblia. Yehova atatumia Ufalme huo kutimiza kusudi lake la mwanzoni la kuifanya dunia iwe paradiso. Ufalme huo ni nini? Tunajuaje kwamba umeanza kutawala? Ufalme huo umetimiza mambo gani? Na utatimiza mambo gani wakati ujao? Maswali hayo yatajibiwa katika somo hili na masomo mawili yanayofuata.

      1. Ufalme wa Mungu ni nini, na Mfalme wake ni nani?

      Ufalme huo ni serikali iliyoanzishwa na Yehova Mungu mwenyewe. Mfalme wa Ufalme huo ni Yesu Kristo, na anatawala kutoka mbinguni. (Mathayo 4:17; Yohana 18:36) Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Atatawala akiwa Mfalme . . . milele.” (Luka 1:32, 33) Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu atatawala watu wote duniani.

      2. Ni nani wanaotawala pamoja na Yesu?

      Yesu anatawala pamoja na wengine. “Watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa . . . watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10) Ni watu wangapi watakaotawala pamoja na Kristo? Tangu Yesu alipokuja duniani, mamilioni ya watu wamekuwa wafuasi wake. Lakini watu 144,000 ndio tu wanaoenda mbinguni kutawala pamoja na Yesu. (Soma Ufunuo 14:1-4.) Wakristo wengine wote walio duniani watakuwa raia wa Ufalme huo.​—Zaburi 37:29.

      3. Kwa nini Ufalme wa Mungu ni bora kuliko serikali za wanadamu?

      Ingawa watawala wa serikali za wanadamu wanajitahidi kufanya mambo mazuri, hawana uwezo wa kufanya mambo yote wanayotaka. Baada ya kipindi chao cha kutawala kwisha, huenda watawala wengine wabinafsi wakaanza kutawala na hawawajali raia wao. Lakini kuhusu Yesu Mtawala wa Ufalme wa Mungu, hakuna mtawala mwingine atakayechukua nafasi yake. Mungu “[ameusimamisha] ufalme ambao hautaangamizwa kamwe.” (Danieli 2:44) Yesu atatawala dunia yote, na hatakuwa na ubaguzi. Yesu ni mwenye upendo, fadhili, na haki, naye atawafundisha watu kuwatendea wengine kwa njia hiyohiyo, yaani, kwa upendo, fadhili, na haki.​—Soma Isaya 11:9.

      CHIMBA ZAIDI

      Chunguza uone kwa nini Ufalme wa Mungu ni serikali bora kuliko serikali zote za wanadamu.

      Yesu Kristo akiitawala dunia akiwa kwenye kiti chake cha ufalme mbinguni. Watawala wenzake wameketi nyuma yake. Nuru ya Yehova inaangaza nyuma yao.

      4. Serikali yenye nguvu itaitawala dunia yote

      Yesu Kristo ana nguvu nyingi sana za kutawala kuliko mtawala yeyote katika historia. Soma Mathayo 28:18, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kwa nini Yesu ana mamlaka kubwa zaidi kuliko mtawala yeyote wa serikali za wanadamu?

      Serikali za wanadamu hubadilika-badilika, na kila serikali hutawala sehemu fulani ya dunia. Namna gani Ufalme wa Mungu? Soma Danieli 7:14, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Kwa nini inafurahisha kujua kwamba Ufalme wa Mungu “hautaangamizwa”?

      • Kwa nini tunafurahi kujua kwamba utaitawala dunia yote?

      5. Ni lazima serikali za wanadamu ziondolewe

      Kwa nini ni lazima Ufalme wa Mungu uondoe serikali za wanadamu? Onyesha video, kisha mzungumzie swali linalofuata.

      VIDEO: Ufalme wa Mungu Ni Nini?​—Kisehemu (1:41)

      • Utawala wa serikali za wanadamu umekuwa na matokeo gani?

      Soma Mhubiri 8:9, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Je, unafikiri Ufalme wa Mungu unapaswa kuondoa serikali za wanadamu? Kwa nini?

      6. Watawala wa Ufalme wa Mungu wanaelewa hali yetu

      Kwa kuwa Mfalme wetu, Yesu, aliwahi kuwa mwanadamu, anaweza ‘kuusikitikia udhaifu wetu.’ (Waebrania 4:15) Wanaume na wanawake waaminifu 144,000 ambao watatawala pamoja na Yesu wamechaguliwa na Yehova “kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa.”​—Ufunuo 5:9.

      • Je, unafarijika kujua kwamba Yesu na watawala wenzake wanaelewa hali za wanadamu? Kwa nini?

      Wanaume na wanawake watiwa mafuta kutoka malezi mbalimbali ambao waliishi katika vipindi tofauti.

      Yehova amewachagua wanaume na wanawake kutoka katika malezi mbalimbali watawale pamoja na Yesu

      7. Sheria za Ufalme wa Mungu ni bora zaidi

      Serikali huweka sheria ambazo zimekusudiwa kuwanufaisha na kuwalinda raia wake. Ufalme wa Mungu pia una sheria ambazo zinapaswa kufuatwa na raia wake. Soma 1 Wakorintho 6:9-11, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Unafikiri ulimwengu utakuwaje kila mtu atakapofuata sheria za Mungu?a

      • Je, unafikiri Yehova ana haki ya kuwawekea sheria raia wa Ufalme wake? Kwa nini?

      • Ni nini kinachoonyesha kwamba watu ambao hawafuati sheria hizo wanaweza kubadilika?​—Ona mstari wa 11.

      Polisi akielekeza magari barabarani. Watu wenye umri mbalimbali wakivuka barabara.

      Serikali huweka sheria ili kuwalinda na kuwanufaisha raia wake. Ufalme wa Mungu una sheria bora zinazowalinda na kuwanufaisha raia wake

      HUENDA MTU AKAULIZA: “Ufalme wa Mungu ni nini?”

      • Unawezaje kujibu swali hilo?

      MUHTASARI

      Ufalme wa Mungu ni serikali halisi iliyo mbinguni ambayo itaitawala dunia yote.

      Ungejibuje?

      • Watawala wa Ufalme wa Mungu ni nani?

      • Kwa nini Ufalme wa Mungu ni bora kuliko serikali zote za wanadamu?

      • Yehova anatarajia raia wa Ufalme wake wafanye mambo gani?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Chunguza uone Yesu alisema utawala wa Mungu utatawala kutokea wapi.

      “Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanachagua kuwa washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu badala ya serikali za wanadamu?

      Kuunga Mkono Ufalme wa Mungu (1:43)

      Chunguza jinsi Biblia inavyofafanua wale 144,000 ambao wamechaguliwa na Yehova kutawala pamoja na Yesu.

      “Ni Nani Wanaoenda Mbinguni?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Ni nini kilichomsadikishia mwanamke aliyekuwa gerezani kwamba Mungu peke yake ndiye anayeweza kuleta ulimwengu wenye haki?

      “Jinsi Nilivyopata Suluhisho la Ukosefu wa Haki” (Amkeni!, Novemba 2011)

      a Baadhi ya sheria hizo zitazungumziwa katika Sehemu ya 3.

  • Ufalme wa Mungu Umeanza Kutawala!
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Somo la 32. Yesu Kristo Mfalme aliye mbinguni akiwa ameshika fimbo ya utawala akiitawala dunia.

      SOMO LA 32

      Ufalme wa Mungu Umeanza Kutawala!

      Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni mwaka wa 1914. Pia, siku za mwisho za utawala wa wanadamu zilianza mwaka huo. Tunajuaje? Tutachunguza mambo ambayo Biblia ilitabiri, hali zinazoendelea ulimwenguni leo, na jinsi ambavyo watu wamekuwa wakitenda tangu mwaka wa 1914.

      1. Biblia ilitabiri nini?

      Kitabu cha Biblia cha Danieli kinaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala mwishoni mwa kipindi kinachoitwa “nyakati saba.” (Danieli 4:16, 17) Karne nyingi baadaye, Yesu alisema kipindi hicho kinaitwa “nyakati zilizowekwa za mataifa,” na alifundisha kwamba bado kilikuwa kinaendelea. (Luka 21:24) Kama tutakavyoona, zile nyakati saba ziliisha mwaka wa 1914.

      2. Tangu mwaka wa 1914, hali zimekuwaje na watu wamekuwa wakitendaje?

      Wanafunzi wa Yesu walimwuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Yesu aliwajibu kwa kutabiri mambo mengi ambayo yangetokea wakati ambapo angeanza kutawala mbinguni akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Baadhi ya mambo aliyotaja ni vita, upungufu wa chakula, na matetemeko ya ardhi. (Soma Mathayo 24:7.) Pia, Biblia ilitabiri kwamba tabia za watu katika “siku za mwisho” zingefanya hali ziwe “ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Hali na tabia hizo zimeonekana waziwazi hasa tangu mwaka wa 1914.

      3. Kwa nini hali zimekuwa mbaya sana tangu Ufalme wa Mungu ulipoanza kutawala?

      Muda mfupi baada ya kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu alipigana vita mbinguni dhidi ya Shetani na roho waovu. Shetani alishindwa katika vita hivyo. Biblia inasema: “[alitupwa] chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.” (Ufunuo 12:9, 10, 12) Shetani ana hasira kali kwa sababu anajua kwamba ataangamizwa. Kwa hiyo, anasababisha maumivu na kuteseka ulimwenguni pote. Ndiyo sababu hali ni mbaya sana ulimwenguni! Ufalme wa Mungu utaondoa matatizo hayo yote.

      CHIMBA ZAIDI

      Chunguza kwa nini tunaamini kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mwaka wa 1914 na jinsi hilo linavyotuhusu.

      4. Mfuatano wa matukio katika Biblia unaongoza kwenye mwaka wa 1914

      Onyesha VIDEO.

      VIDEO: Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Mwaka wa 1914 (5:03)

      Mungu alifanya Mfalme Nebukadneza wa jiji la kale la Babiloni aote ndoto ya kinabii. Ndoto hiyo na ufafanuzi wa Danieli unahusu utawala wa Nebukadneza na Ufalme wa Mungu.​—Soma Danieli 4:17.a

      Soma Danieli 4:20-26, kisha utumie chati kujibu maswali yanayofuata:

      • (A) Nebukadneza aliona nini katika ndoto yake?​—Ona mstari wa 20 na 21.

      • (B) Ni nini kingeupata mti?​—Ona mstari wa 23.

      • (C) Ni nini kingetokea baada ya zile “nyakati saba” kwisha?​—Ona mstari wa 26.

      Jinsi Ile Ndoto ya Mti Inavyohusiana na Ufalme wa Mungu

      UNABII (Danieli 4:20-36)

      Utawala

      (A) Mti mkubwa sana

      Mti mrefu sana.

      Utawala wakatizwa

      (B) “Ukateni na kuuangusha mti” na acheni “nyakati saba zipite”

      Kisiki cha mti kilichofungwa kwa pingu ya chuma na shaba.

      Utawala warudishwa

      (C) “Utarudishiwa tena ufalme wako”

      Mti mrefu sana.

      Katika utimizo wa kwanza wa unabii huu . . .

      • (D) Mti ulimwakilisha nani?​—Ona mstari wa 22.

      • (E) Utawala wake ulikatizwa jinsi gani?​—Soma Danieli 4:29-33.

      • (F) Ni nini kilichompata Nebukadneza baada ya “nyakati saba” kwisha?​—Soma Danieli 4:34-36.

      UTIMIZO WA KWANZA

      Utawala

      (D) Nebukadneza, Mfalme wa Babiloni

      Mfalme Nebukadneza akiwa amesimama kwa kiburi.

      Utawala wakatizwa

      (E) Baada ya mwaka wa 606 K.W.K., Nebukadneza arukwa na akili na anashindwa kutawala kwa miaka saba

      Nebukadneza akiwa amelala chini akila nyasi kama mnyama.

      Utawala warudishwa

      (F) Nebukadneza arudiwa na fahamu na anaanza kutawala tena

      Mfalme Nebukadneza akitazama mbinguni akiwa ameinua mikono.

      Katika utimizo wa pili wa unabii huu . . .

      • (G) Mti huo uliwakilisha nani?​—Soma 1 Mambo ya Nyakati 29:23.

      • (H) Utawala wao ulikatizwaje? Tunajuaje kwamba bado utawala wao ulikuwa umekatizwa Yesu alipokuwa duniani?​—Soma Luka 21:24.

      • (I) Utawala huo ulirudishwa lini na wapi?

      UTIMIZO WA PILI

      Utawala

      (G) Wafalme Waisraeli ambao waliwakilisha utawala wa Mungu

      Mfuatano wa wafalme wa Israeli wakiwa wameketi kwenye viti vya ufalme. Mwangaza kutoka juu unawamulika.

      Utawala wakatizwa

      (H) Yerusalemu laharibiwa na kukatiza utawala wa wafalme Waisraeli kwa miaka 2,520

      Moto ukiteketeza jiji la kale la Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Baadaye, miaka 2,520 inapita.

      Utawala warudishwa

      (I) Yesu aanza kutawala mbinguni akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu

      Yesu akiitawala dunia akiwa kwenye kiti chake cha ufalme mbinguni tangu mwaka wa 1914 W.K. Nuru inaangaza kutoka kwake.

      Zile nyakati saba zina urefu gani?

      Baadhi ya mistari ya Biblia hueleweka kwa kuchunguza mistari mingine ya Biblia. Kwa mfano, kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinasema kwamba nyakati tatu na nusu ni sawa na siku 1,260. (Ufunuo 12:6, 14) Nyakati saba ni mara mbili ya nyakati tatu na nusu, yaani, siku 2,520. Nyakati nyingine, Biblia hutumia siku moja kuwakilisha mwaka mmoja. (Ezekieli 4:6) Ndivyo ilivyo kuhusu zile nyakati saba zinazotajwa katika kitabu cha Danieli, zinawakilisha miaka 2,520.

      5. Ulimwengu umebadilika tangu mwaka wa 1914

      Onyesha VIDEO.

      VIDEO: Ulimwengu Umebadilika Tangu Mwaka wa 1914 (1:10)

      Yesu alitabiri kuhusu hali ambazo zingekuwa ulimwenguni wakati ambapo angeanza kutawala. Soma Luka 21:9-11, kisha mzungumzie swali hili:

      • Umesikia au kujionea nini kati ya mambo hayo yaliyotabiriwa?

      Mtume Paulo alifafanua jinsi ambavyo watu wangetenda wakati wa siku za mwisho za utawala wa wanadamu. Soma 2 Timotheo 3:1-5, kisha mzungumzie swali hili:

      • Umejionea watu wakiwa na tabia gani kati ya tabia hizo?

      Picha: Picha zinazoonyesha hali za ulimwengu na tabia za watu katika siku za mwisho. 1. Kiongozi wa jeshi akihutubu jukwaani kwa sauti kubwa akiwa ameinua mikono. 2. Majengo yaliyobomoka baada ya tetemeko la ardhi. 3. Ndege za vita. 4. Watu waliovaa barakoa wakitembea. 5. Majengo mawili jijini New York yanawaka moto baada ya shambulizi la kigaidi. 6. Mwanamume akitumia dawa za kulevya. 7. Mume akiwa amekunja ngumi akimgombeza mke wake. 8. Pombe na dawa mbalimbali za kulevya. 9. Wanawake wawili waliovaa mavazi ya kisasa na mapambo ya thamani wakijipiga picha. 10. Mtumbuizaji anatumbuiza umati wa watu. 11. Mwandamanaji akirusha bomu la petroli.

      6. Utawala wa Ufalme wa Mungu unapaswa kutuchochea kutenda

      Soma Mathayo 24:3, 14, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Ni kazi gani muhimu inayoonyesha kwamba Ufalme wa Mungu unatawala?

      • Unawezaje kushiriki kufanya kazi hiyo?

      Sasa Ufalme wa Mungu unatawala, na hivi karibuni utaitawala dunia yote. Soma Waebrania 10:24, 25, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kila mmoja wetu anapaswa kufanya nini ‘kadiri tunavyoona siku ile ikikaribia’?

      Picha: 1. Mwanafunzi wa Biblia akiwa amehudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova. 2. Mwanafunzi huyo wa Biblia anamhubiria mtu anayemfahamu.

      Unapojifunza jambo linaloweza kuwasaidia au kuwaokoa wengine, unapaswa kufanya nini?

      HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanasema mwaka wa 1914 ni muhimu sana?”

      • Wewe ungesemaje?

      MUHTASARI

      Unabii wa Biblia, mfuatano wa matukio, na hali zilizo ulimwenguni zinathibitisha kwamba sasa Ufalme wa Mungu unatawala. Tunaonyesha kwamba tunaamini hilo kwa kuhubiri kuhusu Ufalme na kuhudhuria mikutano ya kutaniko.

      Ungejibuje?

      • Ni nini kilichotokea baada ya nyakati saba zilizotabiriwa katika kitabu cha Biblia cha Danieli?

      • Ni nini kinachokuthibitishia kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mwaka wa 1914?

      • Unaweza kuonyeshaje kwamba unaamini Ufalme wa Mungu unatawala?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Chunguza mambo ambayo wanahistoria na watu wengine husema kuhusu mabadiliko ulimwenguni tangu mwaka wa 1914.

      “Maadili Yalipoporomoka Ghafula” (Amkeni!, Aprili 2007)

      Soma uone jinsi unabii ulio katika Mathayo 24:14 ulivyobadili maisha ya mwanamume fulani.

      “Nilipenda Mchezo wa Besiboli Kuliko Kitu Kingine Chochote!” (Mnara wa Mlinzi, Na. 3 2017)

      Tunajuaje kwamba unabii ulio katika Danieli sura ya 4 unahusu Ufalme wa Mungu?

      “Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini? (Sehemu ya 1)” (Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 2014)

      Ni nini kinachoonyesha kwamba nyakati saba zinazotajwa katika Danieli sura ya 4 ziliisha mwaka wa 1914?

      “Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini? (Sehemu ya 2)” (Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 2014)

      a Ona makala mbili za mwisho kwenye sehemu ya Chunguza Zaidi katika somo hili.

  • Ufalme wa Mungu Utatimiza Nini?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Somo la 33. Watu wakiishi katika paradiso duniani.

      SOMO LA 33

      Ufalme wa Mungu Utatimiza Nini?

      Tayari Ufalme wa Mungu umeanza kutawala. Hivi karibuni utafanya mabadiliko makubwa duniani. Tutachunguza baadhi ya mambo mazuri ambayo tunatazamia kufurahia chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.

      1. Ufalme wa Mungu utaletaje amani na haki duniani?

      Yesu, Mfalme wa Ufalme wa Mungu, atawaangamiza watu waovu na serikali zote katika vita vya Har–​Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Wakati huo, ahadi hii ya Biblia itatimizwa kikamili: “Bado muda mfupi tu, na watu waovu hawatakuwepo tena.” (Zaburi 37:10) Kupitia Ufalme huo, Yesu atahakikisha kwamba kuna amani na haki duniani pote.​—Soma Isaya 11:4.

      2. Maisha yatakuwaje mapenzi ya Mungu yatakapotimizwa duniani?

      Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, “waadilifu wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.” (Zaburi 37:29) Wazia kuishi katika ulimwengu ambao kila mtu ni mwadilifu, watu wote wanampenda Yehova na wanapendana! Watu hawatakuwa wagonjwa tena, na kila mtu ataishi milele.

      3. Ufalme wa Mungu utatimiza nini baada ya waovu kuangamizwa?

      Baada ya waovu kuangamizwa, Yesu atatawala akiwa Mfalme kwa miaka elfu moja. Wakati huo, Yesu na watawala wenzake 144,000 watawasaidia wanadamu walio duniani kuwa wakamilifu na wasio na dhambi. Mwishoni mwa kipindi hicho, dunia itakuwa paradiso maridadi, na watu wote watakuwa na furaha kwa sababu ya kutii sheria za Yehova. Kisha Yesu atamrudishia utawala Yehova Baba yake. Wakati huo, ‘jina la Yehova litakuwa limetakaswa’ kikamili. (Mathayo 6:9, 10) Yehova atakuwa amethibitika kuwa Mtawala mzuri anayewajali raia wake. Kisha Yehova atamwangamiza Shetani, roho waovu, na watu wengine watakaoasi utawala wa Mungu. (Ufunuo 20:7-10) Hali kamilifu zitakazoletwa na Ufalme wa Mungu zitadumu milele.

      CHIMBA ZAIDI

      Chunguza kwa nini tunaweza kuamini kwamba Mungu atatumia Ufalme kutimiza ahadi zote zilizo katika Biblia kuhusu wakati ujao.

      4. Ufalme wa Mungu utakomesha serikali za wanadamu

      “Mwanadamu amemtawala mwanadamu mwenzake kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Kupitia Ufalme wake, Yehova ataondoa ukosefu huo wa haki.

      Soma Danieli 2:44 na 2 Wathesalonike 1:6-8, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Yehova na Mwana wake, Yesu, watachukua hatua gani dhidi ya serikali za wanadamu na wale wanaoziunga mkono?

      • Mambo ambayo umejifunza kumhusu Yehova na Yesu yanakuhakikishiaje kwamba watatenda kwa haki na bila upendeleo?

      Yesu Mfalme aliye mbinguni akiitawala dunia.

      5. Yesu ndiye Mfalme bora

      Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu atafanya mambo mengi ili kuwasaidia raia wake. Onyesha VIDEO ili uone kwamba Yesu amethibitisha anatamani kuwasaidia watu na Mungu amempa nguvu za kufanya hivyo.

      VIDEO: Yesu Alionyesha Mambo Ambayo Ufalme Utatimiza (1:13)

      Yesu alipokuwa duniani, alionyesha mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza. Kati ya baraka zilizoonyeshwa, ni baraka gani unayotazamia kwa hamu? Soma Maandiko yaliyoonyeshwa ili kujifunza mengi kuhusu baraka hizo.

      YESU ALIPOKUWA DUNIANI . . .

      YESU AKIWA MBINGUNI . . .

      • alikuwa na nguvu za kudhibiti hali ya hewa.​—Marko 4:36-41.

      • ataondoa uchafuzi wa mazingira duniani.​—Isaya 35:1, 2.

      • alilisha maelfu ya watu kimuujiza.​—Mathayo 14:17-​21.

      • ataondoa tatizo la njaa ulimwenguni.​—Zaburi 72:16.

      • aliponya watu wenye magonjwa mbalimbali.​—Luka 18:35-43.

      • atahakikisha watu wote wana afya kamilifu.​—Isaya 33:24.

      • aliwafufua watu waliokufa.​—Luka 8:49-55.

      • ataondoa madhara yanayosababishwa na kifo.​—Ufunuo 21:3, 4.

      6. Ufalme wa Mungu utaleta wakati ujao ulio bora

      Ufalme wa Mungu utatimiza kikamili kusudi ambalo Yehova alikuwa nalo mwanzoni kuelekea wanadamu. Wanadamu wataishi milele katika paradiso duniani. Onyesha VIDEO ili uone jinsi Yehova anavyomtumia Mwana wake, Yesu, kutimiza kusudi lake.

      VIDEO: Kionjo cha Wakati Ujao Wenye Kupendeza (4:35)

      Soma Zaburi 145:16, kisha mzungumzie swali hili:

      • Unahisije kujua kwamba Yehova “[atatosheleza] tamaa ya kila kitu kilicho hai”?

      WATU FULANI HUSEMA: “Ikiwa wanadamu wote watashirikiana, tunaweza kutatua matatizo ulimwenguni.”

      • Ufalme wa Mungu utatatua matatizo gani ambayo serikali za wanadamu zimeshindwa kutatua?

      MUHTASARI

      Ufalme wa Mungu utatimiza malengo yake yote. Utaifanya dunia yote kuwa paradiso iliyojaa watu wema watakaomwabudu Yehova milele.

      Ungejibuje?

      • Ufalme wa Mungu utalitakasaje jina la Yehova?

      • Kwa nini tunaweza kuamini kwamba Ufalme wa Mungu utatimiza ahadi zilizo katika Biblia?

      • Ni jambo gani unalotazamia kwa hamu kati ya mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Jifunze maana ya Har–Magedoni.

      “Vita vya Har–Magedoni Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Chunguza kile kitakachotukia katika kipindi ambacho Yesu alikiita “dhiki kuu.”—Mathayo 24:21.

      “Dhiki Kuu Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Ona jinsi familia zinavyoweza kutafakari pamoja kuhusu baraka za wakati ujao za Ufalme wa Mungu.

      Jiwazie Ukiwa Katika Paradiso (1:50)

      Katika makala “Nilikuwa na Maswali Mengi Yaliyonisumbua,” ona jinsi mwasi wa kisiasa alivyopata majibu ya maswali yaliyokuwa yakimhangaisha.

      “Biblia Inabadili Maisha” (Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 2012)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki