Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Hadithi ya Kwanza ya Uwongo: Nafsi Haifi
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Novemba 1
    • Hadithi ya Kwanza ya Uwongo: Nafsi Haifi

      Ni nini chanzo cha hadithi hiyo? “Wanafalsafa wa mapema ambao walikuwa Wakristo walikubali fundisho la Wagiriki la kwamba nafsi haiwezi kufa na walifikiri kwamba nafsi inaumbwa na Mungu na kutiwa ndani ya mwili wakati wa kuzaliwa.”—The New Encyclopædia Britannica (1988), Buku la 11, ukurasa wa 25.

      Biblia inasema nini? “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.”—Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible.

      Kuhusu kuumbwa kwa nafsi ya kwanza ya mwanadamu, Biblia inasema hivi: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai [Kiebrania, neʹphesh].”—Mwanzo 2:7.

      Neno la Kiebrania neʹphesh, linalotafsiriwa “nafsi,” linamaanisha ‘kiumbe kinachopumua.’ Mungu alipomuumba mwanadamu wa kwanza Adamu, hakutia ndani ya mwanadamu huyo nafsi isiyoweza kufa lakini alitia ndani yake nguvu ya uhai ambayo inaendelezwa kwa kupumua. Kwa hiyo, neno “nafsi” katika Biblia linamaanisha kwa ujumla kiumbe hai. Nafsi ikitenganishwa na nguvu ya uhai ambayo ilitoka kwa Mungu, nafsi hiyo inakufa.—Mwanzo 3:19; Ezekieli 18:20.

      Fundisho la kwamba nafsi haifi linatokeza maswali: Nafsi zinaenda wapi baada ya kifo? Nafsi za waovu zinapatwa na nini? Wakati watu waliodai kuwa Wakristo walipokubali hadithi ya uwongo ya kwamba nafsi haifi, hilo liliwafanya wakubali hadithi nyingine ya uwongo, yaani, fundisho la moto wa mateso.

      Linganisha mistari hii ya Biblia: Mhubiri 3:19; Mathayo 10:28; Matendo 3:23

      UKWELI:

      Baada ya kifo mtu haendelei kuishi

  • Hadithi ya Pili ya Uwongo: Waovu Wanateseka Katika Moto wa Mateso
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Novemba 1
    • Hadithi ya Pili ya Uwongo: Waovu Wanateseka Katika Moto wa Mateso

      Ni nini chanzo cha hadithi hiyo? “Kati ya wanafalsafa wote Wagiriki wanaojulikana sana, yule aliyechochea sana mapokeo kuhusu Moto wa Mateso ni Plato.”—Histoire des enfers (Historia ya Moto wa Mateso), kilichoandikwa na Georges Minois, ukurasa wa 50.

      “Kuanzia katikati ya karne ya 2 AD Wakristo ambao walijifunza kwa kadiri fulani falsafa za Kigiriki walianza kuona uhitaji wa kueleza imani yao kwa kutumia falsafa hizo . . . Falsafa ambayo iliwafaa zaidi ilikuwa ile ya Plato [mafundisho ya Plato].”—The New Encyclopædia Britannica (1988), Buku la 25, ukurasa wa 890.

      “Mafundisho ya Kanisa yanathibitisha kwamba kuna moto wa mateso na ni wa milele. Mara tu baada ya kifo, nafsi za wale wanaokufa katika dhambi zinaenda kuzimu [moto wa mateso], mahali ambapo zinateswa kwa kuadhibiwa katika ‘moto wa milele.’ Adhabu kubwa ya kuzimu ni kutengwa milele na Mungu.”—Catechism of the Catholic Church (Katekisimu ya Kanisa Katoliki), chapa ya 1994, ukurasa wa 270.

      Biblia inasema nini? “Maana walio hai wanajua ya kwamba watakufa: lakini wafu hawajui kitu, . . . maana hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima ndani ya kaburi [Sheol au kuzimu], pahali unapokwenda.”—Mhubiri 9:5, 10, Zaire Swahili Bible.

      Neno la Kiebrania Sheol, ambalo linamaanisha “makao ya wafu,” linatafsiriwa kuwa “kuzimu” katika tafsiri fulani za Biblia. Andiko hilo linafunua nini kuhusu hali ya wafu? Je, wanateseka ndani ya Sheol ili walipie makosa yao? Hapana, kwa sababu “hawajui kitu.” Ndiyo sababu mzee wa ukoo Ayubu, alipokuwa akiteseka sana kwa sababu ya ugonjwa mbaya sana, alimwomba Mungu hivi: “Laiti ungenificha kuzimuni [Kiebrania, Sheol].” (Ayubu 14:13; Union Version) Ombi hilo lingekuwa na maana gani ikiwa Sheol au kuzimu ni mahali pa mateso ya milele? Katika Biblia, neno “kuzimu” linamaanisha tu kaburi, mahali ambapo hapana utendaji wowote.

      Je, si kweli kwamba maelezo hayo kuhusu kuzimu yanapatana na akili na ni ya Kimaandiko? Hata hivyo, ni kosa gani baya zaidi ambalo linaweza kumfanya Mungu wa upendo amtese mtu milele? (1 Yohana 4:8) Lakini ikiwa moto wa mateso ni hadithi ya uwongo, namna gani kuhusu mbingu?

      Linganisha mistari hii ya Biblia: Zaburi 146:3, 4; Matendo 2:25-27; Waroma 6:7, 23

      UKWELI:

      Mungu hawaadhibu watu katika moto wa mateso

      [Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

      Barrators—Giampolo/The Doré Illustrations For Dante’s Divine Comedy/Dover Publications Inc.

  • Hadithi ya Tatu ya Uwongo: Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Novemba 1
    • Hadithi ya Tatu ya Uwongo: Watu Wote Wazuri Wanaenda Mbinguni

      Ni nini chanzo cha hadithi hiyo?

      Baada ya kifo cha mitume wa Yesu, mwanzoni mwa karne ya pili W.K., Mababa wa Kanisa wa mapema walipata umaarufu. Kikieleza kuhusu mafundisho yao, kitabu New Catholic Encyclopedia (2003), Buku la 6, ukurasa wa 687, kinasema hivi: “Fundisho lililoenea ni kwamba baada ya kifo nafsi iliyotengana na mwili inaingia papo hapo katika paradiso ya mbinguni baada ya kutakaswa ipasavyo.”

      Biblia inasema nini?

      “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.”—Mathayo 5:5.

      Ingawa Yesu aliwaahidi wanafunzi wake kwamba angeenda ‘kuwatayarishia mahali’ mbinguni, alionyesha kwamba waadilifu hawaendi moja kwa moja mbinguni. (Yohana 3:13; 14:2, 3) Je, hakusali kwamba mapenzi ya Mungu yatendeke “duniani kama ilivyo mbinguni”? (Mathayo 6:9, 10) Kwa kweli, watu waadilifu watapata moja kati ya matumaini hayo. Hesabu ndogo ya waadilifu hao watatawala mbinguni pamoja na Kristo, lakini walio wengi wataishi milele duniani.—Ufunuo 5:10.

      Baadaye, kanisa la mapema lilibadili maoni yake kuhusu daraka lake duniani. Kukawa na matokeo gani? Kitabu The New Encyclopædia Britannica kinasema hivi: “Hatua kwa hatua, kanisa lilichukua mahali pa Ufalme wa Mungu unaotarajiwa.” Kanisa lilianza kuimarisha mamlaka yake kwa kujiingiza katika siasa, na hivyo kupuuza maneno ya waziwazi ya Yesu kwamba wafuasi wake walipaswa kuwa “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19; 17:14-16; 18:36) Chini ya uvutano wa Maliki Mroma Konstantino, kanisa lililegeza mafundisho fulani, kama lile linalohusu utu halisi wa Mungu.

      Linganisha mistari hii ya Biblia: Zaburi 37:10, 11, 29; Yohana 17:3; 2 Timotheo 2:11, 12

      UKWELI:

      Watu wengi wazuri wataishi milele duniani, bali si mbinguni

  • Hadithi ya Nne ya Uwongo: Mungu Ni Utatu
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Novemba 1
    • Hadithi ya Nne ya Uwongo: Mungu Ni Utatu

      Ni nini chanzo cha hadithi hiyo? “Huenda watu wakafikiri kwamba fundisho la Utatu lilianzishwa mwishoni mwa karne ya 4. Kwa njia fulani, hilo ni kweli . . . Fundisho la ‘Mungu mmoja katika Watatu’ halikuwa limetia mizizi, na bila shaka, halikukubalika kabisa katika maisha na imani ya Wakristo kabla ya mwisho wa karne ya 4.”—New Catholic Encyclopedia (1967), Buku la 14, ukurasa wa 299.

      “Baraza la Nisea lilikutana mnamo Mei 20, 325 (20/5/325) [W.K.]. Konstantino mwenyewe alikuwa mwenyekiti, na ndiye aliyeongoza mazungumzo, akapendekeza . . . njia muhimu ya kuonyesha uhusiano kati ya Kristo na Mungu katika fundisho lililotolewa na baraza hilo, kwamba Kristo ‘na Baba ni kitu kimoja.’ . . . Kwa sababu ya kumwogopa maliki au mfalme, maaskofu wote, isipokuwa wawili tu, walitia sahihi hati ya kukubali fundisho hilo, wengi wao walifanya hivyo bila kupenda.”—Encyclopædia Britannica (1970), Buku la 6, ukurasa wa 386.

      Biblia inasema nini? “Akiwa amejaa roho takatifu, [Stefano] akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu, naye akasema: ‘Tazameni! Ninaziona mbingu zimefunguka na Mwana wa binadamu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.’”—Matendo 7:55, 56.

      Maono hayo yalifunua nini? Akiwa amejaa nguvu ya utendaji ya Mungu, Stefano alimwona Yesu “akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” Basi ni wazi kwamba Yesu hakugeuka na kuwa Mungu baada ya kufufuliwa na kwenda mbinguni badala yake, alikuwa mtu wa roho aliye tofauti na Mungu. Simulizi hilo halitaji kwamba kulikuwa na mtu wa tatu kando ya Mungu. Ingawa wanajaribu kutafuta Maandiko yanayounga mkono fundisho la Utatu, padri fulani kutoka Dominika Marie Émile Boismard, aliandika hivi katika kitabu chake À l’aube du christianisme—La naissance des dogmes (Wakati wa Mapambazuko ya Ukristo—Mwanzo wa Mafundisho ya Dini): “Fundisho la kwamba kuna watu watatu katika Mungu mmoja . . . halipatikani mahali popote katika Agano Jipya.”

      Fundisho ambalo lilitetewa na Konstantino lilikusudiwa kukomesha mabishano ndani ya Kanisa la karne ya nne. Hata hivyo, kwa kweli fundisho hilo lilitokeza swala lingine: Je, Maria, mwanamke ambaye alimzaa Yesu, ni “Mama ya Mungu”?

      Linganisha mistari hii ya Biblia: Mathayo 26:39; Yohana 14:28; 1 Wakorintho 15:27, 28; Wakolosai 1:15, 16

      UKWELI:

      Fundisho la Utatu lilianzishwa baadaye katika karne ya nne

      [Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

      Museo Bardini, Florence

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki