GEORGIA | 1924-1990
Mikutano Yawasaidia Wote Kukuza Imani
Mikutano ya Kikristo ilitimiza fungu muhimu katika kuwasaidia wapya kukuza imani. Kwa kweli, Wakristo waliokuwa wamebatizwa kwa muda mfupi walikuwa na hamu ileile ya kukubali mikutano ifanyiwe nyumbani kwao kama Wakristo waliokuwa katika kweli kwa muda mrefu. Wote waliohudhuria walikaribishwa kwa uchangamfu, na hilo liliimarisha upendo wao hata zaidi.
Wanafunzi kadhaa walipokuwa tayari kubatizwa, kwa busara mikutano ya pekee ilifanywa. Katika Agosti 1973, akina ndugu walipanga mkutano huo wa pekee ufanywe karibu na fuo za Bahari Nyeusi, nje ya jiji la Sokhumi. Lakini wanafunzi 35 waliotaka kubatizwa, hawakubatizwa! Kabla ya mkutano kwisha, polisi waliukatiza na kuwakamata baadhi ya ndugu na dada, kutia ndani Vladimir Gladyuk.
Mara tu Vladimir na ndugu wengine walipoachiliwa kutoka gerezani, waliwatafuta tena wanafunzi hao wote waliotaka kubatizwa. Mwishowe, siku mbili baada ya mkutano wa pekee, wanafunzi hao wakabatizwa. Vladimir anakumbuka hivi: “Tulihisi kwamba Yehova anatutegemeza. Baada ya ubatizo, sote tulimshukuru Yehova pamoja.”
Upinzani Wasaidia Kueneza Habari Njema
Siku mbili baada ya ubatizo huo kufanywa, Vladimir Gladyuk alikamatwa tena. Baadaye, yeye, Itta Sudarenko, na Natela Chargeishvili walihukumiwa vifungo vya miaka kadhaa gerezani. Ingawa walisikitishwa na kufungwa kwa ndugu hao, wahubiri waliazimia kuendelea kuhubiri, lakini kwa uangalifu zaidi.
Ili kuepuka kuvuta uangalifu wa wenye mamlaka, badala ya kuhubiri maeneo ya kwao, wahubiri walisafiri kwenye miji na vijiji vya mbali ili kuhubiri. Kwa sababu hiyo, upinzani ulisaidia kueneza habari njema katika maeneo mengi hata zaidi.
Wakati wa utawala wa Kikomunisti, wahubiri walioishi katika majiji makubwa walihubiri kwenye mitaa na bustani zilizokuwa na watu wachache. Kwa kawaida, walikutana na watu waliokuja kutoka majiji na vijiji vingine ili kuwatembelea watu wa ukoo au kununua bidhaa. Mtu alipopendezwa, wahubiri walimwomba maelekezo ya kufika kwake na kufanya mipango ya kukutana tena.
Babutsa Jejelava alikuwa miongoni mwa wahubiri waliosafiri sana kotekote katika maeneo ya magharibi mwa Georgia. Anakumbuka hivi: “Kwa kuwa nilikuwa na watu wa ukoo katika maeneo mbalimbali, hakuna mtu aliyenishuku niliposafiri mara kwa mara katika maeneo hayo. Baada ya miaka miwili hivi, nilikuwa nikijifunza Biblia na watu zaidi ya 20 huko Zugdidi na wengine 5 katika mji wa Chkhorotsku. Wote walibatizwa mwishowe.”
Uhitaji Mkubwa wa Machapisho ya Kigeorgia
Baada ya muda mfupi, ilikuwa wazi kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa wa machapisho katika Kigeorgia. Walipofanya ziara za kurudia au kuongoza mafunzo ya Biblia, wahubiri waligundua kwamba kulikuwa na uhitaji wa Biblia na machapisho ya Biblia katika lugha ambayo wanafunzi wangeelewa vizuri.a
Babutsa anakumbuka jinsi ilivyokuwa vigumu kuongoza funzo la Biblia bila machapisho yoyote katika Kigeorgia. Anasema hivi, “Nilikuwa na Biblia na machapisho katika Kirusi tu, kwa hiyo mara nyingi ilibidi niwatafsirie wanafunzi wa Biblia habari tutakazojifunza.” Akitumia kamusi peke yake, alitafsiri makala za magazeti yetu katika Kigeorgia. Pia, alifaulu kutafsiri Injili yote ya Mathayo!
Mashahidi wenye ujasiri walitumia mashine ndogo za kunakili ili kuchapisha machapisho nyumbani kwao
Watu waliopendezwa walithamini sana makala zilizotafsiriwa katika lugha yao hivi kwamba waliandika nakala zao za kibinafsi. Kwa kuwa ilikuwa vigumu kupata nakala za Biblia katika Kigeorgia, wanafunzi fulani wa Biblia wakawa “waandikaji” wa kisasa wa Neno la Mungu.
“Nilinakili Mchana Kutwa”
Machapisho yaliyotafsiriwa katika Kigeorgia yalisambazwa kati ya akina ndugu na waliopendezwa ili wote wapokezane kuyasoma. Kila mmoja alikuwa na siku au majuma machache tu ya kusoma chapisho fulani. Kwa hiyo, ndugu walipopata nakala ya Maandiko ya Kigiriki, familia moja ilitumia fursa hiyo kuyanakili.
Raul Karchava alikuwa na umri wa miaka 13 tu baba yake alipomwomba anakili Maandiko ya Kigiriki. Anasema hivi: “Baba alinunua sanduku zima la vitabu na kalamu za aina mbalimbali, akitumaini kwamba zingenichochea kunakili. Ingawa nilihisi kwamba ilikuwa kazi kubwa mno, nilikubali kuifanya. Nilinakili mchana kutwa, nikitua tu kwa muda mfupi ili kunyoosha mikono yangu.”
Nakala zilizoandikwa kwa mkono za Mnara wa Mlinzi na Kuyachunguza Maandiko Kila Siku katika Kigeorgia
Watu wa ukoo wa Raul walifurahi sana walipoambiwa kwamba ndugu walikuwa wamekubali kuacha kitabu hicho chenye thamani sana kwa majuma ya ziada ili Raul amalize kazi hiyo ngumu. Kwa miezi miwili tu, alifaulu kunakili vitabu vyote 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo!
Licha ya jitihada zilizofanywa na waandikaji hao wenye bidii, bado njaa ya kiroho ya wanafunzi wa Biblia waliokuwa wakiongezeka haingeweza kutoshelezwa kikamili. Ili kutosheleza uhitaji huo wa haraka, ndugu na dada jasiri walianza kazi iliyohatarisha uhai wao ya kunakili na kusambaza machapisho ya Biblia kutoka nyumbani.
Kazi ya kuhubiri magharibi mwa Georgia ilianza kuongezeka. Lakini vipi kuhusu upande wa mashariki wa nchi? Je, kulikuwa na yeyote katika mji mkuu wa Tbilisi ambaye angeweza kuwasaidia watu wanyoofu ambao walikuwa wakitafuta kweli kama vile Vaso Kveniashvili aliyetajwa awali?
Kweli Yafika Kwenye Mji Mkuu
Katika miaka ya 1970, wenye mamlaka wa Muungano wa Sovieti katika maeneo mbalimbali walitaka kuwavunja moyo Mashahidi kwa kuwafukuza nyumbani kwao. Hicho ndicho kilichowapata ndugu Oleksii na dada Lydia Kurdas, wenzi wa ndoa kutoka Ukrainia waliohamia jiji la Tbilisi. Walikuwa wametumikia kwa miaka mingi katika kambi za gereza za Sovieti kwa sababu ya imani yao.
Larisa Kessaeva (Gudadze) katika miaka ya 1970
Ndugu na dada Kurdas waliwafundisha kweli Zaur na Eteri Kessaev, ambao walishika sana dini. Binti yao Larisa, ambaye alikuwa na umri wa miaka 15 wakati huo, anaeleza kilichotukia mara ya kwanza walipokutana na Oleksii na Lydia: “Tulijaribu kuthibitisha kwamba Kanisa Othodoksi ndilo kanisa pekee la kweli. Baada ya kuwa na mazungumzo mara kadhaa, tulikosa hoja za kujitetea, lakini waliendelea kusababu nasi kwa kutumia Biblia.”
Larisa anaendelea kusema hivi: “Tulipoenda kanisani, mara zote nilisoma zile Amri Kumi zilizokuwa zimeandikwa ukutani katikati ya sanamu mbili. Lakini jioni hiyo Oleksii alipotusomea Kutoka 20:4, 5, nilishangaa sana. Sikuweza kulala usiku huo kwa sababu nilikuwa nikifikiria, ‘Je kweli inawezekana kwamba tunapoabudu sanamu tunavunja amri ya Mungu?’”
Akitamani kupata jibu la swali lake, mapema asubuhi iliyofuata, Larisa alikimbia kwenda kanisani na kusoma tena amri hii, “Usijifanyie sanamu ya kuchongwa . . . Usiviinamie.” Kwa mara ya kwanza maishani mwake, alielewa maana ya amri hiyo takatifu. Baada ya muda mfupi, Larisa na wazazi wake walibatizwa na walikuwa kati ya Mashahidi wa kwanza-kwanza mjini Tbilisi.
Jitihada Zake za Kutafuta Haki Zilithawabishwa
Miaka 20 hivi baada ya kusikia kweli kwa mara ya kwanza, Vaso Kveniashvili alikutana na mtu aliyekuwa akihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova mjini Tbilisi. Vaso alifurahi kukutana na Mashahidi kwa mara nyingine. Alikuwa amesubiri kwa muda mrefu sana.
Miaka 24 hivi baada ya kusikia kweli kwa mara ya kwanza, Vaso Kveniashvili akawa Shahidi
Mwanzoni, Mashahidi wenyeji walisita kumhusisha katika shughuli zao kwa kuwa Vaso alijulikana kwa historia ya uhalifu. Baadhi yao hata walifikiri kwamba alikuwa mpelelezi anayewachunguza Mashahidi kwa niaba ya mamlaka za Sovieti. Hivyo, Vaso hakuruhusiwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa miaka minne.
Ilipokuwa wazi kwamba Vaso alikuwa na nia nzuri, alikubaliwa kuwa sehemu ya kutaniko la kwao na kubatizwa. Hatimaye, Vaso angeweza kumkaribia “Mungu wa haki” aliyekuwa akimtafuta tangu alipokuwa kijana! (Isa. 30:18, Holy Bible in Kiswahili) Alimtumikia Yehova bila kuyumbayumba hadi alipokufa mwaka 2014.
Kufikia mwaka 1990, kazi ya kuhubiri ilikuwa imeanzishwa katika maeneo ya magharibi na mashariki mwa Georgia. Wahubiri 900 hivi walikuwa wakiongoza mafunzo 942 ya Biblia. Msingi ulikuwa umejengwa kwa ukuzi mkubwa ambao ungefuata.
a Nakala za Biblia zilikuwa chache wakati wa utawala wa Kikomunisti ingawa sehemu fulani za Biblia zilikuwa zimetafsiriwa katika Kigeorgia kufikia karne ya tano W.K.—Tazama sanduku, “Biblia katika Kigeorgia.”