Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb17 kur. 118-127
  • Wachungaji Wenye Upendo Waandaa Mazoezi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wachungaji Wenye Upendo Waandaa Mazoezi
  • 2017 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Mikutano Yaboresha Ustadi wa Kuhubiri
  • Uhitaji wa Chakula cha Kiroho Waongezeka
  • Wakati wa Mabadiliko
  • Msaada Katika Kupanga Kazi ya Utafsiri
  • Kusafirisha Chakula cha Kiroho Wakati wa Vita
  • Kitia-Moyo cha Kiroho kwa Wakati Unaofaa
  • Maandalizi Yenye Upendo Yachochea Ongezeko
2017 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb17 kur. 118-127

GEORGIA | 1991-1997

Wachungaji Wenye Upendo Waandaa Mazoezi

Joni Shalamberidze na Tamazi Biblaia mapema katika miaka ya 1990

Joni Shalamberidze na Tamazi Biblaia mwanzoni mwa miaka ya 1990

Mwanzoni mwa miaka ya 1990, makutaniko mengi katika Georgia yalikuwa na mzee au mtumishi wa huduma mmoja tu. Kwa kawaida, makutaniko yalifanyizwa na vikundi kadhaa vilivyokutana katika sehemu tofauti-tofauti, kwa kuwa wahubiri walitawanyika kotekote katika eneo hilo kubwa sana ambalo lilijumuisha miji au vijiji kadhaa.

Joni Shalamberidze na Pavle Abdushelishvili, ambao waliwahi kutumikia katika maeneo ya mbali, walipewa mgawo wa kusaidia mji wa Telavi, uliokuwa katika eneo la Kakheti. Kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri 300, lakini halikuwa na mzee hata mmoja. Lilitia ndani vikundi 13 ambavyo vilikutanika katika maeneo tofauti-tofauti.

Pavle Abdushelishvili

Pavle Abdushelishvili

Baada ya muda mfupi, Joni na Pavle walitambua kikwazo kikubwa kilichozuia maendeleo ya kiroho ya akina ndugu. Joni anasema hivi: “Ndugu wengi walimiliki mashamba makubwa kutia ndani mashamba ya mizabibu. Kwa kuwa ni desturi kwa majirani kusaidiana kazi za shambani katika maeneo ya vijijini, ndugu zetu walitumia muda mwingi pamoja na watu wasio Mashahidi.”—1 Kor. 15:33.

Joni na Pavle walipendekeza kwamba akina ndugu waombe msaada wa kuvuna kutoka kwa Mashahidi wenzao. Kwa kufanya hivyo, wangefaidika kutokana na ushirika mzuri walipofanya kazi za shambani. (Mhu. 4:9, 10) Joni anaeleza, “Upendo wa kindugu uliimarika zaidi kutanikoni.” Joni na Pavle walipoondoka eneo la Kakheti miaka mitatu baadaye, kulikuwa na wazee watano na watumishi wa huduma 12.

Mikutano Yaboresha Ustadi wa Kuhubiri

Kwa kuwa kazi yetu ilikuwa imezuiwa kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1990, Mashahidi walikutanika katika vikundi vidogo kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko na Funzo la Mnara wa Mlinzi pekee. Ingawa mikutano hiyo ilitia moyo, haikuandaliwa ili kuwazoeza wahubiri kwa ajili ya huduma.

Hilo lilibadilika utawala wa Kikomunisti ulipoanguka. Sasa tengenezo la Yehova liliagiza makutaniko yafanye mkutano wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi kuwa sehemu ya mikutano ya kila juma.

Naili Khutsishvili na dada yake Lali Alekperova wanakumbuka jinsi walivyofurahia mikutano hiyo. Lali anakumbuka hivi: “Ilikuwa pindi yenye kusisimua sana. Kila mtu alifurahi sana kwamba sasa akina dada wangeweza kushiriki katika mikutano.”

Naili anakumbuka hivi: “Katika onyesho moja, mwenye nyumba alikuwa anasoma gazeti jukwaani aliposikia mlango ukibishwa. Walipokaribishwa, dada wawili waliingia kupitia mlango wa mbele na kupanda jukwaani.” Lali anaongeza, “Ingawa mikutano hiyo ilifanywa kwa njia isiyo ya kawaida, ilitusaidia kuboresha ustadi wetu wa kuhubiri.”

Uhitaji wa Chakula cha Kiroho Waongezeka

Kwa miaka mingi, ndugu wachache walitokeza machapisho ya Biblia wakiwa nyumbani wakitumia mashine za kufanya nakala ambazo ziliendeshwa kwa mkono. Ili kutosheleza uhitaji wa machapisho uliokuwa ukiongezeka, akina ndugu walienda kwenye makampuni ya kibiashara yanayofanya kazi za kuchapisha ambayo yangechapisha magazeti yetu kwa bei nafuu.

Ndugu akikata herufi katika gazeti fulani

Ili kuandaa nakala za kwanza za magazeti yetu katika Kigeorgia kwa ajili ya kuchapisha, akina ndugu walikata herufi katika magazeti ya habari na kuzibandika katika ukurasa wa kwanza wa nakala ya Kiingereza

Akina ndugu walikuwa wabunifu walipokuwa wakiandaa nakala ya kwanza kwa ajili ya mashine ya kuchapisha. Maandishi ya Kigeorgia yaliyotafsiriwa yalichapwa kwa ustadi kulingana na mpangilio wa gazeti la Kiingereza. Kisha, akina ndugu walikata picha kutoka kwenye gazeti la Kiingereza na kuzibandika kwenye nakala ya kwanza iliyopigwa chapa. Mwishowe, walikata herufi zenye kuvutia kutoka kwenye magazeti ya habari na kuzibandika katika ukurasa wa kwanza. Baada ya kufanya hivyo, sasa nakala ya kwanza ilikuwa tayari kwenda kuchapishwa.

Makala za mapema za magazeti katika Kigeorgia

Nakala za kwanza-kwanza za magazeti yaliyochapishwa katika Kigeorgia

Kompyuta za kibinafsi zilipoanza kupatikana, ndugu wawili vijana Levani Kopaliani na Leri Mirzashvili, walihudhuria masomo ya kujifunza jinsi ya kuzitumia vizuri. Leri anakumbuka: “Hatukuwa na uzoefu, na nyakati nyingine mambo yalikwenda mrama. Lakini kwa msaada wa Yehova, baada ya muda mfupi tulikuwa tunachapa na kupanga magazeti yetu.”

Licha ya changamoto, makutaniko nchini Georgia yalianza kupokea machapisho yenye rangi nne yaliyochapishwa nchini humo. Hata hivyo, baada ya muda ilikuwa vigumu kutosheleza uhitaji uliokuwa ukiongezeka wa machapisho. Lakini kwa wakati unaofaa kabisa, watumishi wa Yehova nchini Georgia walipokea mwongozo wenye upendo kutoka tengenezo la Yehova.

Wakati wa Mabadiliko

Kusanyiko la kimataifa la mwaka 1992 lililofanyika St. Petersburg nchini Urusi, lilitokeza nafasi kwa ajili ya ndugu kutoka Georgia kukutana na wawakilishi wa ofisi ya tawi kutoka Ujerumani. Genadi Gudadze kutoka Georgia anaeleza hivi: “Walitueleza jinsi kazi ya utafsiri inavyofanywa. Wakatuambia kwamba baada ya muda tungetembelewa ili kupata msaada katika kazi ya utafsiri.”

Haikuwa rahisi kuchapisha machapisho ya Biblia katika Kigeorgia. Kwa kuwa lugha hiyo ilikuwa na herufi za pekee, mfumo wa kompyuta wa kutayarisha maandishi kwa ajili ya uchapishaji (MEPS) uliobuniwa na tengenezo haungeweza kutumiwa katika Kigeorgia. Kwa hiyo, maandishi mapya yalihitaji kuundwa kwa ajili ya kuunganisha maneno na picha na kuchapisha.

Mwishoni mwa miaka ya 1970, familia ya Datikashvili ilikuwa imehamia nchini Marekani kutoka Georgia, ambako mtoto mmoja katika familia hiyo anayeitwa Marina, alijifunza kweli. Alisaidia sana wakati ndugu wa Betheli ya Brooklyn walipoanza kuunda herufi za Kigeorgia ili kuunganisha alfabeti kwenye mfumo wa MEPS. Baada ya muda mfupi, baadhi ya trakti na broshua “Tazama! Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya” zilichapishwa nchini Ujerumani.

Msaada Katika Kupanga Kazi ya Utafsiri

Mwaka 1993, Michael Fleckenstein na mke wake Silvia, waliwasili Tbilisi kutoka Ujerumani kuanzisha ofisi ya utafsiri. Michael anasema: “Bado nilikuwa nakumbuka mkutano uliofanyika St. Petersburg. Tulipowasili Tbilisi miezi 18 baada ya mkutano huo, tulishangaa tulipotambulishwa kwa watafsiri ambao tayari walifahamu kazi.”

Leri Mirzashvili, Paata Morbedadze, na Levani Kopaliani wakifanya kazi katika ofisi ya kutafsiri mwaka 1993

Leri Mirzashvili, Paata Morbedadze, na Levani Kopaliani wakifanya kazi katika ofisi ya utafsiri iliyoko Tbilisi mwaka 1993

Miezi michache baadaye, watafsiri 11 wa wakati wote walikuwa wanafanya kazi ya utafsiri kwenye ofisi iliyokuwa katika nyumba fulani ndogo. Kwa sababu ya mazoezi yenye thamani kutoka tengenezo la Yehova, chakula cha kiroho kilianza kupatikana kwa ukawaida kwa ajili ya makutaniko.

Kusafirisha Chakula cha Kiroho Wakati wa Vita

Baada ya kuvunjika kwa Muungano wa Sovieti, vita vya wenyewe kwa wenyewe na mapigano ya kikabila yalizuka katika nchi zilizokuwa kwenye muungano huo, kutia ndani Georgia. Kwa sababu hiyo, ilikuwa hatari kusafiri, hasa kuvuka mipaka ya nchi.

Ndugu Zaza Jikurashvili na Aleko Gvritishvili na wake zao

Ndugu Zaza Jikurashvili na Ndugu Aleko Gvritishvili (kwenye picha na wake zao) walisafirisha machapisho katika kipindi cha vita

Siku moja, mwezi wa Novemba 1994, Aleko Gvritishvili alikuwa anavuka mpaka wa nchi pamoja na ndugu wengine wawili kikundi cha watu wenye silaha kilipowasimamisha na kuwaamuru watoke ndani ya gari lao. Aleko anasema: “Walikasirika walipoona machapisho yetu ya Biblia. Walitupanga katika mstari kana kwamba walitaka kutuua. Tulisali kwa Yehova kwa bidii. Baada ya saa mbili hivi, mmoja wao alituambia, ‘Chukueni machapisho yenu na mwondoke. Lakini mkirudi tena, tutachoma gari lenu na kuwaua.’”

Licha ya vitisho kama hivyo, ndugu waliendelea kusambaza chakula cha kiroho. Ndugu Zaza Jikurashvili, aliyejidhabihu sana kuleta machapisho ya Biblia nchini Georgia anasema: “Tulijua kwamba ndugu zetu walihitaji chakula cha kiroho. Wake zetu wapendwa walituunga mkono sana.”

Aleko anakumbuka, “Ndugu wengi waliotumiwa kusafirisha machapisho walikuwa wanaume wenye familia.” Ni nini kilichowachochea kuendelea licha ya hatari? Anaendelea kusema: “Kwa ujumla, uthamini na upendo wetu kumwelekea Yehova ndio uliotuchochea. Tulitaka pia kuwaonyesha ndugu zetu wapendwa jinsi Yehova anavyowajali.”

Kwa sababu ya kujidhabihu kwa ndugu hao, machapisho yaliendelea kusambazwa katika kipindi hicho chote cha vita. Baadaye, ndugu walianzisha njia salama ya kusafirisha machapisho kupitia Ujerumani hadi Georgia.

Kitia-Moyo cha Kiroho kwa Wakati Unaofaa

Hali ya kisiasa ilipotulia mwaka 1995, Mashahidi walifanya mipango kwa ajili ya kusanyiko la kwanza la wilaya. Katika majira ya joto ya mwaka 1996, wajumbe 6,000 hivi kutoka kotekote nchini Georgia walihudhuria kusanyiko la wilaya katika maeneo matatu: Gori, Marneuli, na Tsnori.

Mashahidi wa Yehova wakiwa kwenye kusanyiko la wilaya karibu na Gori katika 1996

Mashahidi wakiwa kwenye kusanyiko la wilaya karibu na jiji la Gori mwaka 1996

Kusanyiko lililofanyika karibu na Gori lilikumbukwa sana hasa na wale waliohudhuria. Lilikuwa badiliko kubwa sana kutoka wakati ambapo akina ndugu hawakuwa na uhakika ikiwa wangejaza ukumbi walipofanya Ukumbusho. Sasa walikuwa wanatarajia hudhurio la zaidi ya watu 2,000 lakini hawangeweza kupata eneo lenye nafasi ya kutosha kwa ajili ya kusanyiko. Waliamua kufanya kusanyiko katika eneo la wazi lililokuwa karibu na mji wa Gori katika eneo lenye milima.

Ndugu Kako Lomidze, ambaye alikuwa mmoja wa Halmashauri ya Kusanyiko anaeleza: “Baada ya kusanyiko, ndugu na dada walitumia wakati pamoja kuimba nyimbo na kufurahia ushirika wenye kuburudisha. Ilionekana wazi kwa wote kwamba watu wa Mungu walikuwa wameunganishwa kwa vifungo vyenye nguvu vya upendo.”—Yoh. 13:35.

Maandalizi Yenye Upendo Yachochea Ongezeko

Kuanzia mwaka 1996, mipango ilifanywa ili waangalizi wa mzunguko watembelee kila kutaniko nchini kwa wiki nzima. Ili kufikia mradi huo, waangalizi wapya wa mzunguko waliwekwa rasmi wawasaidie ndugu ambao tayari walikuwa wanatumikia wakiwa waangalizi wa mzunguko katika eneo la Georgia magharibi na mashariki.

Bila shaka, ‘kazi ya jasho na yenye upendo’ na utumishi mwaminifu wa waangalizi hao wanaosafiri ilisaidia makutaniko yakue na kufuata mwongozo wa Yehova kwa ukaribu zaidi. (1 The. 1:3) Kuanzia mwaka 1990 hadi 1997, ongezeko lilikuwa la pekee sana. Mwaka 1990 wahubiri 904 pekee ndio walioripoti utumishi, lakini baada ya miaka saba tu, wahubiri 11,082 walikuwa wakihubiri habari njema!

Ukuzi wa kiroho ambao ulianza miongo michache mapema, sasa ulionekana waziwazi kotekote nchini. Lakini bado Yehova alikuwa na baraka nyingi kwa ajili ya watu wake nchini Georgia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki