Kuhubiri kwenye kituo cha kigari kinachoning’inia kwenye nyaya cha Khulo
GEORGIA
“Hilo Ndilo Fungu la Urithi la Watumishi wa Yehova.”— Isa. 54:17.
WATUMISHI wa Yehova nchini Georgia wamehubiri habari njema kwa bidii na Yehova amebariki kazi yao ngumu. Matokeo ni kwamba habari njema imefika karibu kila sehemu ya nchi hiyo.
Wahubiri wakielekea kuhubiri kwenye eneo la Ushguli, lililo mita 2,200 juu ya usawa wa bahari
Katika miaka ya karibuni, wahubiri wenye bidii na mapainia wamekazia fikira kuwafikia watu wanaoishi katika maeneo yasiyohubiriwa kwa ukawaida. Katika maeneo ya milimani, baadhi ya vijiji vya mashambani vinaweza kufikiwa tu kwa kutumia magari yanayoendeshwa kwa magurudumu manne au kwa vigari vinavyoning’inia kwenye nyaya.
Wahubiri katika eneo la Svaneti
Kila mwaka tangu 2009, ofisi ya tawi ya Georgia imekuwa ikiyatumia makutaniko orodha ya maeneo yasiyogawiwa kutaniko lolote na kuwaomba wajitoleaji wakahubiri katika maeneo hayo. Wahubiri wengi wamejidhabihu sana ili wakahubiri huko.
Ana na Temuri Bliadze
Temuri na Ana Bliadze ni wenzi wa ndoa. Muda mfupi baada ya kufunga ndoa walitambua kwamba eneo la milimani la Ajaria lilikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri. Walikuwa tu wamenunua ardhi kwa ajili ya kujenga nyumba. Hata hivyo, sasa walikuwa na nafasi ya kupanua huduma yao.
Walienda kutembelea eneo la Ajaria kwa juma moja. Temuri anaeleza mambo aliyojionea alipofika katika eneo hilo: “Wahubiri walikuwa wakitembea kwa muda mrefu ili kufika kwenye vijiji vidogo. Nyumbani tulikuwa na gari na mara moja nikatambua kwamba litasaidia sana katika eneo hilo.”
Ana anasema hivi: “Haikuwa rahisi kuhama kwa sababu tulilipenda sana kutaniko letu na familia yetu. Lakini tulitambua kwamba Yehova alikuwa akituongoza.” Kwa zaidi ya miaka mitatu, Temuri na Ana wamekuwa wakisaidia kikundi kwenye mji wa Keda katika eneo la Ajaria.
Mapainia Wabunifu
Mapainia wa pekee wa muda wamesaidia sana kazi ya kuhubiri katika maeneo hayo ya vijijini. Migawo yao ilipoisha, mapainia wengi waliamua kubaki kwenye maeneo waliyogawiwa ili kuendelea kuwasaidia wanafunzi wao wa Biblia.
Dada wawili mapainia, ambao wote wanaitwa Khatuna, walipata mgawo kwenye mji maridadi wa Manglisi. Eneo hilo halikuwa na Shahidi hata mmoja, lakini dada zetu walipata matokeo mazuri. Mwezi wa kwanza walipofika waliongoza mafunzo 9 ya Biblia, mwezi uliofuata wakaongoza 12, uliofuata wakaongoza 15, kisha mwezi huo mwingine wakaongoza mafunzo 18 ya Biblia! Ili kuwasaidia wanafunzi hao wa Biblia, waliamua kubaki Manglisi.
Ili kujitegemeza kiuchumi, dada hao walihitaji kuwa wabunifu sana. Watu wengi wanaotembelea Manglisi wanafurahia sana jemu ya kienyeji, inayotengenezwa kwa mbegu za misonobari ambazo zina manufaa kwa afya. Hivyo, mwanzoni dada hao walifanya kazi ya kukusanya mbegu za misonobari ili kutengeneza jemu hiyo na kuiuza sokoni. Hata hivyo, bila kutarajia walipata chanzo kingine cha mapato.
Siku moja mwanafunzi wao wa Biblia aliwaletea vifaranga kadhaa. Aliwaambia kwamba kuku wake mmoja alitaga mayai katika eneo lisilojulikana na mwishowe akarudi nyumbani na vifaranga. Mwanamke huyo alitaka kuwapatia walimu wake wa Biblia vifaranga hao. Kwa kuwa mmoja wa dada hao alikuwa na uzoefu wa kufuga kuku, wakaamua watumie njia hiyo kujitegemeza.
Mmoja wao anasema hivi: “Kwa msaada wa Yehova, na kwa msaada wa akina ndugu na dada na wanafunzi wa Biblia, tulifaulu kuishi Manglisi kwa miaka mitano.” Sasa kuna kikundi cha ndugu na dada wenye bidii katika eneo hilo.
Khatuna Kharebashvili na Khatuna Tsulaia wakiwa Manglisi
Kufanya Upainia kwa Lugha ya Kigeni
Katika miaka ya karibuni, wageni wengi wamehamia nchini Georgia. Mapainia wengi walitambua kwamba shamba jipya la utumishi lilikuwa likifunguka. Hivyo, walianza kujifunza lugha kama vile Kiarabu, Kiajemi, Kiazerbaijani, Kichina, Kiingereza, na Kituruki.
Mapainia wengi wamejiunga na vikundi na makutaniko ya lugha ya kigeni. Wengine wamehamia nchi nyingine ambapo kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri. Giorgi na Gela walikuwa na umri wa zaidi ya miaka 20 walipohamia nchi jirani. Giorgi anasema hivi, “Tulitaka kumpa Yehova kilicho bora na kuhamia huko kulitupa fursa ya kufanya hivyo.”
Gela anasema hivi kuhusu muda aliotumia huko: “Kutumikia nikiwa mzee katika eneo hilo kulinifundisha mambo mengi. Inafurahisha sana Yehova anapokutumia kuwasaidia ‘kondoo wake wadogo.’”—Yohana 21:17.
Giorgi anaongeza kusema hivi: “Kulikuwa na changamoto, lakini tulikazia fikira utumishi wetu na hatukuwazia jambo lingine. Tulihisi kwamba tunafanya kile tulichopaswa kufanya.”
Ndugu mwingine ambaye pia anaitwa Gela, alitumikia nchini Uturuki kwa miaka michache. Anakumbuka hivi: “Mwanzoni nilipokuwa nikijitahidi kujua lugha ya wenyeji, ilikuwa vigumu kwangu kudumisha shangwe yangu. Hata hivyo, mwishowe nilipofaulu kuzungumza lugha hiyo na kuwasiliana na ndugu na dada zangu na pia watu wengine katika eneo, nilikuwa na shangwe siku zote.”
Nino, ambaye alifanya upainia jijini Istanbul, Uturuki, kwa zaidi ya miaka kumi, anaeleza hisia zake kwa njia hii: “Nilihisi ninategemezwa na Yehova tangu siku ya kwanza nilipohamia huko. Unapofanya upainia katika shamba la lugha nyingine, kila siku unapata mambo yaliyoonwa kama yale tunayosoma katika Kitabu cha Mwaka.”