NYONGEZA
Kusalimia Bendera, Kufanya Uchaguzi, Kufanya Kazi za Wanainchi Zinazoombwa na Serikali
Kusalimia bendera. Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba kuinamia ao kuisalimia bendera, mara nyingi wakati wimbo wa taifa unapoimbwa, ni tendo la ibada ya kidini. Ibada hiyo inaonyesha kwamba ni Serikali ao viongozi wake ndio walio na uwezo wa kuokoa mwanadamu, wala si Mungu. (Isaya 43:11; 1 Wakorintho 10:14; 1 Yohana 5:21) Mufalme wa inchi ya Babiloni ya zamani, Nebukadneza, ni kiongozi mumoja aliyejiendesha hivyo. Ili kuwaonyesha watu utukufu wake na bidii yake ya kidini, mutawala huyo mwenye nguvu alisimamisha sanamu kubwa na akawalazimisha watu wake wote kuiinamia wakati muziki ulikuwa unachezwa; muziki huo unaweza kulinganishwa na wimbo wa taifa leo. Lakini, Waebrania watatu: Shadraki, Meshaki, na Abednego, walikataa kuiinamia sanamu hiyo, hata ikiwa jambo hilo lingefanya wauawe.—Danieli, sura ya 3.
Mwanahistoria Carlton Hayes, aliandika hivi: “Leo, alama ya kwanza kabisa ya kuonyesha kama mutu anaipenda inchi yake sana na ambayo huabudiwa na wengi ni bendera. Wakati bendera inapitishwa ao kupandishwa watu wanavua kofia; watu hutunga maneno mazuri ili kusifu bendera na watoto wanaiimbia nyimbo.” Aliongeza pia kwamba kuna siku zilizowekwa ili kuabudu taifa, ni kusema, kuonyesha kwamba mutu anaipenda sana inchi yake. Huko Amerika, siku hiyo ni tarehe 4 Mwezi wa 7; ibada hiyo ina “watakatifu wake ao mashujaa wake,” pia “mahekalu.” Katika inchi ya Brezil, siku fulani kwenye maandamano, waziri anayeangalia mambo ya majeshi alisema waziwazi hivi: “Bendera inaheshimiwa na kuabudiwa . . . kama vile tunavyoabudu inchi yetu ya kuzaliwa.” Kitabu fulani kinasema, “bendera ni kitu kitakatifu kama vile musalaba.”—The Encyclopedia Americana.
Chapa ya karibuni zaidi ya kitabu hicho inasema kwamba kuimba nyimbo za taifa ni “kuonyesha kwamba mutu anaipenda inchi yake sana, na mara nyingi katika maneno ya nyimbo hizo watu wanaomba Mungu aongoze na kulinda taifa na watawala wake.” Kwa hiyo, watumishi wa Yehova hawadanganyike wanaposema kwamba sherehe za kutukuza inchi kutia ndani kusalimia bendera na nyimbo za taifa ni ibada kabisa ya kidini. Kitabu kingine kinazungumuzia namna watoto wa Mashahidi wa Yehova kwenye masomo wanavyokataa kuisalimia bendera ao kufanya kiapo cha kubaki waaminifu kwa inchi ya Amerika. Kitabu hicho kinasema hivi: “Kutokana na mambo mengi ambayo Mahakama Kubwa imeamua, mwishowe imehakikishwa kwamba sherehe hizo mbalimbali zinazofanywa kila siku ni ibada kabisa ya kidini.”—The American Character.
Hata ikiwa watumishi wa Yehova hawajiingize katika sherehe ao sikukuu zinazoonekana kuwa hazipatane na Biblia, wao hawawakataze watu wengine kufanya hivyo; wanaheshimu haki ya watu hao. Pia wanaheshimu bendera ya inchi na wanatambua kwamba serikali ao guvernema yote inayotawala ni “mamlaka zilizo kubwa” na kwamba zinatumika kama “muhudumu [ao mutumishi] wa Mungu.” (Waroma 13:1-4) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova wanatii shauri linalowaomba kusali “kwa ajili ya wafalme na wale wote walio katika cheo cha juu.” Lakini, wanafanya hivyo ili waendelee “kuishi maisha ya shwari [ao ya kimya] na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na kuchukua mambo kwa uzito.”—1 Timotheo 2:2.
Kufanya Uchaguzi. Wakristo wa kweli hawawakataze wengine kufanya uchaguzi; hiyo ni haki yao kufanya uchaguzi. Hawafanye maandamano ili kupinga uchaguzi, na wanatii wakubwa waliochaguliwa. Hata hivyo, wao hawajiingize katika mambo ya politike ya mataifa. (Mathayo 22:21; 1 Petro 3:16) Mukristo atafanya nini ikiwa anaishi katika inchi ambamo wanalazimisha wanainchi kufanya uchaguzi ao wanawachukia wale ambao hawakuenda kufanya uchaguzi? Mukristo anaweza kusema kwamba kwa kuwa Shadraki, Meshaki, na Abednego walienda huko Dura, mahali ambako Mufalme alisimamisha sanamu, basi, si vibaya kwake kuenda kwenye biro ya uchaguzi, kwa kuwa zamiri yake inamuruhusu. Hata akifikia uamuzi huo, anapaswa kuangalia sana ili asiunge mukono upande wowote katika mambo ya politike. Anapaswa kufikiria kanuni sita zifuatazo:
Wafuasi wa Yesu “si sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 15:19.
Wakristo wanamwakilisha Kristo na Ufalme wake.—Yohana 18:36; 2 Wakorintho 5:20.
Kutaniko la Kikristo lina umoja wa imani, na ndugu na dada wameunganishwa na upendo wa Kikristo.—1 Wakorintho 1:10; Wakolosai 3:14.
Ukimuchagua mutu fulani, anapotawala vibaya wewe pia unashiriki mambo yake.—Ona kanuni zilizo katika 1 Samweli 8:5, 10-18 na 1 Timotheo 5:22.
Yehova aliona kwamba Waisraeli walimukataa kwa sababu walipenda wawe na mufalme anayeonekana.—1 Samweli 8:7.
Wakristo wanapaswa kuwa na uhuru wa kusema wanapozungumuza na kila mutu juu ya Ufalme wa Mungu, hata ikiwa mutu huyo ni wa upande gani katika mambo ya politike.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Waebrania 10:35.
Kazi za wanainchi zinazoombwa na serikali. Katika inchi fulani, Serikali inawaomba wale wanaokataa kazi ya askari wafanye kazi nyingine kwa muda fulani. Hali hiyo inapotokea, inafaa kusali, na labda hata kuzungumuza na Mukristo fulani mwenye kukomaa, na kisha unaweza kufanya uamuzi unaotegemea zamiri inayoongozwa na kanuni za Biblia.—Methali 2:1-5; Wafilipi 4:5.
Neno la Mungu linatushauri ‘tuzitii serikali na mamlaka zinazotawala, tuwe tayari kwa ajili ya kila kazi njema, tuwe wenye usawaziko.’ (Tito 3:1, 2) Tukiwa na kanuni hiyo akilini tunaweza kujiuliza hivi: ‘Nikikubali kazi fulani ambayo serikali inaomba wanainchi wafanye, je, nitaonyesha kwamba ninajiingiza katika mambo ya politike ao ninaunga mukono dini ya uongo?’ (Mika 4:3, 5; 2 Wakorintho 6:16, 17) ‘Nikikubali kazi hiyo, je, itakuwa vigumu kwangu kutimiza madaraka yangu ya Kikristo ao itanizuia kabisa kuyatimiza?’ (Mathayo 28:19, 20; Waefeso 6:4; Waebrania 10:24, 25) ‘Ao, je, ninaweza kufanya kazi hiyo na wakati huohuo kuongeza utendaji wangu wa kiroho, labda hata kufanya utumishi wa wakati wote?’—Waebrania 6:11, 12.
Ikiwa zamiri ya Mukristo fulani inamuruhusu kufanya kazi fulani ambayo inaombwa na serikali kuliko kufungwa, Wakristo wenzake wanapaswa kuheshimu uamuzi wake. (Waroma 14:10) Na ikiwa anaona kwamba hawezi kufanya kazi hiyo, wengine wanapaswa pia kuheshimu uamuzi huo.—1 Wakorintho 10:29; 2 Wakorintho 1:24.