Biblia Inabadilisha Maisha ya Watu
NI NINI kilichomusaidia mwanamuke mumoja huko Philippines aache maisha yake ya ulevi na kufanya maisha ya familia yake yawe mazuri? Ni nini kilichomusaidia mwanaume mumoja aliyependa sana muchezo wa karaté huko Australie awe muhubiri wa habari njema mwenye kufanya amani? Soma mambo ambayo watu hao wanaeleza.
“Iliomba wakati ili nifanye mabadiliko.”—CARMEN ALEGRE
ALIZALIWA MWAKA WA 1949
ALIZALIWA KATIKA INCHI YA PHILIPPINES
ALIKUWA MULEVI SANA
MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika San Fernando, muji wa jimbo la Camarines Sur. Nilipokuwa mutu muzima, niliishi miaka mingi huko Antipolo, jimbo la Rizal. Muji wa Antipolo, ulio katika eneo la milima na majani mengi na miti mingi, ulikuwa muji mudogo wenye utulivu wakati nilihamia huko. Watu hawakuzoea kutembea usiku. Lakini, sasa, Antipolo ni muji mukubwa wenye kuendelea ulio na watu wengi sana.
Wakati fulani kisha kuhamia huko Antipolo, nilikutana na mwanaume anayeitwa Benjamin, na baada ya muda tukaoana. Maisha ya ndoa yakakuwa magumu kuliko namna nilivyowazia. Ili kuepuka magumu hayo, nikaanza kunywa pombe sana. Nikakuwa na tabia mbaya, hiyo ilionekana katika namna yangu ya kumutendea bwana yangu na watoto wangu. Sikuonyesha sifa ya kujizuia na uvumilivu katika namna yangu ya kuwatendea. Na sikumuheshimu bwana yangu hata kidogo. Ni wazi kama maisha ya familia yetu hayakuwa mazuri.
NAMNA BIBLIA ILIVYOBADILISHA MAISHA YANGU: Editha, dada mukubwa wa bwana yangu, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alitushauria tujifunze Biblia na Mashahidi wa Yehova. Tulikubali, kwa sababu tulitumaini kama kujifunza Biblia kutatusaidia kufanya maisha ya familia yetu yawe mazuri.
Kujifunza Biblia kulitusaidia kujua mambo mengi. Maneno ya Ufunuo 21:4 yalinigusa moyo sana. Juu ya wale watakaoishi katika paradiso duniani wakati wa utawala wa Ufalme wa Mungu, andiko hilo linasema kama Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” Mimi pia nilitaka kuwa kati ya wale watakaofurahia baraka hizo.
Nilitambua kama iliniomba kufanya mabadiliko makubwa katika hali yangu na tabia zangu. Iliomba wakati ili nifanye mabadiliko, lakini mwishowe nikafikia kuacha maisha ya ulevi. Tena, nilijifunza kumutendea bwana yangu na watoto wetu kwa upole na nikakuwa muvumilivu. Zaidi ya hilo, nilijifunza kumuheshimu bwana yangu, na kumuunga mukono katika kuongoza familia yetu.
Mimi na bwana yangu tulipoanza kuenda kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova, tulivutiwa sana na mambo tuliyoona huko. Mashahidi wa Yehova hawacheze michezo ya feza, hawalewe, na hawana ubaguzi. Wanamuheshimu kila mutu na wanamutendea kwa adabu. Tulikuwa hakika kama tuliipata dini ya kweli.—Yohana 13:34, 35.
FAIDA AMBAYO NIMEPATA: Maisha ya familia yetu yamebadilika sana. Sasa, mimi na Benjamin tuna maisha ya ndoa yenye furaha, na tunafurahia kuwafundisha wengine Biblia. Watoto wetu wawili na wake zao wameanza pia kujifunza Biblia. Tunatumaini kama wakati ujao watakuwa pia watumishi wa Yehova. Kumutumikia Yehova ndiyo njia nzuri zaidi ya maisha.
“Nilijisikia kuwa hakuna mutu anayeweza kunishinda.”—MICHAEL BLUNSDEN
ALIZALIWA MWAKA WA 1967
ALIZALIWA KATIKA INCHI YA AUSTRALIE
ALIPENDA SANA MUCHEZO WA KARATE
MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilikomalia huko Albury, muji muzuri wenye kuendelea wa Nouvelle-Galles du Sud. Kama miji mingi, katika muji huo pia kuna matendo ya uvunjaji wa sheria. Lakini, kwa kawaida, muji huo unajulikana kuwa mahali salama pa kuishi.
Nilikomaa katika maisha ya raha. Hata ikiwa wazazi wangu walivunja ndoa nilipokuwa na miaka saba, walifanya yote wawezayo ili mimi, ndugu yangu mukubwa na dada zangu wawili tusikose kitu chochote. Nilipata elimu nzuri kwa sababu nilisomea kwenye masomo mazuri zaidi ya eneo letu. Baba yangu alipenda niwe mufanya biashara ninapomaliza masomo. Lakini mimi nilipenda michezo, na nikajua sana karaté na kuendesha kinga. Mwishowe nikapata kazi ya kutengeneza motokari, na hilo likaniruhusu kupata wakati mwingi wa kuenda kwenye michezo yangu.
Nilijivuna sana kwa sababu nilikuwa na nguvu. Wakati fulani, nilijisikia kuwa hakuna mutu anayeweza kunishinda. Na ilikuwa vyepesi kwangu kutumia nguvu hiyo ili kuwaonea wengine. Ndiyo sababu mwalimu wangu wa karaté alinipatia sheria kali juu ya kujizuia na kuwa na adabu nzuri, kwa sababu alijua kama ningetumia vibaya nguvu zangu. Kila mara alinikumbusha ulazima wa kutii sheria hizo na kuzifuata kwa uaminifu.
NAMNA BIBLIA ILIVYOBADILISHA MAISHA YANGU: Nilipoanza kujifunza Biblia, nilielewa kama Yehova anachukia jeuri. (Zaburi 11:5) Kwanza, niliwaza kama karaté si jeuri kwa sababu ni muchezo tu. Niliwaza kama sifa nzuri na kanuni za juu za muchezo wa karaté zinapatana na yale ambayo Biblia inafundisha. Mashahidi wawili walionifundisha Biblia walikuwa bibi na bwana, na walinivumilia sana. Hawakuniambia hata siku moja kama ninapaswa kuacha muchezo wa karaté; waliendelea tu kunifundisha Biblia.
Ujuzi wangu wa Biblia ulipoongezeka na urafiki wangu pamoja na Yehova ulipokuwa wenye nguvu zaidi, nilianza kubadilisha mawazo yangu. Niliguswa moyo sana nilipojifunza juu ya mufano wa Yesu, mwana wa Mungu. Hata ikiwa Yesu alikuwa na nguvu nyingi, hakuitumia hata kidogo ili kutenda kwa jeuri. Maneno yake yaliyo katika andiko la Mathayo 26:52 yalinigusa moyo sana. Andiko hilo linasema hivi: “Wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.”
Nilipoendelea kujifunza mengi juu ya Yehova, nilimuheshimu sana na kumupenda. Kujua kama Muumbaji wetu, mwenye hekima sana na nguvu nyingi, anaweza kunihangaikia kulinigusa tena moyo. Nilichochewa sana nilipojifunza kama Yehova hawezi kuniacha ikiwa ninaendelea kujikaza, hata ikiwa ninafanya jambo lenye kumuhuzunisha ao hata wakati ninapoona mambo kuwa nguvu na kufikiri kama siwezi kuendelea. Ahadi hii ya Biblia ilinitia moyo sana: ‘Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mukono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’ (Isaya 41:13) Nilipoona kama Yehova amenionyesha upendo kama huo, sikutaka kumuacha.
Nilijua kama kuacha muchezo wa karaté lilikuwa jambo ngumu sana ambalo nilikuwa sijafanya katika maisha yangu. Lakini, nilijua pia kama kufanya hivyo kutamupendeza Yehova, na nilikuwa hakika kama kumutumikia ndilo jambo lenye kuleta faida kubwa. Mwishowe, nilisadikishwa niliposoma maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:24 yanayosema hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.” Nilitambua kama haiwezekane nimutumikie Yehova kwa moyo wote ikiwa ninaendelea na muchezo wa karaté, kwa sababu nitatia muchezo huo pa nafasi ya kwanza katika maisha yangu. Sasa, wakati wa kuchagua bwana ambaye nitatumikia ulifika.
Haikuwa vyepesi kwangu kuacha muchezo wa karaté. Nilisumbuliwa na mawazo mbalimbali. Nilisikia furaha kwa kujua kama nilikuwa nikimupendeza Yehova. Lakini niliona kama nikiacha muchezo huo, nitamuumiza sana mwalimu wangu. Mara nyingi wale wanaocheza muchezo wa karaté wanaona kumuumiza mwalimu wao kuwa zambi isiyoweza kusamehewa. Wengine wanaweza hata kuamua kujiua ili wasipatwe na haya.
Sikuweza kumuelezea mwalimu wangu sababu iliyonifanya niache muchezo wa karaté. Niliacha tu kufanya mazoezi na nikaacha kuzungumuza na mwalimu wangu na wachezaji wenzangu. Nilijua kama nilifanya vizuri kwa kuacha muchezo huo. Lakini nilijisikia pia kuwa mwenye kosa kwa sababu sikuwaelezea wengine mambo mapya niliyoamini. Nilijisikia kuwa nilimuvunja Yehova moyo mbele hata nianze kumutumikia. Mawazo hayo yote yalinisumbua. Wakati fulani nilijaribu kusali kwa Yehova lakini nilijikuta kuwa mwenye kulia.
Inawezekana Yehova aliona jambo fulani nzuri katika moyo wangu, kwa sababu aliwachochea ndugu na dada wa kutaniko wanitegemeze. Upendo walionionyesha, kitia moyo ambacho walinitolea, na hali yao ya urafiki vilinigusa moyo sana. Habari inayoelezwa katika Biblia juu ya Daudi na Bath-sheba ilinitia pia moyo. Hata ikiwa Daudi alifanya zambi nzito, alitubu kwelikweli na Yehova alimusamehe. Kufikiri sana juu ya habari hiyo kulinisaidia kuwa na maoni yanayofaa juu ya makosa yangu.
FAIDA AMBAYO NIMEPATA: Mbele ya kujifunza Biblia, sikuhangaikia mutu yeyote—niliishi kwa ajili yangu tu. Lakini, kwa musaada wa Yehova na bibi yangu mwenye sura nzuri ambaye nilikuwa nimeoana naye kwa miaka saba, nilianza kuwahangaikia watu wengine. Tumebarikiwa sana kwa kupata pendeleo la kujifunza Biblia na watu wengi sana, hata wale waliopatwa na hali ngumu. Ninapoona namna watu wengine wanavyobadilisha maisha yao kwa sababu ya kumupenda Yehova, hilo linaniletea furaha zaidi kuliko ile ningepata ikiwa ningeendelea kuwa muchezaji mukubwa wa karaté.
[Wazo la fungu kwenye ukurasa 14]
“Kujua kama Muumbaji wetu, mwenye hekima sana na nguvu nyingi, anaweza kunihangaikia kulinigusa tena moyo”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]
“Asante kwa Habari Hizi Nzuri Sana!”
Je, umefurahia kusoma habari zenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha” zinazozungumuziwa katika Munara wa Mulinzi tangu mwezi wa 8, 2008? Kati ya habari hizo zaidi ya 50, kuna habari 2 zilizovutia sana wasomaji wetu. Sababu gani habari zenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha” zimevutia sana watu wengi?
Watu wanaozungumuziwa katika habari hizo ni watu waliokuwa na maisha mbalimbali. Mbele ya kumujua Yehova Mungu, wamoja kati yao walikuwa na maisha mazuri, lakini hawakuwa na kusudi katika maisha. Wengine walikuwa na tabia mbaya kama vile hasira kali, kutumia dawa za kulewesha ao walikuwa na maisha ya ulevi. Wachache kati yao walikomalia katika familia za Mashahidi wa Yehova lakini wakati fulani wakaacha kumuabudu Yehova. Mifano ya watu hao inaonyesha kama inawezekana kufanya mabadiliko ili kumupendeza Mungu. Na kufanya hivyo kunaleta faida sikuzote. Namna gani habari hizo zimesaidia wasomaji wetu?
Musomaji mumoja anaeleza namna habari iliyo katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 mwezi wa 2, 2009, ilivyosaidia wafungwa fulani katika gereza la wanawake.
◼ Anasema kama “wengi kati ya wafungwa wanaweza kuelewa hali ya watu wanaozungumuziwa katika habari hizo.” Picha za watu hao ‘mbele’ ya kumujua Mungu na ‘kisha’ kumujua Mungu na pia maelezo juu ya namna maisha yao yalivyokuwa zamani vinasaidia sana. Wafungwa wengi walikuwa na maisha yenye kufanana na yale ya watu wanaozungumuziwa katika gazeti hilo. Kisha kusoma habari hizo, wafungwa wawili walianza kujifunza Biblia.”—C. W.
Mifano ya watu wanaozungumuziwa katika habari hizi imegusa kabisa mioyo ya watu fulani. Kwa mufano, Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 mwezi wa 4, 2011, ulizungumuzia habari ya Guadalupe Villarreal, ambaye aliacha tabia yake ya kulala na wanaume wenzake ili amutumikie Yehova. Ona barua mbili tu kati ya barua nyingi ambazo wasomaji waliandika juu ya habari ya Guadalupe Villarreal.
◼ “Habari ya Guadalupe ilinigusa moyo sana. Ni jambo la kufurahisha sana kuona namna kumupenda Yehova na Neno lake kunaweza kumusaidia mutu abadilishe kabisa maisha yake!”—L. F.
◼ “Zamani, nilijaribu kuzungumuzia kila mutu mambo ninayoamini, hata wanaume wanaolala na wanaume na wanawake wanaolala na wanawake. Lakini, wakati fulani, nilitambua kama nilianza kuwazarau watu hao ao hata kuwaepuka. Nilikuwa na lazima ya habari hiyo kabisa. Ilinisaidia kuwaona watu hao kama Yehova anavyowaona, maana yake, kuwaoana kama watu wanaoweza kuwa waabudu wa Yehova.”—M. K.
Habari nyingine ambayo ilipendeza wasomaji wengi ni ile ya Victoria Tong, iliyoelezwa katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1, mwezi wa 8, 2011. Victoria alieleza kama aliteseka sana katika utoto wake. Anasema kama alisumbuliwa na mawazo ya kujisikia kama Yehova hawezi kumupenda, hata kisha kumutumikia kwa miaka mingi. Na alieleza kile kilichomusaidia polepole akubali kama Yehova anamupenda. Ona yale wasomaji fulani walisema juu ya habari yake.
◼ “Habari ya Victoria ilinigusa moyo sana. Katika maisha yangu, nimepatwa na mambo mengi yenye kuhuzunisha. Hata miaka mingi kisha kubatizwa, niliendelea kushindana na mawazo yasiyofaa. Lakini habari ya Victoria inanifanya nijikaze sana ili nione kile kitu kizuri ambacho Yehova anaona kwangu.”—M. M.
◼ “Nilipokuwa kijana, nilipiganisha tabia ya kutazama ponografia (picha ao habari za ngono). Hivi karibuni, nilirudilia tena tabia hiyo. Niliendea wazee ili kuwaomba wanisaidie, na nimefanya maendeleo katika kushinda tabia hiyo. Wazee wamenihakikishia kama Yehova ananipenda na kama yeye ni mwenye rehema. Lakini, wakati fulani, ninaendelea kujisikia kuwa mutu wa bure kabisa, na kama Yehova hawezi kunipenda. Habari ya Victoria ilinisaidia kabisa. Sasa ninatambua kama ninapowaza kama Mungu hawezi kunisamehe, ni sawa vile ninasema kama zabihu ya Mwana wake haitoshi ili kufunika zambi zangu. Nilikata ukurasa uliokuwa na habari hiyo ili niwe nayo kila mahali na kuisoma na kuitafakari kila wakati ninapojisikia kuwa mimi ni mutu wa bure kabisa. Asante kwa habari hizi nzuri sana!”—L. K.