Mashahidi Wa Yehova—Waeneza-Evangeli Wa Kweli
1 Yesu Kristo aliwakabadhi wanafunzi wake wote daraka la kueneza evangeli, akiwaamuru waziwazi kuhubiri habari njema za Ufalme. (Mt. 24:14; Mdo. 10:42) Katika njia hiyo, wanafunzi wa kwanza walitoa kielelezo kwa kusema bila kuacha juu ya Ufalme, si katika mahali pa ibada tu, bali pia kila mahali walipowakuta watu, hadharani na nyumba kwa nyumba. (Mdo. 5:42; 20:20) Leo, sisi tulio Mashahidi wa Yehova, tunajionyesha kuwa waeneza-evangeli wa kweli kupitia mahubiri ya ujumbe wa Ufalme katika nchi 232 na kupitia hesabu ya wale wanaobatizwa iliyofikia zaidi ya wanafunzi wapya milioni moja katika miaka mitatu tu! Kwa nini kazi yetu ya kueneza evangeli imepata fanikio kama hilo?
2 Tunafurahishwa na Habari Njema: Waeneza-evangeli ni wahubiri, au wajumbe, wa habari njema. Tukiwa hivyo, tunalo pendeleo lisilolinganika la kutangaza Ufalme wa Yehova, habari njema pekee ya kweli iwezayo kutolewa kwa wanadamu wanaoteseka. Sisi ni wenye furaha kujua kimbele kwamba mbingu mpya zitaendesha utawala wenye haki juu ya dunia mpya itakayoundwa na wanadamu waaminifu katika Paradiso inayokuja. (2 Pet. 3:13, 17) Tuko peke yetu tulio na tumaini hilo na tunayo tamaa yenye kina ya kulijulisha wengine.
3 Upendo wa Kweli Hutusukuma: Kueneza evangeli ni kazi yenye kuokoa uhai. (Rom. 1:16) Ni kwa sababu hiyo tunahisi furaha kubwa kueneza ujumbe wa Ufalme. Tukiwa waeneza-evangeli wa kweli, tunawapenda wanadamu wenzetu, jambo linalotusukuma kujulisha habari njema kwa familia yetu, kwa majirani zetu, kwa watu tunaowajua na kwa watu wengi iwezekanavyo. Kutimiza kazi hiyo kwa nafsi yetu yote hufanyiza moja ya njia nzuri zaidi za kuonyesha upendo tulio nao kuelekea jirani yetu.—1 Thes. 2:8.
4 Roho Takatifu ya Mungu Hutusaidia: Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba wakati tunapopanda na kutilia maji mbegu ya Ufalme, ni Yehova ndiye “aikuzaye.” Ni roho ya Mungu ndiyo hututegemeza katika utendaji wa kueneza evangeli na inayotuwezesha kupata matokeo bora.—Yoeli 2:28, 29.
5 Tukilinda akilini kitia-moyo kinachotolewa kwenye 2 Timoteo 4:5 cha ‘kufanya kazi ya mweneza-evangeli’ na tukihisi upendo kwa jirani yetu, na tuwe na tamaa ya kujulisha habari njema ya Ufalme yenye kuvutia kwa wakati wote, tukiwa hakika kwamba Yehova ataendelea kubariki kazi yetu!