Watoto—Nyinyi Ni Furaha Yetu!
1 Wavulana na wasichana wadogo, je! mnajua amri ya Yehova ya kwamba mhusishwe katika utendaji wa kutaniko? (Kum. 31:12; Zab. 127:3) Ni furaha kuwa nanyi kando yetu kwa kumwabudu Yehova! Mnachangamsha moyo wetu wakati mnapokaa kwa utulivu kwenye mikutano na kusikiliza kwa uangalifu. Inatufurahisha tena zaidi wakati mnapojaribu kujibu katika maneno yenu wenyewe. Kutaniko lote nzima linafurahishwa wakati mnapotoa vipindi kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, wakati mnapojiunga nasi kwa bidii katika utumishi wa shambani, na wakati tunaposikia kwamba mnatoa ushahidi kwa ujasiri kwa wanashule wenzenu na kwa walimu.—Zab. 148:12, 13.
2 Tunapenda mjue kwamba nyinyi ni kitu cha kujivunia kwetu tunapoona tabia zenu nzuri, utu wenu mzuri wa nje, mwenendo wenu safi, na heshima yenu kuelekea watu wenye umri mkubwa. Furaha yetu ni kubwa tena zaidi wakati mnapoonyesha kwamba ‘mnakumbuka Muumba wenu Mkuu’ kwa kujiwekea wenyewe miradi ya Kitheokrasi.—Mhu. 12:1; Zab. 110:3.
3 Tujulisheni Miradi Yenu: Mvulana mmoja wa miaka nane alimwambia mwangalizi wa wilaya: ‘Kwanza ningependa kubatizwa, ndipo ningependa kusaidia katika kutaniko kwa kushughulika na vikuza-sauti, kwa kuwa mhudumu, nikisaidia katika jumba la vichapo, nikisoma kwenye mafunzo ya kitabu na kwenye mafunzo ya Mnara wa Mlinzi. Ndipo ningependa kuwa mtumishi wa huduma, baadaye mzee. Ningependa vilevile kuwa painia na kwenda kwenye masomo ya mapainia. Ndipo ningependa kwenda kwenye Betheli, kuwa mwangalizi wa mzunguko au mwangalizi wa wilaya.’ Ni uthamini mzuri kama nini aliyouonyesha kuelekea pendeleo la kumtumikia Mungu.
4 Kwa kadiri mnavyofanya maendeleo kimwili na kiroho, tunafurahi kuwaona mkitimiza miradi yenu. (Linganisha Luka 2:52.) Kila mwaka, maelfu kati yenu huwa wahubiri wasiobatizwa na hivyo kujifanya kuwa wenye sifa za kustahili ubatizo kama vile watumishi wa Yehova walio wakfu. Furaha yetu inakomaa wakati tunapowaona baadaye mkifikia kuwa mapainia wasaidizi na hata kuingia katika utumishi wa wakati wote. Kwa kweli, watoto, nyinyi ni furaha yetu na chanzo kizuri ajabu cha sifa kwa Baba yetu wa kimbingu. Yehova na awabariki sana!—Mez. 23:24, 25.