Machozi Yako Yanashangaza
TUNAANZA kulia tangu siku tunazaliwa. Mutu fulani mwenye elimu anaeleza kwamba tulipokuwa watoto wachanga, kulia kulikuwa kama “kitofu kinachounganisha mama na mutoto,” kwa sababu tulilia ili mahitaji yetu ya kimwili na ya kimoyoni yashugulikiwe. Lakini sababu gani tunalia tunapokomaa, wakati ambapo tunaweza kueleza mahitaji yetu katika njia zingine?
Tunatoa machozi ya huzuni ao ya furaha kwa sababu mbalimbali. Tunaweza kutoa machozi kwa sababu ya huzuni, kuvunjika moyo, ao kwa sababu ya kuteseka kimwili ao kiakili. Lakini mambo kama vile musisimuko ao furaha kubwa, kitulizo, na kutimiza jambo fulani yanatokeza pia machozi, ni kusema, machozi ya furaha. Machozi yanaweza pia kuambukiza wengine. Maria anasema hivi: “Ninapomuona mutu fulani akilia, hata sababu iwe nini, ninasukumwa pia kulia.” Pengine hali za kuwazia tu ulizoona katika sinema ao kusoma katika kitabu zimekufanya pia ulie.
Hata kama tunalia kwa sababu gani, kulia ni njia yenye nguvu ya kutoa ujumbe bila kusema neno lolote. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Kuna njia zingine za kusema mambo mengi katika muda huo kidogo sana.” (Adult Crying) Machozi yanachochea watu kutenda. Kwa mufano, wengi kati yetu wanaona kuwa ni vigumu kumuepuka mutu anayelia kwa sababu ya huzuni kwa kuwa machozi hayo yanatuonyesha kwamba mutu fulani anateseka. Hilo linatuchochea tujaribu kumufariji ao kumusaidia mutu anayelia.
Watu fulani wenye elimu wanaamini kwamba kulia ni njia inayofaa ya kuondoa mahangaiko na kwamba kujizuia kila mara kulia kunaweza kuharibu afya yetu. Wengine wanabisha kwamba sayansi haijaonyesha faida za kimwili na za kiakili zinazotokana na kulia. Hata hivyo, uchunguzi mbalimbali uliofanywa unakadiria kwamba wanawake 85 juu ya 100 na wanaume 73 juu ya 100 walisema kwamba, kisha kulia, wanajisikia vizuri. Noemí anaeleza hivi: “Wakati fulani, ninajua kwamba ninahitaji kulia. Kisha kulia, ninaweza kutulia na kuona mambo namna yalivyo kabisa, ni kusema, kuwa na maoni mazuri juu ya mambo hayo.”
Uchunguzi mbalimbali uliofanywa unakadiria kwamba wanawake 85 juu ya 100 na wanaume 73 juu ya 100 walisema kwamba, kisha kulia, wanajisikia vizuri
Lakini kulia haitoshe tu ili kumufanya mutu ajisikie kuwa anatulia. Jambo lingine la maana ni namna watu wengine wanatutendea tunapolia. Kwa mufano, wengine wanapotufariji ao kutusaidia kwa sababu wanaona tunalia, hilo linafanya tutulie. Lakini ikiwa watu hawatuhangaikie tunapolia, tunaweza kusikia haya ao kujisikia kuwa wenye kutupwa.
Ni wazi kwamba kuna mambo mengi ambayo hayajaeleweka kabisa kuhusu kulia. Jambo tunalojua ni kwamba kutoa machozi ni njia moja ya ajabu ya kuonyesha huzuni ao furaha ambayo Mungu ametupatia.