SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO | FRÉDÉRIC DUMOULIN
“Nimeitika Kwamba Kuna Muumbaji”
Kwa zaidi ya miaka kumi, Frédéric Dumoulin alifanya kazi ya utafiti juu ya madawa kwenye Masomo ya Juu ya Ghent, inchi ya Ubelgiji. Wakati fulani hakukuwa anaamini kwamba kuna Mungu. Lakini kisha, Frédéric aliitika kwamba Mungu ndiye aliumba uzima. Gazeti Amuka! lilimuuliza Frédéric, aliye sasa Shahidi wa Yehova, juu ya kazi yake na imani yake.
Ulikuwa katika dini fulani ulipokuwa mutoto?
Ndiyo. Mama yangu alikuwa Mukatoliki. Lakini niliposoma juu ya vita za kidini za kulazimisha watu kuwa Wakristo na mahakama za kuwahukumu watu walioasi dini ya Katoliki, nilichukizwa na dini na sikutaka tena kuingia katika dini yoyote. Nilisoma pia juu ya dini zisizokuwa za Kikristo na nikaona kwamba hazikuwa nzuri. Nilipokuwa na miaka 14, niliona kuwa kuenea kwa mambo mabaya katika dini kunaonyesha kwamba hakuna Mungu. Kwa hiyo, wakati nilijifunza juu ya fundisho la mageuzi kwenye masomo, niliamua kwamba uzima ulitokana na hatua za asili.
Namna gani ulifikia kupendezwa na sayansi?
Nilipokuwa na miaka saba, nilipewa mikroskope na ikakuwa kitu changu cha kuchezea nilichopenda sana. Niliitumia kwa njia nyingi, kwa mufano kuchunguza wadudu wenye kuvutia, kama vile vipepeo.
Namna gani ulipendezwa na jinsi uzima ulianza?
Nilipokuwa na miaka 22, nilikutana na mwanasayansi mumoja mwanamuke aliyekuwa Shahidi wa Yehova. Aliamini kwamba Mungu aliumba uzima. Hilo lilionekana kuwa jambo jipya kwangu. Nilifikiri kwamba nitamusadikisha kwa vyepesi kuwa imani yake ni ya kipumbavu. Lakini nilishangaa nilipoona kwamba alikuwa na majibu mazuri kwa maulizo yangu. Nilianza kutafuta kujua mambo mengi juu ya watu wanaoamini Mungu.
Miezi michache kisha hapo, nilikutana na Shahidi mwengine wa Yehova aliyekuwa anajua mambo ya matunzo. Wakati aliniambia kwamba anataka kunifasiria mambo anayoamini, nilikubali kwa sababu nilipenda kujua sababu gani watu wanaamini Mungu. Nilitaka kumuondoa katika udanganyifu wake.
Ulimuitikisha kwamba alikuwa anadanganyika?
Hapana, sikuweza. Nilianza kutafuta habari juu ya namna uzima ulianza. Nilishangaa kuona kwamba wanasayansi fulani wenye kujulikana sana wanasema kuwa hata chembe yenye uzima iliyo nyepesi zaidi ni ngumu sana kueleweka hivi kwamba haingewezekana ijitokeze yenyewe duniani. Wamoja kati yao wanafikiri kwamba chembe kama hizo zilitoka katika anga. Hawaelewane katika mambo mengi juu ya namna uzima ulianza.
Wanapatana katika jambo fulani?
Jambo la kushangaza ni kwamba wanasayansi wengi wanakubali kuwa, kwa njia fulani, hatua za asili zilifanya uzima utokane na vitu visivyo na uzima. Nilianza kujiuliza, ‘Ikiwa hawajue namna uzima ulitokea bila Muumbaji, namna gani wanaweza kuwa na uhakika kwamba ulitokea kwa njia hiyo?’ Nilianza kuchunguza mambo Biblia inasema juu ya namna uzima ulianza.
Ulifikia kuwa na maoni gani juu ya Biblia?
Nilipoendelea kujifunza Biblia zaidi, niliendelea kusadikishwa zaidi kuwa inasema kweli. Kwa mufano, ni hivi karibuni tu ndipo wanasayansi walipata mambo yanayosadikisha kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Lakini andiko la kwanza la Biblia, lililoandikwa kumepita miaka 3500 hivi, linasema: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”a Tena nilitambua kwamba, kila mara Biblia inapozungumuzia mambo ya sayansi, haidanganyike.
Nilitambua kwamba, kila mara Biblia inapozungumuzia mambo ya sayansi, haidanganyike
Kujua kwako mambo ya sayansi kulifanya iwe vigumu kwako kuamini Mungu?
Hapana. Wakati niliamini Mungu, nilikuwa nimefanya miaka tatu nikijifunza sayansi kwenye masomo ya juu. Kufikia leo, kadiri ninajifunza namna vitu vilivyo na uzima vilifanywa, ndivyo ninasadiki zaidi kwamba kuna Muumbaji.
Unaweza kutupatia mufano?
Ndiyo. Nimejifunza matokeo ya dawa na ya sumu katika viumbe vilivyo na uzima. Kitu kinachonishangaza ni namna ubongo wetu unalindwa na vitu hatari na bakteria. Kuna kizuizi kinachotenganisha damu na chembe za ubongo wetu.
Ni nini inashangaza juu ya jambo hilo?
Zaidi ya miaka mia moja iliyopita, wachunguzi walitambua kwamba vitu vinavyoingia ndani ya damu vinafika katika sehemu zote za mwili, lakini havifike katika ubongo na katika uti wa mugongo. Jambo hilo linanishangaza sana, kwa sababu mufumo mukubwa wa mishipa midogo-midogo sana unapeleka damu katika kila chembe ya ubongo. Chembe zote za ubongo zinasafishwa, zinalishwa, na kupata hewa kupitia damu. Sasa, namna gani damu yetu inatenganishwa na chembe za ubongo wetu? Kwa miaka mingi, jambo hilo halikueleweka.
Kizuizi hicho kinatumika namna gani?
Mishipa ya damu iliyo midogo sana si kama mirija (tuyeaux) ya plastiki inayotenganisha vitu vilivyo ndani na vile vilivyo inje. Vizuizi vya mishipa ya damu vimetengenezwa na chembe. Chembe hizo zinaruhusu vitu na mikrobi vipite ndani yazo na kati yazo. Lakini, chembe zinazofanyiza mishipa ya damu katika ubongo wetu ziko tofauti. Zinaunganishwa sana kati yazo. Chembe hizo na maunganisho yazo ni mambo yanayoshangaza sana. Utendaji mbalimbali ulio mugumu sana kueleweka unahakikisha kwamba vitu kama vile oksijeni, kaboni dioksidi, na sukari, vinapita ndani ya damu na ubongo kwa njia yenye kuongozwa vizuri. Lakini protini, chembe mbalimbali, na vitu vingine haviruhusiwe kuingia ndani. Kwa hiyo, kizuizi kinachozuia damu isiingie katika ubongo kinafanya kazi kama molekuli ili kutokeza vizuizi vingine vya kimwili, kikemikali, na kielektriki. Mimi niliona kuwa namna kizuizi hicho kilifanywa haingejitokeza kupitia mageuzi.
a 1. Mwanzo 1:1.