MAONI YA BIBLIA
Ubaguzi Wa Rangi
Rangi mbalimbali za wanadamu zilianza namna gani?
‘Adamu akamuita muke wake jina lake Hawa [ao Eva], kwa sababu ndiye angekuja kuwa mama ya kila mutu anayeishi.’—Mwanzo 3:20.
MAMBO WATU WENYE ELIMU WANASEMA
: Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) linasema kwamba “wanadamu wote ni wa aina moja na wametoka katika ukoo moja.”—Maelezo Juu ya Rangi na Ubaguzi wa Rangi, 1978.
MAMBO BIBLIA INASEMA
: Mungu aliumba wanadamu wawili, Adamu na Eva, na akawaambia hivi: ‘Zaeni, muwe wengi, mujaze dunia na kuitiisha.’ (Mwanzo 1:28) Kwa hiyo, Adamu na Eva walikuja kuwa baba na mama wa wanadamu wote. Kisha, wakati garika iliua kabisa karibu wakaaji wote wa dunia, wanaume ine pamoja na bibi zao waliokoka, ni kusema, Noa na bibi yake pamoja na watoto wao wanaume watatu na bibi zao. Biblia inafundisha kwamba sisi wote tulitokana na watoto wa Noa.—Mwanzo 9:18, 19.
Kuna rangi iliyo nzuri zaidi kupita nyingine?
‘[Mungu] alifanya kutoka kwa mutu mumoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima.’—Matendo 17:26.
MAMBO WATU FULANI WAMESEMA
: Kati ya mwaka wa 1901 na 2000, watu wengi walianza kuwa na mawazo ya ubaguzi wa rangi. Kwa mufano, Wanazi walisema kwamba rangi yao ilikuwa nzuri zaidi kupita zingine kwa sababu ya chembe zao za uriti. Kwa upande mwengine, maandishi ya UNESCO yaliyotajwa hapo nyuma yalionyesha “umaana wa umoja wa rangi ya wanadamu na kwa hiyo usawa wa musingi wa wanadamu wote na watu wote.”
MAMBO BIBLIA INASEMA
: Andiko la Matendo 10:34, 35 linasema hivi: ‘Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mutu ambaye anamuogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.’ Kwa sababu hiyo, hakuna mutu aliye na haki ya kuona rangi moja kuwa nzuri zaidi kupita nyingine.
Yesu aliwawekea Wakristo kanuni alipowaambia wanafunzi wake hivi: ‘Ninyi wote ni ndugu.’ (Mathayo 23:8) Alisali kwamba wafuasi wake wawe na umoja na “kukamilishwa kuwa kitu kimoja,” ni kusema, wasitengane wala kubaguana.—Yohana 17:20-23; 1 Wakorintho 1:10.
Ubaguzi wa rangi utaisha siku fulani?
‘Katika siku za mwisho mulima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara . . . , na mataifa yote yatamiminika huko.’—Isaya 2:2.
MAMBO WATU FULANI WANAWAZA: Ubaguzi wa rangi unaoendelea kuongezeka unafanya watu katika inchi nyingi wajiulize ikiwa kwa kweli kuna maendeleo fulani makubwa ambayo yamefanywa ili kushugulikia ubaguzi wa rangi. Wamoja kati yao wanasema kuwa ubaguzi wa rangi hautaisha hata siku moja.
MAMBO BIBLIA INASEMA: Mungu hataacha chuki inayotokana na ubaguzi wa rangi iendelee milele. Lakini, katika Ufalme wake, wanaume na wanawake ‘kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na luga’ watamutumikia kwa umoja, wakionyeshana upendo wa kweli. (Ufunuo 7:9) Ufalme wa Mungu si hali ya kuwazia ya moyo wa mutu. Lakini, ni serikali itakayoleta mabadiliko makubwa katika dunia yetu, mahali Mungu alikusudia watu wote waishi bila vizuizi vinavyotokana na ubaguzi wa rangi.a
a Ili kupata habari zingine, soma sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Unaweza pia kupata kitabu hicho kwenye adresi yetu ya Internete www.jw.org.