SURA YA 14
Uwe Mutu Mwenye Kuaminika Katika Mambo Yote
“Tunataka kujiendesha kwa unyoofu [ao kwa kuaminika] katika mambo yote.”—WAEBRANIA 13:18.
1, 2. Sababu gani Yehova anafurahi anapotuona tunajikaza kuwa watu wenye kuaminika? Toa mufano.
MAMA na mutoto wake wanatoka katika magazini fulani. Mara moja mutoto anasimama, na uso wake una wasiwasi. Katika mukono ana kitu cha kuchezea ambacho alikamata na alisahau kukirudisha; alitaka kumuomba mama yake amununulie kitu hicho lakini alisahau. Analia sana na anamuuliza mama yake afanye nini. Mama anamutuliza na anarudi naye katika magazini ili arudishe kitu hicho na kuomba musamaha. Wakati mutoto anapofanya hivyo, mama anamuangalia; moyo wa mama unajaa na furaha na anajivunia mutoto wake. Sababu gani?
2 Wazazi wanafurahi sana wanapoona watoto wao wanajifunza kuwa watu wenye kuaminika. Baba yetu wa mbinguni, ambaye ni “Mungu wa ukweli,” anajisikia hivyo pia. (Zaburi 31:5) Anafurahi wakati anatuona tunaendelea kukomaa kiroho na namna tunavyofanya nguvu ya kuwa watu wenye kuaminika. Kwa kuwa tunataka kumupendeza na kubaki katika upendo wake, sisi pia tunasema kama mutume Paulo: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu [ao kwa kuaminika] katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Tuchunguze sehemu ine kubwa za maisha yetu ambamo wakati mwengine inaweza kuwa vigumu kuwa watu wenye kuaminika. Kisha tutazungumuzia faida fulani za kuwa watu wenye kuaminika.
EPUKA KUJIDANGANYA
3-5. (a) Neno la Mungu linatupa maonyo gani kuhusu hatari za kujidanganya? (b) Ni nini itakayotusaidia tujichunguze kabisa vile tulivyo?
3 Tatizo letu la kwanza ni lile la kujichunguza sisi wenyewe ikiwa tuko wenye kuaminika. Kwa kuwa sisi ni watu wasio wakamilifu, ni rahisi sana kujidanganya. Kwa mufano, Yesu aliwaambia Wakristo wa Laodikia kwamba walikuwa wanajidanganya kwa sababu walikuwa wanafikiri kwamba wao ni matajiri, kumbe kwa kweli walikuwa ‘masikini na vipofu na uchi’ kiroho; hali yao ilikuwa yenye kusikitisha kwelikweli. (Ufunuo 3:17) Kwa sababu walikuwa wenye kujidanganya, hali yao ilikuwa katika hatari zaidi.
4 Unakumbuka pia kama mwanafunzi Yakobo aliwaonya Wakristo hivi: ‘Ikiwa mutu yeyote anajiona kuwa muabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongoze [ao hazuie] ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mutu huyo ni ya ubatili [ao bure].’ (Yakobo 1:26) Ikiwa tunawaza kwamba hata tukitumia ulimi wetu vibaya Yehova ataikubali ibada yetu, tunajidanganya. Ibada yetu kwa Yehova itakuwa bure, kupoteza tu wakati. Ni nini inayoweza kutusaidia ili tusipatwe na jambo hilo mbaya?
5 Katika sura hiyohiyo, Yakobo analinganisha kweli ya Neno la Mungu na kioo. Anatushauri tujichunguze katika sheria kamilifu ya Mungu ili tutengeneze yale tunayopaswa kutengeneza katika maisha yetu. (Yakobo 1:23-25) Biblia inaweza kutusaidia kujichunguza kwa uaminifu na kuona mabadiliko tunayopaswa kufanya. (Maombolezo 3:40; Hagai 1:5) Pia, tunaweza kusali kwa Yehova na kumuomba atuchunguze, na kutusaidia tutambue mahali tuna uzaifu sana ili tuutengeneze. (Zaburi 139:23, 24) Hali ya kukosa kuaminika ni uzaifu usiotambulika vyepesi, na tunapaswa kuona uzaifu huo kama Baba yetu wa mbinguni anavyouona. Andiko la Methali 3:32, linasema: “Mutu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova, lakini urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu [ao watu wenye kuaminika].” Yehova anaweza kutusaidia ili tuwe na maoni kama yake na kujiona kama anavyotuona. Kumbuka kama mutume Paulo alisema: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu.” Leo, sisi si watu wenye kukamilika, hata hivyo, kwa kweli tunataka na tunajikaza sana kuwa watu wenye kuaminika.
EPUKA KUDANGANYA WENGINE KATIKA FAMILIA
Kuonyesha uaminifu kunatusaidia kuepuka matendo fulani yenye tunaweza kujaribu kuficha
6. Sababu gani bwana na bibi wanapaswa kuwa watu wenye kuaminika, wakiwa hivyo wataepuka hatari gani?
6 Katika familia ya Kikristo kila mutu anapaswa kujulikana kuwa mwenye kuaminika. Kwa hiyo, bwana na bibi hawapaswe kufichana mambo. Mukristo mwenye kuoa ao kuolewa hapaswe kufanya mambo machafu na yenye kuumiza mwengine. Kwa mufano, hapaswe kuchezeana kimapenzi na mutu asiyekuwa bibi yake ao bwana yake, kuwa na urafiki wa kisiri na mutu mwengine kupitia Internete, kutazama picha za watu walio uchi ao wanaofanya mambo machafu kwenye Internete. Wakristo wengine wenye kuoa ao kuolewa waliangukia katika mambo mabaya kama hayo na kuwaficha bwana zao ao bibi zao mambo hayo. Kufanya hivyo ni kuwa mudanganyifu. Fikiria maneno ambayo Mufalme mwaminifu Daudi, alisema: ‘Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingie pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.’ (Zaburi 26:4) Ikiwa umekwisha kuoa ao kuolewa, usifanye hata kidogo mambo yanayoweza kukushawishi kumuficha mwenzi wako jinsi ulivyo!
7, 8. Ni mifano gani iliyo katika Biblia inayoweza kusaidia watoto wajifunze faida ya kuwa watu wenye kuaminika?
7 Wazazi wanapofundisha watoto wao faida za kuwa watu wenye kuaminika, ni vizuri zaidi watumie mifano iliyo katika Biblia. Wazazi wanapozungumuzia mifano ya watu wasioaminika, wanaweza kutaja habari ya Akani, ambaye aliiba na kujaribu kuficha tendo lake; Gehazi, ambaye alisema uongo ili wamupatie feza; na Yuda, ambaye aliiba na kusema uongo ili Yesu auawe.—Yoshua 6:17-19; 7:11-25; 2 Wafalme 5:14-16, 20-27; Mathayo 26:14, 15; Yohana 12:6.
8 Wazazi wanapowafundisha watoto wao faida za kuwa watu wenye kuaminika, wanaweza kutaja habari ya Yakobo, ambaye aliwaomba watoto wake warudishe feza ambazo walikuta katika mifuko yao, kwa kuwa alifikiri mutu fulani alisahau na kuzitia humo. Mufano mwengine ni ule wa Yeftha na binti yake: walitimiza naziri ya Yeftha kwa kujizabihu sana. Pia, Yesu ambaye hakujificha wakati kundi kubwa la watu walikuja kumufunga; alifanya hivyo kwa uhodari ili atimize unabii na kuwalinda marafiki wake. (Mwanzo 43:12; Waamuzi 11:30-40; Yohana 18:3-11) Mifano hiyo michache inaweza kusaidia wazazi waone kama Neno la Mungu lina habari za maana sana wanazoweza kutumia ili kufundisha watoto wao kupenda tabia ya kuaminika na kuona faida ya kuwa mutu mwenye kuaminika.
9. Wazazi wanapaswa kuepuka nini ikiwa wanataka kuwawekea watoto wao mufano wa kuwa watu wenye kuaminika, na kwa nini mufano wao ni wa maana?
9 Mafundisho hayo yanawasaidia wazazi wajue kama wao wenyewe wana daraka kubwa. Mutume Paulo aliuliza hivi: ‘Je, wewe unayemufundisha mutu mwengine, haujifundishe mwenyewe? Wewe, unayehubiri usiibe, je, wewe unaiba?’ (Waroma 2:21) Wazazi fulani wanavuruga watoto akili, kwa sababu wanawafundisha watoto wao wawe watu wenye kuaminika, lakini wao wenyewe si wenye kuaminika. Wakati wanaiba vitu vidogo-vidogo na kusema uongo, wanatoa visababu na kujitetea; wanaweza kusema “Aa! Bwana wangu wa kazi anajua kama wafanyakazi wanachukua vitu hivi” ao “Huo ni uongo mudogo tu.” Lakini, kusema kweli, wizi ni wizi, iwe mutu anachukua kitu kidogo ao kikubwa; na uongo ni uongo, iwe mazungumuzo ni juu ya nini ao kutia chumvi katika habari fulani.a (Luka 16:10) Ni vyepesi kwa watoto kutambua unafiki na jambo hilo linawaharibisha sana. (Waefeso 6:4) Lakini, wanapojifunza kuwa watu wenye kuaminika kwa kufuata mifano ya wazazi wao, labda watakapokomaa watamutukuza Yehova katika ulimwengu huu wa watu wadanganyifu.—Methali 22:6.
EPUKA KUDANGANYA KUTANIKO
10. Ili tuwe wenye kuaminika, tunapozungumuza na ndugu na dada zetu, tunapaswa kuepuka nini?
10 Kuwa pamoja na ndugu na dada zetu Wakristo kunatutolea nafasi nyingi za kuonyesha kama sisi ni wenye kuaminika. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 12, tunapaswa kuwa waangalifu juu ya kutumia zawadi ya kusema, hasa tunapokuwa na ndugu na dada zetu wa kiroho. Mazungumuzo ya kawaida yanaweza kugeuka na kuwa kuteta, na hata kusingizia wengine! Tukiwaelezea wengine mambo ambayo hatujue yametoka wapi, labda tunaweza kusaidia kueneza uongo; kwa hiyo, ni vizuri kuzuia midomo yetu. (Methali 10:19) Kwa upande mwengine, hata ikiwa tunajua kwamba jambo fulani ni la kweli, hatulazimishwe kulisema. Kwa mufano, labda jambo hilo halituangalie, ao si vizuri tu kulisema. (1 Wathesalonike 4:11) Watu fulani wanasema bila adabu, kisha wanajitetea kwamba wako hivyo kwa sababu wao si wanafiki, lakini maneno yetu yanapaswa kuwa yenye neema na yenye fazili.—Wakolosai 4:6.
11, 12. (a) Namna gani ndugu fulani waliofanya zambi nzito wanafanya mambo yawe mabaya zaidi? (b) Ni mambo gani ya uongo Shetani ameeneza juu ya zambi nzito, na tunaweza kupinga mambo hayo namna gani? (c) Namna gani tunaweza kuonyesha kuwa sisi ni watu wenye kuaminika kuelekea tengenezo la Yehova?
11 Ni lazima sana tusiwadanganye wale wanaoongoza kutaniko. Ndugu fulani waliofanya zambi nzito wamefanya mambo yawe mabaya zaidi kwa kujaribu kuficha zambi yao na kuwadanganya wazee wa kutaniko wakati wanapowauliza. Wanaanza hata kuishi maisha ya unafiki; wanajifanya kuwa wanamutumikia Yehova na kwa upande mwengine wanaendelea kutenda zambi nzito. Kwa kweli, watu kama hao wanaishi katika uongo. (Zaburi 12:2) Wengine wanawaambia wazee ukweli nusu na wanaficha mambo ya lazima. (Matendo 5:1-11) Mara nyingi udanganyifu kama huo unatokana na kuamini mambo ya uongo ambayo Shetani ameeneza.—Soma kisanduku “Mawazo ya Uongo ya Shetani Kuhusu Zambi Nzito.”
12 Jambo lingine la lazima ni kwamba hatupaswe kudanganya tengenezo la Yehova tunapojaza fomu mbalimbali. Kwa mufano, tunapotoa ripoti ya mahubiri, tunapaswa kuwa waangalifu tusiandike mambo ya uongo. Vilevile, tunapojaza fomu kuhusu pendeleo fulani la utumishi, hatupaswe kujaza habari zisizo za kweli juu ya afya yetu ao kudanganya kuhusu mambo mengine yanayoombwa.—Methali 6:16-19.
13. Namna gani tunaweza kuonyesha kama sisi ni watu wenye kuaminika tunapofanya mambo ya biashara na Wakristo wenzetu, tunapokuwa bwana wa kazi ao wafanyakazi wa ndugu zetu?
13 Tunapaswa kuwa watu wenye kuaminika kwa ndugu zetu Wakristo tunapofanya pia mambo ya biashara ao kazi. Kuna wakati ndugu fulani anaweza kusikilizana kufanya biashara na ndugu ao dada mwengine. Lakini, hawapaswe kufanya mambo yao ya biashara wanapokuwa kwenye Jumba la Ufalme kwa ajili ya ibada ao mahubiri. Na inawezekana pia ndugu fulani awe mufanyakazi wa ndugu mwengine. Ikiwa ndugu fulani ni bwana wa kazi wa ndugu na dada fulani, anapaswa kuwatendea bila udanganyifu, ni kusema, kuwalipa mushahara wao tarehe na saa waliyosikilizana, kiasi cha feza walichosikilizana, na kuwatimizia mambo mengine ambayo walisikilizana ao ambayo sheria ya serikali inaomba. (1 Timotheo 5:18; Yakobo 5:1-4) Kwa upande mwengine, ikiwa sisi ni wafanyakazi wa ndugu ao dada yetu, tunapaswa kufanya kazi vizuri kwa ajili ya mushahara tutakaolipwa. (2 Wathesalonike 3:10) Hatupaswe kutazamia bwana wa kazi kwa sababu ni ndugu wa kiroho atutendee tofauti na wengine; bwana huyo wa kazi hata ikiwa ni ndugu halazimishwe kutupatia mapumuziko ao faida zingine ambazo wafanyakazi wengine hawapewe.—Waefeso 6:5-8.
14. Wakristo wanapofanya biashara pamoja, wanapaswa kufanya nini ili kuepuka magumu, na kwa nini?
14 Tutafanya nini ikiwa tumesikilizana na ndugu fulani kufanya biashara pamoja ao tunapenda atukopeshe feza ili kufanya biashara? Biblia inatutolea kanuni moja ya lazima inayoweza kutusaidia: Muandike mambo yote muliyosikilizana! Tuchukue mufano wa Yeremia, aliponunua sehemu ya shamba, waliandikiana karatasi ya makubaliano iliyokuwa na kopi mbili, kulikuwa pia na mashahidi walioshuhudia, naye aliichunga mahali salama ili iweze kurudiliwa wakati ujao ikiwa ilihitajiwa. (Yeremia 32:9-12; soma pia Mwanzo 23:16-20.) Tunapofanya biashara na Wakristo wenzetu, kuandika makubaliano yote, kutia sinyatire, na kuwa na mashahidi wanaoshuhudia ni vizuri, na kufanya hivyo hakumaanishe kwamba hatuwaaminie ndugu zetu. Badala yake, kufanya hivyo kunawasaidia kuepuka kukorogana, kuvunjika moyo, na hata ugomvi; mambo ambayo yanaweza kutokeza migawanyiko. Wakristo wanaofanya biashara pamoja wanapaswa kukumbuka kwamba biashara yoyote haipaswe kuhatarisha umoja na amani ya kutaniko.b—1 Wakorintho 6:1-8.
UWE MUTU MWENYE KUAMINIKA
15. Yehova anaona namna gani mazoea ya udanganyifu katika mambo ya biashara, na Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani juu ya mazoea hayo hata ikiwa yanaenea sana leo?
15 Mukristo anapaswa kuwa mwenye kuaminika si katika kutaniko tu. Mutume Paulo alisema: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Muumbaji wetu anatazamia tuwe kabisa wenye kuaminika katika kazi zetu. Katika kitabu cha Methali peke yake, mistari ine inazungumuzia mizani ao kipimo cha kudanganya. (Methali 11:1; 16:11; 20:10, 23) Wakati wa zamani, kwa kawaida watu walitumia mizani na mawe ya mizani katika mambo ya biashara ili kupima uzito wa vitu vinavyouzishwa ao kuuzwa na pia feza ambazo mutu alilipa. Wafanyabiashara wasioaminika ao wadanganyifu walitumia mizani ya namna mbili za mawe ili kuwadanganya na kuwaibia watu wenye kununua vitu vyao.c Yehova anachukia matendo kama hayo! Ili tubaki katika upendo wake, tunapaswa kuepuka kabisa mazoea yote ya udanganyifu katika mambo ya biashara.
16, 17. Leo, watu wengi wanajiingiza katika mazoea gani ya udanganyifu, na Wakristo wa kweli wanapaswa kuazimia kufanya nini?
16 Kwa sababu Shetani ndiye mutawala wa ulimwengu huu, si jambo la kushangaza kwamba udanganyifu unaenea kila mahali. Kila siku tunaweza kujaribiwa ili tufanye mambo ya udanganyifu. Watu wanaotafuta kazi wanapoandika mambo juu yao wenyewe wanadanganya ao kutia chumvi juu ya kazi ambayo wanajua ao masomo waliyosoma. Watu wengine wanadanganya wanapotafuta vikaratasi ili kuenda katika inchi za kigeni, wanapoombwa kulipa kodi ao wakati wa kuvukisha vitu kwenye mupaka wa inchi, na mambo mengine kama hayo. Wanafunzi wengi wanaiba majibu wakati wa mashindano, ao wanatumia habari zilizoandikwa na watu wengine kwenye Internete ili kufanya devuare yao na hivyo wanadanganya kwamba walitumia akili zao na kumbe walitegemea akili ya mutu mwengine. Watu wengine wanawapatia wafanyakazi wa serikali ao polisi “kata-midomo ao rushwa” ili kupata wanachotaka. Mambo hayo hayatushangaze kwa sababu watu wengi sana katika ulimwengu ni “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiopenda wema.”—2 Timotheo 3:1-5.
17 Wakristo wa kweli wameazimia kutojiingiza katika mazoea hayo hata kidogo. Wakati mwengine ni vigumu kuwa mutu mwenye kuaminika kwa sababu katika dunia ya leo inaonekana kwamba mara nyingi ni watu wadanganyifu ao wasioaminika ndio wanakuwa kama wenye kubarikiwa na kusonga mbele. (Zaburi 73:1-8) Wakati huohuo, Wakristo wanaweza kuwa na matatizo ya feza kwa sababu wanataka kubaki wenye kuaminika “katika mambo yote.” Je, kujinyima hivyo kuna faida yoyote? Ndiyo kabisa! Sababu gani tunajibu hivyo? Kuwa mutu mwenye kuaminika kuna faida gani?
FAIDA ZA KUWA MUTU MWENYE KUAMINIKA
18. Sababu gani kujulikana kuwa mutu mwenye kuaminika ni jambo la lazima sana?
18 Katika maisha, kujulikana kuwa mwenye kuaminika ao asiyekuwa mudanganyifu ni jambo la maana sana kuliko mambo mengine yote. (Soma kisanduku “Je, Mimi Ni Mwenye Kuaminika Kabisa?”) Na jambo la ajabu ni kwamba kila mutu anaweza kuwa na sifa hiyo! Haitegemee akili ya mutu, mali yake, sura yake, mahali mutu amezaliwa, ao hali nyingine yoyote inayopita uwezo wako. Hata hivyo, ni watu wachache tu ndio walio na sifa hiyo ya maana sana. Watu wenye kuaminika si wengi. (Mika 7:2) Watu wengine wanaweza kukuchekelea kwa sababu wewe ni mutu mwenye kuaminika, lakini wengine watakufurahia, na kwa hiyo watakutumainia na kukuheshimu. Mashahidi wa Yehova wengi wamejionea kwamba kuwa watu wenye kuaminika kumewaletea faida nyingi. Wengine walibaki katika kazi yao wakati wale wafanyakazi wasiokuwa wenye kuaminika walifukuzwa; wengine walipata kazi kwa sababu bwana wa kazi alikuwa anatafuta tu mutu mwenye kuaminika.
19. Kuwa watu wenye kuaminika kunaweza kuwa na matokeo gani juu ya zamiri yetu na juu ya uhusiano wetu pamoja na Yehova?
19 Hata ikiwa mambo ya namna hiyo hayajakufikia, jua kama kuwa mutu mwenye kuaminika kunaleta faida nyingi hata zaidi. Utakuwa na zamiri safi. Kwa mufano, mutume Paulo aliandika: ‘Sisi tuna uhakika kwamba tuna zamiri nyoofu ao safi.’ (Waebrania 13:18) Zaidi ya hilo, Baba yetu wa mbinguni hakose kuona jina lako nzuri, naye anawapenda watu wenye kuaminika. (Zaburi 15:1, 2; Methali 22:1) Ndiyo, kuwa mutu mwenye kuaminika kunakusaidia ubakie katika upendo wa Mungu, na hiyo ndio zawabu ya maana sana kwa Mukristo. Acha tuchunguze sasa jambo lingine linalopatana na sifa hiyo ya kuaminika: Mawazo ya Yehova juu ya kazi.
a Katika kutaniko, Mukristo anapozoea kusema uongo kimakusudi ili kuwaumiza wengine, halmashauri ya hukumu inaweza kuundwa.
b Ili ujue yale unayoweza kufanya wakati matatizo yanatokea katika mapatano ya biashara, soma Nyongeza “Namna ya Kumaliza Kutoelewana Katika Mambo ya Biashara.”
c Wafanyabiashara walikuwa wanatumia aina moja ya mawe ya mizani waliponunua vitu na ile nyingine walipouzisha vitu, katika njia zote mbili walijifaidi wenyewe tu. Pia, wakati mwengine walitumia mizani ambayo upande wake mumoja ulikuwa murefu zaidi ao muzito zaidi ya ule mwengine ili kumudanganya mutu anayenunua vitu.