SURA YA 8
Ufalme wa Mungu Ni Nini?
1. Tutazungumuzia sala gani yenye kujulikana sana?
MAMILIONI ya watu wanajua sala yenye kuitwa, sala ya Baba Yetu ao Sala ya Bwana. Yesu alitumia sala hiyo ili kufundisha wanafunzi wake namna ya kusali. Yesu alisali juu ya mambo gani? Na juu ya nini tunaona sala hiyo kuwa ya maana leo?
2. Yesu alitufundisha tusali juu ya mambo gani tatu ya maana?
2 Yesu alisema hivi: “Basi ninyi munapaswa kusali hivi: ‘Baba yetu mwenye kuwa mbinguni, jina lako litakaswe [ao, lifanywe kuwa takatifu]. Ufalme wako ukuje. Mapenzi yako yafanyike duniani kama mbinguni.’” (Soma Matayo 6:9-13.) Juu ya nini Yesu alitufundisha tusali juu ya mambo hayo tatu?—Ona Mafasirio Ingine ya 20.
3. Tunapaswa kujua nini juu ya Ufalme wa Mungu?
3 Tumejifunza kama jina la Mungu ni Yehova. Na tumejifunza mapenzi ya Mungu ni nini juu ya wanadamu na dunia. Lakini Yesu alipenda kusema nini wakati alisema: “Ufalme wako ukuje”? Mu habari hii, tutajua Ufalme wa Mungu ni nini, mambo yenye utafanya, na namna utatakasa jina la Mungu.
UFALME WA MUNGU NI NINI?
4. Ufalme wa Mungu ni nini? Mufalme wa Ufalme huo ni nani?
4 Yehova alisimamisha serikali ao guvernema mbinguni, na akamuchagua Yesu akuwe Mufalme wa serikali hiyo. Biblia inaita serikali hiyo, Ufalme wa Mungu. Yesu ni “Mufalme wa wale wenye kutawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale wenye kutawala wakiwa mabwana.” (1 Timoteo 6:15) Yesu anaweza kufanyia watu mambo ya muzuri sana kupita watawala wote wanadamu. Na hata kama watawala wote wanadamu wanawekwa pamoja, Yesu iko na nguvu kupita watawala hao wote.
5. Ufalme wa Mungu uko wapi? Utatawala nini?
5 Siku makumi ine kisha Yesu kufufuliwa, alirudia mbinguni. Na kisha wakati fulani, Yehova alimufanya Yesu kuwa Mufalme wa Ufalme wake. (Matendo 2:33) Ufalme wa Mungu uko mbinguni lakini utatawala dunia. (Ufunuo 11:15) Njo maana Biblia inaita Ufalme wa Mungu ‘Ufalme wa mbinguni.’—2 Timoteo 4:18.
6, 7. Juu ya nini Yesu njo mufalme muzuri zaidi kupita wafalme wote wanadamu?
6 Biblia inasema kama Yesu ni mukubwa kupita wafalme wote wanadamu juu ni “yeye peke yake mwenye hawezi kufa.” (1 Timoteo 6:16) Viongozi wote wanadamu wanafikia kufa, lakini Yesu hatakufa hata siku moja. Mambo yote ya muzuri yenye Yesu atatufanyia yataendelea milele.
7 Unabii wa Biblia unasema kama Yesu atakuwa Mufalme mwenye haki na huruma. Biblia inasema hivi: “Roho ya Yehova itakaa juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumuogopa Yehova. Na atapata shangwe katika kumuogopa Yehova. Hatahukumu kulingana na mambo yenye anaona kwa macho yake, wala kukaripia [ao, kushauria] kulingana tu na mambo yenye anasikia kwa masikio yake. Atahukumu kwa haki watu wa hali ya chini [ao, maskini].” (Isaya 11:2-4) Unapenda kuwa na mufalme kama huyo?
8. Ni nini inaonyesha kama Yesu hatatawala yeye mwenyewe?
8 Mungu amechagua watu fulani ili watawale pamoja na Yesu katika serikali ya mbinguni. Kwa mufano, mutume Paulo alimuambia Timoteo hivi: “Kama tunaendelea kuvumilia, tutatawala pia pamoja naye tukiwa wafalme.” (2 Timoteo 2:12) Ni watu ngapi watakuwa wafalme pamoja na Yesu?
9. Ni watu ngapi watatawala pamoja na Yesu? Mungu alianza kuwachagua wakati gani?
9 Kama vile tulijifunza mu Sura ya 7, mutume Yohana alipewa maono. Mu maono hayo aliona Yesu iko Mufalme mbinguni pamoja na wafalme wengine 144 000. Wale 144 000 ni nani? Yohana anaeleza kama ‘jina [la Yesu] na la Baba yake limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao.’ Anaongeza hivi: “Hao ndio wale wenye wanaendelea kumufuata Mwana-Kondoo [ni kusema, Yesu] kila mahali anaenda. Hao walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu.” (Soma Ufunuo 14:1, 4.) Wale 144 000 ni Wakristo waaminifu wenye Mungu amechagua ili ‘watawale wakiwa wafalme juu ya dunia’ pamoja na Yesu. Wakati wanakufa, wanafufuliwa kusudi waishi mbinguni. (Ufunuo 5:10) Kuanzia wakati wa mitume, Yehova anachagua Wakristo waaminifu ili wakuwe mu kikundi cha wale wafalme 144 000.
10. Yehova alifanya mipango ili Yesu na wale 144 000 watawale wanadamu. Juu ya nini jambo hilo linaonyesha kama anatupenda?
10 Yehova anatuhangaikia sana njo maana amefanya mipango ili wanadamu watawale pamoja na Yesu. Yesu atakuwa mutawala muzuri juu anatuelewa. Yeye pia alikuwa mwanadamu na aliteseka. Paulo alisema kama Yesu anatusikilia huruma, anaweza “kusikilia uzaifu wetu huruma,” na “amejaribiwa katika mambo yote kama vile sisi.” (Waebrania 4:15; 5:8) Wale 144 000 nao pia wanaweza kuelewa magumu yetu. Nao wamepiganisha hali ya kukosa kukamilika na magonjwa. Kwa hiyo, tunaweza kuamini kabisa kama Yesu na wale 144 000 wataelewa namna tunajisikia na wataelewa magumu yetu.
UFALME WA MUNGU UTAFANYA NINI?
11. Juu ya nini Yesu alifundisha wanafunzi wake wasali ili mapenzi ya Mungu yafanyike mbinguni?
11 Yesu alifundisha wanafunzi wake wasali ili mapenzi ya Mungu yafanyike mbinguni. Juu ya nini? Tulijifunza mu Sura ya 3 kama Shetani Ibilisi alimupinga Yehova. Kisha Shetani kumupinga, Yehova alimuacha yeye na malaika wenye hawakukuwa waaminifu, ni kusema, pepo wachafu, wabakie mbinguni kwa wakati fulani. Kwa hiyo, haiko malaika wote njo walikuwa wanafanya mapenzi ya Mungu mbinguni. Mu Sura ya 10, tutajifunza mambo mingi zaidi juu ya Shetani na pepo wake wachafu.
12. Ni mambo gani mbili ya maana yenye kuzungumuziwa mu Ufunuo 12:10?
12 Biblia inasema kama kisha tu Yesu kufanywa kuwa Mufalme wa Ufalme wa Mungu, angepigana vita na Shetani. (Soma Ufunuo 12:7-10.) Ufunuo 12:10 inazungumuzia mambo mbili ya maana sana: 1) Ufalme wa Mungu wenye kuongozwa na Yesu Kristo, unaanza kutawala. 2) Shetani anafukuzwa mbinguni na kutupwa ku dunia. Kama vile tutajifunza, mambo hayo yamekwisha kutokea.
13. Ni nini ilitokea mbinguni kisha Shetani kufukuzwa?
13 Biblia inaeleza furaha yenye malaika waaminifu walikuwa nayo wakati Shetani na pepo wake wachafu walifukuzwa mbinguni. Inasema hivi: “Mufurahi, ninyi mbingu na ninyi wenye kukaa ndani yake!” (Ufunuo 12:12) Sasa mbinguni kuko amani na umoja kabisa kwa sababu wote wenye kuwa kule wanafanya mapenzi ya Mungu.
Kuanzia wakati Shetani na pepo wake wachafu walifukuzwa mbinguni, mateso yameongezeka mu dunia. Lakini mateso hayo yataisha hivi karibuni
14. Ni mambo gani yenye yametokea mu dunia juu Shetani amefukuzwa mbinguni?
14 Lakini hali iko tofauti kabisa mu dunia. Watu wanapatwa na mambo ya mubaya sana “kwa sababu Ibilisi ameshuka” na iko na “kasirani kali, akijua kwamba iko na kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Shetani iko na kasirani sana. Amefukuzwa mbinguni, na anajua kama ataharibiwa hivi karibuni. Anafanya nguvu yake yote ili alete magumu, maumivu, na mateso mu dunia yote.
15. Mapenzi ya Mungu juu ya dunia ni nini?
15 Lakini mapenzi ya Mungu juu ya dunia hayajabadilika. Anapenda watu wakamilifu waishi milele mu dunia paradiso. (Zaburi 37:29) Kwa hiyo, namna gani Ufalme utatimiza mapenzi ya Mungu?
16, 17. Andiko la Danieli 2:44 linatuambia nini juu ya Ufalme wa Mungu?
16 Unabii wenye kuwa mu Danieli 2:44 unasema hivi: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atasimamisha ufalme wenye hautaharibiwa hata siku moja. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utaponda na kumaliza falme hizi zote, na ufalme huo peke yake utasimama milele.” Unabii huo unatufundisha nini juu ya Ufalme wa Mungu?
17 Kwanza, Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala “katika siku za wafalme hao.” Hilo linaonyesha kama serikali zingine zingekuwa zingali zinatawala wakati Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala. 2) Ufalme wa Mungu utatawala milele na hakuna serikali yenye itakamata nafasi ya ufalme huo. 3) Kutakuwa vita kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za dunia. Ufalme wa Mungu utapata ushindi. Kisha serikali hiyo moja tu njo itatawala dunia yote. Watu watatawaliwa na serikali ya muzuri zaidi.
18. Vita ya mwisho kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za wanadamu inaitwa namna gani?
18 Namna gani Ufalme wa Mungu utatosha serikali za watu? Mbele ya vita ya mwisho yenye kuitwa Armagedoni, pepo wachafu watadanganya “wafalme wa dunia yote yenye kuikaliwa na watu, ili kuwakusanya pamoja kwa ajili ya vita ya ile siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote.” Ndiyo, serikali za wanadamu zitapigana na Ufalme wa Mungu.—Ufunuo 16:14, 16; ona Mafasirio Ingine ya 10.
19, 20. Juu ya nini tuko na lazima ya Ufalme wa Mungu?
19 Juu ya nini tuko na lazima ya Ufalme wa Mungu? Kuko sababu tatu hivi. 1) Tuko watenda-zambi, kwa hiyo tunagonjwa na tunakufa. Lakini, Biblia inasema kama wakati wa utawala wa Ufalme wa Mungu, tutaishi milele. Andiko la Yohana 3:16 linasema hivi: “Mungu alipenda ulimwengu sana na hivyo akamutoa Mwana wake muzaliwa-pekee, ili kila mutu mwenye anamuamini asiharibiwe lakini apate uzima wa milele.”
20 Pili, tuko na lazima ya Ufalme wa Mungu juu tunazungukwa na watu wabaya sana. Watu wengi wanasema uongo, wanadanganya na wanafanya mambo ya uasherati. Hatuwezi kutosha watu hao, lakini Mungu anaweza. Watu wenye wanaendelea kufanya mambo ya mubaya, wataharibiwa ku vita ya Armagedoni. (Soma Zaburi 37:10.) 3) Tuko na lazima ya Ufalme wa Mungu juu serikali za wanadamu ziko zaifu, zinatendea watu mubaya na ziko zenye udanganyifu. Hazichochee watu wamutii ao kumusikia Mungu. Biblia inasema kama “mwanadamu ametawala mwanadamu mwenzake ili kumuumiza.”—Muhubiri 8:9.
21. Namna gani Ufalme utafanya mapenzi ya Mungu yafanyike ku dunia?
21 Kisha vita ya Armagedoni, Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yafanyike ku dunia. Kwa mufano, utatosha Shetani na pepo wake wachafu. (Ufunuo 20:1-3) Mwishowe, hakuna mutu mwenye atagonjwa ao kufa. Kupitia bei ya ukombozi, watu wote waaminifu wataishi milele mu Paradiso. (Ufunuo 22:1-3) Ufalme huo utatakasa jina la Mungu. Maana yake nini? Maana yake, wakati serikali ya Mungu itatawala dunia, watu wote watatukuza jina la Yehova.—Ona Mafasirio Ingine ya 21.
YESU ALIFANYWA KUWA MUFALME WAKATI GANI?
22. Yesu hakufanywa kuwa Mufalme wakati alikuwa ku dunia ao kisha tu kufufuliwa kwake. Namna gani tunajua jambo hilo?
22 Yesu alifundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Ufalme wako ukuje.” Kwa hiyo, ni wazi kama ufalme wa Mungu ungekuja wakati wenye kuja. Yehova angeanzisha kwanza serikali yake na kumufanya Yesu kuwa Mufalme wa serikali hiyo. Je, Yesu alifanywa kuwa Mufalme kisha tu kurudia mbinguni? Hapana, alipaswa kungojea. Namna gani tunajua jambo hilo? Wakati kidogo kisha Yesu kufufuliwa, Petro na Paulo walionyesha wazi kama unabii wenye kuwa mu Zaburi 110:1 ulizungumuzia Yesu. Mu unabii huo Yehova anasema hivi: “Kaa kwenye mukono wangu wa kuume mupaka niweke maadui wako kuwa kiti cha miguu yako.” (Matendo 2:32-35; Waebrania 10:12, 13) Yesu alipaswa kungojea kwa muda gani mbele Yehova amufanye kuwa Mufalme?
Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yafanyike ku dunia
23. (a) Ni wakati gani Yesu alianza kutawala Ufalme wa Mungu? (b) Tutajifunza nini mu habari yenye kufuata?
23 Kwa miaka mingi mbele ya mwaka wa 1914, kikundi cha Wakristo waaminifu walielewa kama mwaka huo ungekuwa wa maana mu unabii wa Biblia. Kuanzia mwaka wa 1914 mambo yenye kufanyika mu dunia yanaonyesha kama walisema kweli. Yesu alianza kutawala mu mwaka huo. (Zaburi 110:2) Wakati kidogo kisha pale, Shetani alitupwa ku dunia. Sasa “iko na kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Mu habari yenye kufuata, tutaona mambo mingi zaidi yenye kuonyesha kama tunaishi wakati huo. Tutajifunza pia kama hivi karibuni Ufalme wa Mungu utatimiza mapenzi ya Mungu ku dunia.—Ona Mafasirio Ingine ya 22.