KICHWA
Sababu Inayofanya Watu Wengi Waone Ni Vigumu Kumupenda Mungu
‘Lazima umupende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote. Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza.’—Yesu Kristo, mwaka wa 33.a
Watu fulani wanaona ni vigumu kumupenda Mungu. Kulingana na maoni yao, Mungu anaonekana kuwa asiyeeleweka, aliye mbali na watu, ao hata asiyekuwa na huruma. Fikiria maneno haya ya watu fulani:
“Nilimuomba Mungu musaada, lakini wakati huohuo, nilijisikia kwamba alikuwa mbali na mimi, na hata asiyeweza kukaribiwa. Kwa maoni yangu, sikumuona Mungu kuwa mutu ambaye ana huruma.”—Marco, anaishi Italia.
“Hata ikiwa nilitaka kabisa kumutumikia Mungu, alionekana kuwa asiyeweza kukaribiwa. Nilifikiri kwamba Mungu alikuwa mukali ambaye kazi yake tu ni kutuazibu. Sikuamini kwamba Mungu ana huruma.”—Rosa, anaishi Guatemala.
“Nilipokuwa mutoto, niliamini kwamba Mungu anatafuta-tafuta tu makosa yetu, na yuko tayari kutuazibu ikiwa tunastahili azabu hiyo. Kisha, nilimuona kuwa asiyependezwa na watu. Mungu alikuwa kama waziri mukubwa anayesimamia mambo ya watu ambao anaongoza, lakini ambaye hapendezwe kabisa na watu hao.”—Raymonde, anaishi Kanada.
Unawaza namna gani? Je, Mungu hastahili kupendwa? Wakristo wameuliza ulizo hilo kwa miaka mingi. Kwa kweli, katika kipindi kati ya mwaka wa 500 na 1 500 kisha kuzaliwa kwa Yesu, watu wengi katika inchi zinazojiita kuwa za Kikristo hawakutoa sala zao kwa Mungu Mweza -Yote. Sababu gani? Watu walikuwa na woga usiofaa wa Mungu. Kuhusu woga huo, mwanahistoria Will Durant alisema hivi: “Namna gani mutenda-zambi anaweza kusali kwa Mungu mwenye kuogopesha na aliye mbali na watu?”
Namna gani watu walifikia kumuona Mungu kuwa “mwenye kuogopesha na aliye mbali na watu”? Biblia inafundisha kabisa nini kumuhusu Mungu? Je, kujifunza kweli juu ya Mungu kunaweza kukusaidia umupende?