Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • wp17 na. 4 uku. 4-7
  • Biblia Inasema Nini Juu ya Uzima na Kifo?

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Biblia Inasema Nini Juu ya Uzima na Kifo?
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Watu Wote)—2017
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • BIBLIA INANYOOSHA MAMBO
  • FUNDISHO LA KIPAGANI LINAENEA
  • “KWELI ITAWAWEKA NINYI HURU”
  • Watu Waliokufa Wako Wapi?
    Biblia Inafundisha Kabisa Nini?
  • Nafsi Ni Nini?
    Maulizo Juu ya Habari za Biblia Yanajibiwa
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Watu Wote)—2017
wp17 na. 4 uku. 4-7
Maiti yenye kuwa katika kaburi

HABARI KUBWA | BIBLIA INASEMA NINI JUU YA UZIMA NA KIFO?

Biblia Inasema Nini Juu ya Uzima na Kifo?

Wakati tunasoma habari ya uumbaji yenye kuwa katika kitabu cha Mwanzo, tunaona kwamba Mungu alimuambia Adamu, mwanaume wa kwanza, maneno haya: ‘Matunda ya kila muti wa bustani unaweza kula mupaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya muti wa ujuzi wa mema na mabaya usikule, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.’ (Mwanzo 2:16, 17) Maneno hayo yanaonyesha wazi kwamba kama Adamu angetii sheria ya Mungu, hangekufa na angeendelea kuishi katika bustani ya Edeni.

Adamu na Eva katika uzee wao

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, kuliko kutii ili kuishi milele, Adamu aliamua kupuuza amri ya Mungu na akakula tunda la muti wenye kukatazwa, wakati Eva, bibi yake, alimupatia tunda hilo. (Mwanzo 3:1-6) Mupaka leo tunaendelea kupata matokeo ya kukosa kutii kwao. Mutume Paulo alifasiria jambo hilo hivi: ‘Hiyo ndiyo sababu, kama vile kupitia mutu mumoja zambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia zambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya zambi.’ (Waroma 5:12) Bila shaka ‘mutu mumoja’ huyo alikuwa Adamu. Lakini zambi hiyo ilikuwa nini, na sababu gani iliongoza kwenye kifo?

Adamu alifanya zambi kwa kuvunja ao kukataa kimakusudi kutii sheria ya Mungu. (1 Yohana 3:4) Na malipizi ya zambi ni kifo, kama vile Mungu alimuambia Adamu. Kama Adamu na watoto wenye angezaa wangeendelea kutii amri ya Mungu, hawangekuwa na zambi wala hawangeonja kifo. Mungu hakuumba wanadamu ili wakufe lakini ili waishi​—waishi hata milele.

Kama tu vile Biblia ilisema, hatuwezi kupinga kwamba ‘kifo kimeenea kwa watu wote.’ Lakini, sehemu fulani ya mwili inaendelea kuishi kisha mutu kufa? Watu wengi wanaweza kusema kwamba sehemu fulani ya mwili wetu yenye kuitwa nafsi haikufe. Kusema hivyo, kunaweza kuonyesha kama Mungu alimudanganya Adamu. Namna gani? Kama sehemu fulani ya mwili inaendelea kuishi katika makao fulani kisha mutu kufa, tunaweza kusema kwamba malipizi ya zambi haiko kifo, kama vile Mungu alisema. Biblia inasema hivi: “Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.” (Waebrania 6:18) Lakini kwa kweli, ni Shetani ndiye alisema uongo kwa kumuambia Eva hivi: ‘Hakika hamutakufa.’​—Mwanzo 3:4.

Hilo linaleta ulizo hili: Kama fundisho la kutokufa kwa nafsi ni la uongo, sasa, ni nini inatokea wakati mutu anakufa?

BIBLIA INANYOOSHA MAMBO

Habari juu ya uumbaji yenye kuwa katika Mwanzo inasema hivi: ‘Yehova Mungu akamufanya mutu kutoka katika mavumbi ya inchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mutu akawa nafsi hai.’ Maneno “nafsi hai” yanatafsiriwa kutoka katika neno la Kiebrania ne’phesh,a lenye linamaanisha kiumbe chenye kupumua.​—Mwanzo 2:7.

Kwa hiyo, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba watu hawakuumbwa na nafsi yenye haiwezi kufa. Lakini, kila mutu ni “nafsi hai.” Ndiyo sababu, hata kama unatafuta namna gani, hauwezi kupata andiko la Biblia lenye kutumia maneno “nafsi yenye haiwezi kufa.”

Kwa sababu Biblia haiseme kama mwanadamu iko na kile watu fulani wanaita nafsi yenye haiwezi kufa, sababu gani dini nyingi zinafundisha mawazo yenye kupingana na Biblia? Turudie katika Misri ya zamani ili kupata jibu.

FUNDISHO LA KIPAGANI LINAENEA

Hérodote, mwanahistoria Mugiriki, mwenye aliishi katika miaka ya 400 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, alisema kama Wamisri walikuwa “watu wa kwanza kutetea fundisho la kutokufa kwa nafsi.” Katika desturi ya zamani ya Babiloni, watu waliamini fundisho la kutokufa kwa nafsi. Wakati Alexandre Mukubwa alikamata sehemu yote ya Mashariki ya Kati katika mwaka wa 332 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, wanafilozofia Wagiriki walifanya fundisho hilo lijulikane sana, na bila kukawia fundisho hilo likaenea katika Utawala wa Ugiriki.

Hauwezi kupata andiko la Biblia lenye kutumia maneno “nafsi yenye haiwezi kufa”

Katika kipindi kati ya mwaka wa 1 mupaka mwaka wa 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu, vikundi viwili vya Wayahudi vyenye kujulikana sana, Waesene na Mafarisayo, vilifundisha kwamba nafsi inaendelea kuishi kisha mwili kufa. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Imani ya kutokufa kwa nafsi iliwafikia Wayahudi kupitia wazo la Wagiriki na zaidi sana kupitia filozofia ya Plato.” (The Jewish Encyclopedia) Vilevile, Josèphe, mwanahistoria Muyahudi wa kile kipindi, alionyesha kwamba fundisho hilo haliko la Maandiko Matakatifu, lakini ni la “imani ya watoto wa Ugiriki,” imani yenye aliona kuwa mukusanyo wa hadisi za kuwazia-wazia.

Kadiri desturi ya Wagiriki iliendelea kuenea sana, watu wenye kujiita Wakristo walikubali pia fundisho hilo la kipagani. Kulingana na mwanahistoria Jona Lendering, “wazo la Plato la kwamba nafsi yetu ilikuwa kwanza katika nafasi nzuri, na sasa inaishi katika ulimwengu mubaya, ilifanya ikuwe mwepesi kuchanga filozofia ya Plato na Ukristo.” Kwa hiyo, fundisho la kipagani la kutokufa kwa nafsi lilikubaliwa katika kanisa la “Kikristo” na likafikia kuwa kati ya mafundisho ya musingi ya kanisa.

“KWELI ITAWAWEKA NINYI HURU”

Wakati wa mitume, mutume Paulo alitoa angalisho hili: “Neno lililoongozwa na roho linasema kwa hakika kwamba katika vipindi vya nyakati za mwisho wengine wataanguka kutoka kwenye imani, wakisikiliza maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha na mafundisho ya roho waovu.” (1 Timotheo 4:1) Ni maneno ya kweli kabisa! Lakini fundisho la kutokufa kwa nafsi ni moja tu kati ya “mafundisho ya roho waovu.” Biblia haiunge mukono fundisho hilo, lakini linatoka katika filozofia na dini za kipagani za zamani.

Jambo la kufurahisha ni kwamba, Yesu alisema hivi: ‘Mutajua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.’ (Yohana 8:32) Kwa kujifunza kujua kweli ya Biblia, tunakuwa huru kutoka katika mafundisho yenye kumushushia Mungu heshima na katika matendo mabaya yenye kukubaliwa na dini zenye kuwa katika dunia. Zaidi ya hilo, kweli ya Neno la Mungu inatuweka huru kutoka katika utumwa wa desturi na imani ya uongo kuhusu kifo.​—Ona sehemu “Wafu Wako Wapi?”

Muumbaji wetu hakupenda wanadamu waishi miaka 70 ao 80 tu duniani na kisha waende kuishi milele katika makao mengine. Kusudi lake la kwanza ni hili: Wanadamu waishi milele katika dunia wakiwa watoto watiifu. Kusudi hilo nzuri sana linaonyesha kwamba Mungu anatupenda, na hakuna kitu kitamuzuia kutimiza mapenzi yake. (Malaki 3:6) Muandikaji mumoja wa zaburi alituhakikishia jambo hilo kwa kusema hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”​—Zaburi 37:29.

Ili kupata habari zaidi kuhusu mambo yenye Biblia inasema juu ya uzima na kifo, ona sura ya 6 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? chenye kuchapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kinapatikana pia kwenye www.jw.org, ao tumia chombo cha kusoma alama hii.

a Tafsiri fulani za Biblia, kama vile Union Version inatafsiri neno ne’phesh kwa kutumia maneno “nafsi hai,” lakini tafsiri zingine zinatafsiri neno hilo “kiumbe hai,” Biblia Habari Njema kwa Watu Wote; ao “kiumbe chenye uzima,” Verbum Bible.

Wanadamu Wanaweza Kuishi Milele?

Katika miaka fulani yenye imepita, wachunguzi wamevumbua aina fulani ya mimea yenye kuishi chini ya maji yenye wanaamini kama imeishi maelfu ya miaka​—pengine ndio imefanya miaka mingi kuliko kiumbe kingine chochote chenye kuishi duniani. Mimea hiyo ni aina ya Posidonia oceanica, yenye inafunika eneo kubwa lenye kuwa chini ya bahari ya Mediterania kati ya Uhispania na Kipro.

Kama mimea inaweza kuishi miaka mingi sana, sasa wanadamu? Wanasayansi fulani wenye kujifunza kuhusu kuzeeka wako hakika kwamba kuko tumaini la kuongeza urefu wa maisha. Kwa mufano, kitabu kimoja kuhusu habari hiyo, kinasema kwamba kinafanya uchunguzi kuhusu “maendeleo mengi ya sasa ya kisayansi” juu ya jambo hilo. Mupaka sasa hatujue kama maendeleo katika mambo ya sayansi yatakuwa kabisa na matokeo fulani juu ya urefu wa maisha ya watu.

Lakini, tumaini la kweli juu ya kuishi milele halitegemee sayansi ya siku zetu. Biblia inasema hivi juu ya Yehova Mungu na Muumbaji wetu: “Kwa maana kwako wewe iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Yesu Kristo alisema hivi juu ya Yehova katika sala: ‘Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemutuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Kwa kweli, wakati tunajikaza kujua na kupendeza Yehova Mungu na Yesu Kristo, Mwana wake, tutapata baraka za milele.

Seagrass

Wachunguzi wanaamini kama aina hii ya mimea yenye kuwa chini ya bahari imeishi maelfu ya miaka

WAFU WAKO WAPI?

Yesu anafufua Lazaro

Kwa kifupi, Biblia inasema kwamba wafu wako katika kaburi, wakingojea ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Hawateseke wala hawana maumivu yoyote, kwa sababu “wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Katika mafundisho yake, Yesu alilinganisha kifo na usingizi muzito. (Yohana 11:11-14) Kwa hiyo, hatuna sababu ya kuogopa wale wenye kulala katika usingizi wa kifo ao kuwatuliza kwa kuwatolea vitu mbalimbali. Hawawezi kutusaidia wala kutufanyia mambo ya mubaya, kwa sababu “hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi.” (Mhubiri 9:10) Lakini, kupitia ufufuo, Mungu ataondoa kifo milele.​—1 Wakorintho 15:26, 55; Ufunuo 21:4.

Sababu Gani Ukuwe Hakika na Mambo Biblia Inasema?

Tunaweza kuwa hakika kwamba mambo yenye Biblia inasema ni yenye kutegemeka. Sababu gani? Ona mifano yenye kufuata:

  • Kalamu na kidau cha wino

    Mutungaji Mumoja: Biblia inafanyizwa na vitabu vidogo-vidogo 66 vyenye viliandikwa na watu 40 hivi katika kipindi cha miaka 1600 hivi, kuanzia mwaka wa 1513 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu mupaka mwaka wa 98 hivi kisha kuzaliwa kwa Yesu. Hata hivyo, mambo yote yenye kuwa katika Biblia yanapatana. Hilo linaonyesha kwamba Mutungaji wa kweli wa Biblia ni Mungu Mweza-Yote. Alifunulia wanaume wenye waliandika Biblia mawazo yake.

  • Nguzo

    Inasema Kweli Katika Mambo ya Historia: Matukio yenye kuandikwa katika Biblia yanapatana kabisa na mambo yenye historia inasema. Kitabu A Lawyer Examines the Bible kinasema hivi: “Hata kama vitabu vya hadisi za kimapenzi, habari za kuwazia tu na ushuhuda wa uongo vinaweka kwa uangalifu matukio yenye kuzungumuziwa katika mahali na wakati wenye haujulikane muzuri, . . . habari yenye kuwa katika Biblia inatupatia kwa usahihi mukubwa tarehe na mahali penye mambo yenye kuzungumuziwa yalifanyika.”

  • Atomu

    Inasema Kweli Katika Mambo ya Sayansi: Biblia haiko kitabu cha sayansi, lakini wakati inazungumuzia mambo ya sayansi, inasema kweli kabisa hata mbele mambo hayo yavumbuliwe na wanasayansi. Kwa mufano, katika sura ya 13 na 14 ya kitabu cha Mambo ya Walawi, kunapatikana sheria zenye zilitolewa kwa Waisraeli kuhusu usafi na kutenga watu wenye kugonjwa, miaka mingi mbele watu wajue jambo lolote kuhusu kuambukizwa na mikrobe. Biblia inaonyesha pia kwamba dunia iko muviringo na haikamatwe na kitu fulani. Sayansi imefikia kuelewa jambo hilo kisha miaka mingi sana.​—Ayubu 26:7; Isaya 40:22.

Hii ni mifano kidogo tu yenye kushuhudia kwamba Biblia ni ya kweli wakati inasema hivi: ‘Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nizamu katika uadilifu.’​—2 Timotheo 3:16.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine