Zawadi ya Mungu ya zabihu ya ukombozi, yenye inafanya uzima wa milele uwezekane, ndiyo zawadi kubwa kuliko zote
HABARI KUBWA | NI ZAWADI GANI YA MUZURI KULIKO ZOTE?
Ni Zawadi Gani ya Muzuri Kuliko Zote?
“Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.” (Yakobo 1:17) Bila shaka, andiko hilo linazungumuzia ukarimu wa Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu. Hata hivyo, kati ya zawadi nyingi zenye Mungu ametolea wanadamu, kuko moja yenye kuwa kubwa kuliko zote. Ni zawadi gani? Maneno ya Yesu yenye kujulikana sana, yenye kupatikana katika Yohana 3:16, yanasema hivi: ‘Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa-pekee, ili kila mutu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’
Zawadi ya Mwana muzaliwa-pekee wa Mungu ndiyo zawadi kubwa kuliko yoyote yenye kila mumoja wetu amekwisha kupokea, kwa sababu kupitia zawadi hiyo tunaweza kukombolewa kutoka katika utumwa wa zambi, uzee, na kifo. (Zaburi 51:5; Yohana 8:34) Hata kama tunajikaza kufanya yetu yote, hatuwezi kujikomboa kutoka katika utumwa huo. Lakini, kwa sababu ya upendo wake, Mungu alitoa kitu chenye kiliombwa kwa ajili ya ukombozi huo. Kwa kumutoa Mwana wake muzaliwa-pekee, Yesu Kristo, kama zabihu ya ukombozi, Yehova Mungu alipatia wanadamu wenye kutii tumaini la uzima wa milele. Lakini, namna gani zabihu ya Yesu ililipa bei yenye iliombwa ili tukombolewe kutoka katika utumwa wa zambi na kifo? Sababu gani ilikuwa lazima kufanya hivyo? Na namna gani zabihu yake inaweza kutuletea faida?
Zabihu ya uzima wa Yesu ilikuwa kama bei yenye kulipwa ili kurudisha kitu fulani chenye kilipotea ao kukomboa kutoka katika utumwa. Biblia inaonyesha kwamba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Eva, waliumbwa bila zambi, wakiwa na tumaini la kufurahia maisha milele duniani pamoja na watoto wenye wangefikia kuzaa. (Mwanzo 1:26-28) Jambo la huzuni ni kwamba walipoteza mambo yote hayo kwa kuchagua kumuasi Mungu—kwa hiyo, wakawa wenye zambi. Matokeo? Biblia inajibu hivi: ‘Kupitia mutu mumoja zambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia zambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya zambi.’ (Waroma 5:12) Kuliko kuwapitishia watoto wake uzima mukamilifu, Adamu aliwapitishia zambi na matokeo yake, ni kusema, kifo.
Bei yenye ililipwa ili kutukomboa kutoka katika zambi na kifo ilipaswa kulingana na bei ya kitu chenye kilipotezwa. Wakati Adamu aliasi Mungu kimakusudi, alifanya zambi, na matokeo ni kwamba alipoteza uzima wake mukamilifu. Kulingana na Biblia, jambo hilo lilifanya watoto wa Adamu wakuwe watumwa wa zambi na kifo. Kwa hiyo, iliomba uzima wa mwanadamu mwengine mukamilifu—uzima wa Yesu—utolewe kuwa zabihu ili wanadamu wakombolewe kutoka katika utumwa. (Waroma 5:19; Waefeso 1:7) Kama wanadamu wako na tumaini la kufurahia jambo lenye Adamu na Eva walipoteza, ni kusema, uzima wa milele katika dunia paradiso, ni kwa sababu Mungu alitoa kwa upendo zabihu ya ukombozi.—Ufunuo 21:3-5.
Kwa sababu ya jambo ambalo inatimiza, hakuna shaka kwamba zawadi ya Mungu ya zabihu ya ukombozi, yenye inafanya uzima wa milele uwezekane, ndiyo zawadi kubwa kuliko zote. Ili kufurahia “tuzo kamilifu,” tuone namna gani, katika njia kubwa, linatimiza mambo yenye yanafaa ili zawadi zikuwe za maana sana, kama vile tuliona katika habari yenye kutangulia.
Inatimiza tamaa yetu. Sisi wanadamu tuko na tamaa kubwa ya asili ya kuendelea kuishi. (Mhubiri 3:11) Hata kama sisi wenyewe hatuna uwezo wa kutimiza tamaa hiyo, zabihu ya ukombozi inatuwezesha kuitimiza. Biblia inasema hivi: ‘Kwa maana mushahara ambao zambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.’—Waroma 6:23.
Inatimiza mahitaji yetu. Wanadamu hawangeweza kutoa zabihu ya ukombozi. Biblia inasema hivi: ‘Nayo bei ya ukombozi wa nafsi yao ni yenye samani sana hivi kwamba imekoma mupaka wakati usio na kipimo.’ (Zaburi 49:8) Kwa hiyo tulikuwa tu na lazima ya musaada wa Mungu ili kukombolewa kutoka katika utumwa wa zambi na kifo. Lakini “kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia [ao, bei ya ukombozi] ambayo Kristo Yesu alilipa,” Mungu alitoa kile kiliombwa.—Waroma 3:23, 24.
Inatolewa kwa wakati wenye kufaa kabisa. Biblia inasema hivi: ‘Tulipokuwa tungali watenda-zambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.’ (Waroma 5:8) Kwa sababu ilitolewa ‘tulipokuwa tungali watenda-zambi,’ zabihu ya ukombozi inatuhakikishia kwamba Mungu anatupenda sana hata kama tuko katika hali ya zambi. Na inatupatia tumaini kubwa hata kama tunapaswa kuvumilia matokeo ya zambi.
Inaonyesha nia nzuri na yenye haiko ya kichoyo. Biblia inafunua jambo lenye lilichochea Mungu kutoa Mwana wake kuwa zabihu ya ukombozi: ‘Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimutuma Mwana wake muzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye. Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumemupenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda.’—1 Yohana 4:9, 10.
Namna gani unaweza kuonyesha shukrani kwa zawadi ya muzuri kuliko zote? Kumbuka kwamba maneno ya Yesu katika andiko la Yohana 3:16 yanaonyesha kwamba ni wale tu ‘wanamwamini’ yeye ndiyo wataokolewa. Kulingana na Biblia, imani ni “tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa.” (Waebrania 11:1) Ili kupata uhakikisho huo, ni lazima kupata ujuzi sahihi. Kwa sababu hiyo, tunakuomba kuchukua wakati ili kujifunza kumuhusu Yehova Mungu, Mutoaji wa hii “tuzo kamilifu” ili kujua mambo unapaswa kufanya ili kufurahia uzima wa milele wenye unawezekana kupitia zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo.
Unaweza kujifunza mambo yote haya kwa kuchunguza habari za Biblia zenye kupatikana kwenye www.jw.org. Mashahidi wa Yehova watafurahia kukusaidia. Tuko hakika kwamba, kadiri unajifunza na kupata faida kupitia zawadi hii kubwa kuliko zote, utachochewa kusema: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu.”—Waroma 7:25.