Wanashughulika Na Mali Ya Bwana-mukubwa
1 Katika nyakati za kibiblia, msimamizi-nyumba alikabidhiwa mambo mengi. Hivyo, Abrahamu alimpa msimamizi-nyumba wake fursa ya kutafuta mke kwa ajili ya mwana wake, Isaka. (Mwa. 24:1-4) Msimamizi-nyumba huyo alikuwa na daraka la kuhakikisha uendelezaji wa ukoo wa Abrahamu. Lilikuwa daraka kubwa sana. Basi, si jambo la kushangaza kwamba Paulo alisema: “Kitafutwacho katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu.”—1 Kor. 4:2.
Usimamizi-Nyumba wa Kikristo
2 Biblia huita pande fulani za huduma ya Kikristo kuwa usimamizi-nyumba. Kwa mfano, mtume Paulo alisimulia na Waefeso juu ya ‘usimamizi-nyumba wa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu ambao alipewa kwa ajili yao.’ (Efe. 3:2; Kol. 1:25) Yeye aliona utume wake wa kutangaza habari njema kwa mataifa kuwa usimamizi-nyumba ambao alipaswa kutimiza kwa uaminifu. (Mdo. 9:15; 22:21) Mtume Petro aliandikia ndugu zake wapakwa-mafuta: “Iweni wakaribishaji-wageni nyinyi kwa nyinyi bila kuguna. Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba walio wema wa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iliyoonyeshwa katika njia mbalimbali.” (1 Pet. 4:9, 10; Ebr. 13:16) Yote ambayo Wakristo hao wa karne ya kwanza waliyokuwa nayo yalitokana na fadhili isiyostahiliwa ya Yehova. Basi, walikuwa wasimamizi-nyumba wa vitu hivyo na walipaswa kuvitumia kwa njia ya Kikristo.
3 Leo, Mashahidi wa Yehova huona mambo namna iyohiyo. Wakiwa wamejitoa kwa Yehova Mungu, wanaona yote waliyo nayo—maisha yao, nguvu zao za kimwili, mali yao—kuwa matunda mbalimbali ya “fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iliyoonyeshwa katika njia mbalimbali.” Kama wasimamizi-nyumba walio wema, wanajisikia wenye madaraka mbele ya Mungu kuhusiana na namna wanavyotumia vitu hivyo. Zaidi ya hilo, ujuzi wa habari njema umetolewa kwao. Hiyo pia ni dhamana wanayopenda kutumia kwa njia bora iwezekanavyo, yaani ili kutukuza jina la Yehova na kusaidia watu wengine waje kwenye ujuzi sahihi wa kweli.—Mt. 28:19, 20; 1 Tim. 2:3, 4; 2 Tim. 1:13, 14.
4 Mashahidi wa Yehova wanatimizaje daraka lao la wasimamizi-nyumba? Ripoti ya mwaka inaonyesha kwamba, mwaka uliopita, walitoa zaidi ya saa bilioni moja katika mahubiri ya “habari njema ya Ufalme” ulimwenguni pote na waliongoza zaidi ya mafunzo ya Biblia 4 500 000 pamoja na watu wanaopendezwa na habari njema hiyo. (Mt. 24:14) Walithibitisha pia kwamba wao ni wasimamizi-nyumba waaminifu wa Yehova kwa kutoa zawadi za ukarimu ili kutegemeza kazi ulimwenguni na kutunza Majumba ya Ufalme yao, kwa kuonyesha ukaribishaji-wageni kuelekea waangalizi wasafiri na Wakristo wengine, na kwa kuonyesha wema unaozidi ulio wa kawaida kuelekea wale walio katika uhitaji, kwa mfano wale wanaoteseka kwa sababu ya vita. Kama kikundi, Wakristo wa kweli hushughulika na mali ya Bwana-Mkubwa kwa njia bora.
“Msimamizi-Nyumba Mwaminifu, Mwenye Busara”
5 Usimamizi-nyumba huo haufanywi tu na watu kibinafsi, lakini unafanywa pia na tengenezo. Yesu alisema juu ya kutaniko la Kikristo lililopakwa mafuta duniani kuwa “msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara.” (Lk. 12:42) “Msimamizi-nyumba mwaminifu” huyo ana daraka la kutoa “chakula” na kuchukua uongozi katika mahubiri ya habari njema katika mataifa yote. (Ufu. 12:17) Kuhusiana na hilo, jamii ya msimamizi-nyumba mwaminifu, ikiwakilishwa na Baraza Linaloongoza, ni yenye daraka kuhusiana na jinsi zawadi zinazotolewa kwa ajili ya kutegemeza kazi ulimwenguni zinavyotumiwa. Zawadi hizo zinafanywa pakiwa na matumaini, na “msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara,” analo daraka la kuangalia kwamba hizo zitumiwe kwa kile ambacho kwa ajili yake zilitolewa, lakini pia kwa hekima, kwa kuhangaikia matumizi yenye kiasi na kwa matokeo.
6 Tunapata mfano wa utumiaji wenye hekima wa zawadi hizo katika ukuzi wa kazi za uchapaji za Mashahidi wa Yehova katika karne ya 20. Ugawaji wa Biblia na maandishi ya kibiblia—magazeti, vitabu, broshua, trakti na Habari za Ufalme—ulitimiza kazi ya maana sana katika utangazaji wa “habari njema” katika “siku za mwisho.” (Mk. 13:10; 2 Tim. 3:1) Kuhusu Mnara wa Mlinzi, hicho ndicho chombo kikubwa kinachotumiwa ili kutoa “chakula kwa wakati ufaao” kwa watu wa “nyumbani mwa Mungu” na kwa wenzi wao, “umati mkubwa” wa “kondoo wengine.”—Mt. 24:45; Efe. 2:19; Ufu. 7:9; Yn. 10:16.
7 Mwanzoni, vichapo vyote vya Mashahidi wa Yehova vilichapwa na viwanda vya kibiashara, lakini mnamo miaka ya 1920 iliamuliwa kwamba lingekuwa jambo lenye matokeo zaidi na lisilogharimu fedha nyingi kwamba watumishi wa Yehova wavichape wao wenyewe. Baada ya mianzo midogo katika 1920, kazi ya uchapaji iliongezeka hatua kwa hatua huko Brooklyn na kuwa kubwa sana. Mnamo 1967, kiwanda cha uchapaji kilichukua majengo manne. Uchapaji ulianza pia katika nchi nyinginezo, lakini kazi hiyo ilikatizwa na Vita ya Pili ya Ulimwengu.
8 Hata hivyo, ujapokuwa mpanuko wake, kazi ya uchapaji katika Shirikisho la Amerika haikutosha kuandaa vichapo katika dunia yote. Mnamo miaka iliyofuata vita, kazi za uchapaji zilifunguliwa na kuendelezwa katika nchi nyingine nyingi, kutia ndani Afrika ya Kusini, Muungano wa Ujerumani, Uingereza, Kanada, Danemark, Ugiriki na Uswisi. Mwanzoni mwa miaka ya 70, Australia, Brazili, Finland, Ghana, Japani, Nigeria na Ufilipino ziliongezeka kwenye orodha. Viwanda vya baadhi ya nchi hizo vilichapa vitabu. Wakati uohuo, wamishonari wa Gileadi walizoezwa katika kiwanda cha uchapaji na kutumwa katika baadhi ya nchi hizo ili kusaidia ndugu huko watimize kazi hiyo.
9 Katika miaka ya 1980, hesabu ya nchi ambako magazeti yalichapwa ilifikia kiwango kikubwa zaidi cha nchi 51a. Hesabu hiyo yote ilionekana kuwa njia bora ya kutumia mali ya Bwana-Mkubwa. Ulikuwa ni uthibitisho mkubwa wa mpanuko wa kazi ya Ufalme na ushahidi wenye nguvu wa utegemezo mwingi wa mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ‘walioheshimu Yehova kwa mali yao.’ (Mez. 3:9) Hivyo, walijionyesha wao wenyewe kuwa wasimamizi-nyumba wema wa yale ambayo kwa hayo Yehova amewathawabisha katika njia mbalimbali.
Badiliko la Mtazamo [W 1focus 5b]
10 Katika miaka ya 1970 na mwanzoni mwa miaka ya 1980, maendeleo makubwa yalifanywa katika uchapaji, na Mashahidi wa Yehova walianza kutumia mbinu mpya. Hadi hapo, walichapa kulingana na njia za kale za kupanga herufi za kuchapa. Hayo yote yalibadilika pole pole, na walianza kutumia uchapaji wa ofseti, wa kisasa zaidi. Ndiyo sababu sasa vichapo vizuri huchapwa vikiwa na picha zenye rangi nne badala ya mbili (nyeusi na rangi nyingine moja) zilizotokezwa na njia ya zamani ya kupanga herufi za kuchapa. Baada ya hayo, kompyuta ilibadili mambo yanayofanywa kabla ya uchapaji wenyewe. Mashahidi wa Yehova walitengeneza Mfumo wa Elektroni wa Kupanga Chapa kwa Picha Katika Lugha Nyingi (MEPS), mfumo wa kompyuta unaofanya iwezekane kuchapa katika zaidi ya lugha 370 tofauti tofauti. Hakuna programu ya kibiashara inayolingana na MEPS kuhusiana na kutumika katika lugha nyingi hivyo.
11 Kupitia mfumo wa MEPS na mbinu mpya zingine, kama vile barua za elektroni, maendeleo mengine makubwa yaliweza kufanywa katika kutoa chakula kwa wakati ufaao. Zamani, kupitia zile mbinu za kale, makala za magazeti katika lugha zingine ambazo si Kiingereza zilitokea miezi, wakati mwingine mwaka mmoja, baada ya zile za chapa ya Kiingereza. Sasa, Mnara wa Mlinzi unatokea kwa wakati uleule katika lugha 115, na Amkeni! katika lugha 62. Hilo linamaanisha kwamba, katika dunia, zaidi ya asilimia 95 ya wahudhuriaji kwenye funzo la kila juma la Mnara wa Mlinzi linalopangwa na Mashahidi wa Yehova huchunguza habari ileile kwa wakati uleule. Ni baraka kama nini! Akiba inayotumiwa katika mbinu hizo mpya imekuwa bila shaka utumiaji mzuri wa mali ya Bwana-Mkubwa.
Mahitaji Tofauti Kuhusu Upangaji-Mambo Kitengenezo
12 Kwa sababu ya njia hizo mpya, uhitaji mbalimbali wa kupanga mambo kitengenezo wa Mashahidi wa Yehova kuhusu uchapaji umebadilika. Matbaa makubwa ya mviringo huwa na mwendo wa kasi zaidi kuliko matbaa-mabamba-mviringo, lakini pia huwa yenye bei ya juu zaidi. Mifumo ya elektroni na ya kompyuta inayohitajiwa kwa ajili ya kazi za kabla ya uchapaji—uhariri, tafsiri, kazi ya sanaa, upangaji—inatoa uwezekano mwingi zaidi kuliko mifumo ya kale, lakini ni yenye bei sana. Ilikuja kuwa wazi kwamba halikuwa tena jambo lisilogharimu fedha sana kuchapa magazeti katika nchi 51 tofauti. Kwa sababu hiyo, katika miaka ya 1990, “msimamizi-nyumba mwaminifu” amechunguza upya hali hiyo. Uamuzi wa mwisho ulikuwa nini?
13 Uchunguzi ulionyesha kwamba “mali” iliyotolewa na Mashahidi wa Yehova na marafiki zao ingetumiwa vizuri zaidi ikiwa kazi ya uchapaji ingepangwa upya. Hivyo, matawi yanayofanya uchapaji yalipunguzwa pole pole. Ujerumani ulirudilia uchapaji wa magazeti kwa ajili ya nchi nyingi za Ulaya ya Mashariki na ya Magharibi, kutia nchi fulani ambazo mpaka hapo zilikuwa zikichapa magazeti yazo zenyewe. Italia inaandaa vichapo kwa nchi za Afrika na Ulaya ya Kusini-Mashariki, kutia ndani Ugiriki na Albania. Katika Afrika, magazeti huchapwa tu katika Nigeria na Afrika ya Kusini (note: reformulation). Upangaji-mambo mpya wa namna hiyo umefanywa katika sehemu zote za dunia.
Mambo Yanayopaswa Kufikiriwa
14 Mnamo Julai 1998, uchapaji wa magazeti utakuwa umesimamishwa katika nchi fulani za Ulaya, kama vile Austria, Denmark, Ufaransa, Ugiriki, Uholanzi na Uswisi. Uchapaji wa magazeti katika Ulaya utafanywa na Ujerumani, Uingereza, Hispania, Finland, Italia na Sweden. Nchi ambazo zingeendelea kuchapa na zile ambazo zingekomesha kufanya hivyo zilichaguliwa kwa kufuatana na kanuni gani? Kwa kupatana na utume wake wa kushughulika na mali ya Bwana-Mkubwa kwa hekima, “msimamizi-nyumba mwaminifu” alikadiria bei ya uchapaji na ugawaji wa magazeti katika kila nchi. Alichunguza pia sheria za nchi hizo ili kuona ni wapi ambapo vichapo vingeweza kuchapwa na kugawiwa katika hali za kisheria zenye kufaa zaidi sana.
15 Ni kwa sababu zenye kufaa hasa kwamba kazi za uchapaji zilisimamishwa katika nchi fulani na kuongezwa katika nchi zingine. Ni jambo lenye kufaa zaidi kufanya uchapaji wa vichapo vinavyohitajiwa na nchi nyingi katika nchi moja; hivyo vifaa vinavyogharimu fedha nyingi vinatumiwa vizuri zaidi. Kazi za uchapaji zinafanywa sasa mahali ambapo gharama ni za chini zaidi, ambapo vifaa vinapatikana na ambapo matakwa ya usafirishaji ni mazuri. Hivyo, mali ya Bwana-Mkubwa inatumiwa vema. Ni wazi kwamba jambo la kusimamisha uchapaji katika nchi fulani halimaanishi kwamba mahubiri yatakoma huko. Kutakuwako kiasi kikubwa cha vichapo kitakachopatikana, na mamia ya maelfu ya Mashahidi wanaoishi katika nchi hizo wataendelea kutangaza “habari njema ya amani” kwa wanadamu wenzao. (Efe. 2:17) Zaidi ya faida za kifedha, upangaji-mambo mpya huo una matokeo mengine mazuri.
16 Kwa mfano, mengi ya matbaa ya kisasa yaliyokuwa Denmark, Ugiriki, Uholanzi na Uswisi yamesafirishwa kwenda Nigeria na Ufilipino. Waendeshaji wa matbaa wenye ujuzi walikubali mwaliko wa kusindikiza matbaa hayo na kuzoeza akina ndugu wa mahali hapo ili waziendeshe baadaye. Kutokana na hilo, nchi hizo sasa zinayo magazeti ya hali ya juu kama vile nchi zingine.
17 Acheni tufikirie faida ifuatayo: gharama ya uchapaji wa magazeti sasa inalipiwa na zile nchi chache ambako uchapaji huo unaendelea. Kama tokeo, katika nchi ambako uchapji ulikomeshwa, fedha hupatikana sasa kwa ajili ya mambo mengine, kwa mfano kwa ajili ya kujenga Majumba ya Ufalme au kutimiza mahitaji ya ndugu zetu katika nchi silizo maskini zaidi. Hivyo, kupitia matumizi mazuri ya mali ya Bwana-Mkubwa, maneno haya ya mtume Paulo kwa Wakorintho yanaweza kutumiwa kwa matokeo zaidi ulimwenguni pote: “Sikusudii iwe rahisi kwa wengine, lakini vigumu kwenu; bali kwamba kupitia usawazisho wa ziada yenu sasa hivi ipate kujazia upungufu wao, . . . ili usawazisho upate kutukia.”—2 Kor. 8:13, 14.
18 Kutokana na huo upangaji-mambo mpya, Mashahidi wa Yehova wa ulimwenguni pote wanajisikia wenye kukaribiana zaidi. Kuhusu Mashahidi wa Denmark, kuchapwa kwa magazeti yao Ujerumani si tatizo, ingawa hapo awali walizoea kuyachapa wao wenyewe. Wao ni wenye shukrani kwa kazi inayotimizwa na ndugu zao wa Ujerumani. Je! Mashahidi wa Yehova wa Ujerumani wanaudhika kuona kwamba zawadi zao zinatumiwa ili kuchapa vichapo vya kibiblia kwa ajili ya Denmark—au Urusi, Ukrainia na nchi zinginezo? Bila shaka hapana. Wao ni wenye furaha kujua kwamba zawadi za ndugu zao katika nchi hizo zinaweza kutumiwa sasa ili kutimiza mahitaji mengine.
Tulinde Mali
19 Katika Majumba ya Ufalme yote ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kuna kibweta cha zawadi kiitwacho “Zawadi kwa Ajili ya Kutegemeza Kazi ya Ulimwenguni ya Sosaiti—Mathayo 24:14.” Zawadi za kujipendea zinazotiwa katika vibweta hivyo zinatumiwa mahali pote panapokuwa uhitaji. “Msimamizi-nyumba mwaminifu” ndiye anayeamua matumizi ya zawadi hizo. Hivyo, zawadi zilizowekwa katika kibweta katika nchi fulani zinaweza kutegemeza kazi katika nchi nyingine ya mbali kwenye maelfu ya kilometa. Zawadi za namna hiyo zilitumiwa ili kusaidia Wakristo wenzetu waliopatwa na tufani, dhoruba, mtetemeko wa dunia au vita. Hizo zinatumika pia kwa kutegemeza wamishonari katika zaidi ya nchi 200.
20 Kwa kawaida, katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, mambo ya fedha huzungumziwa mara moja tu kwa mwezi, na hilo kwa dakika chache tu. Hakuna kudai sadaka, wala katika Majumba ya Ufalme wala katika makusanyiko. Hakuna mtu anayebembelezwa ili kupata fedha na hakuna wakusanya-fedha wanaokodishwa. Kwa kawaida, Mnara wa Mlinzi hutangaza makala moja tu kwa mwaka ambayo hufasiria namna wale wanaotaka wanaweza kutoa zawadi kwa Sosaiti Watch Tower ili kutegemeza kazi ya ulimwenguni. Kwa kawaida, fedha za Sosaiti hazitajwi hata mara moja katika kurasa za Amkeni! Iliwezekanaje basi kutimiza kazi kubwa ya ulimwenguni pote ya mahubiri, kujenga Majumba ya Ufalme yanayohitajiwa, kutegemeza utumishi wa pekee wa wakati wote na kusaidia Wakristo waliokuwa katika uhitaji? Yehova alibariki watumishi wake kwa njia bora sana kwa kutokeza ukarimu. (2 Kor. 8:2) Tunatumia nafasi inayotolewa kwetu ili kushukuru wale wote ‘waliomuheshimu Yehova kwa mali yao.’ Wote na wawe hakika kwamba “msimamizi-nyumba mwaminifu” ataendelea kulinda mali ya Bwana-Mkubwa. Tunamwomba Yehova abariki mipango yote iliyochukuliwa kwa ajili ya mpanuko wa kazi ulimwenguni.
[Footnotes]
a Katika nchi saba kati ya hizo, uchapaji wa vichapo ulifanywa na mashirika ya kibiashara.