Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • km 2/00 uku. 3-6
  • Kuhubiri habari njema ukiwa na usadikisho wenye nguvu

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Kuhubiri habari njema ukiwa na usadikisho wenye nguvu
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2000
  • Habari za Kufanana na Zile
  • Wazazi—Musaidie Watoto Wenu Wakuwe na “Hekima kwa Ajili ya Wokovu”
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2017
  • Ukuwe Hakika Kama Mambo Yenye Unaamini Ni ya Kweli
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2020
  • Ukuwe Hakika Kabisa Kama Uko na Kweli
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2021
  • “Vuka Uingie Makedonia”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” juu ya Ufalme wa Mungu
Ona Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2000
km 2/00 uku. 3-6

Kuhubiri habari njema ukiwa na usadikisho wenye nguvu

1 Mapema katika karne ya kwanza, Yesu Kristo aliwatuma wafuasi wake wahubiri habari njema ya Ufalme na ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mt. 24:14; 28:19, 20) Mashahidi wa Yehova wamechukua agizo hilo kwa uzito, hivi kwamba kufikia mwisho wa karne ya 20, udugu wetu wa Kikristo uliongezeka hadi zaidi ya wanafunzi 5 900 000 katika mabara 234. Ni mlio wa sifa mkubwa kama nini kwa Baba yetu wa kimbingu!

2 Sasa tumeingia karne ya 21. Mpinzani wetu hujaribu kwa hila kuzuia kazi yetu kubwa ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Yeye hutumia mikazo kutoka kwa mfumo huu wa mambo ili kujitahidi kukengeusha uangalifu wetu, kula wakati wetu, na kumaliza nguvu zetu katika mambo mengi na faida zisizo za lazima. Badala ya kuruhusu mfumo huu wa mambo uamue lililo la maana maishani, sisi hutumia Neno la Mungu ili kujihakikishia lililo la maana zaidi—kufanya mapenzi ya Yehova. (Rom. 12:2) Hilo lamaanisha kutii himizo la Kimaandiko la ‘kuhubiri neno katika majira yenye kufaa na yale yenye taabu, na kutimiza kikamili huduma yetu.’—2 Tim. 4:2, 5.

3 Sitawisha usadikisho thabiti: Wakristo wanahitaji “kusimama [wa]kiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu.” (Kol. 4:12) Neno “usadikisho” linafafanuliwa kuwa “ushawishi au imani; hali ya kuwa mwenye kusadikishwa.” Tukiwa Wakristo, tunapaswa kusadikishwa kwamba neno la Mungu la kiunabii ni hakika na kwamba sasa tumeingia sana katika wakati wa mwisho. Tunapaswa kuwa na imani yenye nguvu kama ile ya mtume Paulo, aliyesema kwamba habari njema ‘kwa kweli ni nguvu ya Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila mtu mwenye imani.’—Rom. 1:16.

4 Ibilisi hutumia watu waovu na wadanganyi, ambao wamedanganywa wao wenyewe, ili kuvuta na kudanganya wengine. (2 Tim. 3:13) Tukiwa wenye kuonywa kimbele kuhusu jambo hilo, sisi huchukua hatua ili kutia nguvu usadikisho wetu kwamba tunayo kweli. Badala ya kuacha mahangaiko ya maisha yapunguze bidii yetu, tunaendelea kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza. (Mt. 6:33, 34) Hatutaki pia kusahau ile hali ya haraka ya nyakati, labda tukifikiri kwamba mwisho wa mfumo huu uko mbali sana. Huo unakaribia zaidi na zaidi. (1 Pet. 4:7) Ingawa tunaweza kufikiri kwamba kueneza habari njema hakuna matokeo mengi katika mabara mengine kwa sababu ya ushahidi ambao umekwisha kutolewa, sharti kazi ya kutoa onyo iendelee.—Ezek. 33:7-9.

5 Haya ni maulizo ya msingi ya kujiuliza sasa: ‘Je, ninachukua kwa uzito amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi? Wakati ninapohubiri habari njema, je, ninaonyesha usadikisho wenye nguvu kwamba Ufalme ni jambo halisi? Je, mimi ninaazimia kushiriki zaidi iwezekanavyo katika huduma hii yenye kuokoa uhai?’ Tukitambua jinsi tumeingia mbali sana katika wakati wa mwisho, tunapaswa kuwa waangalifu juu yetu wenyewe na juu ya utume wetu wa kuhubiri na kufundisha. Kwa kufanya hivyo tutajiokoa sisi wenyewe na wale wanaotusikiliza. (1 Tim. 4:16) Tunawezaje sote kutia nguvu usadikisho wetu tukiwa wahudumu?

6 Igeni wathesalonike: Akikumbuka kazi ngumu ya akina ndugu katika Thesalonike, mtume Paulo aliwaambia: “Habari njema tuhubiriyo haikutokea miongoni mwenu kwa usemi pekee bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na usadikisho wenye nguvu, kama vile nyinyi mjuavyo ni watu wa namna gani sisi tulipata kuwa kwenu kwa ajili yenu; nanyi mkawa waigaji wetu na wa Bwana, kwa vile mlilipokea neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu.” (1 Thes. 1:5, 6) Ndiyo, Paulo alisifu kutaniko la Wathesalonike kwa sababu walihubiri kwa bidii na usadikisho wenye nguvu ingawa mateso mengi. Ni nini kilichowawezesha wao kufanya hivyo? Kwa kiasi kikubwa, bidii na usadikisho walioona kwa mtume Paulo na wafanyakazi wenzake vilikuwa na uvutano wenye kufaa juu yao. Namna gani hivyo?

7 Maisha yenyewe ya Paulo na waandamani wenzake wasafiri yalihakikisha kwamba roho ya Mungu ilikuwa juu yao na kwamba waliamini kwa moyo wote yale waliyokuwa wakihubiri. Kabla ya kuja Thesalonike, Paulo na Sila walikuwa wametendewa bila adabu katika Filipi. Bila kuhukumiwa, walipigwa, walitiwa gerezani, na walifungwa katika mikatale (miti yenye kuchongwa ili kufunga watumwa). Hata hivyo, jaribu hilo halikupunguza bidii yao kwa ajili ya habari njema. Kuingilia mambo kwa Mungu kulifanya waachiliwe, kuliongoza mlinzi wa gereza na watu wa nyumba yake wawe waamini, na kuliongoza ndugu hao waendelee katika huduma yao.—Mdo. 16:19-34.

8 Katika nguvu ya roho ya Mungu, Paulo alikuja Thesalonike. Huko alifanya kazi ya jasho ili kutosheleza mahitaji yake mwenyewe na kisha akajitoa kikamili katika kufundisha kweli kwa Wathesalonike. Hakuepuka kutangaza habari njema kila wakati nafasi ilipojitokeza. (1 Thes. 2:9) Kuhubiri kwa Paulo akiwa na usadikisho wenye nguvu kulikuwa na uvutano wenye nguvu juu ya watu wa mahali hapo hivi kwamba waliacha ibada yao ya sanamu ya zamani na wakawa watumishi wa Mungu wa kweli, Yehova.—1 Thes. 1:8-10.

9 Mnyanyaso haukuzuia waamini hao wapya kuhubiri habari njema. Wakichochewa na imani yao mpya na wakiwa na hakika kwamba wangepata baraka za milele, Wathesalonike walilazimika kutangaza kweli ambayo walikuwa wamekubali kwa shauku. Kutaniko hilo likawa lenye kutenda sana hivi kwamba habari kuhusu imani na bidii yao ikaenea hadi sehemu nyinginezo za Makedonia na hata Akaya. Kwa hiyo, wakati Paulo alipoandika barua yake ya kwanza kwa Wathesalonike, kazi zao nzuri zilikuwa tayari zinajulikana vema. (1 Thes. 1:7) Ni kielelezo chenye kutokeza kama nini!

10 Wenye kuchochewa na upendo kwa Mungu na kwa watu: Kama Wathesalonike, tunawezaje leo kudumisha usadikisho wa binafsi wenye nguvu wakati tunapohubiri habari njema? Paulo aliandika kuhusu hao: “Bila kukoma twazingatia akilini kazi yenu ya uaminifu na jitihada yenu kwa sababu ya upendo.” (1 Thes. 1:3, kielezi-chini) Ni wazi kwamba walikuwa na upendo wenye kina kirefu na wenye kutoka moyoni kwa Yehova Mungu na kwa watu waliohubiria. Upendo huohuo ndio ulichochea Paulo na waandamani wenzake kuwapa Wathesalonike, “si habari njema ya Mungu tu bali pia nafsi [zao] wenyewe.”—1 Thes. 2:8.

11 Vivyo hivyo, upendo wetu wenye kina kirefu kwa Yehova na kwa wanadamu wenzetu hutuchochea kutaka kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri ambayo Mungu ametutolea kufanya. Kwa upendo kama huo, tunatambua kwamba kueneza habari njema ni daraka letu binafsi tulilopewa na Mungu. Kwa kutafakari ifaavyo na kwa uthamini yote ambayo Yehova amefanya kwa ajili yetu katika kutuongoza kwenye “uhai ulio halisi,” tunachochewa kuambia wengine kweli hizohizo nzuri ajabu ambazo tunaamini kwa moyo wetu wote.—1 Tim. 6:19.

12 Kadiri tunavyoendelea kuwa wenye shughuli katika kazi ya kuhubiri, upendo wetu kwa Yehova na kwa watu unapaswa kuendelea kukomaa. Ikiwa upendo huo unakomaa, tutachochewa kuzidisha kushiriki kwetu katika huduma ya nyumba kwa nyumba na kufuatia aina nyingine zote za kutoa ushahidi zinazofunguliwa kwa ajili yetu. Tutafaidika na nafasi zote ili kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa watu wa jamaa, majirani, na watu tunaojuana nao. Ijapokuwa watu wengi wanaweza kukataa habari njema tunayowatolea na kwamba wengine watajitahidi kuzuia kule kutangaza Ufalme, sisi tunapata furaha ya moyoni kwa kuwa tunajua kwamba tumefanya yote tuwezayo ili kutoa ushahidi kuhusu Ufalme na kusaidia watu wapate wokovu. Naye Yehova atabariki jitihada zetu za kupata wale wenye mioyo minyofu. Hata wakati mikazo ya maisha inapotulemea na Shetani anapotafuta kuharibu furaha yetu, tunaweza kudumisha usadikisho wetu wenye nguvu na bidii yetu katika kutoa ushahidi kwa wengine. Wakati sisi sote tunapotimiza fungu letu, hilo hutokeza makutaniko yenye nguvu na yenye bidii kama lile la Thesalonike.

13 Usikate tamaa kamwe chini ya jaribu: Usadikisho unahitajiwa pia wakati tunapokabiliana na majaribu mbalimbali. (1 Pet. 1:6, 7) Yesu alionyesha wazi wanafunzi wake kwamba ikiwa wangemfuata, wangekuwa “vitu vya kuchukiwa na mataifa yote.” (Mt. 24:9) Paulo na Sila walijionea hilo walipokuwa katika Filipi. Simulizi katika Matendo sura 16 lasema kwamba Paulo na Sila walitupwa katika gereza ya ndani zaidi na kufungwa katika mikatale. Kwa kawaida, gereza kubwa ilikuwa aina ya uwanja au sebule; kwenye mpaka wa sebule hiyo kulikuwa vyumba vilivyofaidika na mwangaza na hewa. Hata hivyo, hakuna uandalizi uliofanywa kwa ajili ya mwangaza na nuru katika gereza ya ndani zaidi. Paulo na Sila walilazimika kukabiliana na giza, joto, na harufu mbaya ya mahali hapo pa kifungo penye taabu. Je, unaweza kufikiria maumivu ambayo sharti walisikia wakati walipokuwa wenye kufungwa kwa saa nyingi katika mikatale, huku migongo yao ikiwa tupu na yenye kutoka damu kwa sababu ya kupigwa fimbo?

14 Ijapokuwa majaribu hayo, Paulo na Sila walibaki waaminifu. Walionyesha usadikisho wenye kutoka moyoni, ukiwatia nguvu watumikie Yehova yajapokuwa majaribu. Usadikisho wao unakaziwa katika mstari 25 wa sura 16, ambapo inasemwa kwamba Paulo na Sila walikuwa “wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” Kwa kweli, ijapokuwa walikuwa katika gereza ya ndani zaidi, walikuwa na hakika ya kuwa na kibali cha Mungu hivi kwamba wanaume hao waliimba kwa sauti kubwa ambayo ilisikiwa na wafungwa wengine! Tunapaswa kuwa na usadikisho huohuo leo wakati tunapokabiliana na majaribu ya imani yetu.

15 Majaribu ambayo Ibilisi huweka juu yetu ni mengi. Kwa wengine, huenda ukawa mnyanyaso kutoka kwa familia. Wengi kati ya ndugu zetu hukabiliana na matatizo ya kisheria. Huenda tukapambana na upinzani kutoka kwa waasi-imani. Kuna mizigo ya kifedha na mahangaiko kuhusu jinsi ya kupata riziki. Vijana hukabiliana na mkazo kutoka kwa vijana wengine shuleni. Tunawezaje kukabiliana na majaribu hayo kwa matokeo? Ni nini linalohitajiwa ili kuonyesha usadikisho?

16 Jambo la kwanza na la maana zaidi ni kwamba tunahitaji kudumisha uhusiano wa karibu na wa binafsi pamoja na Yehova. Wakati Paulo na Sila walipokuwa katika gereza ya ndani zaidi, hawakutumia wakati huo ili kulalamika kuhusu hali yao maishani au kujihurumia wenyewe. Mara moja walimwendea Mungu katika sala na kumsifu katika wimbo. Kwa nini? Kwa kuwa walikuwa na uhusiano wa karibu na wa binafsi pamoja na Baba yao wa kimbingu. Walitambua kwamba walikuwa wakiteseka kwa ajili ya uadilifu na kwamba wokovu wao ulikuwa mikononi mwa Yehova. —Zab. 3:8.

17 Wakati tunapokabiliana na majaribu leo, sisi pia tunapaswa kumwendea Yehova. Tukiwa Wakristo, Paulo atutia moyo ‘tuache maombi yetu ya bidii yajulikane kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili.’ (Flp. 4:6, 7) Ni jambo lenye kuburudisha kama nini kujua kwamba Yehova hatatuachilia pekee yetu tunapokuwa katika majaribu! (Isa. 41:10) Yeye yuko pamoja nasi sikuzote kadiri tunavyomtumikia tukiwa na usadikisho wa kweli. —Zab. 46:7.

18 Msaada mwingine wa maana sana katika kuonyesha usadikisho ni kubaki wenye shughuli katika utumishi wa Yehova. (1 Kor. 15:58) Paulo na Sila walitupwa gerezani kwa sababu walikuwa wamekuwa wenye shughuli ya kuhubiri habari njema. Je, waliacha kuhubiri kwa sababu ya majaribu yao? Hapana, waliendelea kuhubiri hata walipokuwa gerezani, na baada ya kuachiliwa, walisafiri kwenda Thesalonike na wakaenda katika sinagogi la Wayahudi ili ‘kutoa sababu pamoja nao kutokana na Maandiko.’ (Mdo. 17:1-3) Wakati tunapokuwa na usadikisho wenye nguvu au imani katika Yehova, na wakati tunapokuwa hakika kwamba tunayo kweli, hakuna kitu ambacho ‘kitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.’—Rom. 8:35-39.

19 Vielelezo vya ki-siku-hizi vya usadikisho wenye nguvu: Kuna vielelezo vingi vyenye kutokeza vya wale ambao, kama Paulo na Sila, wameonyesha katika siku yetu usadikisho wenye nguvu. Dada mmoja aliyeokoka kambi ya mateso ya Auschwitz asimulia kuhusu imani na usadikisho usiotikisika ambao ulionyeshwa na ndugu na dada zetu huko. Yeye aeleza: “Wakati mmoja tulipokuwa tukiulizwa-ulizwa maswali, ofisa mmoja alikuja kuelekea mahali nilipokuwa, ngumi zake zikiwa zenye kukunjwa. ‘Tutafanya nini nanyi?’ akasema. ‘Tukiwakamata, hamjali. Tukiwatuma gerezani, hamjali hata kidogo. Tukiwatuma kwenye kambi ya mateso, hilo haliwatii wasiwasi. Wakati tunapowahukumia kifo, mnasimama tu hapo bila kujali. Tutafanya nini nanyi?’ ” Ni jambo lenye kutia nguvu imani kama nini kuona imani ambayo ndugu zetu walikuwa nayo chini ya hali ngumu kama hizo! Walimwendea Yehova sikuzote awasaidie wavumilie.

20 Bila shaka tunakumbuka usadikisho wa wengi wa ndugu zetu wakati walipokabiliana na chuki ya kikabila ambayo ilionekana wazi miaka ya karibuni. Ijapokuwa wao hujikuta katika hali zenye hatari, akina ndugu wenye madaraka hukaza fikira waangalie kwamba ndugu na dada zao ni wenye kulishwa kiroho. Wote hubaki waaminifu wakiwa na usadikisho wenye nguvu kwamba ‘kila silaha inayotengenezwa juu yao haitasitawi.’—Isa. 54:17.

21 Wengi kati ya ndugu na dada zetu walio na wenzi wasioamini ni wenye kuonyesha pia imani yenye nguvu, na uvumilivu. Ndugu mmoja huko Guadeloupe alipambana na upinzani wenye nguvu kutoka kwa mke wake asiyeamini. Ili kumvunja moyo na kuzuia kuhudhuria kwake mikutano ya Kikristo, mke huyo hangempikia chakula wala kufua, kupiga pasi, na kunyoosha mavazi yake. Kwa muda mrefu, mke huyo alikataa kumsemesha. Lakini kwa kuonyesha usadikisho wenye kutoka moyoni katika kutumikia Yehova na kwa kumwendea katika sala ili kupata msaada, ndugu huyo aliweza kuvumilia hayo yote. Kwa muda gani? Kwa miaka 20 hivi; baada ya miaka hiyo, hatua kwa hatua moyo wa mke wake ukabadilika. Mwishowe, ndugu huyo angeweza kufurahi kwelikweli kwa sababu mke wake alikubali tumaini la Ufalme wa Mungu.

22 Kwa kumalizia, hatupaswi kusahau usadikisho wenye nguvu wa ndugu na dada zetu vijana wanaohudhuria shule kila siku na wanaokabiliana na mikazo kutoka kwa vijana wenzao na matatizo mengine. Kuhusu mikazo ya kufanya kama wengine shuleni, binti mmoja Shahidi alisema: “Wakati unapokuwa shuleni, kila mtu anakutia moyo sikuzote uwe mwasi kwa kiasi fulani. Watoto hukuheshimu zaidi ikiwa unafanya jambo fulani la uasi.” Vijana wetu hupambana na mikazo kama nini! Wanapaswa kuazimia kwa uthabiti akilini na moyoni kushinda kishawishi.

23 Wengi kati ya vijana wetu ni wenye kufanikiwa katika kudumisha uaminifu-maadili wao ingawa majaribu. Mfano mmoja ni ule wa dada kijana anayeishi Ufaransa. Siku moja baada ya mlo, vijana wanaume fulani walijaribu kumkaza awabusu, lakini yeye alisali na akakataa kwa nguvu hivi kwamba vijana wanaume hao wakamwacha. Baadaye, mmoja wao akarudi na kumwambia kwamba alivutiwa naye kwa sababu ya ujasiri wake. Dada huyo aliweza kumtolea ushahidi mzuri kuhusu Ufalme, akimfasiria viwango vya juu ambavyo Yehova anaweka mbele ya wale wote wanaotaka kushiriki katika baraka za Ufalme huo. Mnamo mwaka huo wa shule, yeye alifasiri pia imani zake kwa darasa lote.

24 Ni pendeleo lenye thamani kama nini tulilo nalo kuhesabiwa kati ya wale ambao Yehova anafurahi kutumia ili kusema kwa usadikisho thabiti kuhusu mapenzi yake! (Kol. 4:12) Kwa kuongezea, tunayo nafasi nzuri ajabu ya kuonyesha uaminifu-maadili wetu tunaposhambuliwa na Mpinzani wetu aliye kama simba, Shetani Ibilisi. (1 Pet. 5:8, 9) Usisahau kamwe kwamba Yehova ni mwenye kutumia ujumbe wa Ufalme ili kuleta wokovu kwetu sisi tunaouhubiri na kwa wale wanaosikiliza. Acheni maamuzi tunayofanya na njia yetu ya kila siku ya maisha vihakikishe kwamba tunaweka Ufalme pa nafasi ya kwanza. Acheni tuendelee kuhubiri habari njema kwa usadikisho wenye nguvu!

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine