Wazazi—ingizeni mazoea mazuri ndani ya watoto wenu
1 Hatuzaliwi na mazoea mazuri; hayo pia hayapatikani kama kwa bahati tu. Zaidi ya hayo, kuingiza mazoea mazuri ndani ya watoto kunaomba wakati. ‘Kuingiza’ kunamaanisha ‘kufanya kitu kiende ndani’ au ‘kupenyeza.’ Kutobadilika-badilika kunahitajiwa kwa upande wa wazazi ili ‘waendelee kulea [watoto wao] katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’—Efe. 6:4.
2 Anzeni tangu utoto mchanga sana: Uwezo wa watoto wachanga wa kujifunza na kufanya mambo mapya ni wa ajabu. Ingawa watu wazima huona kuwa ni vigumu kujifunza lugha mpya, watoto wenye umri wa kabla ya kwenda shuleni wanaweza kujifunza lugha mbili au tatu kwa wakati uleule. Msifikiri kamwe kwamba mtoto wenu ni mdogo mno ili kukomaza mazoea mazuri. Ikiwa maagizo katika kweli ya Biblia yanaanza mapema na kwamba hayo yanaendelezwa, kufikia wakati ambapo mtoto ana umri wa miaka michache, akili yake itakuwa imejaa ujuzi ambao utamfanya awe “mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.”—2 Tim. 3:15.
3 Fanyeni utumishi wa shambani kuwa zoea: Zoea zuri linalopaswa kuingizwa ndani ya mtoto katika miaka ya kujenga utu wake ni lile la kuhubiri kikawaida habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wazazi wengi huanza hilo kwa kupeleka watoto wao katika huduma ya nyumba kwa nyumba wakati watoto wao wangali wachanga. Kuhusika kikawaida kwa wazazi katika kazi ya kutoa ushahidi kunasaidia watoto wao wakomaze uthamini na bidii kuelekea huduma. Wazazi wanaweza kuonyesha watoto jinsi ya kushiriki katika kutoa ushahidi katika kila upande wa utumishi wa shambani.
4 Kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi pia kunasaidia watoto. Kunawafundisha mazoea mazuri ya funzo na jinsi ya kusoma kwa uelewevu. Wanajifunza kuzungumza kuhusu Biblia, kufanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mazoezi kama hayo yanaweza kuwachochea wawe mapainia na kujitahidi kufikia mapendeleo ya pekee ya utumishi. Wanabetheli na wamishonari wengi hukumbuka kwa hamu miaka yao ya mapema katika shule hiyo, nao huiona kuwa uandalizi uliowasaidia kukomaza mazoea mazuri.
5 Sisi sote ni kama udongo katika mikono ya Mfinyanzi Mkuu, Yehova. (Isa. 64:8) Udongo ni mwepesi zaidi kupatia umbo ikiwa haujabadilishwa. Huo unakuwa mgumu zaidi kadiri unavyokauka. Mambo ni hivyohivyo kuhusu watu. Wakati wanapokuwa wachanga, wanaweza kurekebishwa zaidi—na matokeo ni mazuri zaidi ikiwa hao ni wachanga zaidi. Miaka yao ya uchanga ni miaka ya kujenga utu wao, wakati ambapo jambo hilo linaweza kufanywa kwa ajili ya mema au mabaya. Ukiwa mzazi mwenye kujali, anza mapema kuingiza ndani ya watoto wako mazoea mazuri katika huduma ya Kikristo.