“Tumetumika Eneo Letu Mara Nyingi!”
1 Je, umepata kufikiri kwamba eneo lenu linatumikwa mara nyingi sana hivi kwamba hakuna tena watu wenye mfano wa kondoo wanaobaki ndani yake? Labda ulifikiri: ‘Ninajua jinsi watu watakavyoitikia. Kwa nini kuendelea kurudi kuona wale wasiopendezwa?’ Ni kweli kwamba maeneo mengi yanatumikwa mara nyingi. Hata hivyo, jambo hilo linapaswa kuonwa kwa njia yenye kufaa, si kwa njia isiyofaa. Kwa nini hivyo? Ona sababu nne zinazotolewa hapa chini.
2 Sala Zetu Zimejibiwa: Yesu alisema: “Kwa kweli, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Luka 10:2) Kwa makumi mengi ya miaka, tumeomba kwa unyenyekevu Yehova atusaidie. Mahali pengi, sasa tuna wafanyakazi wa ziada waliohitajiwa, na tunamaliza kutembelea eneo kwa ukawaida zaidi. Je, jambo la kwamba Yehova amejibu sala zetu halipaswi kutufanya tushangilie?
3 Kuendelea Bila Kuacha Huzaa Matunda Mazuri: Hata katika maeneo yanayotumikwa kwa ukawaida, watu ni wenye kuitikia ujumbe wa Ufalme, nao ni wenye kufikia ujuzi wa kweli. Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kutembelea watu tena na tena tukiwa na tumaini la kupata wengine zaidi walio na mioyo minyofu. (Isa. 6:8-11) Kama wanafunzi wa mapema wa Yesu walivyofanya, “nendeni kwa kuendelea” kwa watu katika eneo mlilogawiwa, mkijitahidi kuamsha kupendezwa kwao na Ufalme wa Mungu.—Mt. 10:6, 7.
4 Huko Ureno, makutaniko mengi humaliza kutembelea eneo layo kila juma, lakini yangali yanapata watu wenye mfano wa kondoo. Dada mmoja hasa ana mtazamo wenye kufaa sana. Anasema: “Kabla ya kuondoka kwenda katika utumishi kila asubuhi, ninasali kwa Yehova ili anisaidie nipate mtu fulani mwenye kupendezwa na kujifunza Biblia.” Siku moja alipanga kujifunza na wafanyakazi katika duka la mtengenezaji wa nywele. Lakini, baadaye, mtu mmoja tu ndiye aliyeonekana kwa ajili ya funzo. Mtu huyo akasema: “Wale wengine hawapendezwi, lakini mimi ninapendezwa.” Baada ya mwezi mmoja, mwanamke huyo alikuwa akiongoza mafunzo ya Biblia mawili yeye mwenyewe. Upesi baada ya hapo akabatizwa, na baadaye akaingia katika utumishi wa painia!
5 Kazi Ni Yenye Kutimizwa: Habari njema ni yenye kuhubiriwa, kama vile tu Yesu alivyotabiri. (Mt. 24:14) Hata mahali ambapo watu ‘hawatusikilizi,’ wao ni wenye kuonywa kupitia kazi ya kuhubiri. Tunatazamia kwamba wengine hawatakuwa tayari kusikiliza au hata kwamba watapinga kweli. Hata hivyo, watu kama hao wanapaswa kuonywa ifaavyo kuhusu hukumu inayokuja kutoka kwa Yehova.—Ezek. 2:4, 5; 3:7, 8, 19.
6 Hatujamaliza Bado: Si daraka letu kuamua wakati wa kusimamisha kazi ya kuhubiri. Yehova anajua kikamili wakati ambapo hiyo inapaswa kwisha. Anajua ikiwa kuna watu katika eneo letu ambao bado wanaweza kuitikia habari njema. Leo, watu fulani husema kwamba hawapendezwi, lakini mabadiliko makubwa katika maisha yao—kupoteza kazi, ugonjwa mkali, kifo cha mpendwa—yanaweza kuwafanya wawe tayari kusikiliza wakati mwingine. Kwa sababu ya chuki isiyo na sababu au kwa sababu ya kuwa tu na shughuli nyingi hivi kwamba hakuna wakati wa kusikiliza, watu wengi hawajapata kamwe kusikia kwa kweli yale tunayohubiri. Ziara za kirafiki za wakati kwa wakati huenda zikawafanya watambue na kusikiliza.
7 Wale waliokomaa katika miaka ya karibuni na ambao sasa wana familia zao wenyewe ni wenye kuchukua maisha kwa uzito zaidi, nao ni wenye kuuliza maulizo ambayo ni Neno la Mungu tu ndilo linaloweza kujibu. Mama mmoja kijana alialika Mashahidi wawili wa kike katika nyumba yake, naye akasema: “Nilipokuwa binti mdogo, singeweza kamwe kuelewa kwa nini mama yangu alirudisha Mashahidi na kuwaambia kwamba hakuwa mwenye kupendezwa, ingawa walitaka tu kuongea kuhusu Biblia. Wakati huo niliamua kwamba wakati ambapo ningekomaa, ambapo ningeolewa, na kuwa na nyumba yangu mwenyewe, ningeomba Mashahidi wa Yehova waingie na kunifasiria Biblia.” Hivyo ndivyo alivyofanya, kwa furaha ya Mashahidi waliomtembelea.
8 Je, Unaweza Kuwa Mwenye Matokeo Zaidi? Huenda isiwe sikuzote kwamba watu tunaotembelea ndio hufanya kutumika kwa ukawaida eneo letu kuwe jambo gumu. Nyakati nyingine ni sisi wenyewe. Je, tunaanza kwenda tukiwa na mawazo yasiyofaa? Hilo linaweza kuwa na uvutano juu ya mtazamo wetu na, huenda, sauti yetu na sura ya uso wetu. Onyesha roho yenye kufaa na sura yenye kupendeza. Jaribu ufundi mpya. Fanya utoaji wako uwe wenye kubadilika-badilika, na ujaribu kuufanya kuwa bora. Labda unaweza kubadili ulizo lako la kuanza au kutumia andiko tofauti katika mazungumzo. Uliza ndugu na dada wengine yale ambayo wameona kuwa yenye mafanikio katika kutumika eneo. Fanya kazi katika utumishi pamoja na wahubiri na mapainia mbalimbali, na uone kile kinachofanya huduma yao kuwa yenye matokeo.
9 Kazi ya kuhubiri Ufalme ina ukubali na baraka ya Yehova, na kushiriki kwetu katika kazi hiyo ni uhakikisho wa upendo wetu kwake na kwa jirani yetu. (Mt. 22:37-39) Kwa hiyo, acheni tutimize kazi yetu mpaka mwisho, bila kuchoka kwa sababu ya kutumika eneo wakati kwa wakati.