Je, Unaweza Kujitoa?
1 Tukio lisilo la kawaida lafanyika mnamo mwaka wa 778 K.W.K. Katika ono, nabii Isaya aona ‘Yehova akikaa juu ya kiti cha ufalme, kilicho juu na chenye kunyanyuliwa.’ Kisha, Isaya asikia maserafi wakivuta uangalifu juu ya utukufu wa Yehova, wakisema: “Mutakatifu, mutakatifu, mutakatifu ni [Yehova] wa majeshi.” Hilo lapaswa kuwa jambo lililochochea heshima yenye kuchanganyika na woga kama nini! Katika hali hiyo, Yehova auliza ulizo lenye mwito wa kushindana: “Mimi nitamutuma nani, na nani atakayekwenda kwa [ajili yetu]?” Hakuna maelezo yanayotolewa kuhusu aina ya mgawo au ikiwa mtu anayejitoa atapata faida kutokana na mgawo huo. Hata hivyo, bila kusita, Isaya ajibu: “Mimi hapa; nitume mimi.”—Isa. 6:1, 3, 8.
2 Roho hiyo ya kuwa tayari kufanya lolote ambalo Yehova anaomba ni alama inayotofautisha watu wake. (Zab. 110:3) Na sasa mwaliko wa pekee ni wenye kutolewa kwa wale wanaoweza kujitoa. Je, wewe ni tayari kuitikia kwa roho yenye nia tayari, kama ile ya Isaya?
3 Kuna uhitaji wenye kuongezeka wa akina ndugu ili kutumikia kwenye Betheli. Hilo linaomba wawe na tamaa yenye nguvu ya kuweka faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza na kuwa na nia tayari ya kufanya lolote wanaloweza kuombwa ili kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri. (Mt. 6:33) Kwa kweli, kutumikia kuwa mshiriki wa familia ya Betheli kunatolea mtu nafasi ya pekee ya kutumikia Yehova kwa moyo wote. Namna gani hivyo?
4 Kazi Inayofanywa Kwenye Betheli: Fikiria yale yote yanayotimizwa kikawaida katika yale majengo matatu ya Betheli yanayopatikana katika Shirikisho la Amerika, huko Brooklyn, Patterson, na Wallkill, New York. Wale ndugu na dada 5,730 wanaofanyiza familia ya Betheli mahali hapo patatu wanalo pendeleo la kuhusika kwa ukaribu katika kutegemeza jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara na Baraza lake Linaloongoza katika kutokeza Biblia na vichapo vya kibiblia vinavyotumiwa katika shamba la ulimwenguni pote na katika funzo la kibinafsi. (Mt. 24:45) Kwa mfano, mwaka huu wa utumishi uliopita, vitabu 24,364,670, vijitabu na broshua 39,813,464, magazeti 270,528,000, na kaseti za kusikiliza 1,271,041 zilitokezwa na kusafirishwa; hilo lilikuwa tokeo la jitihada ya pamoja ya familia ya Betheli ya Shirikisho la Amerika. Kwa ajili ya vichapo hivyo, jitihada kubwa sana hufanywa ili kutafuta na kuchagua “maneno ya kupendeza, na yale yaliyoandikwa kwa haki, maneno ya kweli.” (Mhu. 12:9, 10) Mwongozo pia unatolewa kwa wale watafsiri zaidi ya 1,900 ulimwenguni pote ambao husaidia kutokeza vichapo katika lugha zaidi ya 300. Mengi yanafanywa ili kusawazisha kazi inayotimizwa katika yale matawi 111 ulimwenguni pote, kutia ndani yale zaidi ya makutaniko 11, 500 katika Shirikisho la Amerika. Msaada unatolewa pia kwa yale matawi yanayohusika katika kupanga na kujenga makao ya ziada ya Betheli na Majumba ya Makusanyiko, na yale Majumba ya Ufalme 15,248 yanayohitajiwa sasa katika nchi zisizo na mali nyingi. Mamia ya wajitoleaji wenye nia tayari wanahitajiwa ili kushughulikia uchapishaji na usafirishaji wa vichapo, usafishaji, utunzaji wa vifaa, utayarishaji wa chakula, ununuzi, utunzaji wa kiafya, na shughuli nyinginezo nyingi kwenye Betheli.
5 Kutimiza kazi hiyo yote ni shughuli kubwa lakini yenye kutosheleza kiroho. Kujua kwamba nguvu na nishati yetu yote ni yenye kutumiwa ili kutegemeza kazi ya kuhubiri na kufundisha kunatokeza furaha nyingi. Utumishi wa Betheli unatusaidia tupate kujua tengenezo la Yehova katika mambo madogo-madogo zaidi. Tunakumbushwa kwamba mtunga-zaburi alitia Waisraeli moyo wapate kujua kwa ukaribu zaidi kitovu cha kidunia cha utawala wa kitheokrasi katika siku yao.—Zab. 48:12, 13.
6 Baraka Zinazotokana na Utumishi wa Betheli: Wale wanaotumikia Betheli wanahisi namna gani kuhusu mapendeleo yao ya utumishi? Ona maneno yafuatayo kutoka kwa washiriki wa familia ya Betheli, vijana na wale wenye umri mkubwa zaidi. Mshiriki mmoja wa familia ya Betheli ambaye amefurahia miaka mitatu ya utumishi wa Betheli anaeleza: “Kuwa kwenye Betheli kumetia nguvu uhusiano wangu pamoja na Yehova. Kadiri ninavyoendelea kutumikia hapa na kujifunza kuhusu jinsi Betheli inavyofanya kazi, hiyo inanifundisha mengi zaidi kuhusu utu wa Yehova. Pia, utumishi wa Betheli umenifungua macho ili nione kwamba Yehova anatumia watu—aina zote za watu. Nawe hauhitaji kuwa mkamilifu ili ukubaliwe naye.”
7 Ndugu mmoja kijana anajiwa tena na fikira ya jambo lililopita: “Ninakumbuka nikifikiri mwenyewe, ‘Itakuwa vizuri kama nini kuingia katika ulimwengu mpya na kuambia wale wanaume waaminifu wa zamani kwamba nilitumikia miaka mingi kwenye Betheli, si nje nikichuma fedha.’ ”
8 Ndugu mmoja kijana anatafakari juu ya mazoezi aliyopata: “Kujifunza juu yangu mwenyewe na mahali ninapopaswa kufanya marekebisho, na kisha kukomaza sifa hizo kumekuwa baraka kubwa. Sasa, ninahisi kwamba ninaweza kumtumikia Yehova kwa njia bora zaidi. Ninatambua kwamba mimi ni mvumilivu zaidi, ninajizuiza zaidi, nami ninaweza kuonyesha upendo kwa kiasi kikubwa zaidi.”
9 Dada mmoja anafikiri kuhusu baraka alizopata mpaka sasa: “Programu za kiroho hapa zimenifundisha mengi zaidi kuhusu Yehova na jinsi ninavyoweza kumwiga vizuri zaidi katika mawazo, hisia-moyo, na matendo. Na kwa kuwa mazoezi hayo ni yenye kuendelea, baraka ni yenye kuendelea pia.”
10 Ndugu mmoja ambaye amepitisha jumla ya miaka 59 katika huduma ya wakati wote, zaidi ya 43 ya miaka hiyo kwenye Betheli, alisema: “Betheli si kama nyumba ya watawa, kama wengine wanavyoweza kufikiri. Tunatimiza mengi kwa sababu ya njia yetu ya maisha yenye utaratibu. . . . Hakujapata kuwa siku ambapo nilikuja kazini bila kufurahia yale niliyofanya. Kwa nini? Kwa kuwa wakati tunapojitoa kwa Yehova kwa nafsi yote, tunatosheka kwa kujua kwamba ‘tumefanya tulilopaswa kufanya.’ ”—Luka 17:10.
11 Ndugu mwingine, ambaye ametumikia kwenye Betheli muda wa miaka 62, alisema: “Ninaamini kwa nguvu kwamba Betheli ndiyo nafasi bora zaidi duniani kabla ya kuja kwa Paradiso ya kidunia. Sijapata kamwe kujuta hata kwa sekunde moja kuona nimefanya utumishi wa wakati wote kuwa kazi yangu ya maisha yote. Imekuwa furaha kama nini kuona na kushiriki katika ule ukuzi mkubwa wa tengenezo la kidunia la Yehova! Ninaazimia, kwa msaada wa Yehova, kuendelea kufanya Betheli kuwa makao yangu na kujitahidi kwa nafsi yote ili kuendeleza faida za Ufalme.”
12 Washiriki hao wa familia ya Betheli wametaja tu chache kati ya zile baraka nyingi unazoweza kufurahia ikiwa unajitoa kwa ajili ya utumishi wa Betheli. Lakini kama ilivyo kweli kuhusu kupokea pendeleo lolote la utumishi, unapaswa kwanza kutimiza matakwa. Ni nini matakwa fulani-fulani ya kutimiza ili kutumikia kuwa mshiriki wa familia ya Betheli?
13 Matakwa kwa Ajili ya Utumishi wa Betheli: Matakwa ya msingi kwa wale wanaojaza ombi kwa ajili ya utumishi wa Betheli yanaonyeshwa katika kisanduku chenye kuambatana na makala hii. Zaidi ya hayo, ni jambo la maana kwamba wawe na nia tayari ya kufanya kazi ngumu, wasiwe “wenye kuzipenda raha.” (2 Tim. 3:4; 1 Kor. 13:11) Washiriki wa familia ya Betheli wanapaswa kuwa wanaume na wanawake wa kiroho ambao wamekomaza mazoea mazuri ya funzo la kibinafsi na ambao wamezoeza nguvu zao za ufahamu ili “kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa pia.” (Ebr. 5:14) Ukomavu wao wa Kikristo unapaswa kuwa tayari umeonyeshwa katika sehemu zote za maisha, kutia ndani mavazi, kujipamba, na uchaguzi wao wa muziki na viburudisho. Washiriki wa familia ya Betheli wenye nia tayari hutumikia mahali popote wanapoweza kuhitajiwa. Mara nyingi, washiriki walio vijana zaidi hupewa migawo inayohusisha kazi yenye kuomba nguvu za kimwili, kutia ndani uchapishaji, utayarishaji na usafirishaji wa vichapo, utunzaji wa vifaa, ulinzi wa makao, usafishaji, ufuaji wa mavazi, na utayarishaji wa chakula. (Mez. 20:29) Hata hivyo, tofauti na kazi ya kilimwengu, kila mgawo hutokeza kutosheka kwingi kwa kuwa huo ni utumishi mtakatifu unaoletea Yehova utukufu.—Kol. 3:23.
14 Wale wanaoalikwa kwa ajili ya utumishi wa Betheli wanapaswa kukaa Betheli angalau mwaka mmoja. Hilo huwawezesha kupata mazoezi ili kuwa wafanyakazi wenye matokeo. Tumaini ni kwamba wataweza kufanya Betheli kuwa makao yao. Ni upendo kwa Yehova ndio huchochea washiriki wa familia ya Betheli waweke faida za Ufalme mbele ya faida zao wenyewe, jambo linalopendeza Yehova.—Mt. 16:24.
15 Mahitaji ya Sasa: Kwa sababu ya aina ya kazi inayofanywa kwenye Betheli, uhitaji tulio nao sasa ni wa akina ndugu waseja kwanza. Hata ikiwa hilo si takwa, wanaopendelewa zaidi ni wale walio mapainia wa kawaida, kwa kuwa tayari wako katika kazi ya wakati wote. Nyakati nyingine, kunaweza kuwa nafasi kwa ajili ya akina dada waseja na wenzi wa ndoa wenye umri wa kuanzia miaka 19 mpaka 35 ambao wanaweza kuwa na ufundi fulani-fulani unaohitajiwa kwenye Betheli. Kwa kuongezea, ndugu na dada fulani ambao huenda wakawa na umri wa zaidi kidogo ya miaka 35 na ambao wana ufundi mbalimbali au mazoezi ya pekee yanayoweza kutumiwa kwenye Betheli wanatiwa moyo wajaze ombi. Kwa mfano, hao wanatia ndani waganga wa meno, madaktari, watu wanaojulikana kuwa wenye kushughulika na akaunti, mafundi wa ujenzi, mainjinia, wauguzi, watengenezaji wa magari, au mafundi wa kielektroniki, na kadhalika. Lakini, hatutii watu moyo wapate elimu au mazoezi ya pekee, wakifikiri kwamba hilo litaongeza bahati yao ya kuitwa kwenye Betheli. Wale ambao tayari wamepata mazoezi ya pekee, labda kabla ya kuamini kweli, huenda wakataka kuandika kifupi chenye habari zote na kukitia pamoja na fomu kwa ajili ya utumishi wa Betheli.
16 Ikiwa unajaza ombi na kwamba haualikwi kutumikia kwenye Betheli, usivunjike moyo. Unaweza kufikiria kufanya upya ombi lako mara moja kila mwaka. Ndugu fulani wenye mazoezi au ufundi mbalimbali wa pekee unaoweza kuhitajiwa kwenye Betheli wamejitoa kwa ajili ya utumishi wa kujitolea kwa muda. Huenda wakajaza ombi ili kutumikia kwenye Betheli kwa muda—juma moja, majuma mawili, majuma matatu, au majuma manne au mpaka miezi mitatu. Mwandishi wa kutaniko anayo fomu ya ombi la wajitoleaji wa muda kwa ajili ya wale wanaopenda kusaidia katika njia hiyo. Maombi ya ziada ya wajitoleaji yanaweza kuombwa kwenye fomu Demande de publications.
17 Kutumikia Yehova katika ushirikiano wa karibu pamoja na ndugu za Kristo ni pendeleo la pekee kwa wale wanaotumikia kwenye Betheli. Baraza Linaloongoza linathamini ile roho ya kujinyima ya wale wote wanaojitoa ili kushughulikia mahitaji ya undugu wetu wa ulimwenguni pote.—Flp. 2:20-22; 2 Tim. 4:11.
18 Vijana—Jitayarisheni Sasa kwa Ajili ya Utumishi wa Betheli: Matayarisho kwa ajili ya utumishi wa Betheli huanza mbele kabisa ya kufikia kile kiwango cha chini zaidi cha umri wa miaka 19. Vijana wanaweza kufanya nini ili kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa Betheli? Yesu alisema: “Nani kati yenu atakaye kujenga mnara asiyeketi kwanza na kupiga hesabu ya gharama?” (Luka 14:28) Kwa kuwa matayarisho na kupanga mambo ni vya maana sana kwa ajili ya mafanikio ya mpango wowote wa ujenzi, ni jambo la maana kama nini kwa vijana kuwa waangalifu kuhusu jinsi wanavyojenga kwa ajili ya wakati wao ujao katika utumishi wa Yehova! Msingi wenye nguvu unapaswa kuwekwa mapema katika maisha ili wafikie miradi ya kiroho. Ukiwa kijana, wewe ni mwenye kuweka msingi mzuri kadiri gani? Ikiwa unataka kutumikia kwenye Betheli, utafaidika kwa kufikiria kwa uangalifu mambo yafuatayo.
19 ‘Fanyeni Nafasi’ kwa Ajili ya Pendeleo Hili la Pekee la Utumishi: Kama inavyoandikwa kwenye Mathayo 19:12, Yesu alitia wanafunzi wake moyo ‘wafanye nafasi’ kwa ajili ya useja. Kwa nini? Si kwa sababu za kibinafsi, lakini “kwa sababu ya ufalme wa mbingu.” Vivyo hivyo, Paulo alichochea “kuhudumia Bwana daima bila kukengeushwa.” (1 Kor. 7:32-35) Kwa kusikitisha, wengine hupoteza pendeleo la kutumikia wakiwa wanaume waseja kwenye Betheli kwa sababu ya kufuatia ndoa wakiwa na umri mdogo. Tunataka kutia moyo ndugu zetu vijana watumie nguvu zao katika kufuatia huduma ya wakati wote wanapokuwa bado hawana madaraka ya kifamilia. Kisha, ikiwa baada ya kipindi fulani cha wakati wanaamua kuoa, watakuwa waume bora zaidi kwa sababu watakuwa wamepata ujuzi zaidi katika maisha na katika huduma ya Kikristo. Baada ya kutumikia kwa miaka fulani kwenye Betheli, wengine wameoa, nao wamekuwa na uwezo wa kuendelea kutumikia kwenye Betheli wakiwa wenzi wa ndoa. Ikiwa baadaye wanapata mapendeleo mengine, kama vile kazi ya usafiri au utumishi wa mishonari, bila shaka hawajutii wakati walioweka kando ili kufanya nafasi kwa ajili ya utumishi wa Betheli.
20 Msikengeushwe na Ufuatiaji wa Vitu vya Kimwili: Ingekuwa vizuri kila kijana ajiulize: ‘Je, mradi wangu baada ya kumaliza shule ya juu ni kufuatia kazi-maisha ya kimwili ya wakati wote au ni kutumikia Yehova wakati wote?’ Ni kweli kwamba kuchagua kutumikia Yehova wakati wote kutaomba kujinyima. Lakini ni vivyo hivyo kuhusu kufuatia kazi-maisha ya kimwili! Mwishowe, ni mwendo gani utakaokuwa na matokeo yenye kudumu na yenye faida kwelikweli? Yesu alitoa jibu lililo wazi. Kulingana na Mathayo 6:19-21, yeye alisema: “Komeni kujiwekea akiba ya hazina duniani, ambako nondo na kutu hula kabisa, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala ya hivyo, jiwekeeni akiba ya hazina mbinguni, ambako wala nondo wala kutu haili kabisa, na ambako wezi hawavunji na kuiba. Kwa maana ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.” Mioyo yetu na isituchochee kamwe kufuatia kazi-maisha ya ulimwengu au mambo ya kimwili badala ya utumishi wa moyo wote kwa Yehova. Sisi sote tunapaswa kutambua kwamba hazina moja tu inayostahili kufuatiwa ni uhusiano mzuri pamoja na Yehova, kusudi tufurahishe moyo wake. (Mez. 27:11) Kwa kuweka Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu wakati tunapokuwa vijana, tunaonyesha ni mambo gani tunayothamini na jinsi Ufalme ulivyo wa maana kwetu. Kumbuka, “baraka ya Yehova inatajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.” (Mez. 10:22) Vijana wanayo nafasi bora ya kuonyesha mahali mioyo yao ilipo kwa kutoa kitu fulani kizuri kwa Yehova kwa sababu ya yale yote aliyowapa. Utumishi wa Betheli unatoa nafasi nzuri ajabu kama hiyo kwa wale wanaotimiza matakwa.
21 Wale Wanaotumikia Kwenye Betheli Wanapaswa Kuwa Safi Kiadili: Mtunga-zaburi aliuliza: “Kijana atasafisha njia yake namna gani?” Akajibu: “Kwa [kuwa macho], akifuata neno [la Yehova].” (Zab. 119:9) Hilo linaweza kutia ndani kuepuka jambo lolote linalohusiana na ufisadi wa kiadili wa mfumo wa mambo wa Shetani. Kutazama picha za umalaya kupitia Internet, mwenendo usiofaa pamoja na mtu wa jinsia tofauti, muziki na viburudisho vyenye kushusha heshima, na kunywa pombe mbele ya umri wenye kufaa ni mitego fulani tu kati ya ile mitego mingi ambayo Shetani anatumia ili kuzuia vijana wetu wasifikie miradi ya kiroho. Azimio lenye nguvu linahitajiwa ili kupinga mbinu hizo. Ikiwa wewe, ukiwa kijana, unajikuta ukihusika katika lolote la mambo hayo, zungumza na wazee katika kutaniko lako na utatue mambo hayo kabla ya wewe kujaza fomu kwa ajili ya utumishi wa Betheli. Kuwa na dhamiri safi ni jambo la maana sana ili kutumikia Yehova kikamili.—1 Tim. 1:5.
22 Jifunze Kupatana na Wengine: Takwa la maana kwa ajili ya kufanya utumishi wa Betheli ufanikiwe ni kujifunza kupatana na wengine. Familia ya Betheli katika Shirikisho la Amerika inaundwa na maelfu ya ndugu na dada kutoka hali zote za maisha. Ingawa nyutu hizo mbalimbali huongeza uzuri wa Betheli, hilo linaweza pia kutokeza matatizo nyakati nyingi. Ikiwa unafikiria utumishi wa Betheli, huenda ikawa vizuri ujiulize: ‘Je, ninaudhika kwa vyepesi wakati wengine wanapokuwa hawashiriki maoni yangu? Je, wengine huniona kuwa mwepesi kushirikiana naye?’ Ikiwa unahitaji kufanya maendeleo katika sehemu hizo, anza kutumika juu ya jambo hilo sasa. Kufanya hivyo kutakusaidia ujirekebishe ili kuzoea kwa vyepesi zaidi maisha na kazi pamoja na washiriki wa familia ya Betheli.
23 Jitahidi kuwa mtu wa kiroho kwa kukomaza uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Sitawisha programu nzuri ya funzo la kibinafsi, ambayo inaweza kutia ndani usomaji wa Biblia wa kila siku. Uwe mwenye kutenda kwa kushiriki habari njema na wengine. Kwa kutumikisha mambo hayo, utafanya maendeleo yako yawe wazi. (1 Tim. 4:15) Ni matazamio mazuri ajabu kama nini yanayongojea wale wanaojitayarisha sasa kwa ajili ya kazi-maisha katika utumishi wa wakati wote!
24 Wazazi, Zoezeni Watoto Wenu: Wazazi wanaweza kufanya nini ili kutia vijana moyo wafuatie huduma ya wakati wote? Yesu alisema: “Kila mtu aliyefunzwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.” (Luka 6:40, 41) Kwa kawaida, mwanafunzi aliyezoezwa kikamili ataonyesha zile sifa bora za mwalimu wake mwenye kujitolea. Kanuni hiyo inapaswa kufanya wazazi Wakristo wafikiri kadiri wanavyojitahidi kuzoeza watoto wao “ujitoaji-kimungu ukiwa shabaha [yao].” (1 Tim. 4:7) Kwa kuwa watoto wana mwelekeo wa kuonyesha mtazamo wa wazazi wao kuelekea mambo ya kiroho, itakuwa vizuri wazazi wajiulize: ‘Je, sisi binafsi tunathamini kazi inayofanywa kwenye Betheli ili kuendeleza faida za ibada ya kweli ya Yehova? Je, tunatambua baraka ya Yehova juu ya mpango wa Betheli? Je, tunaamini kwamba maisha katika utumishi wa Yehova ndio uchaguzi bora wa kazi-maisha ambao watoto wetu wanaweza kufanya?’ Uthamini wetu wenyewe wenye kutoka moyoni kuelekea utumishi wa Betheli na kazi inayofanywa huko utatusaidia tuingize uthamini wenye kufanana na huo ndani ya watoto wetu.
25 Elkana na Hana walikuwa na uthamini wenye kina kirefu kuelekea ibada ya kweli. Waliacha kwa wazazi Wakristo leo mfano wenye kustahili kuangaliwa. Katika Israeli ya kale, wanaume Waisraeli tu ndio walioombwa “kutokea mbele ya [Yehova] Mungu” mara tatu kwa mwaka kwenye tabenakulo. Hata hivyo, Elkana alisafiri karibu kilometa 30, yaelekea zaidi kwa mguu, pamoja na familia yake yote “mwaka kwa mwaka” ili kutoa dhabihu kwenye kitovu hicho cha ibada ya Yehova. (Kut. 23:17; 1 Sam. 1:3, 4, 9, 19; 2:19) Yaonekana kwamba baba huyo wa familia alitaka familia yake yote ishiriki upendezi aliokuwa nao kuelekea mambo ya kiroho.
26 Hana alishiriki kupendezwa kwa mume wake na ibada ya kweli. Alihisi sana wajibu wake wa kuchangia katika kutegemeza ibada ya kweli kwenye tabenakulo. Hana aliweka nadhiri kwamba ikiwa Yehova angempa mwana, yeye angetoa mwana huyo kwa ajili ya utumishi wa tabenakulo. (1 Sam. 1:11) Sheria ya Musa ilimpa mume ruhusa ya kufanya nadhiri isiyofaa ya mke wake isiwe na thamani yoyote. (Hes. 30:6-8) Lakini, yaonekana kwamba Elkana alikubaliana na nadhiri ya Hana, akionyesha kwamba yeye pia alitegemeza wonyesho huo wa ibada ya kweli!—1 Sam. 1:22, 23.
27 Je, mwana wao Samweli alipatwa na uvutano wenye kufaa kutokana na uthamini na mtazamo bora ulioonyeshwa na wazazi wake? Ndiyo, kwa kweli. Akiwa kijana mwanamume, Samweli alishughulikia kazi alizopewa kwa nia tayari na kwa uaminifu, naye alizoezwa kwa ajili ya mapendeleo zaidi yenye kufurahiwa katika utumishi wa Mungu. Kupendezwa ambako Elkana na Hana walionyesha kuhusiana na utumishi wa Samweli kwenye tabenakulo hakukumalizika baada ya yeye kutimiza wajibu wake mbalimbali huko. Waliendelea kumtembelea kwa ukawaida ili kumtia moyo na kumtegemeza kadiri alivyoendelea na utumishi wa wakati wote.—1 Sam. 2:18, 19.
28 Ni mfano wenye kutokeza kama nini ambao Elkana na Hana walitoa kwa wazazi Wakristo leo! Wakati watoto wetu wanaposikia uthamini wetu wenye kutoka moyoni kuelekea pendeleo la utumishi wa Betheli na kuona ile roho ya kujinyima tunayoonyesha katika kuendeleza faida za Ufalme, wao pia watakomaza moyo ulio na mwelekeo wa kuhudumia wengine. Wazazi wengi ni wenye kuingiza kwa mafanikio mwelekeo huo wenye kufaa ndani ya watoto wao. Binti mmoja mwenye umri wa miaka saba aliandika: “Ninataka kuwa kwenye Betheli wakati nitakapokomaa, nami nina mambo machache ambayo ningetaka kufanya huko. (1) Kuandika kwa mashini magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, (2) kutumika katika idara yenu ya sanaa, (3) kukunja mavazi yaliyofuliwa. Kazi yoyote itakayopatikana. Haidhuru.” Ni jambo lenye kufurahisha kama nini kuona roho kama hiyo yenye nia tayari ikikomaa ndani ya moyo wa watoto wetu!
29 Vijana, kumbukeni kwamba “ulimwengu unapitilia mbali . . . na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yn. 2:17) Endeleeni kufuatia miradi ya kiroho, kutia ndani pendeleo la pekee la utumishi wa Betheli. Wazazi, igeni mfano wa waaminifu wa kale waliotia watoto wao moyo wakomaze ujitoaji-kimungu. (2 Pet. 3:11) Na sisi sote, acheni tutimize fungu letu ili kusaidia ndugu na dada vijana watumikie Muumba wao Mtukufu kikamili zaidi iwezekanavyo, kwa kuwa hilo ‘lina ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.’—1 Tim. 4:8; Mhu. 12:1.
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 4]
Matakwa ya Msingi kwa Ajili ya Utumishi wa Betheli
● Kuwa mwenye kubatizwa tangu angalau mwaka mmoja
● Kuwa mtu wa kiroho aliye na upendo wenye kina kirefu kwa Yehova na kwa tengenezo lake
● Kuwa na afya nzuri kiroho, kiakili, kihisia-moyo, na kimwili
● Kuwa mwananchi au mkaaji mwenye kuishi kihalali Congo-Kinshasa au Congo-Brazzaville
● Kuwa na uwezo wa kusoma, kuandika, na kusema Kifaransa vizuri
● Kuwa na umri wa miaka 19-35