Kupanda kwa Wingi Kunaleta
Baraka Tele
1 Sisi sote tunangojea kwa hamu utimizo wa ahadi bora zinazopatikana katika Neno la Mungu. Hata sasa, Yehova anatutolea baraka nyingi zinazotuongezea furaha maishani. Hata hivyo, kiasi cha faida tunayopata kibinafsi kinategemea kwa kadiri kubwa jitihada tunayofanya. Kama mtume Paulo alivyoeleza, “yeye apandaye kwa wingi atavuna pia kwa wingi.” (2 Kor. 9:6) Fikiria sehemu mbili ambazo katika hizo kanuni hii inatumika.
2 Huduma Yetu Binafsi: Kushiriki habari njema na watu tunapokuwa na uwezo wa kutoa ushahidi kunathawabisha sana. (Mez. 3:27, 28) Jambo la kusifiwa
ni kwamba wahubiri wengi wanapanda kwa wingi kwa kuongeza kushiriki kwao katika huduma, wakitumikia wakiwa mapainia wasaidizi au wa kawaida. Sisi sote tunaweza kupanda kwa wingi kwa kurudi tukisukumwa na dhamiri ili kuendeleza kupendezwa kokote kunakopatikana na kupendekeza funzo la Biblia wakati wowote nafasi inapojitokeza. (Rom. 12:11) Kufanya bidii katika njia hizo kunatokeza mambo yaliyoonwa yenye kujenga na furaha yenye kuongezeka katika huduma yetu.
3 Kutegemeza Faida za Ufalme: Paulo alitoa maelezo yake kuhusu ‘kupanda kwa wingi’ kuhusiana na utoaji wa kimwili. (2 Kor. 9:6, 7, 11, 13) Leo, kuna mengi tunayoweza kufanya tukitumia nguvu na mali zetu ili kutegemeza faida za Ufalme. Tunaweza kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Tunaweza pia kujitolea ili kushiriki katika kusafisha na kutunza nafasi hizo za ibada ya kweli. Zaidi ya hilo, tunaweza kuchanga fedha kwa ajili ya gharama za kutaniko letu na vilevile kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Tunapotimiza sote fungu letu, tunafurahi kama nini kuona baraka tele za Yehova juu ya kazi hii iliyoamuriwa na Mungu!—Mal. 3:10; Luka 6:38.
4 Neno la Mungu linatuhimiza “kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki.” Tunapofuata shauri hilo, tunapata baraka tele sasa. Wakati ule ule, ‘tunajiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao na uhai ulio halisi’ unaokuja.—1 Tim. 6:18, 19.