Jivikeni Unyenyekevu
1 Mvulana mchungaji amtumaini Yehova na kumshinda mpiganaji mwenye nguvu. (1 Sam. 17:45-47) Mwanamume mwenye mali nyingi avumilia msiba. (Yobu 1:20-22; 2:9, 10) Mwana wa Mungu ampelekea Baba yake sifa zote zinazotokana na ufundishaji wake. (Yoh. 7:15-18; 8:28) Katika kila mmoja wa mifano hiyo, unyenyekevu ulitimiza fungu la maana sana. Vivyohivyo leo, unyenyekevu ni wa maana sana katika hali tunazopambana nazo.—Kol. 3:12.
2 Tunapohubiri: Tukiwa wahudumu Wakristo, tunashiriki kwa unyenyekevu habari njema na watu wa aina zote, bila kuwahukumu kimbele kwa msingi wa rangi, wa utamaduni, au wa malezi. (1 Kor. 9:22, 23) Ikiwa watu fulani ni wenye kukosa adabu au wanakataa kwa kiburi ujumbe wa Ufalme, hatuitikii kwa njia hiyohiyo lakini kwa uvumilivu tunaendelea kutafuta wale wanaostahili. (Mt. 10:11, 14) Badala ya kujaribu kufanya wengine waone ujuzi wetu au elimu yetu, tunaelekeza uangalifu kwa Neno la Mungu, tukijua kwamba ni lenye kusadikisha zaidi kuliko jambo lolote tunaloweza kusema. (1 Kor. 2:1-5; Ebr. 4:12) Kwa kuiga Yesu, tunampa Yehova sifa yote.—Marko 10:17, 18.
3 Katika Kutaniko: Wakristo wanapaswa pia ‘kujifunga hali ya akili ya kujishusha chini kuelekea mtu na mwenzake.’ (1 Pet. 5:5) Ikiwa tunawaona wengine kuwa wa hali ya juu kuliko sisi, tutatafuta njia za kutumikia ndugu zetu badala ya kuwatazamia wao watutumikie. (Yoh. 13:12-17; Flp. 2:3, 4) Hatutafikiri kwamba hatustahili kufanya kazi kama vile kusafisha Jumba la Ufalme.
4 Unyenyekevu unatusaidia ‘tuchukuliane mtu na mwenzake katika upendo’ na hivyo unaendeleza amani na umoja katika kutaniko. (Efe. 4:1-3) Unatusaidia tujitiishe kwa wale waliowekwa rasmi ili kuongoza. (Ebr. 13:17) Unatuchochea tukubali shauri au nidhamu yoyote tunayoweza kupewa. (Zab. 141:5) Na unyenyekevu unatuchochea tutegemee Yehova tunaposhughulikia mapendeleo yoyote tunayoweza kupokea katika kutaniko. (1 Pet. 4:11) Kama Daudi, tunatambua kwamba kufanikiwa hakutegemei uwezo wa kibinadamu lakini kunategemea baraka za Mungu.—1 Sam. 17:37.
5 Mbele za Mungu Wetu: Zaidi ya yote, tunahitaji ‘kujinyenyekeza chini ya mkono wa Mungu wenye uweza.’ (1 Pet. 5:6) Ikiwa tunapambana na hali zenye kujaribu, tunaweza kutamani sana kitulizo ambacho Ufalme utaleta. Lakini kwa unyenyekevu tunajizoeza uvumilivu, tukingojea Yehova atimize ahadi zake kwa wakati wake. (Yak. 5:7-11) Kama ilivyokuwa kweli kuhusu Yobu aliyeshika uaminifu wa maadili, hangaiko letu kubwa zaidi ni kwamba ‘jina la Yehova libarikiwe.’—Yobu 1:21.
6 Nabii Danieli ‘alijinyenyekeza mbele ya Mungu wake’ na alikubaliwa na Yehova na kupewa mapendeleo mengi bora. (Dan. 10:11, 12) Acheni sisi pia tujivike unyenyekevu, tukijua kwamba “zawabu ya unyenyekevu na woga wa BWANA ni mali na heshima na uzima.”—Mit. 22:4.