Shule ya Mazoezi ya Kihuduma—Mlango Mkubwa Unaoongoza Kwenye Utendaji
1 Kupitia nabii Yeremia, Yehova alitabiri: “Nami nitasimamisha juu ya [watu wangu] wachungaji ambao kweli watawachunga; nao hawataogopa tena, wala hawataingiwa na hofu yoyote, na hakuna hata mmoja atakayekosekana.” (Yer. 23:4) Kazi hiyo ya uchungaji ni yenye kutimizwa leo kati ya watu wa mataifa yote. Kazi hiyo ni yenye kufanywa na makumi ya maelfu ya wazee wa makutaniko. Kwa kuongezea, kundi la vijana walio wengi kama matone ya umande wamejitoa kwa kujitakia katika utumishi wa Yehova. (Zab. 110:3) Vijana hawa ni baraka kwelikweli kwa makutaniko ya watu wa Mungu. Kwa kuwa kazi ya ukusanyaji wa kiroho inaendelea, bado kuna uhitaji wa wanaume wenye kustahili walio na nia tayari ili kutumikia ndugu zao.
2 Mpango mzuri wa kuzoeza wazee na watumishi wa huduma waseja kwa ajili ya madaraka yenye kuongezeka ni Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Zaidi ya wanafunzi 22,000 kutoka nchi 140 hivi wamepata mazoezi haya katika madarasa 999 ambayo yamefanyika kuanzia mwaka wa 1987 wakati shule ilipoanzishwa. Kwa ndugu hao, shule imeonekana kuwa “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.”—1 Kor. 16:9.
3 Kusudi la Shule: Kusudi la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ni kuzoeza na kutayarisha wanaume wanaostahili kwa ajili ya madaraka mbalimbali mahali pote pale ambapo kunaweza kuwa uhitaji katika tengenezo. Shule inapanua uwezo wao wa kuchukua uongozi katika kazi ya kueneza evanjeli, kushiriki katika kazi ya uchungaji wa kundi, na kufundisha katika kutaniko. Baada ya kuhitimu au kupata vyeti, wanafunzi fulani wanapewa mgawo wa kutumika kama mapainia wa pekee au waangalizi wasafiri katika nchi zao au nchi nyingine. Wengine wanapewa migawo ya kutumika na makutaniko yao au maeneo ambapo kuna uhitaji mkubwa katika eneo linalosimamiwa na tawi lao.
4 Mnamo majuma manane ya masomo, wanafunzi wanajifunza sana Biblia. Wanachunguza kwa uangalifu sehemu nyingi za mafundisho ya Biblia kama vile madaraka ya uchungaji na miongozo kuhusu kushughulika na matatizo katika maisha ya Mkristo. Wanajifunza pia yale ambayo Maandiko yanafundisha kuhusu mambo ya usimamizi, ya hukumu, na ya kitengenezo. Wanapokea mazoezi kamili ya kusema mbele ya watu na wanapewa msaada wa kibinafsi wa kuharakisha maendeleo yao ya kiroho.
5 Matakwa: Kama inavyoweza kutazamiwa, matakwa ili kuhudhuria shule hiyo ni ya hali ya juu. Wale wanaotaka kujaza fomu wanapaswa kuwa wametumika kama wazee au watumishi wa huduma mnamo angalau miaka miwili ya kufuatana. Wote wanapaswa kuwa waseja na wenye umri wa miaka kati ya 23 na 50. Wanapaswa kujua kusoma, kuandika, na kusema bila magumu lugha katika hiyo shule inaongozwa, na wanapaswa kuwa na afya njema, na kutokuwa na uhitaji wa pekee katika mambo ya chakula au ya utunzaji. Wanaopendelewa kwanza ni wale walio katika utumishi wa upainia wa kawaida.
6 Wale wanaojitolea wanapaswa kuwa wenye kujipendea na kuwa na uwezo wa kutumika popote pale wanapohitajiwa. Jambo hilo linaomba mtu awe na mtazamo kama ule wa nabii Isaya, aliyejitoa kwa kupenda ili kufanya utumishi wa pekee, akisema: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Alionyesha pia unyenyekevu maisha yake yote. Wale walio tayari kwa ajili ya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wanapaswa kuchochewa na upendo kwa ajili ya ndugu zao na tamaa ya kuwatumikia badala ya kuchochewa na tamaa ya kuwa watu mashuhuri au walio tofauti na wengine. Baada ya kupata mazoezi hayo bora, wahitimu wanatazamiwa kutumia yale ambayo walijifunza ili kuwafaidi wengine.—Luka 12:48.
7 Faida: Mnamo majuma hayo manane ya mazoezi mazito, wahitimu ‘wanalishwa maneno ya imani na ya fundisho zuri.’ (1 Tim. 4:6) Hilo linawapa vifaa ili wastahili kusaidia na kutia moyo wengine katika makutaniko au mizunguko waliyogawiwa. Mahali pengi ambapo wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wamepewa mgawo, utumishi wa shambani umeongezeka; watu wanatiwa moyo kufanya utumishi wa painia, hasa vijana; na uangalifu wa kibinafsi umetolewa kwa wapya wengi wanaoshirikiana na watu wa Mungu.
8 Je, wewe ni mzee au mtumishi wa huduma mseja aliye na umri wa miaka kati ya 23 na 50? Kwa nini usifikirie kujaza fomu kuhusu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma? Je, wewe ni ndugu kijana aliye na miradi ya wakati ujao katika utumishi wa Yehova? Kwa nini usirahisishe maisha yako yasiwe na vikengeusha-fikira ili uweze kuingia katika “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji”? Hilo linaweza kukuletea furaha na kutosheka kwingi. Kwa kweli, Shule ya Mazoezi ya Kihuduma imeonekana kuwa baraka si kwa wahitimu wa shule tu lakini pia kwa makutaniko ya watu wa Mungu ulimwenguni pote.
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Jinsi Walivyofaidika na Mazoezi
“Mazoezi yameboresha kwelikweli huduma yangu na uwezo wangu wa kuchunga kundi kwa hekima, nikitumia Maandiko.”
“Shule imenitolea uhakika mwingi katika kushughulikia madaraka yangu mbalimbali katika kutaniko.”
“Imebadili karibu kila sehemu ya maisha yangu, kutia ndani maoni yangu kuhusu uongozi wa kitheokrasi na tengenezo la Mungu.”
“Mazoezi niliyopata yalinisaidia kutambua uhitaji wa kuwa tayari ili kutumika mahali ambapo kuna uhitaji.”