Saidia Wengine Wafaidike na Fidia Ukumbusho wa Kifo cha Kristo Utaadhimishwa Mnamo Aprili 12
1 “Mungu apewe shukrani kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.” (2 Kor. 9:15) Maneno hayo yanaonyesha vizuri jinsi tunavyojisikia kuhusu wema na fadhili zenye upendo ambazo Mungu anaonyesha watu wake kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. Kuthamini jambo hilo kutaonekana wazi hasa tutakapokusanyika pamoja mnamo Aprili 12 ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo.
2 Watu karibu milioni kumi wanahudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho kila mwaka pamoja na watumishi wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, wanaonyesha kuthamini dhabihu ya Kristo kwa kiasi fulani. Hata hivyo, ili wafaidike na fidia, wanapaswa kuonyesha kwamba wana imani katika fidia hiyo. (Yoh. 3:16, 36) Tunawezaje kuwasaidia ili wasitawishe imani hiyo? Mnamo majira haya ya Ukumbusho, tunaweza kuwatia moyo wawe na funzo la Biblia la nyumbani na kuhudhuria mikutano ya kutaniko ya kila juma. Fikiria mapendekezo yenye kufuata.
3 Mafunzo ya Biblia: Unapoalika kwenye Ukumbusho watu wenye kupendezwa, kwa nini usijaribu kuanzisha funzo la Biblia pamoja nao katika kitabu Biblia Inafundisha? Jaribu kumfasiria mtu kuhusu mwadhimisho wa Ukumbusho kwa kufungua kwenye ukurasa wa 206-208 na kuchunguza kichwa “Mlo wa Jioni wa Bwana—Maadhimisho Yanayomletea Mungu Heshima.” Mnaweza kuchunguza habari hiyo katika ziara moja au mbili, labda utafanya hivyo kama unavyoongoza funzo la Biblia ukiwa mwenye kusimama mlangoni. Mtakapomaliza habari hiyo, mtu anaweza kuwa tayari ili mzungumzie sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu.” Mara tu funzo la Biblia litakapokuwa limeanzishwa, rudieni nyuma na mchunguze sura nne za mwanzo katika kitabu.
4 Ni nani tunayeweza kuanzisha naye funzo la Biblia kwa kutumia utoaji huo? Labda watu fulani kati ya wafanyakazi wenzako, wanashule wenzako, au majirani watakubali mazungumzo hayo. Ndugu wanaweza kuongea na waume wasioamini wa akina dada katika kutaniko. Msisahau pia watu wa jamaa yenu wasio Mashahidi. Kwa kuongezea, tutapenda kufanya jitihada ya pekee ili kutolea mwaliko wa Ukumbusho wale ambao wakati mmoja walishirikiana kwa bidii na kutaniko. (Luka 15:3-7) Sisi na tujaribu kusaidia watu wote kama hao kufaidika na fidia.
5 Mikutano ya Kutaniko: Ukumbusho ndio mkutano wa maana unaohudhuriwa na wanafunzi wa Biblia wengi na watu wengine wenye kupendezwa. Hata hivyo, tunawezaje kuwatia moyo wahudhurie na kufaidika na mikutano mingine ya kutaniko? Huduma Yetu ya Ufalme ya Aprili 2005, ukurasa wa 8, inatoa mapendekezo yafuatayo: “Uwaelezee kichwa cha hotuba ya watu wote itakayotolewa. Waonyeshe habari itakayochunguzwa kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi na kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko. Zungumzia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Unapokuwa na mgawo kwenye shule, labda unaweza kufanya mazoezi pamoja nao. Shiriki pamoja nao mambo makuu yaliyotolewa kwenye mikutano. Tumia picha zinazopatikana katika vichapo vyetu ili kuwasaidia waone yale yanayofanyika. Kuanzia tu na funzo la kwanza uwaalike kuhudhuria mikutano.”
6 Watu wenye mioyo minyofu wanapojifunza Biblia kwa ukawaida na kuhudhuria mikutano ya kutaniko, mara nyingi wanafanya maendeleo ya kiroho kwa uharaka. Kwa hiyo, sisi na tutie wengine moyo wafaidike na mipango hiyo ya kiroho na kufaidika na zawadi bora zaidi kutoka kwa Mungu, yaani fidia.
[Maulizo ya Funzo]
1. Ni njia moja gani ambayo kwa hiyo watu wa Mungu wanaonyesha kwamba wanathamini fidia?
2. Ni nani wanaohudhuria mwadhimisho wa Ukumbusho pamoja na watumishi wa Yehova, nao wanahitaji kufanya nini ili kufaidika na fidia?
3. Tunawezaje kuanzisha funzo la Biblia na wale tunaoalika kwenye Ukumbusho?
4. Ni nani tunayeweza kuanzisha naye funzo la Biblia mnamo majira haya ya Ukumbusho?
5. Tunawezaje kutia moyo wanafunzi wa Biblia na watu wengine wenye kupendezwa wahudhurie mikutano ya kutaniko ya kila juma?
6. Ni katika njia mbili gani tunaweza kusaidia watu wenye mioyo minyofu wafaidike na fidia?