Je, Unauliza ili Ujulishwe Kuhusu Wale Wanaoweza Kukubali Kujifunza Biblia?
Ikiwa wewe ni mwenye kuongoza funzo la Biblia, kwa nini usiulize mwanafunzi ikiwa kuna yeyote kati ya marafiki zake, watu wa jamaa, au wengine anaojuana nao ambao wangependa kujua yale ambayo Biblia inafundisha? Mara nyingi wanafunzi watakutolea majina. Kwa ruhusa ya mwanafunzi, unaweza kutaja jina lake unapotembelea watu hao ili kuwatolea funzo la Biblia. Unaweza kusema, “[Jina la mwanafunzi] amefurahia kujifunza Biblia, na alifikiri kwamba wewe pia ungependa kufaidika na programu yetu ya funzo la Biblia ya bila malipo.” Kisha fanyeni onyesho fupi kuhusu jinsi funzo linavyoongozwa, mkitumia kitabu Biblia Inafundisha.
Ikiwa una mwanafunzi anayefanya maendeleo bora, unaweza kumtia moyo kuelezea mpango wa funzo kwa marafiki na washiriki wa familia ambao wangependezwa. Anaweza kuwaalika wahudhurie anapojifunza. Au ikiwa hilo halifai, anaweza kufanya mpango ili wewe ukutane nao ili kuwaonyesha namna funzo linavyofanywa. Kufanya hivyo kutatia mwanafunzi moyo aanze kuelezea wengine kuhusu ujuzi wake wa Biblia.
Unaweza kuuliza pia wale unaorudilia kwa kawaida ikiwa wanaweza kukupatia majina ya watu ambao wangependa kufaidika na funzo la Biblia, hata ikiwa wao wenyewe hawajakubali funzo la Biblia la kawaida. Unapowatolea nakala ya kitabu Biblia Inafundisha, unaweza tu kuuliza, “Je, unajua mtu mwingine yeyote ambaye angeweza kupendezwa kupata kitabu hiki?”
Kwa sababu ya uharaka wa nyakati tunamoishi, tunataka kutumia kila nafasi iwezekanayo ili kusaidia watu wasikie na kukubali habari njema. Je, unauliza ili ujulishwe kuhusu wale wanaoweza kukubali kujifunza Biblia?