Rudilia Wale Wote Wanaoonyesha Kupendezwa
1 Wengi wetu tuko katika kweli leo kwa kuwa mtu fulani alitambua kwamba tulipendezwa na ujumbe wa Ufalme na kwa uvumilivu akarudi, labda mara nyingi, ili kutusaidia tupendezwe zaidi. Sisi vilevile tunapaswa kurudilia kwa bidii wale wote wanaonyesha kupendezwa kwa kiasi fulani. Kwa kweli, kurudilia watu ni sehemu ya kazi tuliopewa ya “kufanya wanafunzi.”—Mt. 28:19, 20.
2 Tambua Ikiwa Mtu Anapendezwa: Hata ikiwa mtu anakataa kuchukua kitabu, ishara yake ya uso, sauti yake na maneno anayotumia vinaweza kutuonyesha ikiwa anapendezwa na ujumbe wa Ufalme kwa kiasi fulani. Kwa sababu ya jambo hilo tunaweza kupanga kumrudilia. Ndugu mmoja alimtembelea mtu kwa majuma matano yenye kufuatana bila mtu huyo kukubali kitabu. Alipomrudilia kwa mara ya sita, mtu huyo alikubali kitabu na mwishowe funzo la Biblia likaanzishwa.
3 Ukitambua kwamba mtu anapendezwa, rudi bila kukawia, labda kisha siku chache. Usimpe “yule mwovu” nafasi ya kuondoa kile ambacho kimepandwa moyoni mwa mtu. (Mt. 13:19) Uwe hakika kwamba unatimiza ahadi yako ikiwa ulifanya naye mipango ya kurudi tena.—Mt. 5:37.
4 Unapohubiri Barabarani: Je, unajikaza kurudilia watu walioonyesha kupendezwa ulipohubiri barabarani au ulipohubiri ijapokuwa haukupanga kufanya hivyo? Mwishoni mwa mazungumzo yenu unaweza kusema: “Nilifurahia mazungumzo yetu. Tunaweza kukutana wapi ili tuweze kuzungumza tena?” Inapofaa, wahubiri fulani wanaweza kuchagua kuwapa watu wanaopendezwa namba yao ya telefone au kuwaomba nao pia wawape namba yao. Ikiwa watu wanakuona ukihubiri barabarani mahali palepale kwa kawaida, labda hawatapendezwa kukupa namba yao ya telefone au kukujulisha mahali wanapoishi. Ijapokuwa wanakataa kukuambia namna unaweza kuwaona tena, unaweza kujikaza ili kuwasaidia wapendezwe zaidi unapowakuta barabarani wakati mwingine.
5 Ni jambo lenye kufurahisha tunapoona mimea ambayo tulipanda na kutilia maji inakomaa. Vivyo hivyo, tunaweza kupata furaha nyingi kwa kurudilia watu na kuwasaidia wafanye maendeleo ya kiroho. (1 Kor. 3:6) Fanya kusudi lako liwe kurudilia watu ambao wanaonyesha kupendezwa kwa kiasi fulani.