Fuateni Mfano wa Kristo Katika Kazi Yenu ya Kuhubiri
1 Yesu alituachia mfano wa kufuata katika kazi yetu ya kuhubiri. Alionyesha upendo mwingi kwa Mungu na kwa watu katika pindi nyingi na kwa namna nyingi. Alifundisha wapole ile kweli na aliwatendea wema wale waliokuwa wakiteseka na kulemewa.—Mt. 9:35.
2 Mfano na Mafundisho ya Yesu: Yesu hakukengeushwa akili kwa kujiingiza katika mambo ya politike au kujitia katika mambo ya kutolea watu misaada ili kufanya maisha yao yawe mazuri. Wala hakuruhusu ufuatiaji wa mambo mengine yenye kuonekana kuwa yanafaa yamukengeushe au yachukue nafasi ya kazi yake ya maana. (Luka 8:1) Alitilia mkazo kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, akionyesha kwamba Ufalme huo tu ndio utakaomaliza kabisa matatizo ya wanadamu. Yesu alikuwa na kazi ya maana ya kufanya na alipaswa kufanya kazi hiyo katika wakati kidogo. Watu wa Kapernaumu walipopenda Yesu abaki huko, aliwaambia wanafunzi wake: “Twendeni mahali pengine . . . ili nipate kuhubiri huko pia, kwa maana nilitoka kwa kusudi hilo.”—Marko 1:38.
3 Baada ya kuzoeza wanafunzi wake, Yesu aliwatuma na maagizo haya yaliyo wazi: “Hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:7) Alifundisha wanafunzi wake kwamba wangepaswa kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza katika maisha yao. (Mt. 6:33) Maneno ya Yesu ya mwisho ambayo aliwaambia wanafunzi wake mbele ya kupanda mbinguni, yalionyesha wazi mambo ambayo walipaswa kufanya. Alisema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—Mt. 28:19.
4 Kwa Nini Ufalme Ni wa Maana: Ufalme wa Mungu ulikuwa kichwa kikuu cha mazungumzo ya Yesu, na alitia moyo wanafunzi wake kufuata mfano wake. Ijapokuwa wanajikaza, wanadamu hawana uwezo wa kumaliza matatizo yao. (Yer. 10:23) Ni Ufalme wa Mungu tu ndio utatakasa jina la Mungu na kutuliza milele mateso ya wanadamu. (Mt. 6:9, 10) Kufundisha kweli za Ufalme watu “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanywa” kunawasaidia kuishi maisha yenye kufanikiwa na yenye furaha leo na kushikamana na tumaini la wakati ujao lililo hakika.—Ezek. 9:4.
5 Yesu anaendelea kutusaidia katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, na anatuhakikishia kwamba atatutegemeza. (Mt. 28:20) Ni kwa kadiri gani kazi yetu ya kuhubiri inalingana na mfano ambao Yesu alituachia? (1 Pet. 2:21) Katika siku hizi za mwisho zilizo za maana sana, na tufanye kila jambo tuwezalo ili kufuata mfano ambao Yesu alituachia kuhusu kazi ya kuhubiri!