Endeleeni “Kuzaa Matunda Mengi”
1 Akitumia maneno ya ufananisho, Yesu alijifananisha na mzabibu wa kweli, alifananisha Baba yake na Mlimaji, na wafuasi wake waliotiwa mafuta aliwafananisha na matawi ya mzabibu yenye kuzaa matunda mengi. Akieleza kazi ya Mlimaji wa ufananisho, Yesu alikazia umaana wa kubaki wenye kushikamana sana na mzabibu. (Yoh. 15:1-4) Tunajifunza kwamba kila mtu mwenye kufanya urafiki wa karibu na Yehova anapaswa kuwa kama tawi lenye kuzaa matunda mengi la “mzabibu wa kweli”, yaani Yesu Kristo. Tunapaswa kuendelea kuzaa kwa wingi “matunda ya roho” na matunda ya Ufalme.—Gal. 5:22, 23; Mt. 24:14; 28:19, 20.
2 Matunda ya Roho: Jambo linaloonyesha kabisa kwamba tunafanya maendeleo ya kiroho ni jinsi tunavyojikaza kuonyesha matunda ya roho. Je, unajikaza kuzaa matunda ya roho ya Mungu kwa kujifunza kikawaida na kufikiri sana juu ya Neno la Mungu? (Flp. 1:9-11) Usisite kuomba roho takatifu katika sala, roho ambayo inaweza kutokeza ndani yako sifa zenye kumtukuza Yehova na kukusaidia uendelee kufanya maendeleo ya kiroho.—Luka 11:13; Yoh. 13:35.
3 Kukomalisha matunda ya roho kutatusaidia pia kutumika kwa bidii zaidi katika kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, upendo na imani vinatuchochea kupanga wakati wa kuhubiri kwa ukawaida, hata ikiwa tuna mambo mengi ya kufanya. Sifa kama vile amani, uvumilivu, fazili, upole, na kujizuia, zinatusaidia kutendea inavyofaa wale wenye kutupinga. Furaha inatuwezesha kutosheka katika kazi ya kuhubiri hata ikiwa watu hawapendezwi na habari.
4 Matunda ya Ufalme: Tunataka pia kuzaa matunda ya Ufalme. Hilo linatia ndani ‘zabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina la Yehova tangazo la hazarani.’ (Ebr. 13:15) Tunafanya hivyo kwa kutangaza habari njema kwa bidii na bila kuacha. Je, munajikaza kuzaa matunda ya Ufalme mengi zaidi kwa kufanya kazi yenu ya kuhubiri iwe nzuri zaidi?
5 Yesu alionyesha kwamba wafuasi wake waaminifu wangezaa matunda kwa kiasi tofauti tofauti. (Mt. 13:23) Kwa hiyo, hatupaswi kujilinganisha na wengine, lakini tunapaswa kumtolea Yehova yaliyo mema. (Gal. 6:4) Kuchunguza kweli kweli hali zetu tukitumia Neno la Mungu, kutatusaidia kuendelea kumtukuza Yehova kwa “kuzaa matunda mengi.”—Yoh. 15:8.