Sisi Wote Tuna Kitu Fulani cha Kumtolea Yehova
1 Je, unajua kwamba wanadamu wanaweza kumtolea Mungu kitu fulani? Abeli alimtolea Yehova zabihu za wanyama fulani wazuri zaidi katika mifugo yake; Noa na Ayubu pia walitoa zabihu za namna hiyo. (Mwa. 4:4; 8:20; Ayu. 1:5) Kwa kweli, zabihu kama hizo hazikumtajirisha Muumba hata kidogo, kwa kuwa vitu vyote ni vyake. Lakini zabihu hizo zilionyesha kwamba wanaume hao waaminifu walimpenda Mungu sana. Leo, tunaweza kutumia wakati wetu, nguvu zetu na mali zetu za kimwili ili kumtolea Yehova ‘zabihu ya sifa.’—Ebr. 13:15.
2 Wakati Wetu: Ni jambo la kusifiwa sana ‘kujinunulia’ wakati tunaotumia kufanya mambo yasiyo ya maana sana ili kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri! (Efe. 5:15, 16) Labda tunaweza kubadili programu yetu ili kufanya upainia msaidizi mwezi mmoja ao zaidi katika mwaka. Labda tunaweza kuongeza wakati ambao tunazoea kutumia katika kazi ya kuhubiri. Kwa kuhubiri dakika 30 za zaidi kila juma, tunaweza kuongeza saa mbili hivi kwenye ripoti yetu ya kila mwezi!
3 Nguvu Zetu: Ili kupata nguvu za kutumia katika kazi ya kuhubiri, tunahitaji kuepuka mambo ya kujifurahisha yenye kuchosha mwili na kazi zinazotuchosha na kutufanya tusiweze kumtolea Yehova yaliyo mema zaidi. Ni lazima pia tuepuke mahangaiko ambayo yanaweza kufanya moyo wetu “uiname” na kutuiba nguvu ambazo tungeweza kutumia katika kumtumikia Mungu. (Met. 12:25) Hata ikiwa tuna sababu nzuri ya kuhangaika, ni vizuri zaidi ‘tumtupie Yehova mzigo wetu’!—Zab. 55:22; Flp. 4:6, 7.
4 Mali Zetu za Kimwili: Tunaweza pia kutoa mali zetu za kimwili ili kutegemeza kazi ya kuhubiri. Paulo aliwatia moyo Wakristo wenzake ‘waweke kando kitu fulani’ kwa ukawaida ili wapate kitu fulani cha kutolea wale walio na uhitaji. (1 Kor. 16:1, 2) Katika njia hiyohiyo, tunaweza kujichungia feza fulani za kutoa kwa ajili ya mahitaji ya kutaniko letu na kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Yehova anapendezwa na yale tunayotoa kwa moyo wote, hata kama ni kitu kidogo tu.—Luka 21:1-4.
5 Yehova ametupatia vitu vingi. (Yak. 1:17) Tunaonyesha shukrani yetu kwa kutoa kwa moyo mwema wakati wetu, nguvu zetu na mali zetu zingine za kimwili ili kumtumikia. Tunapofanya hivyo, tunampendeza Yehova, “kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”—2 Kor. 9:7.