“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
1. Kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” kilichapishwa kwa kusudi gani?
1 Tunatazamia kwa hamu sana kujifunza kitabu kipya chenye kichwa “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” kwenye Funzo la Biblia la Kutaniko kuanzia juma tokea tarehe 23 mwezi wa 2, katika Kifaransa na Kiswahili. Barua inayopatikana mwanzoni mwa kitabu hicho, barua ambayo Baraza Linaloongoza liliandikia kila mutu anayempenda Yehova ilimalizia kwa maneno yafuatayo: “tunatumaini kwamba kitabu hiki kitakusaidia kuendelea kutumia kweli maishani mwako na hivyo kujitunza mwenyewe ‘katika upendo wa Mungu . . . kwa kutazamia uzima wa milele.’—Yuda 21.”
2. Kitabu hicho kipya, kitatusaidia katika sehemu gani za maisha?
2 Mambo Tutakayofikiria: Namna gani kanuni za Biblia zinatumiwa katika sehemu za maisha kama vile urafiki, kujiburudisha, kuheshimu mamlaka, tabia za mutu, ndoa, usemi, na desturi? Zamiri zetu zitazoezwa kulingana na kanuni za haki za hali ya juu zilizo katika Neno la Mungu. (Zab. 19:7, 8) Tunapoelewa zaidi namna ya kufikiri ya Yehova, tutakusudia sana kumpendeza, na hilo litatuchochea kuwa watiifu katika sehemu zote za maisha.—Met. 27:11; 1 Yoh. 5:3.
3. Kwa nini tunapaswa kujikaza kutoa maelezo kwenye funzo la kila juma?
3 Kusudia Kabisa Kutoa Maelezo: Unapojitayarisha, kusudi lako liwe kumsifu Mungu kati ya watu wake wenye kukusanyika. (Ebr. 13:15) Kutaniko nzima litakutana pamoja ili kujifunza kitabu hicho kipya. Kwa kuwa sehemu ya kujifunza ya kila juma itakuwa ndogo, hilo litatuwezesha sisi wote kujitayarisha vizuri, na bila kusita, tutatoa maelezo ya mambo ambayo tumejifunza. Maelezo yetu yenye kutayarishwa vizuri na yaliyo wazi, yatachochea wengine katika upendo na matendo mazuri na kufanya habari ya funzo izungumziwe kwa njia changamfu na yenye kuelimisha. (Ebr. 10:24) Pia, tunaweza kupata furaha nyingi tunapotoa maelezo kuhusu imani yetu.
4. Kwa nini ni lazima tutii amri za Yehova?
4 Usiku wa mwisho wa maisha yake hapa duniani akiwa mwanadamu, Yesu alieleza kwamba ni lazima kutii amri za Yehova ili kuendelea kujitunza katika upendo wa Mungu. (Yoh. 15:10) Kitabu “Upendo wa Mungu” kitatusaidia tukusudie zaidi kutumia kanuni za Biblia katika maisha yetu ya kila siku na ‘kujitunza katika upendo wa Mungu.’—Yuda 21.