HABARI YA KUJIFUNZA YA 12
WIMBO 119 Tunapaswa Kuwa na Imani
Endelea Kutembea kwa Imani
“Tunatembea kwa imani, hapana kwa kuona.”—2 KO. 5:7.
WAZO KUBWA
Namna ya kuendelea kutembea kwa imani wakati tunakamata maamuzi ya maana.
1. Juu ya nini Paulo alifurahi wakati alifikiria namna alitumia maisha yake?
WAKATI fulani, mutume Paulo alijua kama balikuwa kumuua. Lakini alifurahi wakati alifikiria namna alitumia maisha yake. Njo maana alisema hivi: “Nimekimbia mbio mupaka mwisho, nimeshika imani.” (2 Ti. 4:6-8) Paulo alikamata maamuzi ya hekima mu utumishi wake kwa Yehova. Na alikuwa hakika kama Yehova alimufurahia. Na siye tunapenda kukamata maamuzi ya muzuri na kukubaliwa na Yehova. Tunaweza kufanya vile namna gani?
2. Kutembea kwa imani maana yake nini?
2 Paulo alisema hivi juu yake na juu ya Wakristo wengine waaminifu: “Tunatembea kwa imani, hapana kwa kuona.” (2 Ko. 5:7) Paulo alipenda kusema nini? Mu Biblia neno ‘kutembea,’ inatumiwa wakati fulani juu ya kuzungumuzia namna mutu anatumia maisha yeke. Wakati mutu anatembea kwa kuona tu, anakamata maamuzi yenye inategemea mambo yenye anaweza kusikia, kuona, ao namna anajisikia. Lakini wakati mutu anatembea kwa imani, anakamata maamuzi yenye inaonyesha kama anamutegemea Yehova. Matendo yake inaonyesha kama iko hakika kama Mungu atamubariki, na kama kufuata mashauri ya Yehova yenye kuwa mu Neno yake, kutamuletea faida.—Zb. 119:66; Ebr. 11:6.
3. Kutembea kwa imani kunaleta faida gani? (2 Wakorinto 4:18)
3 Wakati fulani siye bote tunakamataka maamuzi yenye inategemea namna tunajisikia, mambo yenye tunaona, ao mambo yenye tunasikia. Lakini kukamata maamuzi ya maana kwa kutegemea tu mambo yenye tunaona ao kusikia, kunaweza kutuletea magumu. Juu ya nini? Juu wakati fulani macho na masikio yetu inaweza kutudanganya. Hata kama haitudanganye, kama tunakamata maamuzi kwa kutegemea tu mambo yenye tunaona, tunaweza kuanza kutia pembeni mashauri ya Mungu. (Muh. 11:9; Mt. 24:37-39) Lakini kama tunatembea kwa imani, inawezekana kabisa tukamate maamuzi yenye “kukubaliwa kwa Bwana.” (Efe. 5:10) Kufuata mashauri ya Mungu kutatusaidia tukuwe na amani ya moyo na kutatuletea furaha ya kweli. (Zb. 16:8, 9; Isa. 48:17, 18) Na kama tunaendelea kutembea kwa imani, tutapata uzima wa milele wakati wenye kuya.—Soma 2 Wakorinto 4:18.
4. Mutu anaweza kujua namna gani kama iko natembea kwa imani ao kwa kuona?
4 Sasa, tutajua namna gani kama tuko natembea kwa imani ao kwa kuona? Juu tujue, ni muzuri tujiulize hii maulizo: Maamuzi yangu inategemea nini? Inategemea mambo yenye ninaona, ao inategemea mashauri ya Yehova? Tuone basi namna tunaweza kuendelea kutembea kwa imani mu hii mambo tatu ya maana: Wakati tunachagula kazi, wakati tunachagula mutu wa kuoana naye, na wakati tengenezo inatutolea muongozo. Mu hii mambo yote tatu tutafikiria mambo yenye tunapaswa kuchunguza juu tuweze kukamata maamuzi ya muzuri.
WAKATI TUNACHAGULA KAZI
5. Tunapaswa kufikiria nini wakati tuko nachagula kazi?
5 Siye bote tunapendaka kuwa na kazi yenye itatusaidia kutimiza mahitaji yetu na ya batu ya familia yetu. (Muh. 7:12; 1 Ti. 5:8) Kazi fulani zinalipaka muzuri. Zinaweza kusaidia mutu atimize mahitaji yake ya kila siku na anaweza hata kuweka makuta fulani pembeni. Lakini kazi zingine zinalipaka makuta ya kidogo ya kusaidia tu kupata mambo yenye familia iko nayo lazima. Wakati tuko naamua ikiwa tutakubali kazi fulani ao hapana. Ni jambo ya kawaida kufikiria tutakuwa napata makuta ngapi. Lakini kama ile tu njo jambo yenye tunafikiria mbele ya kukamata uamuzi, ile itaonyesha kama tuko natembea kwa kuona.
6. Namna gani tunaweza kutembea kwa imani wakati tuko nachagula kazi? (Waebrania 13:5)
6 Kama tunatembea kwa imani, tutafikiria pia matokeo yenye kazi itakuwa nayo juu ya uhusiano wetu pamoya na Yehova. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Hii kazi itaniomba nifanye mambo yenye Yehova anachukia?’ (Mez. 6:16-19) ‘Itanizuia kufanya mambo fulani ya kiroho, na pengine kufanya nikuwe mbali na familia yangu kwa wakati murefu?’ (Flp. 1:10) Kusema kweli haikuwake mwepesi kupata kazi. Lakini kama unajibia ndiyo hata ku ulizo moya kati ya ile maulizo, ni jambo ya hekima usikubali ile kazi. Juu tunatembea kwa imani, tunakamata maamuzi yenye inaonyesha kama tuko hakika kama Yehova atatupatia mambo yenye tuko nayo lazima.—Mt. 6:33; soma Waebrania 13:5.
7-8. Namna gani ndugu fulani wa mu Amerika ya Kusini alitembea kwa imani? (Ona pia picha.)
7 Javier,a ndugu wa mu Amerika ya Kusini aliona kama ni jambo ya maana kutembea kwa imani. Anasema hivi: “Niliomba kazi fasi kwenye ningepata mushahara mara mbili kupita yenye nilikuwa napata, na ni kazi yenye nilipenda.” Lakini Javier alipenda kuwa painia. Anaendelea kusema hivi: “Mukubwa fulani wa ile kazi alipaswa kuzungumuza na miye kwanza. Lakini mbele ya ile mazungumuzo, nilisali kwa Yehova anisaidie. Nilikuwa hakika kama Yehova njo alijua mambo yenye ingeniletea furaha. Ni kweli kama nilipenda kuwa na cheo mu kazi na kupata makuta ya mingi, lakini sikupenda kukubali kazi yenye itanizuia kufikia miradi yangu ya kiroho.”
8 Javier anasema tena hivi: “Wakati wa mazungumuzo, ule mukubwa wa kazi aliniambia kama mara mingi nitakuwa natumika kisha saa za kazi. Kwa upole nilimuambia kama singeweza kufanya vile juu ya utumishi wangu kwa Yehova.” Javier alikatala ile kazi. Kisha majuma mbili alianza kazi ya upainia. Na kisha wakati fulani mu ile mwaka, alipata kazi yenye haikumukamata wakati mingi. Anasema hivi: “Yehova alisikiliza sala zangu, na alinisaidia nipate kazi yenye inapatana na programu yangu ya upainia. Niko mwenye furaha sana kuwa na kazi yenye inanipatia wakati zaidi ya kumutumikia Yehova na ndugu zangu.”
Kama banapenda kukupandisha cheo ku kazi, uamuzi wako utaonyesha kama uko hakika kama ni Yehova njo anajua jambo ya muzuri kwako? (Ona fungu ya 7-8)
9. Mufano wa Tresor unakufundisha nini?
9 Utafanya nini kama unatambua kama kazi yenye uko nayo inakuzuia kutembea kwa imani? Fikiria mufano wa Tresor wa mu Congo. Anasema hivi: “Kazi ya mupya yenye nilipata ni kazi yenye sikuwaziaka kama nitakuwa nayo. Nilikuwa napokea mara tatu makuta yenye nilikuwaka napokea mu kazi yangu ya zamani, na watu waliniheshimia sana.” Lakini mara mingi Tresor alikuwa nakosa mikutano juu alikuwa natumika kisha saa za kazi. Pia walimukaza aseme uongo juu afiche mambo fulani ya mubaya yenye ilikuwa nafanyika mu kazi. Tresor alipenda kuacha ile kazi, lakini aliogopa kama hatapata kazi ingine. Nini njo ilimusaidia? Anasema hivi: “Habakuki 3:17-19 ilinisaidia kuelewa kuwa hata kama ninapoteza kazi, Yehova atajua namna ya kunihangaikia. Kwa hiyo, niliacha ile kazi.” Anamalizia hivi: “Wakubwa wengi wa kazi wanawaza kama ikiwa mutu iko na kazi ya makuta mingi, anaweza kuwa tayari kutia pembeni kila kitu, hata wakati yenye angepitisha pamoya na familia ao mu mambo ya kiroho. Ninafurahi juu nililinda uhusiano wangu pamoya na Yehova na pamoya na watu wa familia yangu. Kisha mwaka moya, Yehova alinisaidia kupata kazi ya muzuri yenye inaniwezesha kuwa na maisha mwepesi na kupitisha wakati mingi mu mambo ya kiroho.” Wakati tunatia mambo ya kiroho fasi ya kwanza mu maisha yetu, tunaweza kuwa na matatizo ya kupata makuta kwa wakati fulani, lakini Yehova atatuhangaikia. Kama tunafuata mashauri ya Yehova na kutumainia ahadi zake, tutaendelea kutembea kwa imani na Yehova atatubariki.
WAKATI TUNACHAGULA MUTU WA KUOANA NAYE
10. Ni mambo gani ya maana ya kufikiria wakati wa kuchagula mutu wa kuoana naye, lakini tunapaswa kuwa waangalifu na jambo gani?
10 Ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova. Kwa hiyo ni jambo ya kawaida mutu kupenda kuoa ao kuolewa. Wakati dada iko nafikiria ndugu wa kuoana naye, anaweza kufikiria utu wa ule ndugu, namna anaonekana, namna wengine wanamuonaka, namna anatumikishaka makuta, ikiwa yeye njo anashugulikiaka batu fulani mu familia yake, na dada anaweza pia kufikiria ikiwa anajisikiaka muzuri wakati iko na ule ndugu.b Ile mambo ni ya maana, lakini kama ile mambo tu njo dada anafikiria, ile inaweza kuonyesha kama iko natembea kwa kuona.
11. Namna gani tunaweza kutembea kwa imani wakati wa kuchagua mutu wa kuoana naye? (1 Wakorinto 7:39)
11 Yehova anafurahi sana wakati ndugu ao dada anafuata mashauri yake wakati iko nachagula mutu wa kuoana naye. Kwa mufano, anafuata shauri ya kungoya “kipindi cha ujana” ipite mbele ya kuanza urafiki wa kimapenzi. (1 Ko. 7:36) Wakati iko nachagula mutu wa kuoana naye, jambo ya maana zaidi yenye anafikiria ni ikiwa ule mutu iko na sifa zenye Yehova anaomba bwana muzuri ao bibi muzuri akuwe nazo. (Mez. 31:10-13, 26-28; Efe. 5:33; 1 Ti. 5:8) Ikiwa mutu mwenye haiko Shahidi anamupenda, ule ndugu ao dada anafuata shauri ya kuoa ao kuolewa “katika Bwana tu,” yenye kuwa mu 1 Wakorinto 7:39. (Soma.) Anaendelea kutembea kwa imani na kuwa hakika kama sikuzote Yehova atamuhangaikia na kumusaidia ajisikie muzuri.—Zb. 55:22.
12. Mufano wa Rosa unakufundisha nini?
12 Fikiria mufano wa Rosa, painia wa mu Kolombia. Kazi yake ilifanya akutane mara kwa mara na mwanaume fulani mwenye haiko Shahidi mwenye alianza kumupenda. Rosa pia alimufurahia. Rosa anasema hivi: “Alionekana kuwa mwanaume muzuri, alikuwa nasaidia batu mu eneo yake, na alikuwa naishi maisha ya muzuri. Nilifurahia namna alinitendea. Alikuwa na mambo yote yenye ningependa bwana yangu akuwe nayo. Alikosa tu kitu moya, hakukuwa Shahidi.” Rosa anasema tena hivi: “Ilikuwa nguvu kumuambia hapana, juu mu moyo, na miye nilikuwa namufurahia. Ile wakati nilikuwa najisikia kuwa peke yangu. Na nilipenda kuolewa. Lakini sikupata ndugu mwenye ninafurahia.” Hata vile, Rosa hakukazia tu akili mambo yenye alikuwa naona. Alifikiria matokeo yenye uamuzi wake ungekuwa nao juu ya urafiki wake pamoya na Yehova. Kwa hiyo, aliachana kabisa na ule mwanaume na akaendelea kufanya mambo mingi mu utumishi wake kwa Yehova. Kisha wakati kidogo alialikwa ku masomo ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Na sasa iko painia wa pekee. Rosa anasema hivi: “Yehova amenibariki sana, na ile imeniletea furaha mingi.” Wakati jambo fulani yenye tunapenda haipatane na mapenzi ya Yehova, ni nguvu kutembea kwa imani, lakini kutembea kwa imani kunaletaka tu baraka.
WAKATI TENGENEZO INATUTOLEA MUONGOZO
13. Wakati tengenezo inatupatia muongozo, nini njo inaweza kuonyesha kama tunatembea kwa kuona?
13 Mara mingi tunapataka muongozo juu tuweze kumutumikia Yehova muzuri. Ile muongozo inatoka kwa wazee, waangalizi wa muzunguko, biro ya tawi, ao Baraza Yenye Kuongoza. Lakini tutafanya nini kama hatuelewe juu ya nini tunapewa muongozo fulani? Pengine tunaweza kuanza kuona tu matokeo ya mubaya yenye ule muongozo unaweza kuwa nao. Na hata, tunaweza kuanza kukazia akili uzaifu wa ndugu wenye wanatupatia muongozo.
14. Ni nini itatusaidia tetembee kwa imani wakati tengenezo inatutolea muongozo? (Waebrania 13:17)
14 Wakati tunatembea kwa imani, tuko hakika kama ni Yehova njo anaongoza tengenezo yake, na anajua hali yetu. Kwa hiyo tunatii bila kukawia na tunafanya vile kwa kupenda. (Soma Waebrania 13:17.) Tunajua kama wakati tunatii tunasaidia kutaniko iendelee kuwa na umoja. (Efe. 4:2, 3) Na tunajua kuwa hata kama bandugu benye kutuongoza habakamilike, Yehova atatubariki juu tuko natii. (1 Sa. 15:22) Na kama kuko mambo yenye inaomba kabisa kurekebisha, kwa wakati wenye kufaa Yehova atatengeneza mambo.—Mik. 7:7.
15-16. Ni nini ilisaidia ndugu fulani atembee kwa imani hata kama alikuwa na mashaka? (Ona pia picha.)
15 Ona mufano wenye unaonyesha faida ya kutembea kwa imani. Mu Peru, hata kama luga ya Kihispania njo inazungumuziwa sana, batu mingi banasemaka luga za kienyeji. Kati ya zile luga kuko luga ya Kikechua. Kwa miaka mingi, bandugu na badada benye banasemaka Kikechua balikuwa natafuta mu eneo yao batu benye banasemaka ile luga. Lakini juu ya kujipatanisha na sheria ya serikali, kulikuwa mabadiliko mu namna ya kutafuta batu. (Ro. 13:1) Kwa hiyo, bahubiri fulani balijiuliza ikiwa ile itafanya kazi ya kuhubiri irudie nyuma mu ile eneo. Lakini juu bandugu baliunga mukono ile mabadiliko, Yehova alibariki kazi yabo na balipata batu mingi benye banasemaka Kikechua.
16 Kevin, muzee mu kutaniko ya luga ya Kikechua, alisema hivi: “Nilijiuliza, ‘Sasa tutapata namna gani batu benye banasemaka Kikechua?’” Kevin alifanya nini? Anasema hivi: “Nilikumbuka Mezali 3:5. Na nilifikiria mufano wa Musa. Yehova alimuambia Musa aongoze Waisraeli kutoka Misri mupaka ku Bahari Nyekundu, fasi yenye ilionekana kuwa hawana kwa kukimbilia. Lakini Musa alitii, na Yehova alibariki ule utii mu njia ya ajabu.” (Kut. 14:1, 2, 9-11, 21, 22) Kevin alikuwa tayari kubadilisha namna yake ya kuhubiri. Matokeo ilikuwa nini? Anasema hivi: “Nilishangala kuona namna Yehova alitubariki. Zamani tulikuwa tunatembea sana, na wakati fulani tulipata tu mutu moya ao bawili benye balikukwa nasema Kikechua. Sasa tunahubiri sana mu maeneo kwenye kuko batu mingi benye banasemaka Kikechua. Ile inafanya tukuwe na batu mingi ba kuhubiria, ba kurudilia, na ba kujifunza nabo Biblia. Hesabu ya benye banafika ku mikutano imeongezeka.” Ni kweli, wakati tunatembea kwa imani Yehova anatubariki.
Bandugu baliona kama batu mingi balikuwa nabaonyesha fasi kwenye batapata batu benye banasemaka Kikechua (Ona fungu ya 15-16)
17. Umejifunza nini mu hii habari?
17 Tumeona namna tunaweza kuendelea kutembea kwa imani mu mambo tatu ya maana. Lakini tunapaswa kuendelea kutembea kwa imani mu mambo ingine yote ya mu maisha yetu. Kwa mufano, wakati wa kuchagula mambo ya kujifurahisha, wakati tuko naamua masomo yenye tutasoma, ao namna ya kukomalisha batoto. Maamuzi yoyote yenye tunakamata haipaswe tu kutegemea mambo yenye tunaona, lakini tunapaswa pia kufikiria uhusiano wetu pamoya na Yehova, mashauri yenye anatutolea, na ahadi yake ya kutuhangaikia. Tukifanya vile, “tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu milele na milele.”—Mik. 4:5.
WIMBO 156 Kwa Imani
a Majina fulani imebadilishwa.
b Mu hii fungu, tunazungumuzia dada mwenye iko natafuta bwana, lakini hii mashauri inahusu pia ndugu mwenye iko natafuta bibi.