Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • Mungu Ana Kusudi Gani juu ya Dunia?
    Biblia Inafundisha Kabisa Nini?
    • SURA YA TATU

      Mungu Ana Kusudi Gani juu ya Dunia?

      • Mungu ana kusudi gani juu ya wanadamu?

      • Mungu alipingwa namna gani?

      • Maisha yatakuwa namna gani duniani wakati ujao?

      1. Mungu anakusudia kufanya dunia iwe namna gani?

      MUNGU anakusudia kufanya dunia iwe mahali pazuri sana. Yehova anataka dunia ijae watu wenye furaha na wenye afya nzuri. Biblia inasema kama ‘Mungu alipanda bustani katika Edeni; alichipusha kila muti wenye kutamanika kwa macho ya mutu na ulio [muzuri] kwa chakula.’ Kisha kuumba Adamu na Eva, Aliwaweka katika makao hayo mazuri na akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mujaze dunia na kuitiisha.’ (Mwanzo 1:28; 2:8, 9, 15) Kwa hiyo, Mungu alikusudia wanadamu wazae watoto, waeneze paradiso hiyo duniani pote, na kuwatunza wanyama.

      2. (a) Namna gani tunajua kama kusudi la Mungu juu ya dunia litatimia? (b) Biblia inasema watu wataishi milele wapi?

      2 Unawazia kama kusudi hilo la Yehova Mungu la kufanya wanadamu waishi katika paradiso duniani litatimia siku fulani? Mungu anasema hivi: “Mimi nimesema hilo, pia nitalitenda.” (Isaya 46:9-11; 55:11) Hakika, Mungu atatimiza kabisa kusudi lake! Anasema kama ‘hakuiumba [dunia] bila sababu’ lakini “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Mungu alitaka watu wa namna gani waishi duniani? Naye alitaka waishi duniani kwa miaka ngapi? Biblia inajibu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”​—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

      3. Leo maisha yako namna gani duniani, na hilo linatokeza maulizo gani?

      3 Ni wazi kama kusudi hilo halijatimia. Leo, watu wanagonjwa na kufa; na tena wanaendelea kupigana na kuuana. Kwa kweli, Mungu hakukusudia dunia iwe kama ilivyo leo! Kulitokea nini? Sababu gani kusudi la Mungu juu ya dunia halikutimia? Matatizo hayo yalianzia mbinguni, na kwa hiyo hakuna kitabu chochote cha historia kilichoandikwa na mwanadamu kinachoweza kututolea majibu.

      MUPINZANI FULANI ANAJITOKEZA

      4, 5. (a) Ni nani kwa kweli aliyezungumuza na Eva kupitia nyoka? (b) Namna gani mutu muzuri na mwaminifu anaweza kujifanya mwenyewe kuwa mwizi?

      4 Kitabu cha kwanza cha Biblia kinazungumuzia namna kiumbe fulani alimupinga Mungu katika bustani ya Edeni. Anaitwa “nyoka,” lakini kwa kweli yeye hakuwa nyoka. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia yeye anaitwa “Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” Tena anaitwa “yule nyoka wa zamani.” (Mwanzo 3:1; Ufunuo 12:9) Malaika huyo mwenye nguvu na asiyeonekana, alitumia nyoka ili kuzungumuza na Eva. Alifanya ionekane kama vile nyoka ndiye aliyekuwa akisema. Wakati Mungu alipotayarisha dunia kwa ajili ya wanadamu, kiumbe huyo wa kiroho aliona pia jambo hilo.​—Ayubu 38:4, 7.

      5 Kwa kuwa kila kitu Yehova aliumba ni kikamilifu, basi ni nani aliyemufanya “Shetani Ibilisi”? Kwa kifupi, kati ya wana wa kiroho wa Mungu, mumoja alijifanya mwenyewe kuwa Ibilisi. Je, jambo hilo linawezekana? Ndiyo. Jua kama mutu muzuri na mwaminifu anaweza kujifanya mwenyewe kuwa mwizi. Hilo linaweza kutokea namna gani? Mutu anaweza kuacha tamaa mbaya iingie katika moyo wake. Basi akiacha tamaa hiyo iendelee kubaki katika moyo wake, tamaa hiyo inaweza kukomaa. Kisha, akipata nafasi, anaweza kutenda kulingana na tamaa hiyo mbaya ambayo amekomalisha moyoni mwake.​—Yakobo 1:13-15.

      6. Namna gani mwana mumoja wa Mungu alijifanya mwenyewe Shetani Ibilisi?

      6 Hilo ndilo jambo lililotokea kwa Shetani Ibilisi. Labda alisikia wakati Mungu aliwaambia Adamu na Eva wazae watoto na kuijaza dunia. (Mwanzo 1:27, 28) Kwa hiyo, Shetani aliwaza kama wanadamu wote wanaweza kumuabudu yeye kuliko kumuabudu Mungu. Basi tamaa hiyo mbaya ikaanza kukomaa katika moyo wake. Mwishowe, akatimiza tamaa yake kwa kumudanganya Eva na kumusingizia Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Kwa hiyo akajifanya “Ibilisi,” jina linalomaanisha “Musingiziaji.” Wakati huohuo, akajifanya pia “Shetani,” jina linalomaanisha “Mupinzani.”

      7. (a) Kwa nini Adamu na Eva walikufa? (b) Kwa nini sisi watoto wa Adamu tunazeeka na kufa?

      7 Kwa kutumia uongo na werevu, Shetani Ibilisi aliwafanya Adamu na Eva wakose kumutii Mungu. (Mwanzo 2:17; 3:6) Mwishowe, walikufa kama Mungu alivyosema. (Mwanzo 3:17-19) Adamu alipofanya zambi alipoteza ukamilifu, kwa hiyo, sisi watoto wake wote tuliriti zambi kutoka kwake. (Waroma 5:12) Hali hiyo inaweza kulinganishwa na chombo kinachotumiwa ili kutengeneza mikate. Ikiwa chombo hicho kina alama fulani, kila mukate unaotengenezwa humo utakuwa na alama hiyo, sivyo? Vilevile, kila mwanadamu ameriti kutokamilika kutoka kwa Adamu. Ndiyo sababu wanadamu wote wanazeeka na kufa.​—Waroma 3:23.

      8, 9. (a) Inaonekana ni nini iliyokuwa mashitaka ya Shetani? (b) Kwa nini Mungu hakuwaua waasi hao mara moja?

      8 Shetani alipowafanya Adamu na Eva watende zambi, hakika alianzisha uasi juu ya Mungu. Hivyo, alipinga namna ya Yehova ya kutawala. Ni kama vile Shetani alisema hivi: ‘Mungu ni mutawala mubaya. Anasema uongo na anawaima watu wake vitu vizuri. Wanadamu hawana lazima ya kutawaliwa na Mungu. Wanaweza kujichagulia mema na mabaya. Na mimi nikiwatawala watakuwa na maisha mazuri zaidi.’ Namna gani Mungu angejibu mashitaka hayo yenye kumuchafua? Watu fulani wanawaza kama ingekuwa vizuri Mungu awaue waasi hao mara moja. Lakini, je, kufanya hivyo kungejibu kweli mashitaka hayo ya Shetani? Je, kungeonyesha kama namna ya Mungu ya kutawala ndiyo nzuri?

      9 Yehova hakuwaua waasi hao mara moja kwa sababu yeye ni mwenye haki. Aliona kama iliomba wakati fulani upite ili kujibu mashitaka hayo kwa njia nzuri na kuonyesha kabisa kama Shetani ni muongo. Kwa hiyo, Mungu aliona vizuri kuwaacha wanadamu wajitawale kwa wakati fulani wakiongozwa na Shetani. Sura ya 11 itaeleza kwa nini Yehova aliamua hivyo na kwa nini anaacha wakati wa kutosha upite mbele ya kukata mambo. Basi, ni vizuri kujiuliza: Adamu na Eva walikuwa na sababu yoyote ya kumuamini Shetani, aliyekuwa hajawafanyia jambo lolote nzuri? Je, walikuwa na sababu yoyote ya kuamini kama Yehova, aliyekuwa amewatolea vitu vyote walivyokuwa navyo, alikuwa mutu mubaya na muongo? Wewe ungefanya namna gani?

      10. Namna gani unaweza kumujibu Shetani ili kuonyesha kama unamuunga Yehova mukono?

      10 Ni vizuri kuwaza juu ya maulizo hayo kwa sababu kila mumoja wetu anapaswa pia kumujibu Shetani juu ya mashitaka hayo. Ndiyo, una nafasi ya kumujibu Shetani ili kuonyesha kama unamuunga Yehova mukono. Unaweza kumukubali Yehova kuwa Mutawala wako na kuonyesha kama Shetani ni muongo. (Zaburi 73:28; Methali 27:11) Inahuzunisha sana kuona kama leo ni watu wachache tu ndio wanaofanya hiyo. Hilo linatokeza ulizo hili la lazima, Je, Biblia inafundisha kama Shetani ndiye mutawala wa dunia hii?

      NI NANI ANAYEITAWALA DUNIA HII?

      Mukono wa Shetani wakati alimutolea Yesu serikali zote na falme zote za dunia

      Namna gani Shetani angeahidi kumupa Yesu falme zote za dunia ikiwa hazikuwa zake?

      11, 12. (a) Namna gani Shetani alionyesha kama yeye ndiye mutawala wa dunia hii alipomushawishi Yesu? (b) Ni maandiko gani mengine yanayoonyesha kama Shetani ndiye mutawala wa dunia hii?

      11 Yesu hakupinga kama Shetani ndiye anayeitawala dunia hii. Siku fulani, kwa njia ya muujiza Shetani alimuonyesha Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” Kisha akamuahidi Yesu hivi: “Nitakupa mambo yote hayo ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” (Mathayo 4:8, 9; Luka 4:5, 6) Jiulize hivi: Ikiwa Shetani haiko mutawala wa falme zote za dunia, namna gani angeweza kumutolea Yesu falme hizo? Ikiwa Shetani hakuwa mutawala wa falme hizo, Yesu angepinga jambo hilo.

      12 Kwa kweli, Yehova ndiye Mungu Mweza-Yote, Muumbaji wa ulimwengu wote wa ajabu. (Ufunuo 4:11) Lakini, hakuna andiko la Biblia linalosema kama Yehova Mungu ao Yesu Kristo ni watawala wa dunia hii. Yesu alimuita Shetani ‘mutawala wa ulimwengu huu.’ (Yohana 12:31; 14:30; 16:11) Hata Biblia inamuita Shetani Ibilisi ‘mungu wa mufumo huu wa mambo.’ (2 Wakorintho 4:3, 4) Mutume Yohana aliandika juu ya Shetani hivi: ‘Ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za yule muovu.’​—1 Yohana 5:19.

      NAMNA UTAWALA WA SHETANI UTAKAVYOONDOLEWA

      13. Sababu gani tunahitaji dunia mupya?

      13 Dunia inaendelea kuwa mahali penye hatari, siku baada ya siku. Inajaa maaskari wenye kupigana vita, viongozi wa politike wanaodanganya watu, viongozi wa kidini wanafiki, na watu wanaokusudia kutenda mambo mabaya tu. Hakuna mutu anayeweza kuondoa mambo hayo. Biblia inasema kama hivi karibuni, kwenye vita yake ya Har-Magedoni, Mungu atayaondoa mambo yote yenye kuharibu dunia hii na atafanya dunia mupya ya haki.​—Ufunuo 16:14-16.

      14. Mungu amemuchagua nani ili awe Mutawala wa Ufalme Wake, na juu ya hilo Biblia ilisema nini tangu zamani?

      14 Yehova Mungu alimuchagua Yesu Kristo awe Mutawala wa Ufalme Wake wa mbinguni ao serikali Yake. Tangu zamani Biblia ilisema hivi: ‘Kwa maana kuna mutoto ambaye amezaliwa kwetu, kuna mwana ambaye tumepewa; na utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake. Naye ataitwa Mukuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.’ (Isaya 9:6, 7) Juu ya serikali hiyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Kama tutakavyojifunza, karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za dunia hii, nao utachukua nafasi ya serikali hizo. (Danieli 2:44) Kisha Ufalme wa Mungu utaifanya dunia yote kuwa paradiso.

      DUNIA MUPYA INAKARIBIA!

      Watu wenye kuimba, kupiga muziki, na kufurahia maisha katika dunia mupya

      15. ‘Dunia mupya’ inamaanisha nini?

      15 Biblia inatuambia hivi: ‘Kulingana na ahadi yake [Mungu] tunangojea mbingu mupya na dunia mupya, na humo [haki itakakaa].’ (2 Petro 3:13; Isaya 65:17) Nyakati fulani Biblia inatumia neno “dunia,” ili kumaanisha watu wanaoishi duniani. (Mwanzo 11:1) Kwa hiyo, ‘dunia mupya’ inamaanisha watu wanaokubaliwa na Mungu.

      16. Wale wanaokubaliwa na Mungu watapata nini, na tunapaswa kufanya nini ili kupokea zawadi hiyo?

      16 Yesu aliahidi kama katika dunia mupya, wale wanaokubaliwa na Mungu watapata “uzima wa milele.” (Marko 10:30) Tafazali, fungua Biblia yako kwenye Yohana 3:16 na 17:3, na usome yale ambayo Yesu alisema tunapaswa kufanya ili kupata uzima huo wa milele. Acha sasa tuone baraka watakazopata wale wanaostahili kuingia katika dunia itakayokuwa Paradiso.

      17, 18. Sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kama kutakuwa amani na usalama duniani pote?

      17 Hakutakuwa tena mambo mabaya, vita, uvunjaji wa sheria, na jeuri. ‘Mutu mubaya hatakuwako tena. Bali wapole wataimiliki dunia.’ (Zaburi 37:10, 11) Kutakuwa amani kwa kuwa ‘Mungu atakomesha vita mupaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9; Isaya 2:4) Kisha ‘muadilifu atachipuka, na wingi wa amani mupaka mwezi utakapokuwa haupo tena,’ yaani, milele!​—Zaburi 72:7.

      18 Waabudu wa Yehova wataishi kwa usalama. Nyakati zote ambazo Waisraeli walimutii Mungu, waliishi kwa usalama. (Walawi 25:18, 19) Itakuwa ajabu sana kufurahia usalama kama huo katika Paradiso!​—Isaya 32:18; Mika 4:4.

      19. Namna gani tunajua kama tutakuwa na chakula kingi katika dunia mupya ya Mungu?

      19 Kutakuwa na chakula kingi. Mutunga-zaburi aliimba hivi: “Kutakuwa na wingi wa [chakula] duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Yehova Mungu atawabariki waadilifu wake, na “hakika dunia itatoa mazao yake.”​—Zaburi 67:6.

      20. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kama dunia nzima itakuwa paradiso?

      20 Dunia nzima itakuwa paradiso. Wanadamu watajenga nyumba nzuri na watapanda bustani zenye kupendeza katika sehemu zilizoharibiwa na wanadamu wenye zambi. (Isaya 65:21-24; Ufunuo 11:18) Polepole, dunia nzima itafikia kuwa paradiso yenye kupendeza na kuzaa matunda sana kama bustani ya Edeni. Tena, Mungu ‘ataufumbua mukono wake na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’​—Zaburi 145:16.

      21. Ni nini kinachoonyesha kama wanadamu na wanyama wataishi pamoja kwa amani?

      21 Wanadamu na wanyama wataishi pamoja kwa amani. Wanyama wa porini na wanyama wa kufugwa watakula pamoja. Hata mutoto mudogo hataogopa wanyama walio hatari leo.​—Isaya 11:6-9; 65:25.

      22. Je, magonjwa yatakuwapo katika dunia mupya?

      22 Magonjwa hayatakuwapo tena. Yesu, Mutawala wa Ufalme wa Mungu huko mbinguni, atawaponyesha watu wengi sana kuliko wale alioponyesha alipokuwa duniani. (Mathayo 9:35; Marko 1:40-42; Yohana 5:5-9) Kwa hiyo, ‘hakuna mukaaji atakayesema: Mimi ni mugonjwa.’​—Isaya 33:24; 35:5, 6.

      23. Kwa nini ufufuo utatuletea furaha kubwa?

      23 Watu tuliowapenda waliokufa watafufuliwa ili kuishi milele. Wale wote waliokufa walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa. “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”​—Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29.

      24. Je, wewe pia unafurahia wazo la kuishi katika Paradiso hapa duniani?

      24 Mambo mazuri sana yanawangojea wale wanaoamua kujifunza juu ya Yehova Mungu, Muumbaji wetu Mukubwa, na kumutumikia! Paradiso itakayokuwa duniani wakati ujao ndio paradiso ambayo Yesu alimuahidi yule mutenda-mabaya aliyetundikwa pamoja naye. Alimuambia hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Ni jambo la lazima tujifunze mengi juu ya Yesu Kristo, kwa sababu tutapata baraka hizo zote kupitia Yesu.

      BIBLIA INAFUNDISHA KWAMBA

      • Kusudi la Mungu la kuifanya dunia iwe paradiso litatimia.​—Isaya 45:18; 55:11.

      • Shetani ndiye anayeitawala dunia hii.​—Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19.

      • Katika dunia mupya inayokuja, Mungu atawabariki sana wanadamu.​—Zaburi 37:10, 11, 29.

  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Biblia Inafundisha Kabisa Nini?
    • SURA YA MUNANE

      Ufalme wa Mungu Ni Nini?

      • Biblia inasema nini juu ya Ufalme wa Mungu?

      • Ufalme wa Mungu utafanya nini?

      • Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yatimizwe hapa duniani wakati gani?

      1. Ni sala gani inayojulikana sana tunayotaka kuzungumuzia?

      MAMILIONI ya watu duniani wanajua ile sala inayoitwa Sala ya Baba Yetu, ao Sala ya Bwana. Sala hiyo ambayo Yesu Kristo yeye mwenyewe alifundisha kuwa sala ya mufano inajulikana sana. Maneno yanayopatikana katika sala hiyo ni ya lazima sana. Basi tujifunze mambo matatu ya kwanza ya kuomba katika sala hiyo; kujifunza mambo hayo kutakusaidia kujua mambo mengi ambayo Biblia inafundisha.

      2. Yesu alifundisha wanafunzi wake kusali juu ya mambo gani matatu?

      2 Mwanzoni mwa sala hiyo, Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9-13) Mambo hayo matatu ambayo tunapaswa kuomba yanamaanisha nini?

      3. Tuna lazima ya kujua nini juu ya Ufalme wa Mungu?

      3 Tumekwisha kujifunza mengi juu ya jina la Mungu, Yehova. Tena tumezungumuzia juu ya mapenzi ya Mungu, yaani, mambo ambayo amewafanyia wanadamu na yale atakayowafanyia tena. Yesu alikuwa akiwazia nini alipotuambia tusali: “Ufalme wako na uje”? Ufalme wa Mungu ni nini? Ufalme huo utakapokuja, utalitakasa namna gani jina la Mungu, ao kulifanya liwe takatifu? Na pia namna gani mapenzi ya Mungu yatafanyika wakati Ufalme huo utakapokuja?

      UFALME WA MUNGU NI NINI?

      4. Ufalme wa Mungu ni nini? Na Mufalme wa Ufalme huo ni nani?

      4 Ufalme wa Mungu ni serikali iliyotiwa na Yehova Mungu na itakayoongozwa na Mufalme ambaye amechaguliwa na Mungu mwenyewe. Basi, Mufalme wa Ufalme wa Mungu ni nani? Ni Yesu Kristo. Yesu ni Mufalme mukubwa kuliko watawala wengine wote wanadamu, ndio sababu anaitwa ‘Mufalme wa wale wanaotawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale wanaotawala wakiwa mabwana.’ (1 Timotheo 6:15) Ana nguvu za kufanya mambo mengi mazuri kuliko watawala hao wote, kuliko hata watawala ambao wanaonekana kuwa na moyo muzuri kuliko wengine.

      5. Ufalme wa Mungu unatawala kutoka wapi, na utatawala nini?

      5 Ufalme wa Mungu unatawala kutoka wapi? Ujiulize, Yesu iko wapi? Unakumbuka, tulijifunza kama aliuawa kwenye muti wa mateso, kisha akafufuliwa. Na kisha siku 40 akaenda mbinguni. (Matendo 2:33) Kwa hivyo, Ufalme wa Mungu uko mbinguni. Ndiyo sababu Biblia inaita ufalme huo “ufalme wa mbinguni.” (2 Timotheo 4:18) Hata hivyo, ufalme huo utatawala ao kuongoza dunia.​—Ufunuo 11:15.

      6, 7. Sababu gani Yesu ni Mufalme asiyelingana na wafalme wengine wanadamu?

      6 Sababu gani Yesu ni Mufalme asiyelingana na wafalme wengine wanadamu? Sababu moja ni hii: Yesu hatakufa tena kamwe. Biblia inapomulinganisha Yesu na wafalme wanadamu, inasema: “Yeye peke yake asiyeweza kufa, anayekaa katika nuru isiyoweza kufikiwa.” (1 Timotheo 6:16) Hilo linamaanisha kama mambo yote mazuri ambayo Yesu anafanya yatadumu milele. Na tunajua vizuri kama atafanyia watu wake mambo mengi mazuri.

      7 Wazia kidogo namna unabii huu wa Biblia unavyosema juu ya Yesu: ‘Roho ya Yehova itatua juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumuogopa Yehova; naye atakuwa na shangwe katika kumuogopa Yehova. Na hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.’ (Isaya 11:2-4) Maneno hayo yalionyesha kama Yesu atakuwa Mufalme wa haki na atawasikilia huruma watu atakaotawala hapa duniani. Ungependa Mufalme kama huyo akutawale, sivyo?

      8. Ni nani watakaotawala pamoja na Yesu?

      8 Jambo lingine ni hili: Katika Ufalme huo Yesu hatatawala yeye mwenyewe. Kuna watu watakaotawala pamoja naye. Kwa mufano, mutume Paulo alimuambia Timotheo: “Tukiendelea kuvumilia, tutatawala pamoja pia tukiwa wafalme.” (2 Timotheo 2:12) Paulo, Timotheo, na Wakristo wengine waaminifu ambao wamechaguliwa na Mungu watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa mbinguni. Ni watu wangapi watakuwa na pendeleo hilo?

      9. Ni watu wangapi watakaotawala pamoja na Yesu, na Mungu alianza kuwachagua tangu wakati gani?

      9 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 7, mutume Yohana aliona katika maono ‘Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] amesimama juu ya Mulima Sayuni [inaonyesha cheo chake cha mufalme mbinguni], na pamoja naye 144 000 wakiwa na jina lake na jina la Baba yake limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao.’ Hao watu 144 000 ni nani? Yohana mwenyewe anajibu: ‘Hao ndio wale wanaoendelea kumufuata Mwana-Kondoo popote anapoenda. Hao walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.’ (Ufunuo 14:1, 4) Ndiyo, wao ni wanafunzi waaminifu wa Yesu Kristo waliochaguliwa ili watawale pamoja naye mbinguni. Wakiisha kufufuliwa na kwenda mbinguni, ‘watatawala na watakuwa wafalme juu ya dunia,’ pamoja na Yesu. (Ufunuo 5:10) Tangu siku za mitume, Mungu ameendelea kuchagua Wakristo waaminifu ili kutimiza hesabu hiyo ya watu 144 000.

      10. Sababu gani mupango wa kuwafanya Yesu na watu 144 000 watawale wanadamu unaonyesha kama Mungu anatupenda?

      10 Mupango wa kuwafanya Yesu na watu 144 000 watawale wanadamu unaoonyesha kama Mungu anatupenda. Sababu gani? Kumbuka, Yesu alikuwa mwanadamu na aliteseka kama sisi. Paulo alisema hivi: ‘Si mutu ambaye hawezi kuusikitikia uzaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na zambi.’ (Waebrania 4:15; 5:8) Tena wale watakaotawala pamoja naye wameteseka pia na kuvumilia kama wanadamu wengine wote. Zaidi ya hilo, wamekuwa watu wasio wakamilifu na wamevumilia magonjwa ya kila aina. Hakika, wataelewa vizuri matatizo ya wanadamu!

      UFALME WA MUNGU UTAFANYA NINI?

      11. Sababu gani Yesu aliwaambia wanafunzi wake wasali mapenzi ya Mungu yafanyike huko mbinguni?

      11 Yesu aliwaambia wanafunzi wake wasali Ufalme wa Mungu uje, tena aliwaambia wasali mapenzi ya Mungu yafanyike “duniani kama ilivyo mbinguni.” Mungu anaishi mbinguni; malaika waaminifu huko mbinguni wanafanya sikuzote mapenzi yake. Lakini, katika Sura ya 3, tulijifunza kama malaika fulani muasi aliacha kufanya mapenzi ya Mungu na akawafanya Adamu na Eva watende zambi. Katika Sura ya 10, tutajifunza mambo mengi ambayo Biblia inafundisha juu ya malaika huyo mubaya, anayeitwa Shetani Ibilisi. Mungu alimuacha Shetani na malaika wengine waliomufuata, wanaoitwa mashetani, waishi mbinguni kwa muda. Hilo linaonyesha kama, wakati huo huko mbinguni kulikuwa na viumbe ambavyo havikuwa vikifanya mapenzi ya Mungu. Mambo yalipaswa kubadilika wakati Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala. Yesu Kristo, Mufalme mupya, alipaswa kupigana vita na Shetani.​—Ufunuo 12:7-9.

      12. Ni mambo gani mawili ya lazima yanayotajwa katika Ufunuo 12:10?

      12 Maneno ya unabii yanayofuata yanaeleza jambo ambalo lingetokea: ‘Nami nikaisikia sauti kubwa mbinguni ikisema: Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake, kwa sababu mushitaki wa ndugu zetu ametupwa chini, anayewashitaki muchana na usiku mbele za Mungu wetu!’ (Ufunuo 12:10) Umeona mambo mawili ya lazima yanayotajwa katika andiko hilo? Jambo la kwanza, Ufalme wa Mungu, chini ya uongozi wa Yesu Kristo, unaanza kutawala. Jambo la pili, Shetani anafukuzwa mbinguni na kutupwa duniani.

      13. Kwa sababu Shetani amefukuzwa mbinguni, hali imekuwa namna gani huko?

      13 Mambo hayo mawili yameleta nini? Juu ya hali inayopatikana sasa mbinguni, tunasoma hivi: ‘Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi munaokaa ndani yake!’ (Ufunuo 12:12) Ndiyo, malaika waaminifu mbinguni wanafurahi, kwa sababu sasa Shetani na mashetani wake wamefukuzwa; wote wanaobaki mbinguni ni waaminifu kwa Yehova Mungu. Sasa huko kuna amani yenye kudumu na upatano kamili. Mapenzi ya Mungu yanafanyika mbinguni.

      Picha yenye kuonyesha mateso, vita, kuuana, na kuchafuliwa kwa hewa na mambo mengine

      Tangu wakati Shetani na mashetani wake walipotupwa duniani, watu wanateseka sana. Mateso hayo yatakwisha hivi karibuni

      14. Kwa sababu Shetani ametupwa duniani, hali iko namna gani?

      14 Lakini, hali iko namna gani duniani? Biblia inasema: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Kwa sababu amefukuzwa mbinguni na ana wakati mufupi, Shetani anakasirika sana. Hasira yake inaleta mateso, ao “ole,” duniani. Katika sura inayofuata tutajifunza mengi juu ya ole hiyo. Kwa kuwa tunajua jambo lililomufikia Shetani na mateso anayotuletea, tunaweza kujiuliza, Ufalme wa Mungu utafanya nini ili mapenzi ya Mungu yafanyike duniani?

      15. Mapenzi ya Mungu ni nini juu ya dunia?

      15 Kumbuka tena yale tuliyojifunza katika Sura ya 3, tulizungumuzia mapenzi ya Mungu juu ya dunia. Katika Edeni, Mungu alionyesha mapenzi yake; alipenda dunia iwe paradiso inayojaa watu waaminifu na wanaoishi milele. Shetani aliwafanya Adamu na Eva watende zambi, na hilo lilifanya mapenzi ya Mungu yasifanyike tena duniani wakati huo, lakini Mungu hakubadilisha kusudi lake. Yehova angali anakusudia ‘waadilifu wenyewe waimiliki dunia, nao wakae milele juu yake.’ (Zaburi 37:29) Ni Ufalme wa Mungu ndio utatimiza jambo hilo. Namna gani?

      16, 17. Andiko la Danieli 2:44 linatufundisha nini juu ya Ufalme wa Mungu?

      16 Ona namna unabii ulio katika Danieli 2:44 unavyosema. Tunasoma: ‘Na katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mupaka wakati usio na kipimo.’ Andiko hilo linatufundisha nini juu ya Ufalme wa Mungu?

      17 Jambo la kwanza: Ufalme wa Mungu ungepaswa kuanza kutawala “katika siku za wafalme hao,” yaani, wakati falme zingine zitakuwa bado zikitawala. Jambo la pili: Ufalme huo utadumu milele. Hautashindwa wala kupinduliwa na serikali nyingine. Jambo la tatu: Tunaona kama kutakuwa vita kati ya Ufalme wa Mungu na falme za dunia. Ufalme wa Mungu utashinda. Mwishowe, wanadamu wote watatawaliwa na serikali hiyo moja tu. Kwa hiyo, wanadamu watatawaliwa na serikali bora zaidi kuliko serikali zote zilizokwisha kuwatawala.

      18. Vita ya mwisho kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za wanadamu inaitwa namna gani?

      18 Biblia inazungumuzia mambo mengi yatakayofanyika wakati vita hiyo ya mwisho itakapopiganwa kati ya Ufalme wa Mungu na serikali za wanadamu. Kwa mufano, inafundisha kama kadiri tunavyokaribia mwisho, roho waovu ao mashetani, wataeneza uongo ili kuwadanganya “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa.” Kwa sababu gani? “Ili kuwakusanya [wafalme hao] pamoja kwa vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” Wafalme wa dunia watakusanywa pamoja “mahali panapoitwa katika Kiebrania Har-Magedoni.” (Ufunuo 16:14, 16) Kulingana na andiko hilo, vita ya mwisho kati ya serikali za wanadamu na Ufalme wa Mungu inaitwa vita ya Har-Magedoni.

      19, 20. Ni nini inayozuia mapenzi ya Mungu kufanyika leo?

      19 Kupitia Har-Magedoni, Ufalme wa Mungu utatimiza mambo gani? Kumbuka tena mapenzi ya Mungu juu ya dunia. Yehova Mungu alikusudia dunia ijae wanadamu waaminifu na wakamilifu wanaomutumikia katika Paradiso. Ni nini inayozuia mapenzi hayo ya Mungu kufanyika leo? Jambo la kwanza, sisi ni watenda zambi, tunagonjwa na kisha tunakufa. Lakini, katika Sura ya 5 tulijifunza kama Yesu alikufa kwa ajili yetu ili tuweze kuishi milele. Labda unakumbuka tena maneno haya yaliyoandikwa na Yohana: ‘Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa-pekee, ili kila mutu anayemuamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’​—Yohana 3:16.

      20 Jambo la pili, watu wengi wanatenda mambo maovu. Wanasema uongo, wanaiba, na wanafanya mambo ya uasherati. Hawapendi kufanya mapenzi ya Mungu. Watu wanaofanya mambo mabaya wataharibiwa kwenye vita ya Mungu inayoitwa Har-Magedoni. (Zaburi 37:10) Jambo la tatu, serikali haziwatie watu moyo wafanye mapenzi ya Mungu. Serikali nyingi hazina uwezo, zinatesa watu na kufanya mambo mengi mabaya. Biblia inasema waziwazi hivi: ‘Mwanadamu amemutawala mwanadamu kwa kumuumiza.’​—Mhubiri 8:9.

      21. Namna gani kupitia Ufalme mapenzi ya Mungu yatafanyika hapa duniani?

      21 Kisha Har-Magedoni, wanadamu watatawaliwa na serikali moja tu, Ufalme wa Mungu. Ufalme huo utafanya mapenzi ya Mungu na utaleta baraka nzuri sana. Kwa mufano, utamuondoa Shetani na mashetani wake. (Ufunuo 20:1-3) Zabihu ya Yesu itafanya kazi; itaondolea watu waaminifu magonjwa na kifo. Watu wataishi milele chini ya utawala wa Ufalme. (Ufunuo 22:1-3) Dunia itafanywa kuwa paradiso. Hivyo, kupitia Ufalme, mapenzi ya Mungu yatafanyika hapa duniani na jina la Mungu litatakaswa. Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kama mwishowe, chini ya Ufalme wa Mungu, kila kiumbe kilicho na uzima kitalitukuza jina la Mungu.

      UFALME WA MUNGU UTAFANYA MAMBO HAYO WAKATI GANI?

      22. Namna gani tunajua kama Ufalme wa Mungu haukuja wakati Yesu alipokuwa duniani ao aliporudia tu mbinguni?

      22 Wakati Yesu aliwaambia wanafunzi wake wasali ‘Ufalme wako uje,’ ni wazi Ufalme huo ulikuwa bado kuja. Je, ulikuja wakati Yesu aliporudia mbinguni? Hapana, kwa sababu Petro na Paulo walisema kama kisha Yesu kufufuliwa, unabii wa Zaburi 110:1 ulitimizwa. Unasema hivi: ‘Neno la Yehova kwa Bwana wangu ni: Keti kwenye mukono wangu wa kuume mupaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.’ (Matendo 2:32-35; Waebrania 10:12, 13) Yesu alipaswa kungojea.

      Wakati Ufalme wa Mungu utatawala dunia, mapenzi ya Mungu yatafanyika duniani kama ilivyo mbinguni

      23. (a) Ufalme wa Mungu ulianza kutawala wakati gani? (b) Sura inayofuata itazungumuzia nini?

      23 Alipaswa kungojea kwa muda gani? Karibu miaka 40 mbele ya mwaka wa 1914, kupitia hesabu za Biblia, wanafunzi wa kweli wa Biblia walitambua kama Yesu alipaswa kungojea mupaka mwaka wa 1914. (Ikiwa unapenda kujua zaidi juu ya tarehe hiyo, soma Nyongeza, ukurasa wa 215-218.) Mambo ambayo yametokea duniani kuanzia mwaka wa 1914 yanaonyesha kama wanafunzi wa kweli wa Biblia hawakudanganyika. Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kama katika mwaka wa 1914, Kristo aliwekwa kuwa Mufalme na Ufalme wa mbinguni wa Mungu ulianza kutawala. Kwa hiyo, tunaishi katika kile “kipindi kifupi cha wakati” kinachomubakilia Shetani. (Ufunuo 12:12; Zaburi 110:2) Tena, tunaweza kusema hakika kama karibuni Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yafanyike hapa duniani. Hauoni kama hiyo ni habari njema kabisa? Unaamini kama mambo hayo yatafanyika? Sura inayofuata itakusaidia uone kama Biblia inafundisha kabisa mambo hayo.

      BIBLIA INAFUNDISHA KWAMBA

      • Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni inayoongozwa na Yesu Kristo pamoja na watu 144 000 ambao wamechukuliwa duniani.​—Ufunuo 14:1, 4.

      • Ufalme huo ulianza kutawala mwaka wa 1914, na tangu hapo Shetani alifukuzwa mbinguni na kutupwa duniani.​—Ufunuo 12:9.

      • Karibuni Ufalme wa Mungu utaharibu serikali zote za wanadamu, na dunia itakuwa paradiso.​—Ufunuo 16:14, 16.

Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili (Congo)
  • Tumia Wengine
  • Préférences
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Kanuni za Matumizi
  • Kanuni za Kutunza Siri
  • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
  • JW.ORG
  • Ingia
Tumia Wengine