Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • Usiruhusu Kitu Chochote Kikutenganishe na Yehova
    Munara wa Mulinzi—2013 | Mwezi wa 1 15
    • [Picha katika ukurasa wa 12]

      Usiruhusu Kitu Chochote Kikutenganishe na Yehova

      ‘Mujichagulie leo yule mutakayemutumikia.’​—YOS. 24:15.

      JARIBU KUJIBU:

      • Namna gani unaweza kutia kazi ya kimwili pa nafasi yake?

      • Unaweza kufanya nini ili usipitishe kiasi unapojifurahisha?

      • Namna gani tunaweza kuvumilia huzuni tunayopata wakati mutu wa familia yetu anatengwa na kutaniko?

      1-3. (a) Namna gani mufano wa Yoshua unaweza kutusaidia tufanye uamuzi muzuri katika maisha yetu? (b) Hatupaswe kusahau nini tunapojikuta mbele ya maamuzi mawili ao zaidi?

      “KUCHAGUA,” hilo ni neno nzito kabisa. Maamuzi ya mutu yanaweza kuonyesha namna anavyotaka kutumia maisha yake. Tuchukue mufano: Wazia mutu fulani anatembea katika barabara na mara moja anafika mahali ambapo barabara hiyo inagawanyika na kuwa njia mbili zinazoelekea mahali tofauti. Mutu huyo atachagua njia gani? Ikiwa anajua mahali anapoenda, atachagua njia ambayo itamufikisha mahali amapoenda na kuacha ile inayoweza kumupoteza ao kumupeleka mbali na kusudi lake.

      2 Biblia ina mifano ya watu wengi waliojikuta katika hali kama hiyo. Kwa mufano, Kaini alipaswa kuamua ikiwa atatenda kwa hasira ao ikiwa ataizuia hasira yake. (Mwa. 4:6, 7) Yoshua alipaswa kuamua kama atatumikia Mungu wa kweli ao miungu ya uongo. (Yos. 24:15) Kwa kuwa muradi wa Yoshua ulikuwa kumukaribia Yehova; yeye alichagua njia iliyomusaidia kufanya hivyo. Kaini hakuwa na muradi kama huo, kwa hiyo alichagua njia iliyomutenganisha na Yehova.

      3 Wakati fulani, tunaweza kujikuta mbele ya maamuzi mawili ao zaidi. Ikiwa tunajikuta katika hali hiyo, tusisahau mahali tunapoenda, ao muradi wetu maishani, ni kusema, kumutukuza Mungu katika mambo yote tunayofanya na kuepuka kitu chochote kinachoweza kututenganisha naye. (Soma Waebrania 3:12.) Katika habari hii na ile inayofuata, tutaona mambo saba yanayoweza kututenganisha na Yehova.

      KAZI

      4. Kwa nini kazi ya kimwili ni ya maana katika maisha?

      4 Wakristo wanapaswa kutosheleza mahitaji yao na ya familia zao. Biblia inaonyesha kama mutu asiyetaka kuwatimizia watu wa familia yake mahitaji yao, ni mubaya sana kuliko hata mupagani. (2 Thes. 3:10; 1 Tim. 5:8) Bila shaka, kazi ya kimwili ni ya maana katika maisha, lakini ikiwa sisi si waangalifu, inaweza kututenganisha na Yehova. Namna gani?

      5. Ni mambo gani ya lazima tunapaswa kufikiria tunapotafuta kazi?

      5 Wazia kwamba unatafuta kazi. Ikiwa unaishi katika inchi ambamo kupata kazi ni vigumu, unaweza kujaribiwa kuitika kazi yoyote inayojitokeza kwa mara ya kwanza. Lakini, namna gani ikiwa kazi hiyo inapingana na kanuni za Biblia? Namna gani ikiwa kazi hiyo itakuzuia kufanya mambo ya kiroho ao itakupeleka mbali na familia yako? Je, unapaswa tu kuikubali, ukifikiri kama ni afazali kuwa na kazi hata isiyofaa kuliko kubaki bila kazi? Kumbuka kwamba, kuchagua njia mbaya inaweza kukufanya uende mbali na Yehova. (Ebr. 2:1) Iwe unatafuta kazi ao unachunguza kazi uliyo nayo sasa ili kuona kama inafaa kwa Mukristo, namna gani unaweza kufanya maamuzi mazuri?

      6, 7. (a) Mutu anaweza kuwa na miradi gani kuhusu kazi ya kimwili? (b) Ni muradi gani unaoweza kukusaidia umukaribie zaidi Yehova, na sababu gani?

      6 Kama tulivyosema mwanzoni, usisahau mahali unapoenda, ao muradi wako. Jiulize hivi: ‘Ninataka kazi hii inifikishe wapi?’ Ukiona kazi ya kimwili kuwa tu ni njia ya kukutegemeza na kutegemeza familia yako ili kufanya mapenzi ya Yehova, basi, Yehova atakubariki. (Mt. 6:33) Yehova anajua namna anavyoweza kukusaidia wakati unapoteza kazi ao wakati unapatwa bila kutazamia na matatizo ya feza. (Isa. 59:1) Yeye “anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”​—2 Pet. 2:9.

      7 Lakini, namna gani ikiwa muradi wako ni kutaka tu kuwa na mali? Labda unaweza kufanikiwa. Lakini, usisahau kwamba “mafanikio” hayo hayatakosa kukuletea matatizo mengi. (Soma 1 Timotheo 6:9, 10.) Kufuatilia sana mali na kazi kutakutenganisha kabisa na Yehova.

      8, 9. Wazazi wanapaswa kujiuliza nini kuhusu kazi yao ya kimwili? Eleza.

      8 Ikiwa wewe ni muzazi, jiulize ikiwa unawapa watoto wako mufano muzuri. Ni mambo gani wanayoona ukitia pa nafasi ya kwanza katika maisha? Je, ni kazi yako ao urafiki wako pamoja na Yehova? Ikiwa wanaona kwamba unahangaikia sana cheo, sifa, na mali, je, hawatakufuata katika njia hiyo yenye hatari? je, jambo hilo haliweze kupunguza heshima yao kwako? Binti mumoja Mukristo mwenye miaka 17 alisema hivi: “Ninakumbuka kama zamani baba yangu alihangaikia sana kazi yake. Mwanzoni, ilionekana kama alitumika sana sababu alitaka tuwe na maisha mazuri kabisa; alitaka kuitunza familia yake vizuri. Lakini katika miaka ya hivi karibuni, mambo fulani yamebadilika. Yeye ni kazi tu, na analeta nyumbani vitu vya bei kali ambavyo hatuhitaji kabisa. Sasa watu wanatuwazia kuwa familia yenye feza nyingi, kuliko kujulikana kuwa familia inayowatia wengine moyo wafuatilie mambo ya kiroho. Ningependelea baba yangu atumike sana ili kuisaidia familia yake imukaribie zaidi Yehova kuliko kutafuta feza sana.”

      9 Wazazi, musijitenge na Yehova kwa kuhangaikia sana kazi. Muwaonyeshe watoto wenu kupitia mufano wenu muzuri kwamba munaamini kwelikweli kama mambo ya kiroho ndio utajiri mukubwa zaidi ambao mutu anaweza kuwa nao, na si vitu vya kimwili.​—Mat. 5:3.

      10. Kijana anapaswa kujiuliza nini anapotafuta kazi?

      10 Ikiwa wewe ni kijana anayetafuta kazi, namna gani unaweza kufanya maamuzi mazuri? Kama tulivyosema mwanzoni, ni vizuri kujua mahali unapoenda, nikusema, muradi wako katika maisha. Ikiwa unajifunza kazi fulani, je, mazoezi hayo na kazi hiyo itakuruhusu kutia mambo ya Ufalme pa nafasi ya kwanza, ao itakutenganisha na Yehova? (2 Tim. 4:10) Je, unataka kuwaiga watu ambao furaha yao inategemea tu feza zao? Ao utachagua kuwa mwenye tumaini kama Daudi ambaye aliandika: ‘Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, Na bado sijamuona mutu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mukate.’ (Zab. 37:25) Kumbuka kwamba kuna njia mbili: moja ni ile inayokutenganisha na Yehova, na nyingine ni ile inayokupeleka kwenye maisha mazuri ya milele. (Soma Methali 10:22; Malaki 3:10.) Wewe utachagua njia gani?a

      MAMBO YA KUJIFURAHISHA

      11. Biblia inafundisha nini kuhusu kujifurahisha, lakini tunapaswa kuwa waangalifu na nini?

      11 Biblia haikataze kujiburudisha ao kujifurahisha, wala haiseme kama kufanya hivyo ni kupoteza wakati. Mutume Paulo alimuandikia Timotheo hivi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.” (1 Tim. 4:8) Biblia inasema pia kama kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kurukaruka,” na inatutia moyo tupumuzike kwa kiasi fulani ili tuwe na afya nzuri. (Mhu. 3:4; 4:6) Hata hivyo, ikiwa hatuko waangalifu, kujifurahisha huko kunaweza kututenganisha na Yehova. Namna gani? Kujifurahisha kunaweza kutokeza hatari mbili: namna ya kujifurahisha na wakati tunaopitisha kwa kujifurahisha.

      [Picha katika ukurasa wa 14]

      Kujifurahisha kwa njia nzuri na kwa kiasi kunapumuzisha kabisa

      12. Mutu anapaswa kujiuliza nini kuhusu mambo anayotazama ili kujifurahisha?

      12 Kwanza, tuzungumuzie namna mbalimbali za kujifurahisha. Uwe hakika kwamba kuna namna mbalimbali za kujifurahisha nzuri. Lakini, jua kwamba namna nyingi ya kujifurahisha leo inahusu mambo ambayo Mungu anachukia sana: mambo ya kuuana, mambo ya kushirikiana na roho waovu, na mambo ya uasherati. Kwa hiyo, tunapaswa kuchunguza sana yale tunayotazama kwa kujifurahisha. Ujiulize hivi: Mambo ninayotazama kwa kujifurahisha yatakuwa na matokeo gani juu yangu? Je, yananichochea kuwa na roho isiyo na huruma, roho ya mashindano, ao roho ya mutu kujivunia sana inchi yake? (Met. 3:31) Je, kujifurahisha huko kunanichukua feza nyingi? Je, kunawakwaza wengine? (Rom. 14:21) Ninajifurahisha na watu wa aina gani? (Met. 13:20) Je, mambo ninayoona ninapojifurahisha yanaamusha ndani ya moyo wangu tamaa ya kufanya mambo mabaya?​—Yak. 1:14, 15.

      13, 14. Unapaswa kujiuliza nini kuhusu wakati unaopitisha katika kujifurahisha?

      13 Acheni tuzungumuzie pia wakati tunaopitisha katika kujifurahisha. Ujiulize hivi: ‘Je, ninapitisha wakati mwingi katika mambo ya kujifurahisha hivi kwamba ninabaki na wakati mudogo tu kwa ajili ya mambo ya kiroho?’ Ikiwa unachagua kupitisha wakati mwingi katika kujifurahisha, utaona kwamba kuliko kukupumuzisha mambo hayo yatakuchokesha kabisa. Ni kweli, wale wasiopitisha kipimo wanafurahia kabisa kujifurahisha kwao. Sababu gani? Kwa sababu wanajua kwamba wametimiza kwanza “mambo yaliyo ya maana zaidi,” kwa hiyo, wanapojifurahisha zamiri haiwasumbue.​—Soma Wafilipi 1:10, 11.

      14 Hata ikiwa mutu anaweza kushawishiwa apitishe wakati mwingi katika mambo ya kujifurahisha, tusisahau kwamba njia hiyo inaweza kututenganisha na Yehova. Dada Kim aliye na miaka 20 alijionea jambo hilo. Yeye anasema hivi: “Nilienda kila mahali nilipoalikwa ili kujifurahisha. Kila mwisho wa juma, ni kusema Siku ya Tano, Siku ya Posho, na Siku ya Yenga, kulikuwa na karamu. Lakini sasa, ninaona kwamba kuna mambo mengi sana ya maana ambayo ninapaswa kufanya. Kwa mufano, kwa kuwa mimi ni painia, ninaamuka saa 12 ya asubui ili niende katika mahubiri, kwa hiyo siweze tena kubaki na marafiki mupaka saa saba ao saa munane ya usiku. Ninajua kwamba karamu zote si mbaya, lakini zinaweza kukengeusha sana. Kama vile katika kila jambo, hatupaswe kupitisha kiasi.”

      15. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wajifurahishe kwa njia inayofaa?

      15 Wazazi wanapaswa kutimiza mahitaji yao na ya watoto wao ya kimwili, ya kiroho, na kuhusu mambo ya kujifurahisha. Hiyo inamaanisha inafaa wawe na wakati wa kujifurahisha na watoto wao. Ikiwa wewe ni muzazi, usiwafanye watoto wako wajisikie kama wafungwa kwa kuwakataza wasijifurahishe hata kidogo. Lakini, uwe mwangalifu kuhusu mambo ya kujifurahisha yasiyo mazuri. (1 Kor. 5:6) Kufikiri vizuri mbele ya wakati, kunaweza kukusaidia upate mambo mazuri ya kujifurahisha yatakayomufanya kila mutu katika familia yako ajisikie vizuri.b Ukifanya hivyo, wewe na familia yako mutakuwa mumechagua njia nzuri ambayo itawafanya mumukaribie Yehova zaidi.

      UPENDO WA KIFAMILIA

      16, 17. Wazazi wengi wamepatwa na jambo gani lenye kuhuzunisha, na tunajua namna gani kama Yehova anaelewa uchungu wao?

      16 Upendo ulio kati ya muzazi na mutoto wake ni wenye nguvu sana hivi kwamba Mungu aliutumia ili kuonyesha namna anavyowapenda watu wake. (Isa. 49:15) Kwa hiyo, ni jambo la kawaida kuhuzunika sana wakati mutu wa familia yetu anatengwa na kutaniko. Dada mumoja ambaye binti yake alitengwa, alisema hivi: “Nilihuzunika sana. Nilijiuliza, ‘Kwa nini binti yangu amemuacha Yehova?’ Nilifikiri kama kosa ni langu, na nilijilaumu.”

      17 Yehova anaelewa uchungu wako. Yeye pia ‘aliumia moyoni mwake’ wakati mwana wake wa kwanza wa kibinadamu alimuasi, na baadaye, wakati watu wengi walioishi mbele ya Garika, walipomuasi pia. (Mwa. 6:5, 6) Labda wale ambao mutu wa familia yao hajatengwa hawaweze kuelewa kabisa namna uchungu huo unavyomukoseha mutu usingizi. Hata hivyo, usiruhusu mwenendo mubaya wa mutengwa katika familia yenu ukutenganishe na Yehova. Kwa hiyo, namna gani unaweza kuvumilia huzuni inayotokana na kutengwa kwa mutu fulani wa familia yenu?

      18. Sababu gani wazazi hawapaswe kujilaumu wakati mutoto wao anatengwa na ushirika?

      18 Usijilaumu wakati jambo hilo linatokea. Yehova amemuachia kila mutu uhuru wa kuchagua, na kila mutu wa familia yetu ambaye amejitoa katika sala kwa Yehova na kubatizwa anapaswa ‘kubeba muzigo wake mwenyewe.’ (Gal. 6:5) Kwa vyovyote, Yehova anamuona yule aliyechagua kufanya zambi kuwa ndiye mwenye kosa, wala si wewe. (Eze. 18:20) Tena, usiwalaumu wengine. Heshimu mupango ambao Yehova anatumia ili kuwanyoosha watu wake. Umupinge Shetani, kuliko kuwapinga wazee wanaolinda kutaniko.​—1 Pet. 5:8, 9.

      [Picha katika ukurasa wa 16]

      Si vibaya kutumaini kama siku fulani mutu tunayemupenda atamurudilia Yehova

      19, 20. (a) Wazazi walio na watoto waliotengwa wanaweza kufanya nini ili kuvumilia huzuni yao? (b) Wazazi hao wanaendelea kuwa na tumaini gani?

      19 Kwa upande mwengine, ukichagua kumuwekea Yehova kinyongo ao kumukasirikia, hilo linaweza kukufanya ujitenge naye. Kwa kweli, jambo ambalo mutu huyo wa familia unayemupenda anahitaji, ni kuona kwamba upendo wako kwa Yehova ndilo jambo la maana zaidi kwako kuliko hata kifungo chenu cha familia. Kwa hiyo, ili uvumilie hali hiyo, unapaswa kuchunga hali yako mwenyewe ya kiroho. Usijitenge na ndugu na dada zako waaminifu. (Met. 18:1) Katika sala, umuambie Yehova namna unavyojisikia. (Zab. 62:7, 8) Usijipatie visababu na kuanza kushirikiana na mutu wa familia aliyetengwa; kwa mufano, kwa kuanza kuandikiana naye kupitia Internete. (1 Kor. 5:11) Uwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. (1 Kor. 15:58) Dada tuliyezungumuzia hapo juu anaendelea kusema hivi: “Ninajua kwamba ninapaswa kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Yehova, na kufanya hali yangu ya kiroho iwe nguvu, ili niweze kumusaidia binti yangu wakati atakapomurudilia Yehova.”

      20 Biblia inasema kwamba upendo ‘unatumaini mambo yote.’ (1 Kor. 13:4, 7) Kwa hiyo, ni vizuri kuendelea kutumaini kama siku moja, mutu wa familia unayemupenda atamurudilia Yehova. Kila mwaka, watengwa wengi wanatubu na kurudishwa katika tengenezo la Yehova. Yehova hatilie mashaka kutubu kwao. Lakini, yeye ‘iko tayari kusamehe.’—Zab. 86:5.

      FANYA MAAMUZI YA HEKIMA

      21, 22. Unapaswa kutumia namna gani uhuru wako wa kuchagua?

      21 Yehova, aliwaumba wanadamu wakiwa na uhuru wa kuchagua. (Soma Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.) Lakini uhuru huo unawapa wanadamu daraka nzito. Kila Mukristo anapaswa kujiuliza hivi: ‘Mimi ninafuata njia gani? Je, nimeruhusu kazi, mambo ya kujifurahisha, ao upendo wa familia unitenganishe na Yehova?’

      22 Upendo wa Yehova kwa watu wake haubadilike hata kidogo. Tunaweza tu kujitenga na Yehova ikiwa tu tunachagua kufuata njia mbaya. (Rom. 8:38, 39) Lakini, hatutake jambo hilo litupate! Kwa hiyo, tusiruhusu jambo lolote litutenganishe na Yehova. Habari inayofuata itazungumuzia mambo mengine mane yanayoweza kututenganisha na Yehova.

      a Ili kupata maelezo zaidi juu ya kuchagua kazi, soma sura ya 38 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2.

      b Kwa maelezo zaidi, soma Amkeni! ya Mwezi wa 11, 2011 ukurasa 17-19.

  • Endelea Kumukaribia Yehova
    Munara wa Mulinzi—2013 | Mwezi wa 1 15
    • [Picha katika ukurasa wa 17]

      Endelea Kumukaribia Yehova

      ‘Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia ninyi.’—YAK. 4:8.

      UNAWEZA KUJIBU?

      • Tunaweza kufanya nini ili vyombo vya kiteknolojia na mambo ya matunzo yasitutenganishe na Yehova?

      • Namna gani tunaweza kuwa na maoni yenye kufaa kuhusu feza na kujivuna?

      • Tunapaswa kufanya nini ili tubaki karibu na Yehova?

      1, 2. (a) Namna gani Shetani anawadanganya watu? (b) Ni nini itatusaidia tumukaribie Mungu?

      YEHOVA MUNGU aliwaumba wanadamu na tamaa ya kumukaribia. Hata hivyo, Shetani anataka tuwe kama yeye, tufikiri kama hatuna lazima ya Yehova. Tangu wakati alimudanganya Eva katika shamba la Edeni, Shetani anaendelea kuwafanya watu waamini uongo huo. (Mwa. 3:4-6) Katika historia yote, wanadamu wengi wameamini kwamba hawana lazima ya Yehova.

      2 Jambo lenye kufurahisha ni kwamba sisi ‘tunajua mbinu zake [ao njia zake za kudanganya].’ Kwa hiyo, si lazima tuanguke katika mitego ya Shetani (2 Kor. 2:11) Shetani anajaribu kututenganisha na Yehova kwa kutufanya tuchukue maamuzi mabaya. Lakini kama tulivyojifunza katika habari iliyotangulia, tunaweza kufanya maamuzi mazuri kuhusu kazi, kujifurahisha, na kuhusu mambo mengine yanayoweza kutokea katika familia. Habari hii itatuonyesha namna gani kufanya maamuzi ya hekima kuhusu mambo ya kiteknolojia, matunzo, feza na kujivuna kunakofaa, yanavyoweza kutusaidia ‘tumukaribie Mungu.’​—Yak. 4:8.

      MAMBO YA KITEKNOLOJIA

      3. Fasiria namna gani vyombo ambavyo teknolojia inatutolea vinaweza kutumiwa vizuri ao vibaya.

      3 Mashini ao vyombo vya kielektroniki vya kila namna vinapatikana sasa mahali pote. Vyombo hivyo vinaweza kutusaidia ikiwa tunavitumia vizuri. Ikiwa tunavitumia vibaya vinaweza kututenganisha na Baba yetu wa mbinguni. Tuchukue mufano wa ordinatere. Gazeti hili unalosoma sasa liliandikwa na kuchapishwa kwa kutumia ordinatere. Tunaweza kutumia ordinatere ili kutafuta habari fulani, kupashana habari na wengine, na wakati fulani tunaweza kuitumia ili kujifurahisha. Lakini, ordinatere inaweza pia kututawala. Wafanya-biashara wanawachochea watu wanunue ordinatere za kisasa. Kijana mumoja alitamani sana kupata ordinatere ndogo ya hali ya juu, na ili apate feza za kuinunua aliuzisha kwa siri figo yake moja. Huo ni upumbavu kabisa!

      4. Namna gani Joni alifikia kuachana na tabia ya kutumia ordinatere kupita kiasi?

      4 Ni jambo la kusikitisha hata zaidi ikiwa mutu anaharibu uhusiano wake na Yehova sababu ya kutumia vibaya vyombo ambavyo teknolojia inatutolea. Ndugu Jonia, mwenye miaka karibu 30 anasema hivi: “Ninajua kwamba Biblia inashauri ‘tujinunulie wakati unaofaa’ kwa ajili ya mambo ya kiroho. Lakini, ninapokuwa mbele ya ordinatere, ninashindwa kufuata shauri hilo.” Mara nyingi Joni alitumia Internete mupaka usiku sana. Yeye anaeleza hivi: “Kadiri nilivyokuwa mwenye kuchoka, ndivyo ilivyokuwa vigumu kwangu kutoka mbele ya ordinatere, kwa hiyo niliendelea kutumia wengine habari mbalimbali ao kutazama video, hata video fulani zisizofaa.” Ili kuachana na tabia hiyo, Joni alifanya ordinatere yake iwe ikijizimisha wakati saa yake ya kulala inafika.​—Soma Waefeso 5:15, 16.

      [Picha katika ukurasa wa 18]

      Wazazi, muwafundishe watoto wenu kutumia vyombo vya kiteknolojia kwa hekima

      5, 6. (a) Kazi ya wazazi ni nini? (b) Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wawe na marafiki wazuri?

      5 Wazazi, si lazima mujue kila jambo ambalo watoto wenu wanafanya, lakini munapaswa kuangalia sana matumizi yao ya ordinatere. Musiwaache watazame mambo ya uasherati, michezo ya kuuana, mambo ya uchawi ao maji, na kurafikiana na marafiki wabaya kwenye Internete ili tu kuwafanya wawe na jambo fulani la kufanya ao ili wasiwasumbue. Mukiwaacha wafanye hivyo, wanaweza kuwaza hivi: ‘Mambo haya si mabaya sababu Papa na Mama hawaseme kitu.’ Wazazi, kazi yenu ni kuwalinda watoto wenu na jambo lolote linaloweza kuwatenganisha na Yehova. Hata wanyama wanawalinda watoto wao wasipatwe na hatari. Wazia jambo ambalo dubu anaweza kufanya wakati mutu fulani anawachokoza watoto wake.​—Linganisha na Hosea 13:8.

      6 Wafundishe watoto wako namna wanaweza kufanya urafiki na Wakristo vijana na wazee walio mifano mizuri. Na usisahau kama watoto wako wanataka wewe upitishe wakati pamoja nao! Kwa hiyo, tafuta wakati wa kucheka, kucheza, kufanya jambo fulani pamoja na watoto wako, na ‘mumukaribie Mungu’ pamoja.b

      MAMBO YA MATUNZO

      7. Sababu gani sisi sote tunataka kuendelea kuwa na afya nzuri?

      7 “Habari gani?” Kila mara tunauliza wengine ulizo hilo ili kujua ikiwa wana afya nzuri ao hapana. Sisi sote tunagonjwa sababu wazazi wetu wa kwanza waliruhusu Shetani awatenganishe na Yehova. Shetani anafurahi wakati tunagonjwa, sababu katika hali hiyo inakuwa vigumu kwetu kumutumikia Yehova. Na ikiwa tunakufa, hatuweze kumutumikia Yehova hata kidogo. (Zab. 115:17) Kwa hiyo, ni jambo la kawaida, kufanya yote tunayoweza ili kuendelea kuwa na afya nzuri.c Na tunapaswa kuhangaikia afya ya ndugu na dada zetu.

      8, 9. (a) Namna gani tunapaswa kuepuka kuhangaikia afya yetu kupita kiasi? (b) Kuwa na furaha kunaleta faida gani?

      8 Hata hivyo, tunapaswa kuepuka kuhangaikia afya yetu kupita kiasi. Wahubiri fulani wanatia watu moyo sana kuhusu aina fulani ya vyakula, matunzo na dawa mbalimbali, na wanafanya hivyo kwa bidii sana kuliko hata bidii walio nayo katika kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wanaweza kufikiri kwa moyo wote kwamba wanapofanya hivyo wanawasaidia wengine. Hata hivyo, hatupaswe kuja na madawa fulani ao vitu vya kujipondoa kwenye Jumba la Ufalme ao kwenye mikusanyiko na kuanza kutapatapa vitu hivyo mbele na kisha mikutano. Sababu gani hatupaswe kufanya hivyo?

      9 Kusudi letu la kuja kwenye mikutano ao mikusanyiko ni kuzungumuzia habari za kiroho na kuongeza furaha yetu, ambayo ni sehemu moja ya tunda la roho ya Mungu. (Gal. 5:22) Kuzungumuzia ufundi fulani wa matunzo ao madawa kwenye mikutano, hata ikiwa wengine wanatuuliza ao hapana, kunaweza kufanya tusahau kusudi la mikutano yetu na kufanya wengine wapoteze furaha yao. (Rom. 14:17) Mambo ya matunzo ni uamuzi wa pekee. Zaidi ya hayo, hakuna mutu aliye na dawa ya magonjwa yote. Hata waganga wakubwa wanagonjwa na kuzeeka, na mwishowe wanakufa. Na hata ikiwa tunahangaikia afya yetu kupita kiasi, hatuweze kurefusha maisha yetu. (Lu. 12:25) Lakini, “moyo wenye shangwe [ao furaha] ni dawa nzuri.”​—Met. 17:22.

      10. (a) Ni sifa gani zinazotufanya tuwe wenye kupendeza machoni pa Yehova? (b) Ni wakati gani tutakuwa na afya nzuri kabisa?

      10 Vilevile, ni jambo la kawaida mutu kuhangaikia namna anavyoonekana mbele ya watu wengine. Lakini hatupaswe kujitesa ili kuondoa alama zote za uzee. Alama hizo zinaonyesha kwamba tumekomaa, zinawafanya watu watuheshimu na zinaonyesha uzuri wa ndani. Kwa mufano, Biblia inasema hivi: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Met. 16:31) Yehova anatuona namna tulivyo, na sisi tunapaswa kuwa na maoni hayo. (Soma 1 Petro 3:3, 4.) Kwa hiyo, je, ni jambo la hekima kufanyiwa upasuaji hatari ao kutumia njia fulani za utunzaji zilizo hatari ili tu sura yetu iwe yenye kuvutia? “Shangwe ya Yehova” ndio uzuri wetu unaotoka ndani, iwe tuna afya nzuri ao hapana. (Neh. 8:10) Ni katika dunia mupya tu ndio tutakuwa na afya kamilifu na kurudilia tena uzuri wa ujana. (Ayu. 33:25; Isa. 33:24) Lakini sasa, kuwa na hekima inayofaa na kuwa na imani kutatusaidia tubaki karibu ya Yehova na kuendelea kutumia maisha yetu kadiri iwezekanavyo ili kufanya mapenzi yake, iwe tuna afya nzuri ao hapana.​—1 Tim. 4:8.

      MAMBO YA FEZA

      11. Namna gani feza zinaweza kuwa mutego?

      11 Si vibaya kuwa na feza ao kufanya biashara isiyo ya udanganyifu. (Mhu. 7:12; Lu. 19:12, 13) Hata hivyo, ‘kupenda pesa’ kunaweza kabisa kututenganisha na Yehova. (1 Tim. 6:9, 10) ‘Mahangaiko ya mufumo huu wa mambo’ ni kusema, kuhangaikia kupita kiasi mahitaji ya kimwili, kunaweza kusonga hali yetu ya kiroho. “Nguvu za udanganyifu wa utajiri,” ni kusema, kufikiri kama utajiri unaweza kutuletea furaha ya kudumu na kutuepusha na matatizo, kunaweza pia kusonga hali yetu ya kiroho. (Mt. 13:22) Yesu alionyesha waziwazi kama “hakuna anayeweza” kutumikia Mungu na utajiri.​—Mt. 6:24.

      12. Watu wameangukia katika mitego gani leo kwa sababu ya tamaa ya feza, na namna gani tunaweza kuiepuka?

      12 Ikiwa tuna maoni yasiyofaa kuhusu feza, jambo hilo linaweza kutuingiza katika matendo mabaya. (Met. 28:20) Kwa sababu wameahidiwa kupata feza haraka, ndugu fulani wamejiingiza katika mambo ya tombola; ao katika ahadi nyingi za kupata feza na kisha wanatafuta watu wengine wa kujiunga nao, ili waweze kulipwa zaidi. Wamewachochea hata ndugu na dada katika kutaniko wajiunge nao. Wengine wamedanganywa kwa kuahidiwa kama watapata feza nyingi ikiwa wanatia kiasi fulani cha feza katika mipango fulani. Usidanganywe kwa sababu ya tamaa ya feza. Tumia akili. Ikiwa unaambiwa kama utapata feza nyingi sana kuliko ilivyo kawaida, ni uongo.

      13. Maoni ya Yehova kuhusu feza yanatofautiana namna gani na maoni ya watu wa ulimwengu?

      13 Tunapotia “Ufalme na uadilifu wake,” pa nafasi ya kwanza Yehova atabariki mipango tunayofanya ili kupata mahitaji ya lazima ya maisha. (Mt. 6:33; Efe. 4:28) Yehova hapende tuanze kusinzia kwenye mikutano kwa sababu tulitumika kupita kiasi ao hapende tuanze kuwaza-waza juu ya feza tunapokuwa katika Jumba la Ufalme. Watu wengi wanafikiri kama ikiwa wanatumia nguvu zao zote ili kutafuta feza, hawatakosewa kitu wakati wa uzee na maisha yao haitakuwa na mahangaiko wakati huo. Kila mara wanawachochea watoto wao kwenye miradi hiyohiyo ya kupata vitu vya kimwili. Yesu alionyesha kama mawazo hayo ni upumbavu. (Soma Luka 12:15-21.) Hilo linatukumbusha mufano wa Gehazi aliyefikiri kama anaweza kuwa na pupa na wakati huohuo kuendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova.​—2 Fal. 5:20-27.

      14, 15. Sababu gani si jambo la hekima kufikiri kama feza zinaweza kumuondolea mutu mahangaiko katika ulimwengu huu? Toa mufano.

      14 Imeripotiwa kwamba tai fulani zimezama katika maji kwa sababu ya kugangania tu samaki iliyokuwa na uzito mwingi zaidi. Mukristo anaweza kujikuta katika hali kama hiyo kuhusiana na mambo ya feza. Muzee mumoja anayeitwa Alex, anasema hivi: “Kwa kawaida mimi situpetupe feza zangu, ninapenda kuweka feza, sina tabia ya kutumia feza.” Lakini wakati fulani, Alex alifikiri kama ikiwa anapata feza nyingi zaidi ataacha kazi yake ili kuwa painia. Kwa hiyo alijifunza biashara ya kununua vitu ili kuviuzisha wakati ambapo bei ingepanda. Na alitumia feza zote alizokuwa ameweka na alijikopesha zingine ili kununua vitu ambavyo aliambiwa kama vitapanda bei. Kuliko kupanda, bei ilishuka sana. Alex anaeleza hivi: “Sikutaka feza zangu zipotee. Nilifikiri kama ikiwa ninangojea kidogo, bei itapanda na feza zangu zitarudia.”

      15 Kwa miezi mingi, Alex alikuwa tu akiwaza kuhusu biashara yake. Hakuwa tena anawaza mambo ya kiroho, na alikosa usingizi. Lakini bei ya vitu haikupanda na feza zake zilihomba kabisa. Alex alipoteza feza zake zote na alilazimika kuuzisha nyumba yake. Yeye anasema hivi: “Nilihuzunisha sana familia yangu.” Lakini alipata somo. Anaongeza hivi: “Sasa nimetambua kama kila mutu anayetumainia ulimwengu huu wa Shetani anajichokesha bure na atavunjika moyo.” (Met. 11:28) Kwa kweli, katika ulimwengu huu kutumainia feza ulizo nazo, uwezo ulio nao wa kutafuta feza ni kutumainia “mungu wa mufumo huu wa mambo,” ni kusema, Shetani. (2 Kor. 4:4; 1 Tim. 6:17) Kwa sasa Alex amerahisisha maisha yake “kwa ajili ya habari njema.” Ukimuuliza, atakuambia kwamba kufanya hivyo kumemuletea furaha zaidi yeye na familia yake na kumewasaidia wamukaribie Yehova zaidi.​—Soma Marko 10:29, 30.

      KUJIVUNA KUNAKOFAA

      16. Kuna tofauti gani kati ya kujivuna kunakofaa na kiburi?

      16 Si vibaya kujivuna kwa sababu ya mambo mazuri. Kwa mufano, kila siku tunapaswa kujivuna kwa sababu sisi ni Mashahidi wa Yehova. (Yer. 9:24) Kujivuna kwa njia inayofaa kunatusaidia tuchukue maamuzi mazuri na kufuata sheria za Mungu. Lakini kuwa na kiburi na kufikiri kama tunajua mambo mengi sana kupita wengine kunaweza kututenganisha na Yehova.​—Zab. 138:6; Rom. 12:3.

      [Picha katika ukurasa wa 21]

      Kuliko kutafuta madaraka juu chini katika kutaniko, furahia kazi ya kuhubiri!

      17, 18. (a) Biblia inazungumuzia watu gani waliokuwa wanyenyekevu, na watu waliokuwa wenye kiburi? (b) Ndugu mumoja alifanya nini ili kiburi kisimutenganishe na Yehova?

      17 Biblia inazungumuzia watu waliokuwa na kiburi na wengine waliokuwa wanyenyekevu. Mufalme Daudi alimuomba Yehova kwa unyenyekevu amuongoze, na Yehova alimubariki. (Zab. 131:1-3) Lakini Yehova aliwanyenyekeza Nebukadneza na Belshaza sababu walikuwa na kiburi. (Dan. 4:30-37; 5:22-30) Leo, hali fulani zinaweza kufunua ikiwa sisi ni wanyenyekevu ao hapana. Fikiria mufano wa ndugu Ryan, mutumishi wa huduma mwenye miaka 32, aliyehamia katika kutaniko fulani. Yeye anasema hivi: “Nilitazamia kwamba nitapendekezwa mara moja kuwa muzee. Lakini mwaka mumoja ukapita bila mimi kupendekezwa.” Je, Ryan aliwakasirikia wazee na kufikiri kama hawamupende? Je, aliacha kukusanyika, na kuruhusu kiburi kimutenganishe na Yehova na watu Wake? Wewe ungefanya nini?

      18 Ndugu Ryan anasema hivi: “Nilisoma habari mbalimbali kuhusu namna ya kungojea jambo nzuri linalochelewa.” (Met. 13:12) “Nilianza kutambua kama ninapaswa kujifunza kuwa na uvumilivu na unyenyekevu. Nilipaswa kumuacha Yehova anizoeze.” Ryan aliacha kujifikiria sana na akaanza kufikiria namna gani anaweza kuwasaidia ndugu na dada katika kutaniko na wale anaokutana nao katika mahubiri. Kwa wakati kidogo tu alianza kuongoza mafunzo mengi ya Biblia yenye kufanya maendeleo. Yeye anasema hivi: “Kisha mwaka mumoja na nusu baadaye, nilitiwa kuwa muzee. Hilo lilikuwa jambo ambalo sikutazamia. Nilikuwa nimeacha kufikiria jambo hilo sababu kazi ya mahubiri ilikuwa yenye kufurahisha sana.”​—Soma Zaburi 37:3, 4.

      BAKI KARIBU NA YEHOVA!

      19, 20. (a) Tunaweza kufanya nini ili mambo ambayo tumezungumuzia yasitutenganishe na Yehova? (b) Tunaweza kuiga mifano gani ya watu waliobaki karibu na Yehova?

      19 Mambo yote ambayo tumezungumuzia katika habari hii na ile iliyotangulia si mabaya kabisakabisa. Tunajivunia kuwa watumishi wa Yehova. Familia yenye furaha na afya nzuri ni kati ya zawadi nzuri sana ambazo Yehova ametutolea. Tunajua kwamba kazi ya kimwili na feza vinaweza kutusaidia ili kutimiza mahitaji yetu. Kujifurahisha kunaweza kutupumuzisha na vyombo vya kiteknolojia vinaweza kutusaidia sana. Lakini vitu hivyo vinaweza kututenganisha na Yehova ikiwa tunavifuatilia pa wakati usiofaa, ikiwa tunavihangaikia kupita kiasi ao vinatufanya tukose wakati kwa ajili ya mambo ya kiroho.

      Usiruhusu kitu chochote kikutenganishe na Yehova!

      20 Kwa kweli, Shetani anataka vitu hivyo visivyokuwa vibaya kabisakabisa vitutenganishe na Yehova. Lakini, unaweza kuepuka jambo hilo lisikufikie ao kufikia familia yako! (Met. 22:3) Umukaribie Yehova na ubaki karibu naye. Biblia ina mifano mingi inayoweza kutusaidia kufanya hivyo. Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu wa kweli.’ (Mwa. 5:22; 6:9) Musa ‘aliendelea kuwa imara kama mutu anayemuona Yeye asiyeonekana.’ (Ebr. 11:27) Yesu aliendelea kutegemezwa na Mungu kwa sababu siku zote alifanya mambo yanayomupendeza Baba yake wa mbinguni. (Yoh. 8:29) Iga mifano hiyo. ‘Shangilia sikuzote. Sali bila kuacha. Kuhusiana na kila jambo toa shukrani.’ (1 Thes. 5:16-18) Na usiache kitu chochote kikutenganishe na Yehova!

      a Majina yamebadilishwa.

      b Soma habari “Kuwalea Watoto Wenye Kutegemeka” katika Amkeni! ya Mwezi wa 10, 2011.

      c Soma “Njia Tano Ili Kuwa na Afya Bora” katika Amkeni! ya Mwezi wa 3, 2011.

Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili (Congo)
  • Tumia Wengine
  • Préférences
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Kanuni za Matumizi
  • Kanuni za Kutunza Siri
  • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
  • JW.ORG
  • Ingia
Tumia Wengine