Somo 1
Mungu Anataka Uwe Rafiki Yake
Mungu anataka uwe rafiki yake. Je, umewahi kuwazia kwamba unaweza kuwa rafiki ya Mtu mkuu zaidi katika ulimwengu wote? Abrahamu, aliyeishi zamani za kale, aliitwa rafiki ya Mungu. (Yakobo 2:23) Watu wengine pia wanaotajwa katika Biblia walikuwa marafiki wa Mungu, nao walibarikiwa sana. Leo, watu kutoka sehemu zote za dunia wamekuwa marafiki wa Mungu. Wewe pia unaweza kuwa rafiki ya Mungu.
Kuwa rafiki ya Mungu ni bora kuliko kuwa rafiki ya binadamu yeyote. Mungu hawavunji moyo kamwe marafiki wake wenye uaminifu-mshikamanifu. (Zaburi 18:25) Kuwa rafiki ya Mungu ni bora kuliko kuwa na mali. Tajiri anapokufa, fedha zake huchukuliwa na watu wengine. Lakini, wale wanaofurahia urafiki pamoja na Mungu wana kitu fulani chenye thamani ambacho hakuna mtu anayeweza kuwanyang’anya.—Mathayo 6:19.
Huenda watu fulani wakajaribu kukuzuia usijifunze juu ya Mungu. Hata huenda wengine kati ya marafiki wako na familia yako wakajaribu kukuzuia. (Mathayo 10:36, 37) Watu wengine wakikucheka au kukutisha, jiulize hivi, ‘Je, mimi ninataka kumpendeza nani—binadamu au Mungu?’ Fikiria jambo hili: Ikiwa mtu fulani angekuambia uache kula chakula, je, ungemtii? Bila shaka hapana! Unahitaji chakula ili uishi. Mungu anaweza kukufanya uishi milele! Kwa hiyo, usiache kamwe mtu yeyote akuzuie usijifunze jinsi ya kuwa rafiki ya Mungu.—Yohana 17:3.